Thursday, April 2, 2026

CCM PWANI YAISHUKURU SERIKALI YA DK SAMIA SULUHU HASSAN FEDHA MIRADI YA MAENDELEO

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani umeishukuru serikali inayoongozwa na Dk Samia Suluhu Hassan kwa kuuongezea Mkoa bajeti ya fedha za miradi ya maendeleo na kufikia kiasi cha shilingi bilioni 497.1 mwaka 2026/2027.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Katibu wa Siasa Uenezi na Mafunzo wa CCM Mkoa wa Pwani Dk David Mramba alisema kuwa hiyo inaonyesha jinsi gani serikali inavyojali maendeleo ya wananchi.

Alisema kuwa fedha hizo zimeongezeka kutoka kiasi cha shilingi bilioni 473 bajeti ya mwaka 2025/2026 hivyo kufanya Mkoa kupiga mbele hatua za maendeleo.

"Fedha hizi zinakwenda kukabili changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili wananchi kwenye huduma muhimu za kijamii ambapo zinatoa majawabu,"alisema Mramba.

Alisema kuwa baadhi ya miradi ikiwemo huduma za maji zimeboreshwa ambapo wananchi wanapata maji safi na salama ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

"Kwa upande wa elimu madarasa mengi yamejengwa, maabara za kutosha ili kuinua masomo ya sayansi, ujenzi wa vyoo, mabweni, nyumba za walimu na madawati,"alisema Mramba.

Aidha alisema kuwa kwa upande wa huduma za afya nazo zimeboreshwa kwani Hospitali za Rufaa, Hospitali, Zahanati na huduma za kibingwa zinatolewa hapa hapa nchini badala ya kwenda nje ya nchi.

"Kuhusu miundombinu barabara nyingi zimejengwa na kurahisisha shughuli za kiuchumi huku mazao na bidhaa zikisafirishwa kwa urahisi ambapo mikoa na wilaya zinaingiliana kwa urahisi,"alisema Mramba.

Aliongeza kuwa kuna baadhi ya changamoto ambazo zinafanyiwa kazi kwa kuendelea kutengewa bajeti ili kuhakikisha huduma za msingi kwa wananchi zinapatikana kwa urahisi.

No comments:

Post a Comment