Monday, November 13, 2023

KAMATI YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA YARIDHISHWA MRADI WA MAJI WAMI AWAMU YA TATU.

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma imetembelea mradi wa Maji wa Wami awamu ya tatu kwenye chanzo Mto Wami na kufurahishwa na jitihada za Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kuhakikisha huduma ya upatikanaji maji inakuwa ya uhakika.

Hayo yamesemwa na mwenyekiti wa kamati hiyo Deus Sangu wakati wa ziara iliyofanywa kutembelea mradi huo kuangalia maendeleo ya mradi huo ambao kwa awamu zote umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 160.

Sangu amesema kuwa wameridhishwa na jitihada za Dawasa na kuahidi kuendelea kuipambania ili iweze kukabili changamoto za upungufu wa maji na kupitia Bunge kati ya maazimio 14 mawili ni ya kuisaidia mamlaka hiyo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amesema kuwa upatikanaji wa maji kwa mkoa huo ni asilimia 86 ambapo aliomba miradi itekelezwe vizuri ikizingatiwa ni mkoa wa uwekezaji wa viwanda na mahitaji ya maji kwa sasa ni makubwa kwani kuna ongezeko la watu na uwekezaji mkubwa ambapo bila ya maji hakuna uwekezaji.

Naye Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejmenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete ameishukuru kamati hiyo kwa kupambani Chalinze kupata maji kwani kwenye mikutano yake hakuna jambo ambalo lilikuwa kero kwa wananchi kuhitaji maji ambapo kwa sasa changamoto ya maji imepungua kwa kiasi kikubwa.

Awali akiwasilisha taarifa ya mradi huo wa awamu ya tatu Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Dawasa Kiula Kingu amesema kuwa maji yatazalishwa kutoka lita milioni saba hadi lita milioni 21 ambapo mabomba yatatandazwa kwa kilometa 124 na matenki 18 na kutakuwa na vituo vikubwa vya maji Miono, Msoga na Mboga.


Mwisho.

Monday, November 6, 2023

WAFANYABIASHARA WATAKIWA KULIPA KODI KWA HIYARI

WAFANYABIASHARA nchini wametakiwa kulipa kodi kwa hiyari ili wawe huru kufanyabiashara na kuchangia mapato ya serikali ili iweze kutoa huduma bora kwa wananchi.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) Taifa Hamis Livembe alipokuwa akizungumza na wafanyabiashara wa Wilaya ya Kibaha wakati wa ziara yake kutembelea Mkoa wa Pwani.

Livembe alisema kuwa kila upande una wajibu kwa mwenzake ambapo serikali inaweka mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara na kwa wafanyabiashara kazi yao ni kulipa kodi.

"Naombeni wafanyabiashara mlipe kodi kwa hiyari kwani serikali imeweka mazingira mazuri ya sisi kufanya biashara na hata kama kuna changamoto imeacha milango wazi kwa ajili ya majadiliano kama kuna kero kuhusiana na kodi,"alisema Livembe.

Alisema kuwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan ameamua kufungua milango ya biashara ili wafanyabiashara wafanye biashara zao kwa uhuru na hataki kuona wanabughudhiwa.

"Tumuunge mkono jitihada za Rais anazo zifanya kwa wafanyabiashara kwa kutatua kero zetu hivyo tukilipa kodi vizuri nchi itasonga mbele kwenye suala la maendeleo na nchi itafunguka,"alisema Livembe.

Naye Katibu Tawala Mkoa wa Pwani Rashid Mchatta alisema kuwa Jumuiya hiyo inafanya kazi kubwa ya kizalendo kwani nchi inapokusanya vizuri mapato yanarudi kwa wananchi kwa kutoa huduma kwa ufanisi.

Mchatta alisema kuwa wajibu wa kulipa kodi ni muhimu na kama kuna changamoto watashirikiana na wafanyabiashara kuzitatua kwa pamoja ili mazingira ya biashara yawe rafiki.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara (JWT) Mkoa wa Pwani Abdala Ndauka alisema kuwa wanaishukuru serikali kwa kutatua baadhi ya changamoto za wafanyabiashara.

Ndauka alisema kuwa changamoto zao zikitatuliwa watafanyabiashara kwa uhuru na kuwezesha biashara kukua hivyo kulipa kodi kwa hiyari na kuleta maendeleo ya nchi.

Moja ya wafanyabiashara ambaye ni mwanachama wa Jumuiya hiyo Mkoani humo Hassan Msemo alisema kuwa moja ya changamoto wanazozipata ni baadhi ya viwanda kutokuwa na stoo za kuuzia bidhaa wanazozizalisha ambapo nyingi ziko Jijini Dar es Salaam hivyo kuwagharimu kuzifuata.

Msemo alisema kuwa kutokana na changamoto hiyo husababisha kuzifuata Jijini Dar es Salaam hivyo gharama kuwa kubwa na hata bei za kuuzia nazo zinakuwa juu.

Friday, November 3, 2023

MAGONJWA YAONGEZEKA MWINGILIANO WA BINADAMU WANYAMA NA MAZINGIRA

 

DODOMA.

SHUGHULI za kijamii na kiuchumi, mwenendo na mifumo ya maisha na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi kumekuwa na ongezeko la magonjwa yanayoibuka kutokana na mwingiliano uliopo baina ya binadamu, wanyama na mazingira.

Hayo yamebainishwa leo jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu ( Sera, Bunge na Uratibu) Mhe.Jenista Mhagama , wakati akifungua kongamano la kitaifa la Afya Moja ambapo amesema kuwa duniani kote takriban visa bilioni 1 vya ugonjwa na mamilioni ya vifo hutokea kila mwaka kutokana na magonjwa yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.

Aidha amezisihi Wizara za Kisekta kuwa na mipango ya kutekeleza na kuimarisha ushirikiano wa kisekta kwa kutumia mbinu ya Afya Moja na kila sekta kushiriki kikamilifu katika tafiti kuhusu magonjwa yanayoweza kuambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu, utunzaji wa mazingira, usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa, usalama wa chakula na lishe na magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Nao baadhi ya washiriki wa kongamano hilo wamesema kuwa dhana ya Afya moja faida yake ni njia inayowaleta pamoja na sekta mbalimbali ambapo ni afya, mifugo na wanyamapori ili kukabiliana na changamoto zinazohusiana na afya.

Kila ifikapo Novemba 3 ya kila mwaka wadau mbalimbali huadhimisha siku ya Afya Moja kwa lengo la kuimarisha uratibu na utendaji uliopo baina ya sekta katika kuzuia na kupunguza madhara pamoja na kujiandaa kukabiliana na majanga ya milipuko ya magonjwa ya binadamu, wanyama na mimea ambapo kauli mbiu mwaka huu inasema “Afya Moja: Mbinu ya Pamoja kuboresha afya ya binadamu, wanyama, mimea na mfumo wa ikolojia kwa ustahimilivu wa maafa.

SHUGHULI ZA KIJAMII NA KIUCHUMI ZACHANGIA ONGEZEKO LA MAGONJWA

 

DODOMA.

IMEELEZWA kuwa shughuli za kijamii na kiuchumi, mwenendo na mifumo ya maisha na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi kumekuwa na ongezeko la magonjwa yanayoibuka kutokana na mwingiliano uliopo baina ya binadamu, wanyama na mazingira.

Hayo yamebainishwa leo jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu ( Sera, Bunge na Uratibu) Mhe.Jenista Mhagama , wakati akifungua kongamano la kitaifa la Afya Moja ambapo amesema kuwa duniani kote takriban visa bilioni 1 vya ugonjwa na mamilioni ya vifo hutokea kila mwaka kutokana na magonjwa yanayotoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.

Aidha amezisihi Wizara za Kisekta kuwa na mipango ya kutekeleza na kuimarisha ushirikiano wa kisekta kwa kutumia mbinu ya Afya Moja na kila sekta kushiriki kikamilifu katika tafiti kuhusu magonjwa yanayoweza kuambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu, utunzaji wa mazingira, usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa, usalama wa chakula na lishe na magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Nao baadhi ya washiriki wa kongamano hilo wamesema kuwa dhana ya Afya moja faida yake ni njia inayowaleta pamoja na sekta mbalimbali ambapo ni afya, mifugo na wanyamapori ili kukabiliana na changamoto zinazohusiana na afya.

Kila ifikapo Novemba 3 ya kila mwaka wadau mbalimbali huadhimisha siku ya Afya Moja kwa lengo la kuimarisha uratibu na utendaji uliopo baina ya sekta katika kuzuia na kupunguza madhara pamoja na kujiandaa kukabiliana na majanga ya milipuko ya magonjwa ya binadamu, wanyama na mimea ambapo kauli mbiu mwaka huu inasema “Afya Moja: Mbinu ya Pamoja kuboresha afya ya binadamu, wanyama, mimea na mfumo wa ikolojia kwa ustahimilivu wa maafa.

Tuesday, October 31, 2023

TAKUKURU PWANI YAFANIKISHA MTENDAJI KUREJESHA MILIONI 4 ZA KIJIJI ALIZOZICHUKUA ZA MAUZO YA ARDHI

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Pwani imefanikiwa kurejesha kiasi cha shilingi milioni nne za Kijiji cha Kanga zilifanyiwa ubadhirifu na kaimu mtendaji wa Kata ya Kanga wilayani Mafia.

Aidha fedha hizo ambazo ni asilimia tano ni tozo ya mauzo ya kiwanja cha Kijiji hicho ambacho kiko ufukweni mwa Bahari ya Hindi.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha Naibu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Pwani Sadiki Alli akitoa taarifa ya miezi mitatu ya utendaji kazi kuanzia Julai hadi Septemba mwaka huu. 

Alli amsema kuwa mtuhumiwa huyo jina linahifadhiwa fedha hizo hakuziwasilisha ofisini wala kuzipeleka benki kwenye akaunti ya kijiji.

Amesema mtuhumiwa huyo ambaye pia ni ofisa mazingira wa kata alibainika kwenye mkutano wa Takukuru Rafiki ambapo wananchi waliibua kero hiyo na ndipo walipofanya uchunguzi juu ya tukio hilo na kufanya ufuatiliaji.

"Baada ya uchunguzi tulibaini kuwa tukio hilo ni la kweli na alirejesha fedha hizo na tumemwandikia mwajiri wake ili achukuliwe hatua zaidi za kisheria kuhusu tukio hilo,"amesema Alli.

Amesema kuwa mafanikio hayo yanatokana na mkutano wa Takukuru Rafiki na kuwataka wananchi watumie mikutano hiyo ili kutoa kero zao juu ya vitendo vya rushwa.

"Wananchi watoe kero zao za rushwa kupitia mikutano tunayoiandaa kupitia Takukuru Rafiki kwani hapo ni moja ya sehemu wanazoweza kutoa taarifa kama watashindwa kutuletea taarifa ofisini,"amesema Alli.

Katika hatua nyingine amesema kuwa jumla ya matukio 126 ambapo 92 yalihusu masuala ya rushwa huku 34 hayakuhusu rushwa na 27 wahusika walipewa ushauri manne yalifungwa na matatu yalihamishiwa idara nyingine.

Ameanisha idara ambazo zinaongoza kwa malalamiko kuwa ni Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) yenye malalamiko 44, na elimu 17, ardhi 15, ushirika sita, binafsi tano na polisi nne.

Ameongeza kuwa idara nyingine ni afya na kilimo tatu, bandari, fedha, madini, maji, misitu na utawala malalamiko mawili kila moja, idara ya biashara, ofisi ya mkuu wa wilaya, mifugo, maendeleo ya jamii, Mamlaka ya Mapato TRA, uchukuzi, ujenzi, Tanesco, utalii na viwanda lalamiko moja moja kila idara.

Wednesday, October 25, 2023

RC KUNENGE ATAKA UJENZI WA MALL YA HALMASHAURI YA MJI UKAMILIKE NDANI YA SIKU 14


MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ametoa siku 14 kwa Mkandarasi anayejenga Maduka Makubwa (Mall) inayomilikiwa na Halmashauri ya Mji Kibaha kukamilisha ujenzi wa mradi huo wenye thamani ya shilingi bilioni nane.

Ameyasema hayo wakati wa ziara yake kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye Halmashauri hiyo ambapo mradi huo uko kwenye kitovu cha mji karibu na stendi mpya ya Maili Moja Kibaha.

Kunenge amesema kuwa mradi huo ni mkubwa ambao utakapokamilika utagharimu kiasi cha shilingi bilioni nane hivyo lazima ukamilike ndani ya muda huo ambapo matarajio ni kuingiza kiasi cha shilingi milioni 450 kwa mwaka.

"Nataka mkandarasi Elray asizidishe zaidi ya wiki mbili ahakikishe anakamilisha ndani ya muda huo tunachotaka akamilishe mradi huu ili biashara zianze kufanyika na Halmashauri ianze kupata mapato,"amesema Kunenge.

Kwa upande wake Mhandisi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Brighton Kisheo amesema kuwa Halmashauri hiyo ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni nane mwaka 2018-2019 kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo ambapo wafanyabiashara 253 watapata fursa za biashara na litahudumia watu zaidi 2,000 na unatarajiwa kukamilika Novemba mwaka huu.

Naye mwenyekiti wa Wamachinga Mkoa wa Pwani Filemon Maliga amesema kuwa wanaishukuru serikali kwa kuwapatia eneo jirani na Mall hiyo ili wafanye biashara zao na wanamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kulirasimisha kundi lao ambapo sasa wanatambulika na wanapata fursa mbalimbali zikiwemo za mikopo.

Miradi mingine aliyoitembelea mkuu huyo wa mkoa ni barabara, ujenzi wa madarasa ya sekondari kata ya Mkuza na maandalizi ya ujenzi wa kiwanda cha utengenezaji wa mitungi ya gesi ya kampuni ya Taifa Gas.


Mwisho.

Wednesday, October 18, 2023

SOKO LA KISASA KUJENGWA MLANDIZI BILIONI 7 KUTUMIKA

KATIKA kuhakikisha Mji wa Mlandizi unavutia Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha inatarajia kujenga soko kubwa na la kisasa kwa ajili ya wakazi wa mji wa Mlandizi ambalo litagharimu kiasi cha shilingi bilioni saba.

Hayo yamesemwa Mlandizi na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Michael Mwakamo wakati wa kuhitimisha kampeni ya Simika Bendera kwenye Jimbo hilo.

Mwakamo alisema kuwa eneo maarufu kama kwa Mama Salmini tayari limeshapatikana baada ya kununuliwa na mkandarasi wa ujenzi amepatikana na utaratibu unaanza kwa ajili ya ujenzi.

"Soko la sasa ni dogo lakini eneo tulilopata ni kubwa na litachukua wafanyabiashara wengi na litakuwa na huduma nyingi tofauti na la sasa ambalo hata sehemu ya magari kupaki hakuna,"amesema Mwakamo.

Amesema fedha hizo zimetengwa kwenye baheti ya mwaka wa fedha 2023/2024 na tayari bilioni mbili zimetolewa kwa ajili ya kuanza kazi na litaubadilisha Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mlandizi.

Naye Mwenyekiti wa CCM Kibaha Vijijini Mkali Kanusu alisema kuwa chama kinataka viongozi waliopo kwenye madarakani wawe na mahusiano mazuri na wananchi.

Kwa upande wake katibu wa CCM Kibaha Vijijini Zainabu Mketo amesema kuwa hamasa ya Simika Bendera imeleta mafanikio kwani wamevuna wanachama wapya 3,500 na kupitia mabalozi wote lengo likiwa ni kuimarisha chama ndani ya chama.


Mwisho.