Thursday, August 10, 2023

SERIKALI YAIDHINISHA BAJETI YA BILIONI 24 KUBORESHA HUDUMA HOSPITALI YA MKOA WA DODOMA GENERAL

Serikali imeidhinisha bajeti ya bilioni 24 kwa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma General Hospital kwa mwaka wa fedha 2023/24  kuboresha huduma za afya na kufikisha asilimia 99 za utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi.

Akizungumza leo jijini Dodoma, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Dkt. Ernest Ibenzi amesema watumishi wa hospitali hiyo wanaendelea kupata mafunzo sehemu mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Dkt. Ibenzi amesema mafunzo hayo yanawasaidia kujua teknolojia mpya ili kuendeleza juhudi za kuboresha huduma hospitalini hapo.

Amesema hospital hiyo imekua ikipokea wagonjwa wengi kwa siku wa kufikia na kuondoka takribani 1500 huku wanaolazwa wakiwa 250 hadi 350 akisema hospitali hiyo imekua ikipokea wagonjwa kwa asilimia kubwa na siyo watu wa kutembelea.

Amesema hospitali inajumla ya majengo 12 ya vyumba vya kufanyia upasuaji huku ikipokea wagonjwa70 kwa siku wanaofanyiwa upasuaji kwa lengo la Kuboresha  huduma za Afya ndani ya hospitali na kuondoa kero ya ucheleweshwaji wa huduma kwa wananchi.

Dkt. Ibenzi ametoawito kwa Wanawake wajawazito waliofikia hatua za mwisho za kujifungua kuwahi katika vituo vya afya ili kuepusha madhara yatakayoweza kujitokeza na kuepusha vifo vitokanavyo na uzazi.

Kuhusu changamoto ya msongamano wa wagonjwa kwenye wodi ya watoto ambapo watoto hulazwa wawiliwawili katika kila kitanda, Dkt. Ibenzi ameeleza kwamba tatizo hilo litakwisha ndani ya wiki mbili zijazo.

Aidha, Daktari huyo amearifu kwamba hospitali yao inaendelea kutatua changamoto mbalimbali ili wananchi wapate huduma bora.

Kwa miaka miwili iliyopita Hospitali hiyo ya rufaa ya Mkoa wa Dodoma ilikua ya kwanza kidunia kwa kutoa huduma Nzuri za upasuaji kwa wagonjwa na kupona haraka na kwa wakati.

Akitaja Vipaumbele Dkt. Ibenzi amesema kwa miaka miwili ijayo hospitali hiyo itajenga jengo lingine la gorofa 5 kwa lengo la kuimarisha huduma za Afya kuwa bora zaidi.

Hospitali hiyo inafikisha miaka 103 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1920 ikitekeleza kauli mbiu ya Wizara ya kwamba Huduma bora kipaumbele chetu karibu tukuhudumie

Wednesday, August 9, 2023

UJENZI WA HOSPITALI YA MBAGALA RANGI TATU, GHOROFA SITA ITAGHARIMU SH: BIL 10.8

UJENZI WA HOSPITALI YA MBAGALA RANGI TATU, GHOROFA SITA ITAGHARIMU SH: BIL 10.8

Na. WAF - Dar es Salaam

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu leo ametembelea Hospitali ya Mbagala Rangi Tatu na kukagua mradi wa ujenzi wa hospitali hiyo itakayo kuwa na Ghorofa Sita na itagharimu shilingi Bilioni 10.8.

Waziri Ummy amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameahidi kutoa Bilioni Mbili katika ujenzi wa jengo la ghorofa Sita la Hospitali ya Mbagala Rangi tatu ambalo litagharimu Bilioni 10.8 ili kupunguza changamoto za msongamano wa wagonjwa katika Hospitali hiyo iliopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Temeke, Mkoani Dar es Salaam.

“Nilifanya ziara hapa mwaka juzi 2020 na mwaka jana  2021 nikapokea kero ya msongamano wa wagonjwa katika Hospitali hii na kuipeleka kwa Rais Dkt. Samia na ametoa Biloni Mbili ili kukamilisha ujenzi huu”, amesewa Waziri Ummy.

Amesema, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yupo tayari kutoa fedha za huduma kwani idadi ya watu imekua ikiongezeka ndani ya Wilaya ya Temeke ambapo kwa sasa kila mwezi anatoa fedha za dawa. 

“Baada ya Mhe. Rais Dkt. Samia kutoa Bilioni Mbili na Wizara ya Afya imetoa Bilioni Mbili pamoja na Halmashauri ya Manispaa ya Temeke wametenga Bilioni Mbili kwa hiyo tayari kuna Bilioni Sita, nimefanya kazi chini ya Rais Samia kwa karibu sana, fedha hizo zilizobakia ambayo ni Bilioni Nne ni ndogo chini ya uongozi wake”, amesema Waziri Ummy

Katika ziara hiyo Waziri Ummy  amepokea taarifa ya hali ya maendeleo katika Sekta ya Afya ndani ya Wilaya ya Temeke Mkoani Dar es Salaam kutoka kwa Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe.  Mobhare Matinyi.

Wakati akipokea taarifa kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke Waziri Ummy amewataka watendaji wa Wilaya hiyo kuhakikisha wanatafuta maeneo ya kujenga majengo ya huduma za Afya ili kuwapunguzia wananchi changamoto ya msongamano wa kupata huduma. 

Pia, Waziri Ummy amewaagiza watendaji hao kuhakikisha wanasimamia zoezi la kutoa chanjo kwa wasichana walio na umri wa miaka 14 ili waweze kujikinga na saratani ya mlango wa kizazi (HPV) ambapo kwa Mkoa wa Dar es Salaam  wameweza kutoa chanjo hiyo kwa asilimia 106.

Mwisho, Waziri Ummy amesema Kwa sasa hali ya ujenzi wa jengo hilo ni asilimia Tano ambapo linatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 24, kwa fedha za Benki ya Dunia, Fedha za ndani ya Halmshauri na pamoja na fedha za Rais Samia.

WAKULIMA WATAKIWA KUTUMIA ZANA ZA KILIMO ZA KISASA

Wakulima nchini washauriwa kulima kwa kutumia vifaa vya kisasa ili kuendana na kasi ya uchumi wa kati.

Hayo yameelezwa na Ndg.Ramadhani Mrutu ambaye ni Afisa mauzo  kutoka kampuni ya  Reliance Group ambao ni wauzaji na wasambazaji wa matrekta,vipuri na viunganishi vya matrekta aina ya sonalika.

Aidha amesema kuwa kampuni yao imejidhatiti kutoa huduma nzuri yenye kuaminika wakati wote na wanamatreka kuanzia madogo kabisa mpaka makubwa na wanatoa fursa kwa wakulima wadogowadogo kuweza kununua bidhaa hizo kwa gharama nafuu zaidi kwa kuwakopesha wakulima kwani wameingia ubia na taasisi mbalimbali za kifedha ambazo ni takribani 8 ili kuhakikisha wakulima wanaendana na kasi ya kilimo cha kisasa.

"Ningependa kuwashauri wanachi kununua bidhaa zetu ili kutoka kwenye kilimo cha mikono kwa kutumia jembe hadi kilimo cha kisasa kwa kutumia trekta ili kuendana na kasi ya sekta ya kilimo kwa kuokoa muda na kuendana na kasi ya uchumi wa kati"Amesema Ndg.Ramadhani.

Aidha ameongeza kuwa kwa upande wa vikundi na mashirika huwa wanatoa elimu ni namna gani wakulima wanaweza kupata faida kupitia kilimo cha trekta ambapo mpka sasa bidhaa zao zimeshasambaa mikoa mbalimbali ikiwemo kanda ya kati  inayopatikana kibaigwa,kongwa na kanda za juu kusini mbeya,sumbawanga, kaskazini babati,mashariki ifakara morogoro,kanda ya ziwa kahama,Songea ambapo kusini inafika mpaka mtwara,kahama bariadi ili kuhakikisha wanamfikia kila mtanzania.

Aidha amesema kuwa trekta zao ni kuajili ya mkulima mdogo wa heka 20 hadi mkulima wa heka kubwa kuanzia heka 500,1000 na kuendelea hivyo wanamgusa mkulima kuanzia kuandaa shamba hadi mwisho.

Mtaalamu huyo ametoa wito kwa wananchi kuhakikisha wanalima kilimo cha kisasa na chenye tija ili kuendana na kasi ya dunia kwenye sekta ya kilimo kwani kilimo ni uti wa mgongo hivyo walime kilimo biashara ikiwa ni ajenda ya nchi kulisha afrika na dunia kupitia sekta ya kilimo.

Trekta ya sonalika ni imara kutoka India zinazotengenezwa na kiwanda cha International Tractors Limited ambacho ndiyo kiwanda kikubwa kuliko viwanda vingine vyote vya matrekta India na kwa hapa Tanzania zipo sokoni kwa zaidi ya miaka 15 sasa,ni trekta zinazopatikana katika ukubwa tofauti na zinaweza kuhimili kila aina ya udongo na zinafaa kwa kilimo cha kila zao linalolimwa Tanzania.

Kauli mbiu  ya maonyesho haya ya wakulima 88 ni "vijana na wanawake ni msingi imara wa mifumo endelevu ya chakula

MAOFISA UGANI WATAKIWA KWENDA VIJIJINI

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Bahi na Mjumbe wa halmashauri kuu ya CCM Taifa Mhe. Donard Megitii amewataka maafisa ugani kwenda vijijini kutoa elimu juu ya ufugaji bora na wenye tija kwa ajili ya manufaa ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

Megitii ametoa rai hiyo Jijini Dodoma katika ufunguzi wa kongamano la kuku Katika viwanja vya maonesho ya nanenane Nzuguni Jijini Dodoma.

Amesema vijijini bado kuna shida ya wataalam na maafisa hao hawatembelei Wafugaji hivyo kama Mkoa jambo hilo walipe uzito wasiishie kwenye kongamano kwamba watu wameonesha nia njema na ndio maana wanakuja wapate elimu, ujuzi na kuwaunganisha na maafisa ugani kwa maana ya Mifugo, Kilimo kwenda vijijini kuwatembelea Wafugaji na kuwapa elimu.

“Wafugaji wa kuku wanapaswa kuongeza uzalishaji wenye tija Dodoma ili kujivunia uwepo wa makao makuu na nawaomba wataalam nendeni mkawape elimu bora ya kufuga washiriki waliofika na kwamaana wana nia njema ya kutaka kutambua mbinu za ufugaji bora ili waweze kupata tija nakuongeza mitaji pamoja na uchumi wao,”amesema.

Aidha, amewataka wafugaji kuzingatia ulishaji na utunzaji wa chakula cha mifugo pamoja na kuzingatia kanuni za magonjwa.

“Tunashindwa kufuga kwa tija kwasababu hatuzingatii kanuni za kiafya kwa maana ya ufugaji bora kwahiyo tukizingatia kuchanja kuku yaani kuwapatia kinga ili wasipate maradhi ya kuambukiza halafu ukawapa maji ya kutosha nina uhakika tutabadilisha maisha na kuuza kuku kila siku.” amesema.

Akifanya majumuisho baada ya kuzunguka katika baadhi ya mabanda amesema amefurahi kuona kikundi cha vijana wanufaika wa Mikoa ya vijana ya 4% ilivyoweza kubadilisha maisha ya vijana watano na kuajiri vijana wengine watano.

“Hii inaonesha kuwa mafanikio kwa vijana ni makubwa na utayari wa vijana kujifunza ni mkubwa hivyo kinachobaki kwetu Viongozi ni kuhamasisha wananchi kukubali na kuanza kutumi bidhaa zetu,”amesema.

WIZARA YATAMBUA MCHANGO WA WAFUGAJI KWENYE MAENDELEO YA TAIFA

Naibu Waziri Wizara ya Mifugo na Uvuvi Mhe. David Silinde amesema dhamira ya maonyesho ya wanyama wafugwao ni kutambua mchango na juhudi za wafugaji katika kuchangia maendeleo ya Taifa na mtu mmoja mmoja.

Silinde amesema hayo katika viwanja vya Ranchi ya Taifa vilivyopo katika maonyesho ya Nanenane Nzuguni Jijini Dodoma wakati wa Uzinduzi rasmi wa maonyesho ya Mifugo ambayo maonyesho hayo huambatana na mashindano ya kushindanisha na kumpata mfugaji aliyefuga kwa tija na mafanikio katika Mifugo yake.

“Mashindano haya hufanyika katika nchi mbalimbali yakiwa na lengo la kutambua mchango na juhudi za wafugaji katika kuchangia maendeleo ya Taifa na mtu binafsi na huongeza ari kwa wananchi kuongeza uzalishaji kwa kutumia teknolojia”,amesema Silinde.

Aidha Mhe. Silinde amesema kuwa kuendelea kufanyika kwa maonesho na mashindano hayo kunachangia na kuhamasisha kuendeleza ufugaji bora nchini.

“Wizara inaangalia namna ya kufanya maonesho haya kuwa na Taswira na hadhi ya Kitaifa kama ilivyokusudiwa na wafugaji wa walioshinda katika Kanda mbalimbali watakuja Dodoma kushindana hapa Kitaifa hivyo Wizara itaendelea kuboresha tuzo na zawadi kwa washindi ili kuwapa hamasa zaidi”, amedokeza Mhe. Silinde.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma amesema Mkoa wake unashika nafasi ya tano Kitaifa kwa kuwa na Mifugo Mingi hivyo hawana budi kuimarisha juhudi za kukuza uchumi wa wananchi wa Mkoa huo ili kutatua changamoto mbalimbali zinazoyumbisha uzalishaji wenye tija.

“Kwa mujibu wa sensa ya kilimo ya mwaka 2021 mkoa wa Dodoma unashika nafasi ya 5 kwa wingi wa ng’ombe ukikadiriwa kuwa na ng’ombe 2,195,576, mbuzi 1,663,483 na wanyama wengine wafugwao hivyo juhudi zozote za kuimarisha uchumi wa wananchi wa Mkoa huu ni kipaumbele chetu, hatuna budi kushughulikia changamoto mbalimbali zinazosababisha tija ndogo katika uzalishaji wa mazao na Mifugo”,amesema Senyamule.

Maonyesho hayo ya wanyama yanafanyika kwa mara ya 12 tangu kuanzishwa kwake hufanyika katika Kanda mbalimbali na baadae hutamatishwa kwa kunganishwa Kanda zote na mshindi hupatikana akiwa ndiye mshindi wa Taifa na hupatiwa zawadi na motisha kutoka wizara ya Mifugo na Uvuvi.

SERIKALI KUONGEZA UZALISHAJI ZAO LA ALIZETI

Serikali inalenga kuinua uzalishaji wa zao la alizeti na kukuza kipato cha wakulima mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Hayo yameelezwa Agosti 3, 2023 na Mkuu wa Wilaya ya Iramba Mhe.Suleiman Mwenda wakati wa Kongamano na Mafunzo ya wakulima wa zao la alizeti kwenye maonyesho ya nanenane Kanda ya kati katika viwanja vya Nanenane Nzuguni Jijini Dodoma.

Kongamano hilo limelenga kuunga mkono na kutekeleza kwa vitendo Juhudi za Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuinua na kuthamini mchango wa Kilimo katika Taifa letu. Mafunzo hayo amebebwa na kauli mbiu inayosema ”alizeti kwa afya bora na kipato.

”Tumeshuhudia Serikali ya awamu ya sita chini ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Bashe inayotilia mkazo wa kuongeza uzalishaji wa mazao ya alizeti ili kupunguza uingizaji wa mafuta ya kula kutoka nje ya nchi na hivyo kupunguza matumizi ya bidhaa za kigeni. Jitihada hizo ni pamoja na kutoa ruzuku za mbegu bora na alizeti na vitendea kazi kwa maafisa ugani “ameeleza Mwenda.

Hata hivyo, Mhe. Mwenda ametoa wito kwa wadau wa kilimo kupeana uzoefu kuhusu mafanikio, changamoto na mkakati ya kuongeza tija ya uzalishaji na masoko ya zao la alizeti kwani sekta ya kilimo na mifugo inachangia uchumi wa nchi kwa zaidi ya asilimia 75 na kwa wananchi wa Dodoma na Singida huku alizeti ikiwa ni zao kuu la biashara katika Mkoa hiyo miwili .

Mhe. Mwenda amezitaja moja ya sababu zinazokabili mnyororo mzima wa zao la alizeti na hivyo kulazimu kuendelea na uingizaji wa mafuta ya kula kutoka nje ya nchi kuwataka wadau kutumia Kongamano hilo kuweka mikakati ya kuzipatia ufumbuzi, ambazo ni kiwango kidogo cha uzalishaji, mabadiliko ya tabia ya nchi na masoko ya alizeti yasiyo kuwa na mfumo rasmi.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Remidius Mwema amewataka wakulima wa Mikoa ya Singida na Dodoma kutumia fursa hiyo waliyoipata kufanya kilimo cha tija na kuacha kilimo cha mazoea kutokana na mafunzo waliyo yapata kuhakikisha wanafanya kwa vitendo kama ilivyo dhamira ya Serikali.

DC ATAKA MADIWANI WATUNGE SHERIA RAFIKI KWA WAWEKEZAJI

MKUU wa Wilaya ya Kibaha Nickson John amewataka madiwani kutunga sheria ndogo ambazo zitaboresha mazingira mazuri kwa wafanyabiashara na wawekezaji badala ya kuweka mazingira ambayo yatakuwa kikwazo katika ukusanyaji wa mapato.

John aliyasema hayo mjini Kibaha kwenye kikao cha baraza la madiwani wa Hmashauri ya Mji Kibaha na kuwa wanapaswa kuweka mazingira rafiki badala ya kuwa kero.

Alisema kuwa sheria ndogo ndogo wanazotunga ziwavutie wafanyabiashara na wawekezaji siyo ziwe kero na kusababisha kuwakatisha tamaa badala yake ziwe vichocheo vya watu kufanya uwekezaji.

"Zisiwe kikwazo kuwakwamisha wafanyabiashara na wawekezaji na zisiwaongezee gharama bali ziwe zinzoendana na mpango wa taifa wa wa uboreshaji biashara,"alisema John.

Aidha alisema kuwa gharama za tozo mbalimbali za Halmashauri ziendane na mazingira ya biashara na uwekezaji ili kuhakikisha mapato yanapatikana. 

"Mmapaswa kuwa wabunifu katika utendaji kwa kubuni mambo mbalimbali ambayo yataweka mazingira mazuri kwa wafanyabiashara na wawekezaji kwani mazingira yakiwa mazuri yatawavutia na watashiriki katika kukuza uchumi wa nchi,"alisema John.

Aliongeza kuwa wanapaswa kuhasaisha wananchi kushiriki shughuli za maendeleo ili kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati ili itoe matokeo kwani ucheleweshaji hauwezi kuonyesha matokeo ya haraka kwa walengwa.