Sunday, March 30, 2025

WAZIRI MKUU MAJALIWA AUPIGIA DEBE UWANJA WA SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA KUTUMIWA NA TIMU ZA CHAN NA AFCON

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameupigia debe uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha kutumiwa na Timu za Taifa zitakazokuwa zinajiaandaa na michuano ya  CHAN na AFCON kwa ajili ya mazoezi.

Majaliwa aliyasema hayo alipotembelea kuukagua uwanja huo ambao utatumika kwenye usinduzi wa mbio za mwenge 2025.

Majaliwa alisema kuwa jana alifanya ukaguzi wa viwanja vitatu viyakavyotumika kwa ajili hiyo ambavyo ni vichache.

"Tanzania tumepata uenyeji wa mashindano hayo mawili ambayo ni makubwa hivyo lazima tuwe na viwanja vingi kwa ajili ya mazoezi na hichi kikiboreshwa kinaweza kutumika,"alisema Majaliwa.

Alisema kuwa wataangalia uwezekano wa uwanja huo kutumiwa kwa ajili ya mazoezi na tutaongea na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) kama watakikubali itabidi kitumike.

"Kiwanja hichi kikiimarishwa vizuri kinaweza kutumika kwa ajili hata ya ligi kuu ni uwanja mzuri unahitaji maboresho kidogo tu kwani hata taa zipo kwa kweli hapa ni pazuri,"alisema Majaliwa.

Aidha alisema hayo ni matunda ya uwekezaji kwenye sekta ya michezo ambapo Rais Dk Samia Suluhu Hassan ameamua kuwekeza kwenye michezo.

"Kwa vijana wa Halaiki msiishie hapa endeleeni na mazoezi hii iwe ni sehemu ya kuanzia kwa wale watakaocheza mpira wa miguu, pete, riadha na michezo mingine ili muendeleze vipaji vyenu isiwe hapa ndiyo mwisho,"alisema Majaliwa.



WAZIRI MKUU MAJALIWA ARIDHISHWA MAANDALIZI UZINDUZI WA MWENGE WA UHURU PWANI 2025

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa ametembelea kuangalia maandalizi ya uwanja utakaotumika kuzindua mbio za mwenge wa uhuru mwaka 2025 mkoani Pwani.

Majaliwa alitembelea uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha kuangalia maandalizi ya uzinduzi huo na kuridhishwa na maandalizi hayo na kutaka wakamilishe sehemu ambazo bado hazijakamilika.

Alisema kuwa ameridhishwa na maandalizi hayo ambapo pia alitumia muda huo kutembelea watoto wa halaiki na kusema amefurahishwa na jinsi walivyokuwa na hamasa ya uzinduzi huo.

"Nawapongeza kwa maandalizi mnayoendelea nayo nimeridhishwa kamilisheni sehemu zilizosalia ili kukamilisha mapema,"alisema Majaliwa.

Alisema kuwa amefurahishwa kuona viongozi wakiwemo mawaziri na makatibu wakuu wakiwa mstari wa mbele kuhakikisha maandalizi yanakuwa mazuri.

"Alikeni hata mikoa ya jirani Dar es Salaam, Morogoro na Tanga na watu mbalimbali kwani hili ni jambo la kitaifa shirikisheni wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ili hamasa iwe kubwa,"alisema Majaliwa 

Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi Vijana Ajira na Watu Wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete maandalizi yako vizuri ila baadhi ya maeneo ikiwemo katikati ya uwanja ndiyo kunahitaji marekebisho kidogo.

Kikwete alisema kuwa mialiko kwa wageni mbalimbali imetolewa ikiwa ni pamoja na wakuu wa mikoa, wakurugenzi na watu wengine ili kushiriki uzinduzi huo.


Friday, March 28, 2025

VIJANA WAFUNDISHWE UMUHIMU WA MBIO ZA MWENGE

TAASISI mbalimbali nchini zimetakiwa kuwajengea uwezo vijana juu ya umuhimu wa mbio za Mwenge wa Uhuru katika kujenga uzalendo na uwajibikaji katika usimamizi wa shughuli za maendeleo na kutambua fursa za kiuchumi.

Hayo yamesemwa na Skauti Mkuu Nchini na Katibu Tawala (RAS) Mkoa wa Pwani Rashid Mchatta wakati Kongamano la Vijana juu ya umuhimu wa kushiriki Mbio za Mwenge wa Uhuru 2025.

Mchatta amesema kuwa vijana wanapaswa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa namna ambavyo mtaelekezwa na viongozi katika maeneo wanayoishi.

"Tukifanya hivyo tutaupata ujumbe wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa ufasaha ili muweze kushuhudia kwa vitendo yale yote mtakayojifunza katika Kongamano hili,"amesema Mchatta.

Amesema kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kundi la vijana katika kuleta mageuzi ya Kijamii na Kiuchumi kutokana na ari, nguvu na ubunifu walionao. 

"Kwa kutambua hilo serikali kwa kushirikiana na wadau imekuwa ikitoa kipaumbele kwa vijana kupata elimu na makuzi bora kuwapa fursa ya kupata mikopo ya asilimia 10 kupitia Halmashauri na Programu ya Jenga Kesho iliyo Bora (Build Better Tomorrow – BBT) 

Amesema kuwa Mwenge wa Uhuru Mwaka 2025 utazinduliwa mkoa wa Pwani kitendo ambacho kinaonesha nia njema ya Dk Samia Suluhu Hassani Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuendeleza na kuenzi kwa vitendo yale yote aliyoturithisha Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Rais wa Kwanza wa Tanzania. 

Kwa upande wake mratibu wa Kongamano hilo Omary Punzi amesema kuwa ili vijana waweze kufikia mafanikio ya kimaendeleo lazima wazingatie falsafa za Mwalimu Nyerere alizotumia wakati wa kuwashwa Mwenge wa Uhuru.

Punzi amesema moja ya falsafa za Mwenge wa Uhuru ni kuwafanya watu wawe na uzalendo kwa kujitoa kwa ajili ya nchi yao na kutokomeza maadui watatu ujinga umaskini na maradhi. 

Mbio za Mwenge wa Uhuru zitazinduliwa katika viwanja vya Shirika  la Elimu Kibaha Mkoani Pwani na Mgeni rasmi atakuwa Dk Philip Isdor Mpango Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

mwisho.


Wednesday, March 26, 2025

MAKAMU WA RAIS DK MPANGO KUZINDUA MBIO ZA MWENGE KITAIFA PWANI

MAKAMU wa Rais Dk Philip Isdor Mpango atazindua mbio za Mwenge kitaifa Mkoani Pwani Aprili 2 mwaka huu kwenye uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya juu ya uzinduzi huo amesema kuwa maandalizi ya uzinduzi yanaenda vizuri.

Kikwete amesema kuwa tayari Makamu wa Rais ameshathibitisha kuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi huo wa mbio za  Mwenge kwa mwaka 2025.

"Kwa vitu vilivyobakia niwaombe mhakikishe vinafika kwa wakati ili kila kitu kiwe kwenye sehemu yake na bado tutaendelea kuangalia maandalizi ili siku hiyo mambo yawe mazuri,"amesema Kikwete.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amesema kuwa maandalizi yako vizuri ambapo hadi Machi 29 mambo mengi yatakuwa yamekamilika.

Kunenge amesema kuwa huduma zote zitapatikana kuanzia suala la afya, vyoo, maji, taa kubwa, umeme ambapo kutakuwa na jenereta endapo umeme utakatika.

Amewataka wananchi wa Mkoa huo na mikoa jirani na Watanzania kwa ujumla kujitokeza siku hiyo ili kuweka historia ya Pwani kuzindua mbio za Mwenge Kitaifa.

Tuesday, March 25, 2025

JK AWASILISHA UJUMBE MAALUMU KWA RAIS WA SENEGAL KUTOKA KWA RAIS SAMIA

Mhe. Rais Mstaafu  Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amewasilisha  ujumbe maalumu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwenda kwa Rais wa Jamhuri ya Senegal, Mhe. Bassirou Diomaye Faye jijini Dakar.

Katika mazungumzo  yao ya kirafiki,  Rais Mstaafu alieleza dhamira ya dhati ya Rais Samia na Serikali anayoiongoza ya kuendeleza na kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia, kiuchumi na kijamii kati ya Tanzania na Senegal.

Pamoja na masuala ya ushirikiano wa kiserikali, Rais Mstaafu pia alisisitiza umuhimu wa kukuza uhusiano baina ya wananchi wa mataifa haya mawili kupitia sekta za elimu, biashara, utalii, na maendeleo ya vijana na wanawake.

Ziara hii ni sehemu ya juhudi endelevu za Tanzania kuimarisha uhusiano wa kimataifa na mataifa ya Afrika Magharibi, huku ikiweka msisitizo kwa diplomasia ya uchumi na ushirikiano wa watu kwa watu.

MAANDALIZI UWASHWAJI MWENGE WA UHURU KITAIFA PWANI MBIONI KUKAMILIKA



MAANDALIZI ya Uzinduzi wa mbio za Mwenge Kitaifa yamefikia asilimia 96 ambapo Mwenge huo utawashwa Wilayani Kibaha Mkoani Pwani Aprili 2 Mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye Uwanja wa Shirika la Elimu Kibaha (KEC) Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amesema kuwa maandalizi yanaenda vizuri.

Kunenge amesema kuwa kwa sasa zimebaki siku sita ambapo Mwenge utazinduliwa Aprili 2 na utatembelea kwenye Halmashauri tisa za mkoa huo kwa kuanza na Halmashauri ya Mji Kibaha utakapoanzia.

"Uwanja umekamilika yamebaki maeneo machache ambapo hadi leo sehemu kubwa itakuwa imekamilika na kubaki mambo madogo madogo,"amesema Kunenge.

Amesema kuwa majukwaa yamekamilika na matarajio ni kuwa na watu 16,000 ambapo miundombinu ya maji, sehemu ya magari kukaa tayari, taa, mifumo ya majitaka na ulinzi viko tayari.

Thursday, March 20, 2025

TANROADS YATOA UFAFANUZI LORI LILILOZIDISHA UZITO MIZANI YA VIGWAZA.

WAKALA wa Barabara Tanzania (TANROADS) imetoa ufafanuzi juu ya taarifa inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii ya lori la mizigo lililokamatwa kwenye mizani ya Vigwaza kuwa taratibu za kulikamata lori hilo ulifuatwa.

Aidha gari hilo lilipigwa faini hiyo kwa kuzingatia sheria ya udhibiti wa uzito barabarani ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018.

Akizingumza na waandishi wa habari kwenye ofisi za mizani hiyo ya Vigwaza Mtaalamu wa Kitengo cha Mizani Tanroads Makao Makuu Vicent Tarmo amesema kuwa gari hilo lilizidisha uzito zaidi ya tani moja.

Tarmo amesema kuwa gari hilo lenye namba za usajili T 137 DLR na tela namba T 567 CUR lilikuwa limetokea nchini Congo likiwa limebeba madini ya Shaba ambapo uwezo wake ni kubeba tani 48 lakini lilikutwa likiwa na uzito tani 48.1.

"Kutokana na kuzidisha uzito huo gari hilo lilitakiwa kulipiwa faini ya shilingi 900,000 ikiwa ni adhabu ya kuzidisha uzito halisi lakini dereva huyo alisema kuwa amezidishiwa uzito hivyo kupinga faini hiyo,"amesema Tarmo.

Amesema kuwa sheria inataka magari yote yenye uzito kuanzia tani 3 na nusu lazima yapime uzito ili kuepusha uharibifu wa barabara hivyo kutokana na gari hilo kuzidisha uzito alipaswa kulipa faini hiyo.

"Dereva huyo amesema kuwa amepita mizani mbalimbali uzito haukuzidi hivyo kwa nini hapa uzidi lakini kwa mujibu wa sheria alipaswa kulipa na siyo kukaidi kulipa,"amesema Tarmo.

Amesema kuwa gari hilo lilipita hapo Machi 13 ambapo kwa siku hiyo yalipimwa mwagari 819 ambapo saba yalibainika kuzidisha uzito ambapo mengine yalilipa na kuendelea safari lakini gari hilo dereva wake aligoma kulipa akidai amezidishiwa uzito.

"Mzani huu ni automatiki lakini yeye alitaka uzito  urudiwe kupimwa jambo ambalo ni kinyume cha utaratibu ambapo hupaswa kupunguza na kulipa uliizidi na kupima tena na siyo kupima upya,"amesema Tarmo.

Ameongeza kuwa uzito unaweza kuzidi kutokana na sababu kadhaa ikiwa ni pamoja na kuongeza mafuta, abiria na busta endapo zitakuwa na hitilafu ambapo hata walipofuatilia mizani nchini Zambia uzito ulikuwa na mabadiliko ikionekana kuzidi.

"Dereva baada ya kuona hizo tofauti alipaswa kuangalia mfumo wa gari lake kwani kutokana na baadhi ya changamoto kama hizo uzito unaweza kuongezeka,"amesema Tarmo.

Kwa upande wake Meneja wa Tanroads Mkoa wa Pwani Baraka Mwambage amesema kuwa kama kunatokea changamoto yoyote kuna taratibu za kufuata ili kuweza kupata haki zao na si kutumia mitandao kutoa malalamiko yao.

Mwambage amesema kuwa malalamiko yanaweza kupelekwa ofisini au kama wana wasiwasi wanaweza kupeleka kwenye vyombo vingine ikiwa ni pamoja na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Nchini (TAKUKURU) kama sehemu ya kujua ukweli zaidi.

Hivi karibuni zilisambaa habari kupitia mitandao ya kijamii ambapo picha mjongeo ilimuonyesha dereva mmoja akilalamikia mizani ya Vigwaza kuwa imezidisha uzito.