Sunday, December 27, 2015

HABARI MBALIMBALI ZA MKOA WA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unatarajiwa kuwa moja ya mikoa ambayo itakuwa kwa kasi kutokana na kuongezeka kwa shughuli nyingi za uwekezaji za kiuchumi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa bandari wilayani Bagamoyo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa mkoa una fursa nyingi za uwekezaji na watu binafsi pamoja na makampuni yameonyesha nia ya kuwekeza.

Ndikilo alisema kuwa uwekezaji umeanza kuchukua nafasi yake baada ya Jiji la Dar es Salaam kuonekana kuwa limejaa hivyo fursa iliyopo ni mkoa huo ambao uko jirani na Dar es Salaam.

“Kwa sasa tunajivunia na mojawapo ya uwekezaji mkubwa ni ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo ambayo itaongeza pato la mkoa huo kwani utazalisha ajira nyingi na wageni wengi wataingia kwa ajili ya shughuli nyingi za kibiashara,” alisema Ndikilo.

Alisema uwekezaji mwingine ni pale Kisarawe ambapo kimejengwa kiwanda cha saruji, Kibaha kuna viwanda vya Jipsam, Nondo na uwekezaji sehemu nyingine mbalimbali za wilaya zinazounda mkoa huo.

“Tukija kwenye zao kuu la biashara la Korosho nalo limezidi kunufaisha wakulima ambapo kwa sasa kilo ya korosho imepanda na kwa mnada sasa inauzwa kati ya 2,600 na 2,700 kutoka chini ya shilingi 1,000 na hii ni kutokana na mfumo wa stakabadhi ghalani,” alisema Ndikilo.

Aidha alisema kuwa kwa kipindi kirefu mkoa huo haukuwa na fursa nyingi hali ambayo ilisababisha uonekane kama uko nyuma kiuchumi tofauti na ilivyo sasa fursa zimekuwa nyingi sana hivyo mafanikio ya kiuchumi yatakuwa makubwa.

Aliwataka watu wa mkoa huo hususani vijana kutumia fursa hizo zilizopo ambazo zimejitokeza kwa sasa ili kujikwamua na hali ngumu ya kimaisha pia watumie fursa za kilimo ambazo ni nyingi.

Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unaendelea na uhakiki wa watu walioweka mashamba pori ili taarifa zipelekwe kwa Waziri husika na baadaye kwa Rais ili kutengua umiliki wao endapo watashindwa kuyaendeleza hususani wale walionunua kwenye kitovu cha Mji wa Kibaha.

Kwa mujibu wa Mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa kuna mashamba pori mengi makubwa ambayo hayajaendelezwa kwenye wilaya zote za mkoa huo ikiwa ni pamoja na Kibaha, Kisarawe, Rufiji, Bagamoyo na Mkuranga.

Ndikilo alisema kuwa tayari wameshaanza kuyafanyia kazi mashambapori hayo kwa kushirikiana na wakurugenzi wa Halmashauri kwa mashamba yasiyoendelezwa.

“Tayari tumeshawapelekea notisi baadhi yao ili wajieleze ni kwanini wameshindwa kuyaendeleza mashamba hayo na kwanini wasinyanganywe kutokana na kushindwa kuyaendeleza,” alisema Ndikilo.

Kwa upande wa kitovu cha Mji wa Kibaha ambako ndiyo makao makuu ya mkoa huo alisema kuwa wamiliki binafsi pamoja na taasisi ambazo ni nyingi wameshapewa barua kujieleza kwanini hawakuviendeleza viwanja hivyo.

“Tunawashangaa ni kwa nini wameshindwa kuendeleza viwanja hivyo ambavyo endapo vingejengwa vingeweka suraa nzuri ya mji kwani hapo ndiyo kwenye mandari ya uso wa mji,” alisema Ndikilo.

Alisema kuwa licha ya kutakiwa kujieleza kwa nini hawakuviendeleza viwanja hivyo pia waeleze kuwa watavijenga lini na muda watakaokubaliana hawapaswi kuupitisha tena.

“Kwa watakaoshindwa kuviendeleza baada ya makubaliano watanyanganywa viwanja hivyo ili wapewe wengine watakaoweza kuviendeleza kwa kujenga kwa wakati ukaoakuwa umepangwa,” alisema Ndikilo.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

JUMUIYA ya Wazazi kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kibaha Mjini kimezigawia Jumuiya za Kata ardhi yenye ukubwa wa hekari moja kwa lengo la kuziendeleza kiuchumi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha baada ya zoezi hilo la kuwagawia ardhi hiyo ambalo lilifanyika kwenye sherehe za siku ya Uhuru, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Kibaha Mjini Dk Athuman Mokiwa alisema kuwa eneo hilo litakuwa kitovu cha uchumi wa Jumuiya hiyo.

Mokiwa alisema kuwa eneo hilo lenye ukubwa wa hekari 15 wameligawa kwa kata 14 za kichama ambapo kila kata inapaswa kuziendeleza kwa kulima na baadaye kufanya ujenzi.

“Kipindi cha nyuma tulishindwa kuliendeleza kutokana na kukosa fedha kwa ajili ya kulipima lakini baada ya kulipima sasa tumegawa kila kata wawe na eneo lao kwa ajili ya shughuli za kiuchumi,”alisema Dk Mokiwa.

Alisema kuwa shamba hilo lilikuwa likivamiwa na watu kutokana na kutokuwa na hati za umiliki lakini kwa sasa wameshalimiliki kisheria hivyo hakuna mtu atakayeweza kuvamia tena.

Naye katibu wa Wazazi kata ya Kibaha lilipo shamba hilo Rehema Ally alisema kuwa wanaushukuru uongozi kwa kuwapatia eneo ambapo wanatarajia kuliendeleza na hiyo ni rasilimali yao kiuchumi.

Ally alisema kuwa baada ya kupatikana hati watawakaribisha wawekezaji kwa ajili ya kujenga taasisi zikiwemo za shule au zaahanati na huduma nyingine za kijamii.

Viongozi wa Jumuiya hizo za kata wamekubaliana kufanya usafi kila baada ya wiki mbili ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Rais Dk John Magufuli juu ya usafi kukabiliana na magonjwa ya milipuko pia kuweka maeneo mbalimbali katika hali ya usafi.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

KUFUATIA dereva wa Pikipiki wa Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani Ally Rashid (35) kuuwawa kwa kupigwa risasi na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kisha kumpora pikipiki aliyokuwa akiieendesha madereva wenzake wameomba uchunguzi wa kina ufanyike kuhusiana na tukio hilo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha katibu wa Chama Cha Madereva Pikipiki Kibaha (CHAWAMAPIKI) Shaban Kambi alisema tukio hilo ni la kushangaza kwa watu kutumia bunduki kwa ajili ya kupora pikipiki likiwa ni tukio la pili.
Kambi alisema kuwa kumekuwa na matukio ya wizi wa pikipiki lakini kwa kutumia bunduki si hali ya kawaida hivyo tunaomba polisi wafuatilie tukio hilo la kusikitisha kwa mwenzetu kuuwawa.

“Matukio ya kutumia silaha ni matatu ambapo mtu mmoja alivamiwa nyumbani kwake na kupigwa risasi na kufa la pili ni mwenzetu mwingine alipigwa risasi ya mguuni na kuporwa pikipiki lakini hakufa huku mwenzetu wa juzi naye alipigwa risasi na kufa ambapo cha kushangaza matukio yote yametokea upande mmoja,” alisema Kambi.

Alisema matukio yote hayo yametokea maeneo ya machinjioni hali ambayo inawapa hofu wakazi wa Maili Moja kwa kuona kuwa maisha yao sasa yako hatarini kwa watu hao kufanya uahalifu kwa kutumia bunduki.

“Tumesha waambia madereva pikipiki kuwa makini kwani kuna baadhi ya maeneo kwa sasa ni hatarishi pia wakiwa na wasiwasi wasiwabebe watu wasiowafahamu hasa nyakati za usiku hasa katika kipindi hichi cha mwisho wa mwaka,” alisema Kambi.

Aidha alisema kuwa wao wako tayari kushirikiana na jeshi la polisi katika kufuatilia watu wanaojihusisha na matukio hayo ya uporaji wa pikipiki pamoja na mali za watu.

Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha

MKOA wa Pwani unatarajia kujenga Kituo Kikubwa cha Mabasi pamoja na Soko baada ya kupata mkopo toka Benki ya Uwekezaji ya (TIB) na kuufanya mji wa Kibaha kuwa wakisasa.

Hayo yalisemwa na mkuu wa mkoa wa Pwani alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo na kusema kuwa kwa sasa taratibu zinaendelea baina ya Halmashauri ya Mji wa Kibaha na benki hiyo.

Ndikilo alisema kuwa ujenzi huo unatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa mara taratibu za kitaalamu zitakapokamilika ambapo kwa sasa bado zinaendelea.

“Tunatarajia kuwa na stendi ya kisasa pamoja na soko hasa ikizingatiwa mkoa ulikuwa hauna soko kubwa bali lililopo ni dogo na halina uwezo wa kuchukua bidhaa nyingi,” alisema Ndikilo.
Alisema kuwa wafanyabiashara wa mkoa wa Pwani hususani wale wa makao makuu ya mkoa Maili Moja na vitongoji vyake huwalazimu kwenda kununua bidhaa Kariakoo au kwenye masoko mengine Jijini Dar es Salaam jambo ambalo linafanya bei za bidhaa kuwa juu.

“Kibaha ambako ndiyo makao makuu ya mkoa ni kama malango wa Jiji la Dar es Salaam lakini bidhaa zimekuwa zikipita hapa na kwenda huko kisha wafanyabiashara kwenda kununua na kuzirudisha hapa hivyo kupandisha bei kutokana na gharama kuwa kubwa,” alisema Ndikilo.

Aidha alisema kuwa soko hilo ambalo litajengwa sambamba na stendi litakuwa la kisasa ambapo magari yatakuwa na uwezo wa kuingia na kushusha bidhaa na si kama ilivyo sasa ambapo kutokana na udogo wa soko lililopo hubidi magari ya bidhaa yashindwe kuingia.

Mwisho.
  

   

   

  




WATAKA TAFSIRI YA UPANUZI WA BARABARA WAPATE HAKI ZAO

Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI wa Kijiji cha Kiluvya B wilaya ya Kisarawe mkoa wa Pwani wameiomba Wizara ya Ujenzi na Makazi iangalie upya tafsiri ya upanuzi wa barabara kuu kwani upanuzi uliofanyika ni urefu wa mita 120 upande mmoja wakati sheria inasema kila upande wa barabara itapanuliwa kwa urefu wa mita 60 kwa 60 kutoka katikati ya barabara kuu.
Kutokana na sheria hiyo kutafsiriwa mita 120 nyumba zilizojengwa kando ya Barabara ya Morogoro baadhi zimebomolewa na nyingine zimeekewa alama ya X zikitakiwa kubomolewa baada ya muda usiozidi zaidi ya wiki moja na kupelekea kilio kikubwa kwa wakazi hao.
Wakizungumza waandishi wa habari waliotembelea kijiji hicho moja ya wakazi hao aliyejitambulisha kwa jina la Abubakary Yusuph alisema kuwa athari ya kubomolewa nyumba hizo ni kubwa sana hivyo kuomba suala hilo liangaliwe upya.
Yusuph alisema kuwa wao hawana tatizo la kuondoka kwenye eneo hilo kwa ajili ya kupisha shughuli za maendeleo bali wameomba sheria ifuatwe ili wasinyimwe haki zao kwani wao wako hapo tangu vilipoanzishwa vijiji vya ujamaa miaka ya 70.
“Tunaomba wizara na serikali kuliangalia upya suala hili kwani sisi hatuna shida kwa wale waliojenga ndani ya mita 60 kwani tunajua suala hilo ni la kisheria lakini mita 120 tunaona kuwa hatujatendewa haki ni vema wanapotekeleza suala hilo wakazingatia sheria ya barabara na kama wanataka eneo zaidi ni vema wakatulipa ndipo waendelee na zoezi hilo,” alisema Yusuph.
Alisema kuwa watu wengi walijenga umbali zaidi ya mita 60 kwani walikuwa wakijua kuwa kama watakuwa ndani ya mita hizo basi bomobomoa ikija wangebomolewa nyumba zao lakini walikojenga walijua wako salama wanashangaa kuona nyumba zao zinabomolewa.
Naye Alfonce Kejo alisema kuwa baadhi yao ni wastaafu na hawana kipato chochote na waliwekeza kwenye nyumba zao kwa ajili ya makazi mara baada ya kustaafu kazi hivyo wanaomba suala lao lishughulikiwe ili wapate haki yao.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Kijiji hicho Julius Bukoli ambaye naye amekumbwa na bomoa bomoa hiyo alisema kuwa nyumba yake aliijenga kabla ya mwaka 2000 na iko umbali wa karibu mita 100 toka barabara kuu lakini ametakiwa kubomoa.
Bukoli alisema kuwa hata wanaohusika katika kubomoa nyumba hizo hawafuati taratibu za kutoa taarifa kwenye uongozi wa Kijiji bali wanakuja nyakati za jioni na kubomoa au kuweka alama za X kisha kuondoka.
Mwisho.  
Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA Cha Kuweka na Kukopa Cha TCCIA Saccos mkoa wa Pwani kimeweza kukopesha mikopo inayofikia zaidi ya shilingi milioni 398 kwa wanachama wake.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha, Meneja wa chama hicho Arestide Temu alisema kuwa fedha hizo zimetolewa kwa  wanachama waliofuata taratibu za mikopo kwa lengo la kukuza mitaji yao ya biashara.

Temu alisema kuwa hata hivyo biashara nyingi kwenye mkoa huo zinashindwa kukua vizuri kutokana na kutokuwa na mzunguko mkubwa wa fedha kwa sababu ya kuwa na shughuli chache za kiuchumi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa viwanda.

“Sababu nyingine ya wafanyabiashara kushindwa kufikia malengo ni kutokana na kufanya biashara zinazofanana na kusababisha kushindwa kufikia malengo hata hivyo tumepata mafanikio tumeweza kupata faida ya shilingi milioni 26 tofauti na lengo la kupata faida ya shilingi milioni 20 tulizokuwa tumejipangia kwa mwaka huu ambapo faida hiyo ni hadi mwezi Novemba mwaka huu,” alisema Temu.

Alisema kuwa maendeleo ya chama yanakwenda vizuri ambapo kwa sasa wamanachama wanaweza kukopa mara tatu ya fedha walaizojiwekea kama akiba na wanaweza kukopa hadi shilingi milioni 15 kwa mara moja.

“Riba ni asilimia 15 ya mkopo wowote anaoomba mwanachama ambapo hisa moja inauzwa kiasi cha shilingi 10,000 huku mwanachama akitakiwa kununua hisa kuanzia 10 na kuendelea,” alisema Temu.
Aidha alisema kuwa chama hicho cha kuweka na kukopa kilianzishwa mwaka 2001 kikiwa na wanachama 600 ambapo kwa sasa kina wanachama 227 huku wengine wakiwa wameondolewa kwa kushindwa kufuata taratibu za chama.   

Mwisho.




Saturday, December 26, 2015

BONANZA LA KUAGA MWAKA 2015 NA KUUKARIBISHA 2016 KUFANYIKA JANUARI MOSI KIBAHA

Na John Gagarini, Kibaha
BONANZA la kuuaga mwaka 2015 na kuukaribisha mwaka 2016 linatarajiwa kufanyika Januari Mosi mwakani kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha (KEC) Tumbi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Msajili Msaidizi wa Vilabu na Vyama vya Michezo wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Abdul Haufi alisema kuwa Bonanza hilo litakuwa la wazi kwa watu wote.
Haufi alisema kuwa shindano hilo litakuwa la michezo mbalimbali litashirikisha mashirika ya Umma, binafsi pamoja na watu binafsi au mtu mmoja mmoja kwenye michezo ya soka, mpira wa pete kwa wanawake, kuvuta kamba, riadha mita 100.
Alitaja michezo mingine kuwa ni kukimbia na magunia, kurusha kisahani, tufe, mpira wa wavu, kijiko na ndimu ambapo usajili unafanyika kwenye ofisi za Halmashauri hiyo.
“Tunatarajia jumla ya wanamichezo 250 kushiriki Bonanza hilo la aina yake kufanyika mjini Kibaha na vitongoji vyake ambapo lengo ni kuhamasisha watu kushiriki michezo pamoja na kudumisha urafiki baina ya mashirika bianafsi, ya umma pamoja na watu binafsi,” alisema Haufi.
Aidha alisema kuwa juu ya wadhamini tayari baadhi wameshajitokeza huku wakiwasubiri wengine wamalizia taratibu za kudhamini Bonanza hilo na matarajio ni kutolewa zawadi nono.
Bonanza hilo limeandaliwa kwa pamoja na Halmashauri ya Mji Kibaha, Majeshi ya mkoani Pwani ikiwa ni pamoja na Magereza, Polisi na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).
Mwisho.
  


WAVAMIZI WA VIWANJA VYA MICHEZO WAONYWA NA WAZIRI

Na John Gagarini, Kibaha
NAIBU Waziri wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Anastazia Wambura amewataka watu wanaovamia maeneo ya viwanja vya michezo kukomesha tabia hiyo kwani inawanyima fursa vijana kushiriki kwenye michezo.
Aliyasema hayo hivi karibu mjini Kibaha wakati akifunga michuano ya kombe la Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka (Koka Cup) kwenye uwanja wa Mwendapole wilayani humo na kusema kuwa watu hao hawapaswi kuungwa mkono kwani wanawanyima ajira vijana.
Wambura alisema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakivamia maeneo ya michezo na kujenga jambo ambalao linakwenda kinyume na matumizi yaliyopangwa na serikali hivyo vijana kushindwa kuendeleza vipaji vyao.
“Watu wenye tabia hii inabidi waiache kwani inadumaza azma ya serikali kuendeleza michezo mbalimbali hapa nchini hasa ikizingatiwa licha ya michezo kuwa ni burudani lakini pia inatoa fursa ya ajira hasa kwa vijana,” alisema Wambura.
Alisema kuwa serikali imekuwa na mipango mbalimbali ya kuendeleza michezo ikiwa ni pamoja na kuwa na viwanja ambavyo vitawawezesha vijana kushiriki michezo hivyo watu wanaovamia na kujenga ni dhahiri wanakwamisha juhudi hizo.
“Tunaomba wadau wa michezo wahamasishe ujengwaji wa viwanja vya kisasa ambapo baadhi ya watu wameonyesha uzalendo kwa kujenga viwanja ambavyo vinaendeleza jitihada za serikali kuendeleza michezo,” alisema Wambura.
Kwa upande wake Koka alisema kuwa lengo la kuandaa mashindano hayo ni kuwahamasisha vijana kushiriki michezo kwenye Jimbo lake ambapo alizipatia timu zote vifaa vya michezo kwa ajili ya kushiriki ligi hiyo.
Koka alisema kuwa jumla ya timu 168 katika Jimbo hilo zilishiriki ligi hiyo iliyoanzia ngazi ya mitaa hadi kata na baadaye kupata mshindi wa Jimbo ambapo jumla ya wachezaji zaidi ya 4,000 walishiriki michuano hiyo na bingwa alikuwa ni Home City toka kata ya pangani baada ya kuifunga Lisborn kutoka kata ya Kongowe kwa Penati 6-5.
Mshindi wa tatu ni Phata Farm ya Mkuza iliyoifunga Visiga  3-0, Bingwa alijinyakulia kiasi cha shilingi 500,000 na kombe huku mshindi wa pili akijinyakulia 500,000 na medali na mshindi wa tatu akijinyakulia 200,000 ngao na medali 

Mwisho.

KATIBU TFF AWATAKA WABUNGE WAIBUE VIPAJI VYA SOKA VIJIJINI

Na John Gagarini, Bagamoyo

KATIBU Mkuu wa Shirikisho la Soka Nchini (TFF) Selestine Mwesigwa amewaomba wabunge kwenye Majimbo mbalimbali kuendeleza soka ngazi za chini ili kuibua wachezaji watakaokuwa wachezaji wa vilabu vikubwa pamoja na timu ya Taifa kwa siku za baadaye.

Aliyasema hivi karibuni wakati akikabidhi zawadi za washindi wa kombe la Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo Dk Shukuru Kawambwa (Kawambwa Cup) ambapo timu ya Jitegemee iliibuka mabingwa baada ya kuichapa Buma 2-0 kwenye uwanja wa Mwanakalenge wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.

Mwesigwa alisema kuwa wachezaji wengi walianzia ngazi za chini hivyo wabunge wana nafasi kubwa ya kuibua vipaji ambavyo vimejificha huko Vijijini na mashindano kama hayo ndiyo yenye uwezo wa kuwaibua vijana.

“Wabunge wengine wanapaswa kuiga mfano wa mashindano hayo ya Kawawmbwa Cup ni jambo la busara kwani linainua vipaji vya vijana, kujenga afya zao pia nakuomba usiishie hapa anzisha na mashindano ya mpira wa wanawake na sisi TFF tutakuunga mkono kwa hilo”, alisema Mwesigwa.

Aliwataka wachezaji wanaopata nafasi ya kwenda kucheza kwenye timu kubwa kujenga nidhamu na kuzingatia mafunzo ya makocha ili waweze kufikia mafanikio makubwa.

 Kwa upande wake Dk Kawambwa aliwashukuru wadau wote walioshirikiana nae kufanikisha mashindano hayo na kusema kuwa mashindano hayo yamedumu kwa miaka 10 mfululizo ambapo ameahidi kuyaboresha na kuyaendeleza katika kipindi kingine cha miaka mitano ijayo.

Dk.Kawambwa alisema lengo la kuanzisha mashindano hayo ni kuibua vipaji vya vijana kuanzia vijiji, kata na wilaya pamoja na kuwaepusha kukaa vijiweni bila shughuli yoyote.
Timu ya Jitegemee Fc kata ya Magomeni iliibuka Kidedea katika mashindano hayo ya 2015 nakujinyakulia zawadi ya kombe, seti ya jezi, mipira miwili, pikipiki na medali ya dhahabu.

Mshindi wa pili alikuwa ni Buma waliopata seti ya jezi na mipira, na mshindi wa tatu timu ya Mwambao ilikabidhiwa seti ya jezi na mipira na  timu yenye nidhamu pamoja na kipa bora walipatiwa zawadi ya ngao. Mashindano ya Kawambwa Cup yalishirikisha vilabu 73 kutoka kata Saba za Jimbo la Bagamoyo.

Mwisho.

Friday, December 25, 2015

WAKWEPA USHURU WATAKIWA KUTUBU

Na John Gagarini, Kibaha
WATU waliokuwa wakijihusisha na ukwepaji kodi hapa nchini wametakiwa kutubu mbele za Mungu na kurejesha kile walicho kila ikiwa ni sehemu ya kuonyesha utii kwa mamlaka iliyopo madarakani kwani imewekwa na Mungu.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Maili Moja Kibaha Isai Ntele kwenye Ibaada ya Krismasi na kusema kuwa kurejesha kile walichokwepa ni kumwogopa Mungu ambaye anataka kila mtu awajibike kwa kiongozi aliye madarakani.
Mch Ntele alisema kuwa Mungu alisikiliza kilio cha watanzania kwa kuwapa kiongozi ambaye ana uchungu na wananchi wake kwani ameonyesha dhahiri kuwa hataki haki za wanyonge zipotee kwa kudhulumiwa na wachache.
“Hata Biblia ina sema kila mtu aitii mamlaka iliyo kuu kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu na ile iliyopo nimeaminiwa  na Mungu hivyo aisye na mamlaka asipotii anashindana na agizo la Mungu hivyo watapata hukumu,” alisema Mch Ntele.
Alisema wakwepa kodi wanapingana na agizo la Mungu hivyo kwa wale waliofranya hivyo wanapaswa kulipa kodi au ushuru ili kuonyesha utii kwa mamlaka iliyopo sasa na watakuwa wamemweshimu Mungu.
“Waliokuwa wakikwepa wasirfanye hivyo tena na watubu na watasamehewa dhambi hiyo waliyoifanya na Mungu atatuelekeza kwenda kwenye njia sahihi kwani tutapata mema ya nchi yetu kama Mungu alivyo agiza,” alisema Mch Ntele.
Aliwataka wakristo kutumia kumbukumbu ya kuzaliwa kristo kwa kutenda mema na kuachana na matendo maovu ambayo hupelekea uvunjifu wa amani ili kuenzi upendo wa Yesu ambao ndiyo unaobeba sherehe hizi za Krismasi.
Naye mwinjilisti wa mtaa wa Luguruni Huruma Foya alisema kuwa watu wanapaswa kumwombea Rais akae kwenye mkono wa Mungu atatekeleza yale ambayo Mungu atamuelekeza katika kuiongoza nchi.
Foya alisema kuwa wakimwombea atakuwa ni msafi na hatatoa maamuzi ya kukurupuka ambayo yatawaumiza wananchi bali ataongozwa na Mungu katika shughuli mbalimbali za kuwatumikia wananchi.
Mwisho. 

WAVAMIZI WA VIWANJA VYA MICHEZO WAONYWA

John Gagarini, Kibaha
NAIBU Waziri wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Anastazia Wambura amewataka watu wanaovamia maeneo ya viwanja vya michezo kukomesha tabia hiyo kwani inawanyima fursa vijana kushiriki kwenye michezo.
Aliyasema hayo hivi karibu mjini Kibaha wakati akifunga michuano ya kombe la Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka (Koka Cup) kwenye uwanja wa Mwendapole wilayani humo na kusema kuwa watu hao hawapaswi kuungwa mkono kwani wanawanyima ajira vijana.
Wambura alisema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakivamia maeneo ya michezo na kujenga jambo ambalao linakwenda kinyume na matumizi yaliyopangwa na serikali hivyo vijana kushindwa kuendeleza vipaji vyao.
“Watu wenye tabia hii inabidi waiache kwani inadumaza azma ya serikali kuendeleza michezo mbalimbali hapa nchini hasa ikizingatiwa licha ya michezo kuwa ni burudani lakini pia inatoa fursa ya ajira hasa kwa vijana,” alisema Wambura.
Alisema kuwa serikali imekuwa na mipango mbalimbali ya kuendeleza michezo ikiwa ni pamoja na kuwa na viwanja ambavyo vitawawezesha vijana kushiriki michezo hivyo watu wanaovamia na kujenga ni dhahiri wanakwamisha juhudi hizo.
“Tunaomba wadau wa michezo wahamasishe ujengwaji wa viwanja vya kisasa ambapo baadhi ya watu wameonyesha uzalendo kwa kujenga viwanja ambavyo vinaendeleza jitihada za serikali kuendeleza michezo,” alisema Wambura.
Kwa upande wake Koka alisema kuwa lengo la kuandaa mashindano hayo ni kuwahamasisha vijana kushiriki michezo kwenye Jimbo lake ambapo alizipatia timu zote vifaa vya michezo kwa ajili ya kushiriki ligi hiyo.
Koka alisema kuwa jumla ya timu 168 katika Jimbo hilo zilishiriki ligi hiyo iliyoanzia ngazi ya mitaa hadi kata na baadaye kupata mshindi wa Jimbo ambapo jumla ya wachezaji zaidi ya 4,000 walishiriki michuano hiyo na bingwa alikuwa ni Home City toka kata ya pangani baada ya kuifunga Lisborn kutoka kata ya Kongowe kwa Penati 6-5.
Mshindi wa tatu ni Phata Farm ya Mkuza iliyoifunga Visiga  3-0, Bingwa alijinyakulia kiasi cha shilingi 500,000 na kombe huku mshindi wa pili akijinyakulia 500,000 na medali na mshindi wa tatu akijinyakulia 200,000 ngao na medali  
Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha
BONANZA la kuuaga mwaka 2015 na kuukaribisha mwaka 2016 linatarajiwa kufanyika Januari Mosi mwakani kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha (KEC) Tumbi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Msajili Msaidizi wa Vilabu na Vyama vya Michezo wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Abdul Haufi alisema kuwa Bonanza hilo litakuwa la wazi kwa watu wote.
Haufi alisema kuwa shindano hilo litakuwa la michezo mbalimbali litashirikisha mashirika ya Umma, binafsi pamoja na watu binafsi au mtu mmoja mmoja kwenye michezo ya soka, mpira wa pete kwa wanawake, kuvuta kamba, riadha mita 100.
Alitaja michezo mingine kuwa ni kukimbia na magunia, kurusha kisahani, tufe, mpira wa wavu, kijiko na ndimu ambapo usajili unafanyika kwenye ofisi za Halmashauri hiyo.
“Tunatarajia jumla ya wanamichezo 250 kushiriki Bonanza hilo la aina yake kufanyika mjini Kibaha na vitongoji vyake ambapo lengo ni kuhamasisha watu kushiriki michezo pamoja na kudumisha urafiki baina ya mashirika bianafsi, ya umma pamoja na watu binafsi,” alisema Haufi.
Aidha alisema kuwa juu ya wadhamini tayari baadhi wameshajitokeza huku wakiwasubiri wengine wamalizia taratibu za kudhamini Bonanza hilo na matarajio ni kutolewa zawadi nono.
Bonanza hilo limeandaliwa kwa pamoja na Halmashauri ya Mji Kibaha, Majeshi ya mkoani Pwani ikiwa ni pamoja na Magereza, Polisi na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).
Mwisho.
  


Monday, December 21, 2015

WANAFUNZI 204 HAWAKUFANYA MTIHANI WA DARASA LA SABA

Na John Gagarini, Kibaha

WANAFUNZI 204 mkoani Pwani hawakufanya mtihani  wa kumaliza elimu ya Msingi kwa mwaka 2015 kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoro.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Katibu Tawala wa mkoa huo Mgeni Baruan wakati wa kutangaza matokeo ya wanafunzi waliofanya mtihani wa darasa la saba kwa mwaka 2015 na kusema kuwa jumla ya wanafunzi waliofanya mtihani huo walikuwa 22,191 sawa na asilimia 99.1.

Baruan alisema kuwa wanafunzi ambao hawakufanya mtihani kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoro 185, vifo watano, ugonjwa wanane, huku sababu nyingine wakiwa ni wawili.

“Ukiachilia mbali wanafunzi hao ambao hawakufanya mtihani  na ufaulu wa wanafunzi kwa mkoa huo umefikia asilimia 63.1 ikilinganishwa na mwaka 2014 sawa na asilimia 56.2.,” alisema Baruan.

Alisema kuwa wanafunzi 14,010 wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2016 kati ya wanafunzi baada kufaulu mtihani wao wa kumaliza elimu ya Msingi ambapo wanafunzi wote waliofaulu wamepata nafasi na hakuna aliyekosa nafasi.

“Kati ya idadi ya wanafunzi waliofanya mtihani ni wavulana ni 10,024 na wasichana ni 12,167 huku ikionyesha kuwa mkoa haukupata tuhuma za udanganyifu katika zoezi la ufanyaji mtihani,” alisema Baruan.

“Mkoa umeshika nafasi ya 14 kitaifa hata hivyo ufaulu huo hauridhishi kwani haujafikia kiwango cha asilimia 80 kwa mujibu wa mwelekeo wa Matokeo Makubwa Sasa Big Results Now (BRN) hivyo zinahitajika jitihada zaidi ili kufikia kiwango hicho,” alisema Baruan.

Kwa upande wake ofisa elimu mkoa Yusuph Kipengele alisema kuwa agizo la Rais la Dk John Pombe Magufuli la kuondolewa kwa ada na michango mbalimbali kuanzia shule ya msingi na sekondari liko palepale.

Kipengele alisema kuwa baadhi ya michango iliyoondolewa ikiwa ni pamoja na ada ni vitambulisho, mawadati, majengo,  vifaa vya michezo mlinzi haitakuwepo na mwalimu atakayechangisha mchango wowote atakuwa anakiuka agizo la Rais.

Hata hivyo alisema kuwa jukumu la wazazi ni kumnunulia vifaa vya shule mwanae ikiwa ni pamoja sare za shule, madaftari, kalamu, chakula, nauli na vifaa vingine vidogovidogo ambavyo siyo mzigo kwa mzazi yoyote.

Mwisho.

Friday, December 18, 2015

PWANI WAONGEZA UFAULU DARASA LA SABA

Na John Gagarini, Kibaha
JUMLA ya Wanafunzi 14,010 wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2016 kati ya wanafunzi baada kufaulu mtihani wao wa kumaliza elimu ya Msingi ambapo wanafunzi wote waliofaulu wamepata nafasi na hakuna aliyekosa nafasi.
Akitangaza matokeo hayo jana mjini Kibaha kwa wanafunzi waliofanya mtihani wa darasa la saba kwa mwaka 2015 katibu Tawala wa mkoa wa Pwani Mgeni Baruan alisema kuwa jumla ya wanafunzi waliofanya mtihani huo walikuwa 22,191 sawa na asilimia 99.1.
Baruan alisema kuwa waliotarajiwa kufanya mtihani walitarajiwa kuwa ni 22,191 ambapo wanafunzi 204 hawakufanya mtihani huo na ufaulu wa wanafunzi kwa mkoa huo umefikia asilimia 63.1 ikilinganishwa na mwaka 2014 sawa na asilimia 56.2.
“Mkoa umeshika nafasi ya 14 kitaifa hata hivyo ufaulu huo hauridhishi kwani haujafikia kiwango cha asilimia 80 kwa mujibu wa mwelekeo wa Matokeo Makubwa Sasa Big Results Now (BRN) hivyo zinahitajika jitihada zaidi ili kufikia kiwango hicho,” alisema Baruan.
Alisema kuwa alisema kuwa kati ya idadi ya wanafunzi waliofanya mtihani ni wavulana ni 10,024 na wasichana ni 12,167 huku ikionyesha kuwa mkoa haukupata tuhuma za udanganyifu katika zoezi la ufanyaji mtihani.
“Wanafunzi ambao hawakufanya mtihani ni 204 ni kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoro 185, vifo watano, ugonjwa wanane, huku sababu nyingine wakiwa ni wawili,” alisema Baruan.
Kwa upande wake ofisa elimu mkoa Yusuph Kipengele alisema kuwa agizo la Rais la Dk John Pombe Magufuli la kuondolewa kwa ada na michango mbalimbali kuanzia shule ya msingi na sekondari liko palepale.
Kipengele alisema kuwa baadhi ya michango iliyoondolewa ikiwa ni pamoja na ada ni vitambulisho, mawadati, majengo,  vifaa vya michezo mlinzi haitakuwepo na mwalimu atakayechangisha mchango wowote atakuwa anakiuka agizo la Rais.
Hata hivyo alisema kuwa jukumu la wazazi ni kumnunulia vifaa vya shule mwanae ikiwa ni pamoja sare za shule, madaftari, kalamu, chakula, nauli na vifaa vingine vidogovidogo ambavyo siyo mzigo kwa mzazi yoyote.
Mwisho.

WATATU WAFA AJALINI PWANI

Na John Gagarini,Kibaha

WATU watatu wamefariki dunia leo katika matukio mawili ya ajali yaliyotokea mkoani Pwani.

Kamanda wa polisi mkoani Pwani,Boniventura Mushongi amethibitisha kutokea kwa matukio hayo, ambapo amesema katika tukio la kwanza watu wawili walifariki dunia kwenye ajali iyotokea huko Mbala Kijiweni wilaya ya Kipolisi Chalinze .

Amesema katika tukio hilo gari lenye namba za usajili T.743 BTV aina ya scania Lori likiendeshwa na Hashim Sadick(30) mkazi wa Gairo ikitokea Dar es salam kuelekea chalinze iligongana uso kwa uso na gari yenye namba za usajiliT.846 BXU aina ya Fuso ikiendeshwa na Cosmas Mwaifule.

Kamanda Mushongi amesema,madereva wa magari hayo walikufa baada ya ajali hiyo kutokea.
Amesema ajali nyingine imetokea  baada ya gari lenye namba za usajili T.290 DFS aina ya Isuzu mali ya kampuni ya magazeti ya Mwananchi ikiendeshwa na Elisha Mmari ikitokea Dar es salaam kwenda Mbeya ilimgonga mwendesha pikipiki na kumsababishia kifo.
Kamanda Mushongi amesema jina la dereva huyo wa pikipiki halikufahamika  na ajali imetokea eneo la Visiga  wilaya ya Kibaha.

Chanzo cha ajali hizo kinadaiwa kuwa ni kupishana bila tahadhari(overtaking) pasipo uangalifu.

Miili ya marehemu wote watatu imehifadhiwa katika hospitali ya Rufaa ya Tumbi ikisubiri uchunguzi wa daktari.

Mwisho

Thursday, December 17, 2015

MAKANDARASI WANAWAKE WATAKIWA KUJENGA VIWANJA VYA NDEGE

Na John Gagarini, Kibaha
WAKANDARASI wanawake nchini wametakiwa kuomba kandarasi kubwa zikiwemo za ujenzi wa barabara kubwa pamoja na viwanja vya ndege kupitia kampuni zao za ujenzi ili kujiongezea kipato na kuiletea nchi maendeleo.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Mkurugenzi wa iliyokuwa Wizara Ujenzi Kegora wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo makandarasi wanawake katika maandalizi ya zabuni na manunuzi kwa kazi za ujenzi wa barabara yaliyoandaliwa na wizara ya Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano.
Kegora alisema kuwa wanawake wameonyesha uwezo mkubwa kwa kufanya kazi za ujenzi wa barabara kwa viwnago vinavyokubalika hivyo ni vema wakaomba kandarasi za ujenzi mkubwa ambao zinatarajiwa kufanyika.
“Kwa sasa ombeni kazi za ujenzi mkubwa kama vile wa viwanja vya ndege, bandari, madaraja na reli ili muonyeshe umahiri wenu katika kazi za ujenzi na mnapaswa kuacha woga kwani uwezo mnao na mmeonyesha kuwa manaweza,” alisema Kegora.
Alisema wanawake wakandarasi wanapaswa sasa kuacha kubaki nyuma kwa kujenga miradi midogo midogo ya ujenzi bali wafanye miradi mikubwa ili wapate mafanikio kama walivyofanikiwa kupitia ujenzi.
“Jiendelezeni kitaaluma mfikie madaraja ya juu ili mpate kuimarika kitaaluma muwe juu pia muongeze idadi ya wakandarasi wanawake kwani mmeonyesha kazi nzuri na ndiyo maana mnapewa mafunzo haya,” alisema Kegora.
Kwa upande wake mratibu wa mafunzo hayo Mhandisi Rehema Myeya alisema kuwa mafunzo hayo yana lengo la kuwawezesha wakandarasi hao wanawake kujua namna ya ujazaji wa zabuni na mikata wakati wa kuomba kandarasi.
Myeya alisema kuwa makandarasi wanawake wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kushindwa kujaza vizuri zabuni hizo hivyo kusababisha kukosa kandarasi za ujenzi wa barabara hapa nchini hasa ikizingatiwa kuwa wengi wao hawana elimu kubwa.
Jumla ya wakandarasi wanawake 26 kutoka mikoa Dar es Salaam, Morogoro, Tanga, Singida, Kilimanjaro na Arusha ambapo hadi sasa tayari wamewapatia mafunzo makandarasi zaidi ya 200 kwenye mikoa yote hapa nchini.
Mwisho.

Tuesday, December 15, 2015

ASOTA NDANI MIAKA MITANO AOMBA MSAADA

Na John Gagarini, Kibaha
MARIAMU Mpembenwe (85) mkazi wa Mkoani A kata ya Tumbi wilayani Kibaha mkoani Pwani anakabiliwa na tatizo la maumivu ya viungo mbalimbali vya mwili ikiwemo mguu na mkono hali iliyomfanya ashindwe kutoka nje kwa kipindi cha miaka mitano.
Aidha anaomba kupatiwa baiskeli ya watu wenye ulemavu ili iweze kumsaidia kuweza kutembelea kwenda kupata huduma muhimu ikiwemo za matibabu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha waliomtembelea nyumbani kwa mwanae alisema kuwa hali yake kiafya ni mbaya kutokana na kukosa matibabu pamoja na chakula kwani mwanae ambaye anamtegemea hana kipato chochote cha kujikimu zaidi ya kuomba misaada.
Mpembenwe alisema kuwa anakabiliwa na matatizo mengi ikiwa ni pamoja na kutoona huku nyumba anayoishi kuvuja kipindi cha mvua.
“Nawaomba watu mbalimbali weneye uwezo ikiwemo serikali ili niweze kukabiliana na changamoto zinazonikabili kwani sipati huduma bora za afya, chakula, hata sehemu ninayolala kitanda hakina godoro na huduma za haja napata hapa hapa mazingira ni mabaya naomba msaada wa fedha kwa ajili ya kujikimu,” alisema Mpembenwe.
Kwa upande wake mtoto wa mama huyo Iddy Mtegya (65) alisema kuwa ni kweli mama yake anakabiliwa na matatizo mengi likiwemo la kiafya licha ya kwamba amekuwa akipatiwa matibabu hapo hapo nyumbani.
Mtegya alisema kuwa ni kweli hajatoka nje kwa kipindi hicho kwani ana matatizo ya mguu wa kulia na mkono wa kulia hivyo kushindwa kutemebea na kutokana na hali yake ya unene wanashindwa kumbeba kumtoa nje au kumpeleka sehemu nyingine.
“Naomba msaada kwa watu wenye uwezo watusaidie kiti cha magurudumu ili tuweze kumsaidia mama ili tuweze kumtoa mama nje pia kumpeleka sehemu mbalimbali ikiwa ni pamoja na hospitali licha ya kwamba yeye mwenyewe hataki kwenda hospitali,” alisema Mtegya.
Naye diwani wa kata ya Tumbi Hemed Chanyika alisema kuwa suala hilo linasikitisha kwani licha ya hali aliyokuwa nayo mama huyo anapaswa kupatiwa huduma zote za kibinaadamu kwani kumnyima huduma hizo ni kumuongezea matatizo.
Chanyika alisema kuwa hata baadhi ya watendaji wa mtaa walipaswa kulieleza tukio hilo sehemu husika ili aweze kusaidiwa kupitia vitengo mbalimbali vya misaada kwani wameonekana kutoliweka wazi suala hilo kwa kipindi hicho cha miaka mitano.
Mwenyekiti wa mtaa wa Mkoani A Titus Kabora alisema kuwa wanataarifa ya mama huyo na familia hiyo ilianza kuhudumiwa kupitia mfuko wa maendeleo ya jamii TASAF lakini tatizo misaada hiyo ni midogo na haitoshelezi mahitaji.
Mwisho.  




Tuesday, December 8, 2015

TUMIENI MISITU KUJIONGTEZEA KIPATO TOKA WATALII

Na John Gagarini, Kibaha
WANANCHI wanaoishi jirani na Hifadhi ya Msitu wa Ruvu Kusini wametakiwa kuacha kufanya uharibifu wa msitu huo badala yake wautumie kama chanzo cha mapato kwa njia ya Utalii.
Hayo yalisemwa kwenye Kijiji cha Kipangege wilayani Kibaha mkoani Pwani na ofisa miradi wa Shirika lisilo la Kiserikali la Usimamizi wa Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) Yahaya Mtonda wakati wa tamasha la Kimataifa la Utalii wa kutumia Baiskeli.
Mtonda alisema kuwa kutokana na umuhimu wa misitu ukiwemo msituo ambao unatumika kuchuja hewa safi ukiwa ni mapafu ya kupumulia hewa ya Jiji la Dar e s Salaam wananchi wanapaswa kuulinda na kuondokana na dhana kukata miti kwa ajili ya kujiongezea kipato.
“Kwa sasa tumeshaweka mazingira ya kuufanya msitu huu kuwa wakitalii tofauti na ilivyokuwa mwanzo kwani kwa sasa watalii watakuja kuutembelea na kufanya utalii kujionea miti mbalimbali ya asili ambayo inapatikana hapa Tanzania na hakuna sehemu nyingine inakopatikana hivyo ni wakati sasa wa wananchi kutumia fursa hii kujiongezea kipato kupitia utalii badala ya kukata miti kwa ajili ya mbao na kuni au mkaa,” alisema Mtonda.
Alisema kuwa endapo wananchi watatumia fursa hiyo watapata mapato huku wakienedelea kutunza msitu huo pamoja na kuhifadhi mazingira na kukabilian na changamoto ya tatizo la Tabianchi ambayo inasababisha kukosekana mvua na kusababisha hali ya hewa kuwa mbaya hususani kuwa na joto kali.
Kwa upande wake Mshauri wa Ufundi wa (TFCG) Andrew Perkin lengo la tamasha hilo ni kuwapa uelewa wananchi juu ya umuhimu wa kulinda misitu ili waweze kufurahia mazingira mazuri ambayo uoto wake wa asili unasababisha hali ya hewa kuwa safi.
Perkin alisema kuwa misitu hiyo ilikuwa ikiharibiwa sana na wananchi kutokana na kukata miti kwa ajili ya shughuli za kibinadamu zikiwa ni pamoja na uvunaji wa misitu ambapo kwa sasa tayari wameshawaondoa watu waliokuwa kwenye msitu huo na hali yake inaanza kurudi kama ilivyokuwa mwanzo.
Naye mwenyekiti wa Umoja wa Wapanda Baiskeli (UWABA) Meja Mbuya alisema kuwa wamekuwa wakihamasisha watu kupanda baiskeli kwani matumizi ya magari yamekuwa yakiharibu mazingira kutokana na moshi unaotokanan na magari hayo.
Mbuya alisema kuwa mbali ya kupanda baiskeli wamekuwa wakitoa elimu mbalimbali ya juu ya utunzaji wa misitu na kushauri matumizi ya nishati ya jua na upepo katika baadhi ya matumizi ili kutoharibu mazingira. Jumla ya watu zaidi ya 100 toka mataifa mbalimbali walishiriki tamasha hilo ambapo walitembea umbali wa kilometa 30.

Mwisho. 

Saturday, December 5, 2015

WAWILI WAFA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MLINZI wa kampuni ya Ulinzi ya Optima inayolinda kwenye jengo la Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani Primc Bararwirwa amekutwa amekufa jirani na na kituo kikuu cha Mabasi cha Maili Moja Wilayani Kibaha.
Tukio hilo lilitokea Desemba 4 mwaka huu majira ya asubuhi jirani na Grosari ya Kilimani ambapo mwandishi wa habari hizi aliushuhudia mwili wa marehemu ukiwa chali na kufunikwa na shuka huku ukiwa hauna viatu.
Baadhi ya watu waliomshuhudia marehemu kabla ya kifo chake walisema kuwa usiku wake walimwona marehemu akiwa na wenzake huku wakiongea lakini walishangaa asubuhi kuona akiwa amekufa na hakuwa na jeraha lolote mwilini mwake.
Polisi walifika kwenye eneo hilo na kuuchukua mwili wa marehemu kisha kuupeleka Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani kwa ajili ya kuchunguza kifo chake na kusubiri ndugu kwa ajili ya taratibu za mazishi.
Kamanda wa polisi mkoani Pwnai Jafary Mohamed alithibitisha kutokea tukio hilo ambapo wanaendelea na uchunguzi kujua chanzo cha kifo hicho ambacho kimewashtua wakazi wengi wa Maili Moja waliokuwa wanamfahamu marehemu.
Katika tukio lingine mkulima wa Kijiji cha Zogowale kata ya Misugusugu Aloyce Chuma (54) amefariki dunia huku watu wengine watatu wakijeruhiwa  baada ya kupigwa na radi ambayo iliambatana na upepo mkali.
Akizungumza na gazeti hili mwenyekiti wa Mtaa wa Zogowale Rajab Mhanyige alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 10 jioni wakati marehemu akiwa amekaa kwenye gogo na wenzake hao waliojeruhiwa wakati wamepumzika baada ya shughuli za kilimo.
Mhanyige alisema kuwa radi hiyo ilipiga sehemu walipokuwa wamekaa watu hao na kumwua marehemu na kuwajeruhi wenzake huku yeye akifia eneo la tukio na hakuwa na jeraha lolote mwilini mwake.
“Siku hiyo ilipiga radi kali iliyoambatana na upepo mkali ambayo mimi sijawahi kusikia tangu kuzaliwa kwangu ilikuwa na kishindo kikubwa sana na niliamini kuwa itakuwa imeleta matatizo na kweli kwani baada ya muda nilletewa taarifa kuwa kuna mtu kafa kutokana na radi hiyo ambapo baadaye mvua kubwa ilinyesha,” alisema Mhanyige.  
Alisema mara baada ya tukio hilo waliuchukua mwili wa marehemu pamoja na majeruhi na kuwapeleka kwenye kituo cha Afya cha Mlandizi kwa ajili ya kuhifadhi mwili na majeruhi kwa ajili ya matibabu ambao nao hawakuwa na majeraha yoyote.
Aidha aliwataja majeruhi ambao baadaye waliruhusiwa kurudi nyumbani kuwa ni Cosmas Bandula (54), Sultan Kigumu ambaye alirushw aumbali wa mita 10 na mtu aliyetambuliwa kwa jina moja la Kamugisha (48). Polisi walithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Mwisho.