Thursday, July 13, 2023

TASAF YABADILISHA MAISHA YA AKINAMAMA WAJENGA NYUMBA ZA KISASA



MFUKO wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) umeleta mabadiliko makubwa kwa walengwa wake ambapo Zubeda Juma miaka (70) mkazi wa Kijiji cha Kisanga kata ya Masaki Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani amefanikiwa kujenga nyumba ya tofali kutoka nyumba ya udongo aliyokuwa anaishi awali.


Aidha Halima Salehe naye amefanikiwa kujenga nyumba ya tofali kutokana na fedha za mfuko huo ambao umekuwa mkombozi kupitia mpango wa kunusuru kaya masikini.

Juma akitoa ushuhuda mbele ya Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejmenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete alipotembelea Kijiji hicho kuzungumza na walengwa na wananchi.

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejmenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete alimchangia na wadau wengine walimchangia huku Halmashauri ya Kisarawe ikiahidi kuhakikisha inakamilisha sehemu itakayobakia.

Alisema kuwa nyumba yake ambayo ni ya kisasa imekamilika ambapo anaishi ila amebakiza kuweka milango na madirisha ambayo ameyaziba kwa kutumia mabati.

Naye Salehe alisema kuwa nyumba yake imefikia hatua ya boma ili kukamilika na kumshukuru Rais Dk Samii Suluhu Hassan kwa kuendeleza mpango huo kutoka kwa mtangulizi wake na kuwafanikisha kubadilisha maisha yao.

Naibu Waziri Ridhiwani alisema mpango huo una lengo la kuwaondoa wananchi kwenye lindi la umasikini ambapo watu milioni 1.3 wananufaika na mpango huo wa kunusuru kaya maskini na kuondoka kwenye umaskini na utegemezi.

Wednesday, July 12, 2023

WATUMISHI WAFANYE KAZI KIMKAKATI

WATUMISHI wa Umma wametakiwa kufanya kazi kimkakati kwa kuwatumikia wananchi na kwa kuwa na wivu wa maendeleo sehemu wanazozifanyia kazi kwa kuacha alama.

Hayo yalisemwa na NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete alipokuwa akizungumza na Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha kwenye ofisi za Halmashauri hiyo zilizopo Mlandizi.

Alisema kuwa serikali inafanya shughuli zake kimkakati hivyo lazima nao wafanye kazi kwa kuzingatia mikakati hiyo ya serikali ili mipango ya maendeleo kwa wananchi ifikiwe.

"Serikali ina mikakati yake hivyo lazima kila mtumishi wa umma ahakikishe anazingatia mikakati iliyopo ili kufanikisha malengo ya maendeleo kwa wananchi ambapo wanawategemea watumishi kuwaonyesha njia,"alisema Kikwete.

Alisema asingependa kuona watumishi hawawajibiki kwenye maeneo yao ya kazi na kusababisha malengo ya kuwaletea maendeleo wananchi yasifanikiwe hivyo wasije wakajikuta wanaondolewa au kufukuzwa kazi.

"Kutokana na changamoto zilizopo hapa ofisa utumishi Edward Mahona nakutaka ushughulikie chanfamoto za watumishi siyo lazima kuleta kwetu kwani baadhi ya mambo mnaweza kuyatatua wenyewe hivyo tatua mara moja,"alisema Riziwani.

Aidha alisema kuwa ofisa huyo anatakiwa kukaa na watumishi na kuongea nao kujua changamoto zao kwani malalamiko yaliyotolewa yanapaswa kufanyiwa kazi ili wafanye kazi kwa moyo kwani shida zao zinatatuliwa.

Moja ya watumishi Winifrida Toegale ambaye ni ofisa mtendaji wa kijiji alisema kuwa wanatumia fedha zao binafsi kwani hakuna fedha wanazopewa kwa ajili ya kuendeshea ofisi.

Toegale alisema kuwa licha ya kutumia fedha zao za mishahara lakini kwa upande wao walioajiriwa mwaka 2012 hawakupandishwa vyeo hadi mwaka 2020 jambo ambalo limekuwa changamoto kubwa na inawavunja moyo.

Kwa upande wake mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Butamo Ndalahwa alisema kuwa wanakabiliwa na uhaba wa watumishi 441 ambapo waliopo ni 1,571 na mahitaji ni 2,012 na wameweka bajeti ya kuajiri watumishi 211 kwenye kada mbalimbali.

Ndalahwa alisema kuwa madai ya watumishi 342 ni milioni 756 ambapo madai yaliyolipwa ni 251 ya shilingi milioni 455 bado madai 91 yenye thamani ya shilingi milioni 329 kwa upande wa watumishi 70 waliogushi vyeti 56 walijaza fomu huku 12 bado taratibu zinaendelea.

Tuesday, July 11, 2023

VIKUNDI VYA UJASIRIAMALI VYA TASAF VIKOPESHWE ASILIMIA 10 ZA HALMASHAURI



NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejmenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete ameshauri Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha kuvipatia fedha za mikopo za asilimia 10 vikundi vya ujasiriamali vilivyopo kwenye mpango wa kunusuru kaya maskini kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) 

Kikwete ameyasema hayo kwenye Kitongoji cha Mwembebaraza kata ya Janga Mlandizi Wilayani Kibaha alipotembelea vikundi vya wajasiriamali wanaotokana na fedha za kuweka akiba na kukuza uchumi wa kaya (LE) kupitia Tasaf.

Amesema kuwa wajasiriamali watokanao na vikundi hivyo wanafanya shughuli ambazo zinaonekana na ni watunzaji wazuri wa fedha ambapo wanakopeshana wenyewe kwa wenyewe japo ni kidogo lakini manufaa yanaonekana.

"Nafikiri mkurugenzi katika zile asilimia 10 vikopesheni vikundi hivi kwani wanauaminifu mkubwa na wanatumia fedha kwa malengo ambayo yanaonekana kupitia miradi hii kuanzia ile ya uhawilishaji wa fedha, miradi ya ajira za muda na miradi ya ujenzi wa miundombinu,"alisema Kikwete.

Aidha amesema kuwa endapo fedha zitatolewa kwa vikundi hivyo fedha za serikali hazitapotea ambapo vikundi vinavyolengwa vimekuwa havirudishi fedha wanazokopeshwa lakini vikundi vya Tasaf ni waaminifu sana.

"Tasaf imekuwa mkombozi kwani imeweza kubadili maisha ya kaya lengwa kutoka chini na kuinuka kiuchumi na kuondoka kwenye hali ya chini na kuboresha maisha kama malengo ya serikali yalivyowekwa kwani mpango umetafsiriwa kwa vitendo,"alisema Kikwete.

Kwa upande wake mratibu wa Tasaf Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha akisoma taarifa ya mpango huo wa kunusuru kaya masikini Sijaona Muhunzi alisema kuwa kaya lengwa zimenufaika kupitia vikundi na mtu mmoja mmoja.

Muhunzi alisema kuwa baadhi ya walengwa wameweza kujenga nyumba, kufanya ufugaji, kilimo cha mboga mboga, kusomesha watoto na kuongeza maudhurio shuleni na kliniki ambapo ni moja ya masharti kwa familia lengwa watoto kwenda shule na kliniki kwa asilimia 100.

Naye Dalia Hassan amesema kupitia mpango huo amemsomesha mwanae ambaye kwa sasa yuko chuo kikuu anasema alianza kupewa ruzuku ya shilingi 40,000 mwaka 2012 ambapo aliingiza kwenye biashara ya karanga.

Hassan amesema kuwa fedha hizo zilimwezesha kuanza kilimo cha mpunga na pilipili vimemsaidia kumsomesha mwanae huyo na kuwataka walengwa wenzake kuwa na malengo makubwa ya kujiletea maendeleo.

MHE.MASANJA : FILAMU YA "THE ROYAL TOUR" IMEFANIKIWA KWA KIWANGO KIKUBWA SANA

 



NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) amesema filamu ya “The Royal Tour” iliyozinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanikiwa kwa kiwango kikubwa na kwamba kwa sasa watalii wameongezeka.

Mhe. Masanja ameyasema hayo leo Julai 11,2023 alipotembelea Maonesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam maarufu kama Sabasaba yanayoendelea Jijini humo.

“Tunatambua kwamba ni nadra sana kumpata Kiongozi anayeamua kuongoza kwa vitendo  kama alivyofanya  Rais Samia, ametangaza kwa vitendo vivutio vyetu hivyo tunatakiwa kuvitembelea vivutio hivyo  ili kumuunga mkono” Mhe. Masanja amesisitiza.

Mhe. Masanja ametumia nafasi hiyo kuwahimiza Watanzania kutembelea vivutio vya utalii vilivyoko nchini akitolea mfano wa maeneo ya Malikale, Misitu ya Asili, tamaduni za Kitanzania, historia za Tanzania za Waasisi wa Taifa na maeneo mengine ya utalii.

“Tutembelee vivutio vyetu, ukishakitembelea kile kivutio unakuwa umechangia pato la Taifa lakini hata wewe mwenyewe utakuwa umejifunza historia ya nchi ilivyo lakini pia utapunguza hata msongo wa mawazo” Mhe. Masanja amefafanua.

KAMPUNI YA GGML NA WIZARA YA MADINI KWA KUTOA ELIMU

 

WIZARA ya Madini imepongezwa na  Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) kwa kutoa elimu kwa wananchi na wadau wanaotembelea banda la Wizara, taasisi zake na wadau wa Sekta ya Madini.

Pongezi hizo zimetolewa leo  Julai 11, 2023 na Mwanasheria Mkuu wa kampuni ya GGML  David Nzaligo alipotembelea banda la Wizara ya Madini (MADINI PAVILION) katika Maonyesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) jijini Dar es salaam.

Akizungumza mara baada ya kutembelea banda la Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Nzaligo ameipongeza kampuni hiyo kwa kuleta Mkaa Mbadala wa Rafiki Briquettes ambao utasaidia kudhibiti uharibifu wa mazingira hapa nchini.

Akiwa katika banda la  kampuni ya GGML ambalo lipo pia ndani ya banda la madini, Nzaligo amewapongeza wafanyakazi wa GGML na kampuni zingine ndani ya banda hilo kwa kuonyesha weledi mkubwa katika kutoa elimu ya shughuli wanazozifanya ikiwemo uchimbaji madini na mnyororo wake.

"Nafahamu GGML wapo vizuri kwenye miradi mingi ya kijamii pamoja na uwezeshaji wananchi kiuchumi. Nafurahi kwamba  mafanikio hayo wanayaelezea vizuri kwa kila mwananchi anayetembelea banda la GGML," alisema.

MAOFISA UTUMISHI WAONYWA

MAOFISA Utumishi wa Halmashauri nchini wameonywa kwa kutakiwa wabadilike na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kuwaondolea kero watumishi.

Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejmenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete alipokuwa akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Mji Kibaha.

Kikwete alisema kuwa baadhi ya maofisa Utumishi wamekuwa hawatoi haki kwa watumishi hali ambayo inasababisha malalamiko kwa watumishi na kushindwa kufanya kazi kwa moyo jambo ambalo ni kinyume cha utaratibu.

"Maofisa Utumishi ni kama vile baba na mama kwa watoto hivyo lazima wawatendee haki lakini baadhi wanafanya mambo ambayo hayapendezi wanasemwa vibaya hatupendi kuona watumishi wanamalalamiko kila mtu atimize wajibu wake kwa weledi na ubunifu kwani watumishi ndiyo msingi wa serikali,"alisema Kikwete.

Alisema kwa upande wa watumishi aliwataka wafanye kazi kwani wao ni chachu ya maendeleo na wawe na utumishi utakaoweza kupimwa kwa kutoa huduma bora kwa wateja.

"Kuna baadhi ya watumishi wanacheza karata ofisini hii inaonyesha ni kukosa ubunifu haipendezi watu wanachangamoto nyingi wanahitaji kupatiwa huduma na nyie mliajiriwa kwa ajili yao hivyo mnapaswa kuwajibika kwa wananchi,"alisema Kikwete.

"Kwa mwaka wa Fedha 2023/2024 Serikali inategemea kutumia jumla ya shilingi bilioni 10.8 kwa ajili ya Bajeti ya Mishahara kwa watumishi wa Umma katika matukio mbalimbali ya kiutumishi,"alisema Kikwete.

Alibainisha kuwa hata kwa bajeti ya nyuma ya mwaka wa Fedha 2022/2023 Serikali ilitegemea kutumia jumla ya shilingi bilioni 9.7 kwa ajili ya Bajeti ya Mishahara kwa watumishi wa Umma katika matukio mbalimbali ya kiutumishi hali inaoonyesha serikali inakabili changamoto za fedha za watumishi wa umma.

Naye Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge alisema kuwa watumishi wanapaswa kuboresha utendaji kazi wao ili malengo ya Rais Dk Samia Suluhu Hassan ya kuwaletea maendeleo wananchi yafikiwe.

Kunenge alisema kuwa endapo kila mtumishi wa umma atawajibika kwenye sehemu yake malalamiko ya wananchi hayatakuwepo hivyo lazima waongeze uwajibikaji.

Mwisho.

Monday, July 10, 2023

HALMASHAURI YA MJI YAPONGEZWA KUPITIA TASAF

HALMASHAURI ya Mji Kibaha imepongezwa kwa kutekeleza kwa vitendo uhawalishaji wa fedha kwa kaya maskini kiasi kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) cha shilingi bilioni 3.1 kwa kaya 2,583.

Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejmenti ya Utumishi wa Umma Ridhiwani Kikwete kwenye mtaa wa Miwaleni kata ya Visiga alipokea akipokea taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini.

Kikwete alisema kuwa katika kipindi cha miaka miwili ya Rais wa awamu ya Sita Dk Samia Suluhu Hassan serikali imetoa bilioni 51 kwa ajili ya mpango huo wa kusaidia wananchi.

Alisema kuwa wakati Rais wa awamu ya tano Dk John Magufuli aliacha mpango huo ukiwa kwenye awamu ya pili na ulikuwa ukitekelezwa kwa asilimia 75 lakini sasa wananchi wote wanafikiwa.

"Hadi sasa watu milioni 1.3 wananufaika na mpango huu wa kunusuru kaya maskini hali ambayo inaonyesha jinsi gani serikali inavyohakikisha wananchi wananufaika na miradi mbalimbali,"alisema Kikwete.

Alisema kata hiyo ulipo mtaa huo miaka tisa ilikuwa ni moja ya maeneo ysliyofanyiwa majaribio lakini leo watu wamenufaika na kuboresha maisha yao.

"Niwapongeze Halmashauri kwani hapa naona mabadiliko ni makubwa fedha zilizotolewa zinaonyesha matunda kwani zimebadili maisha ya watu kwani wamejikomboa kiuchumi,"alisema Kikwete

Aidha alisema kuwa kulikuwa na changamoto ya ucheleweshaji malipo lakini kwa sasa hilo halipo na mambo yanakwenda vizuri ili kila mwananchi anayelengwa na mpango afikiwe.

Akielezea kuhusu mpango huo mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mhandisi Mshamu Munde alisema kuwa katika malipo ya dirishani kwa mwezi Januari na Februari mwaka 2023 kiasi cha shilingi milioni 12.7 kililipwa kwa kaya 312 huku kiasi cha shilingi milioni 91 zililipwa kwa njia ya mitandao ya simu na benki kwa kaya 2,168.

Munde alisema kuwa kwenye miradi ya uendelezaji miundombinu kumefanyika ujenzi wa nyumba ya watumishi zahanati ya Vikawe na ujenzi zahanati ya Mwanalugali zote zikiwa zimepatiwa milioni 91.9 kila moja.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson John alisema kuwa viashiria bora vya wanufaika ni uundaji wa vikundi ambavyo havina upotevu wa fedha.

John alisema kuwa walengwa wanaunda vikundi ambavyo vinajikopesha na kujikwamua kiuchumi kupitia Tasaf ni mkombozi kwa watu ambao walikuwa na hali mbaya ya kimaisha.

Naye Ester Mlinge ambaye ni mnufaika alisema kuwa ameweza kuboresha maisha yake kutoka kwenye kupanga nyumba hadi kumiliki nyumba ambayo anaishi na familia yake.

Mlinge alisema mbali ya kujenga nyumba pia wameanzisha vikundi vya kukopeshana ambapo hadi sasa wana akiba ya shilingi milioni 1.1.