Wednesday, November 30, 2022

WAWEKA MIKAKATI KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA

WADAU WAENDELEA KUPAMBANA NA UKATILI WA KIJINSIA WILAYA YA KIBAHA



 IMEELEZWA kuwa uanzishwaji wa madawati kwenye shule na makundi mbalimbali ya jamii kutasaidia kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa matukio yanayohusiana na vitendo hivyo.


Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na mwanasheria wa Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika (WiLDAF) Tanzania Zakia Msangi wakati wa kupita msafara unaotoa elimu ya kupambana ukatili wa Kijinsia ikiwa ni sehemu ya siku 16 za kupinga vitendo hivyo.

Alisema kuwa moja ya makundi yanayoathirika na vitendo hivyo ni watoto ambapo madawati hayo yataundwa kwa kushirikiana na walimu wa malezi kwenye shule.

"Madawati haya yatakuwa yakitoa elimu juu ya kupambana na ukatili wa Kijinsia na kuripoti vitendo hivyo kwenye vyombo husika ikiwemo dawati la jinsia na vyombo vingine vya sheria,"alisema Msangi.

Msangi alisema kwa shule kutakuwa na wanafunzi wawili vinara ambao watakuwa na ujasiri wa kujieleza na wenye usiri pia kutakuwa na sanduku la siri la kutolea maoni.

"Makundi mengine ndani ya jamii kama vile waendesha pikipiki nao wataunda madawati kwa ajili ya kupambana na matukio hayo ambapo itasaidia kukabili kwani ni kundi linalokumbana na mambo mengi,"alisema Msangi.

Aidha alisema kuwa Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika (WiLDAF) Tanzania ni waratibu wa kampeni hiyo ambapo wameungana na Mtandao wa Kupambana na Ukatili wa Kijinsia (MKUKI) ambao ndani yake kuna mashirika zaidi ya 100 kupambana na suala hilo.

Kwa upande wake ofisa Mawasiliano wa Shirika linalosaidia mashirika yanayotoa msaada wa sheria (LSF) Wilson Mtapa alisema kuwa wamewezesha msafara huo ili kupinga vitendo hivyo kwa kutoa elimu ya kupinga vitendo hivyo kwa kushirikiana na serikali na wadau wa maendeleo.

Mtapa alisema kuwa elimu hiyo inatolewa kwenye maeneo yenye mikusanyiko ya watu ikiwa ni pamoja na mashuleni madokoni na kwa vikundi vya waendesha bodaboda kwenye Wilaya msafara huo utakapopita kauli mbiu ikiwa ni Kila uhai unathamani tokomeza mauaji na ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Alisema kuwa mashirika hayo mbali ya kupambana na vitendo hivyo pia yanatetea haki za binadamu ambapo wanatoa elimu ya namna ya kukabiliana na vitendo hivyo ndani ya jamii na msafara huo ulioanzia Dar es Salaam Pwani utapita mikoa ya Morogoro, Singida, Shinyanga, Arusha na Musoma.

Naye mwakilishi wa Shirika la Maendeleo kwa Vijana YPC ambalo liko chini ya MKUKI ambao ndiyo walikuwa wenyeji wa msafara huo Fred Mtei alisema kuwa ujumbe uliotolewa wa kukabiliana na vitendo vya ukatili umewafikia watu wengi.

Mtei alisema kuwa wao kama wana harakati wataendelea kutoa elimu na kuielimisha jamii namna ya kukabiliana na vitendo hivyo.

Mkurugenzi wa Kituo Cha Msaada wa Kisheria Kibaha (KPC) Catherine Mlenga alisema kuwa wamekuwa wakipokea wateja ambao wengi wao ni wa vitendo vya ukatili wa Kijinsia.

Mlenga alisema kuwa wamekuwa wakishirikiana na vyombo vya sheria ikiwemo Polisi na mahakama kupambana na vitendo hivyo kwenye Wilaya na Mkoa mzima wa Pwani na wanatoa elimu kwenye maeneo mbalimbali na makundi ya kijamii.

 Kwa upande wake Mratibu wa Chama Cha Majaji na Mahakimu Tanzania kwa Mkoa wa Pwani Honorina Kambadu alisema kuwa wanazingatia haki na usawa mbele ya sheria na kukabili matukio ya ukatili wa Kijinsia.

Kambadu alisema kuwa baadhi ya matukio ni kama vile vipigo, unynyasaji na mauaji na kunyimwa haki zingine kwa wanawake na watoto ambao ndiyo waathirika wakuu wa vitendo hivyo.

Mwisho.

Tuesday, November 29, 2022

WAZIRI MKUU MAJALIWA ASEMA VIJANA WANAAJIRIKA


Na John Gagarini, Mkuranga

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa nchi inauwezo wa kuzingatia Utumishi kwenye sekta binafsi ili wawekezaji watumie vijana wa hapa nchini na kuachana na mawazo ya kuleta wafanyakazi kutoka nje ya nchi kwani Watanzania wanaajirika na ni waaminifu.

Majaliwa aliyasema hayo Kisemvule Wilayani Mkuranga Mkoani Pwani alipokuwa anazindua kiwanda na mabati cha Lodhia Group of Company na kusema kuwa vijana wa Kitanzania wanauwezo wa kufanya kazi na hakuna sababu ya wafanyakazi kutoka nje ya Tanzania.

Alisema kuwa vijana wa Kitanzania wanaajirika na wanafanya kazi kwa bidii na kwa sasa hata vitendo vya kutopenda kufanya kazi hilo halipo tena wanawajibika ipasavyo. 

"Waajiriwa zaidi ya 3,000 kitendo cha kutoa ajira umesaidia sana tutakuunga mkono uendelee kutoa vijana ambao wako mtaani itasaidia kufanya nchi kuwa na amani nchi imepanua wigo na fursa za uwepo wa viwanda,"alisema Majaliwa.

Aidha alisema uwepo wa kiwanda hicho umesaidia kutoa ajira na hiyo ni fursa kwa wengine inasaidia kuzalisha na kupanua wigo ili kusaidia watu wengine zaidi hapa ni ajira zaidi ya 2,500 hilo ni jambo kubwa.

"Serikali ya awamu ya sita imeweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji kuja kuwekeza kwa wale wa ndani na nje maelekezo tuliyopewa kuanzia kuomba kuwekeza na kuanza uwekezaji ni kuhakikisha hawapati shida wala kikwazo chochote ili kila upande unufaike mwekezaji na mwananchi,"alisema Majaliwa. 

Aliongeza kuwa kampuni hiyo ni moja ya kampuni inayolipa kodi kubwa nchini ambapo inalipa zaidi ya bilioni 40 kwa mwezi ni kama lulu watatatua changamoto zinazoikabili kwani nachangia pato la serikali na kusaidia huduma za jamii na inamuunga mkono Rais kwa kupunguza changamoto ya ajira.

"Hapa Tanzania ni sehemu salama ya uwekezaji tunatambua na tunaheshimu uwekezaji huu kwani huyu ni wa kuenziwa na Halmashauri ili wapate fedha zaidi na hatimaye nchi inufaike hakika leo nimefurahi sana kutembelea kiwanda hichi ambapo Arusha nlitembelea walikuwa na kiwanda kidogo sana uwekezaji mkubwa na malengo kuweka mradi mkubwa zaidi naifurahi kutembelea,"alisema Majaliwa.

Alibainisha kuwa kiwanda hicho kinachozalishwa chuma mbalimbali zikiwemo nondo ni kikubwa kuliko viwanda vyote alivyotembelea na kuweka jiwe la msingi la kiwanda ukubwa wake ni hekari nane na nusu kitatengeneza bati.

"Uwepo wa viwanda vya nondo, plastiki, mabomba ya maji na bati itasaidia bidhaa kwani zitapatikana hapa nchini badala ya kuagiza nje na pia zina ubora bado eneo dogo kufikia kiwanda cha Afrika Mashariki itafikia hatua hiyo na kuwa kiwanda kikubwa hapa Afrika Mashariki,"alisema Majaliwa.

Aliongeza kuwa uwepo wa viwanda vijana Teknolojia na hilo limepewa kipaumbele ili wajifunze kupitia mitambo hiyo ya kisasa ni faida ya uwepo wa viwanda nchi itakuunga mkono na milango itakuwa wazi na azma ya kutembelea ni kuangalia uwekezaji unaofanywa ukiwemo kwenye mabomba ya maji na serikali inaona kuwa anafunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan alisema na kuwahakikshia kuwa uwekezaji hautakwama hata kidogo.

Kwa upande wake Mwenyekiti na mwanzilishi wa kampuni hiyo Haroun Lodhia alisema kuwa kiwanda chao kinalipa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 22 kwa ajili ya umeme na gesi ambapo baadaye watakuwa na uwezo wa kuzalisha tani 40,000 za chuma kwa mwezi.

Lodhia alisema kuwa kwa siku za baadaye watazalisha umeme wao wenyewe ambapo wataanza kuzalisha megawati tano na baadaye kva 25 na wanaishukuru serikali kwa kuwawekea mazingira mazuri kuendesha shughuli zao.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Mkuranga Abdala Ulega alisema kuwa kutokana na uwekezaji mkubwa uliopo kwenye Wilaya ya Mkuranga na wingi wa magari yanayokwenda mikoa ya Kusini wangeomba barabara ya Kusini ipanuliwe na kuwa ya barabara nne.

Ulega alisema kuwa barabara hiyo kuanzia Mbagala Rangitatu kwenda Mwandege Vikindu na kuendelea ingepanuliwa ili bidhaa ziweze kwenda kwa urahisi na pia hapo Mkuranga viwanda vingi tumia umeme mkubwa na hakuna gari la Zimamoto ikitokea moto itakuwa ni shida sana hivyo wapatiwe huduma ya gari hilo.

Mwisho.


Friday, November 25, 2022

CHANJO COVID-19


VIJANA WAJITOKEZE KUCHANJA COVID-19

VIJANA nchini wametakiwa kujitokeza kupata chanjo ya ugonjwa COVID 19 na waachane na dhana potofu kuwa hawawezi kuambukizwa ugonjwa huo.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Mtaalam wa chanjo kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) Caroline Akim alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na chanjo ya COVID 19. 

Akim alisema kuwa moja ya kundi kwenye jamii ambalo halijitokezi kuchanja wakidhani kuwa hawawezi kupatwa na ugonjwa huo hivyo kuwa hatarini kuambukizwa ugonjwa huo.

"Vijana wanadhana kuwa hawawezi kupata ugonjwa huo kwani baadhi hawana dalili ya maambukizi licha ya kuwa wao ndiyo wenye pilika pilika nyingi,"alisema Akim.

Alisema kuwa vijana ni kundi ambalo linahimizwa kupata chanjo kutokana na kuwa na mizunguko mingi kwenye jamii na kuwa rahisi zaidi kueneza ugonjwa huo pale wanapoupata.

"Wajawazito pia wanahimizwa kupata chanjo ya COVID-19 kwani wakipata ugonjwa huu wako kwenye hatari ya mimba kutoka au mtoto kuzaliwa kabla ya wakati na hata wanaonyonyesha wanakumbushwa kuwa chanjo ni salama kwao haina madhara kwa mtoto" alisema.

Aidha alisema kuwa waandishi wanatakiwa  sasa kuwakumbusha wananchi umuhimu wa kuchanja lakini pia faida zake ili kuepuka kuingia kwenye athari wanapopata ugonjwa huo.

Naye Mratibu wa chanjo mkoa wa Pwani Abas Hincha alisema kuwa wanatarajia kuanza kampeni ya chanjo ya COVID-19 inaanza Novemba 25 na watawafikia wananchi ambao bado hawajapata chanjo.

Hincha alisema kuwa Mkoa huo unatarajia hadi kufikia Desemba 30 kuwafikia wananchi 757,465 na kwamba hadi kufikia Novemba 22 walengwa 468,187 tayari wamepata chanjo sawa na asilimia 63.

Saturday, November 19, 2022

SAMIA AASA VIONGOZI WA DINI JUU YA AMANI



Wellu Mtaki, Dodoma

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amewaasa viongozi wa dini hapa nchini kuendelea kushikamana na serikali kudumisha uzalendo na amani ya nchi .

Amebainisha hayo leo Novemba 19.2022 Jijini Dodoma katika sherehe ya Jubilee ya miaka 50 ya Kanisa la Waadventista Wasabato Jiji la Dodoma ambapo amesema amani ndiyo msingi wa utulivu wa nchi.

Ametumia fursa hiyo kulipongeza Kanisa la Waadventista Wasabato kwa kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha amani na kuendelea kushirikiana na serikali kwa miradi mbalimbali ya huduma za kijamii ikiwemo katika sekta za afya,elimu na kusaidia wenye uhitaji.

Aidha amekipongeza kikundi cha uimbaji cha watoto wa shule ya Msingi na awali cha Ellen White pamoja na Kwaya ya Nyarugusu SDA kutoka mkoani Geita kwa kuimba wimbo wenye uzalendo na upendo wa taifa la Tanzania.

Kuhusu suala la mmomonyoko wa maadili katika jamii Rais Samia amewaasa viongozi wa dini kuendelea kushirikiana na serikali kukemea vitendo viovu ikiwemo kushirikiana katika mapambano ya dawa za kulevya na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Amesema suala la mabadiliko ya nchi ya ukosefu wa mvua katika baadhi ya maeneo amewaasa viongozi wa dini na washarika kwa ujumla kuliombea Taifa huku akitoa wito kwa viongozi wa dini kuwa mabalozi kuelimisha jamii kuhusu madhara ya uharibifu wa mazingira.

Hata hivyo Rais Samia amehitimisha kwa kusema kuwa ni muhimu sana kutegemea neema na Baraka za mwenyezi Mungu kama isemavyo Zaburi 127:1.

Naye Mwenyekiti Kanisa la Waadventista Wasabato Union ya Kusini mwa Tanzania [STU] Mch.Dkt.Godwin Lekundayo amemhakikishia Rais Samia kuwa Kanisa litaendelea kushirikiana na serikali katika kuwajengea maadili vijana .

Mch.Lekundayo ametumia fursa hiyo kutoa pole kwa serikali ya Tanzania kwa ajali ya ndege ya Precision Air iliyoua watu 19 hivi karibuni mkoani Kagera huku akisisitiza kuwa kanisa litaendelea kuiombea Tanzania kuepusha majanga.

Katibu Mkuu wa Kanisa la Waadventista Wasabato Jimbo la Kusini mwa Tanzania[STU] Mch.Jeremiah Izungo amesema wao kama kanisa wataendelea kushirikiana na serikali kwa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo katika sekta za elimu na afya.

Mch Izungo amesema kanisa linaendelea kusisitiza afya ya jamii ikiwemo kuzingatia kanuni bora za afya,lishe na kuchangia damu salama ambapo huwa kuna utaratibu wa kuchangia damu salama kila mwaka mwezi Machi.

Amesema changamoto zinazolikabili Kanisa ni pamoja na usaili wa nafasi za kazi serikalini siku ya Jumamosi ya ibaada ambapo hukosesha vijana nafasi za ajira serikalini pamoja na mitihani shuleni kufanyika siku ya Jumamosi ya ibaada.

Ameiomba serikali kuwapatia wataalam wabobezi katika hospitali za Kanisa huku akiweka msisitizo kuwa Kanisa linajitegemea haliko kwenye muunganiko wa wa Umoja wa Kikristo Tanzania [CCT].


Wednesday, November 16, 2022

WALIMU WAKUU KUPATIWA MAFUNZO NA ADEM


ADEM KUTOA MAFUNZO YA UONGOZI

Na Wellu Mtaki, Dodoma

WAKALA wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) imesema imejipanga kutoa Mafunzo ya Uongozi na Usimamizi wa Shule kwa Walimu Wakuu 17,000.

Aidha itatoa mafunzo ya utawala Bora kwa wasimamizi wa elimu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Hayo yameelezwa na Mtendaji Mkuu wa Wakala hiyo Dkt Siston Masanja akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Wakala hiyo na mwelekeo wa utekelezaji kwa Mwaka wa Fedha wa 2022/2023.

Dkt Masanja amesema katika mwaka huu wa fedha wa 2022/2023 wakala hiyo imejipanga kudahili Walimu 2,343 katika kozi mbalimbali pamoja na kuandaa kitabu cha kiongozi cha Mwalimu Mkuu na kuandaa Mwongozo wa Utawala Bora kwa viongozi wa Serikali za Mitaa.

Dkt.Masanja amesema moja kati ya malengo ya Wakala hiyo ni kuimarisha usimamizi wa utoaji wa elimu bora shuleni kwa kuzingatia sera, sheria, kanuni na miongozo ya elimu, kuziba ombwe la maarifa na ujuzi ambalo kiongozi au mtendaji hakupata katika mafunzo ya awali ya Ualimu na kuongeza idadi ya viongozi wenye maarifa ya uongozi na usimamizi wa elimu.

Kwa Upande wake Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari Maelezo Gerson Msigwa amesema kuwa Serikali imeweka fedha nyingi kwenye sekta ya elimu nchini ambapo kwa mwaka wa fedha 2022/23 sekta ya elimu pekee imetengewa Shilingi trilioni 5.8.

Aidha, Msigwa ametoa wito kwa waajiri wote nchini kuwaruhusu viongozi wa taasisi za elimu pamoja na wakuu wa shule kwenda kusoma ADEM.

Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu - ADEM ulianzishwa Agosti 31, 2001 ukiwa na majukumu ya kutoa mafunzo ya muda mrefu na mfupi ya Uongozi na Usimamizi wa Elimu kwa viongozi na watendaji mbalimbali wa elimu katika ngazi zote na kutoa ushauri wa kitaalamu katika mambo yanayohusu uongozi na usimamizi wa elimu.

Mwisho. 

Friday, November 11, 2022

MABILIONI YATOLEWA KUBORESHA AFYA

SERIKALI YATOA BILIONI 200 UNUNUZI VIFAA TIBA NA DAWA

Na Wellu Mtaki, Dodoma

NAIBU Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel amebainisha kuwa Serikali imetenga kiasi cha shilingi Bilioni 200 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba katika mwaka wa fedha 2022/2023.

Aidha tayari bilioni 74.3 zimetolewa katika kumaliza changamoto ya upungufu wa dawa na vifaa tiba nchini.

Dkt. Mollel amesema hayo leoJijini Dodoma Novemba 11,2022 wakati akijibu swali la Mhe. Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa viti maalumu katika kikao cha kumi cha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 

Amesema, Serikali ya awamu ya sita imedhamiria kutatua changamoto za huduma za afya kwa wananchi, huku kiasi cha shilingi Bilioni 74.3 zikiwa tayari zimetolewa kati ya Bilioni 200 zilizotengwa katika mwaka wa fedha 2022/2023 kwa ajili ya ununuzi wa dawa pamoja na vifaa tiba.

"Katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga bajeti ya shilingi Bilioni 200 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba na hadi kufikia tarehe 30 Oktoba, 2022 Serikali imekwisha toa jumla ya shilingi bilioni 74.3 kwa ajili ya manunuzi ya dawa na vifaa tiba ili kuimarisha upatikanaji wake katika ngazi zote za utoaji wa huduma za Afya,"amesema Dkt. Mollel. 

Amesisitiza kuwa, Serikali itaendelea kuimarisha upatikanaji wa huduma za Afya nchini kwa kuboresha miundombinu ikiwemo kuweka vifaa tiba vya kisasa, kuajiri Wataalamu wa Afya pamoja na kuwapandisha madaraja ili kuongeza morali ya kuendelea kutoa huduma kwa wananchi.

Akijibu swali la nyongeza Dkt. Mollel amesema, Serikali imepeleka vifaa vyenye thamani ya shilingi Bilioni 3 katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara - Kwangwa vitavyosaidia kutatua changamoto ya wananchi kwenda mikoa ya mbali kutafuta huduma hizo.

Ameendelea kusema kuwa, ifikapo Desemba 12, 2022 hospitali hiyo itaanza kutoa huduma zote, huku akisisitiza tayari CT-SCAN imeshafungwa na MRI ikisubiri chumba kikamilike ili huduma hiyo nayo ianze kuwanufaisha wananchi wa Mkoa wa Mara na nchi za jirani.

Sambamba na hilo, Dkt. Mollel amesema, Serikali imejipanga katika udhibiti wa dawa kwa kutengeneza mfumo mzuri kutoka zinapotoka ngazi ya taifa mpaka zinapofika katika kituo husika, huku akisisitiza ushirikiano baina ya viongozi, kamati za afya na wananchi katika kusimamia dawa ili ziweze kuwafikia walengwa. 

Pia, ameelekeza hospitali kutumia mapato ya ndani kutatua changamoto za dawa endapo zitajitokeza ili kutatua changamoto hizo kwa wagonjwa wanaoenda kupata huduma katika maeneo hayo ya kutolea huduma. 

MTUMISHI KUKATWA MSHAHARA


BARAZA LA MADIWANI LATOA ADHABU KWA MTUMISHI WA HALMASHAURI KUKATWA MSHAHARA.

BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha limemchukulia hatua Mhandisi wake Brighton Kishoa kwa kumkata asilimia 15 ya mshahara kwa kipindi cha miaka mitatu baada ya kushindwa kusimamia mradi wa ujenzi wa nyumba ya mtumishi.

Akitoa maazimio ya kikao hicho cha baraza la madiwani cha robo mwaka Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Musa Ndomba alisema kuwa mtumishi huyo alisababisha mradi huo kuwa na gharama kubwa.

Ndomba alisema kuwa moja ajenda iliyojadiliwa na baraza hilo ni makosa ya kinidhamu ya kiutumishi yaliyofanywa na Mhandisi huyo wa Halmashauri hiyo ambaye hakufuata utaratibu wa manunuzi (BOQ) ya ujenzi wa nyumba hiyo.

"Kutokana na kutofuata taratibu za manunuzi kulitokea changamoto kwenye ununuzi wa vifaa kwani haukufuata bajeti iliyopangwa hivyo gharama za ujenzi kuwa kubwa,"alisema Ndomba.

Alisema baada ya changamoto hiyo kutokea ilibainika kuwa katika usimamizi wa miradi ilionekana kuna maeneo kafanya uzembe hivyo baraza la madiwani na kamati ya fedha ziliamua kumchukulia hatua za kinidhamu.

"Taratibu zote zimefuatwa kwa kamati za uchunguzi na kufanya kazi yake na zikapendekeza adhabu hiyo na hilo litakuwa fundisho kwa watumishi wengine kwa kutakiwa kufanya kazi kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazowaongoza," alisema Ndomba.

Aidha alisema kuwa anawakata watumishi wote kuanzia Halmashauri hadi kwenye Mtaa kufanya kazi kwa kuzingatia sheria na wasipingane na miongozo ya kazi zao kwani miradi ya maendeleo itakuwa haina tija na kurudisha nyuma utoaji huduma kwa wananchi.

"Sisi kama baraza hatutarudi nyuma kwani tutachukua hatua kali kadiri inavyowezekana kwa mtumishi yoyote atakayeonyesha utovu wa nidhamu katika utendaji kazi wake na tutatoa adhabu kali zaidi kwa mtumishi atakayekwenda kinyume na taratibu za kazi yake na kuzorotesha utoaji huduma kwa makusudi,"alisema Ndomba.

Alibainisha kuwa hawapendi kutumia muda mwingi kujadili mtu bali wanapenda muda mwingi wautumie kujadili masuala ya kuwaletea maendeleo wananchi.


RC MADARASA YAKAMILIKE


MKUU WA MKOA ATAKA MADARASA YAKAMILIKE NOVEMBA 20

Na Wellu Mtaki, Dodoma

MKUU wa mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule amewataka wakuu wa shule zote waliokabidhiwa fedha za ujenzi wa madarasa katika mkoa wa Dodoma kukamilisha miradi hiyo ifikapo Novemba 20 mwaka huu.

Senyamule ameyasema hayo Jijini Dodoma wakati wa ziara ya kutembelea baadhi ya shule kuona muendelezo wa hatua zilizofikiwa katika shule hizo huku akifafanua kuwa Rais Samia Suluhu Hassan alitoa fedha kwa ajili ya kuwawezesha watoto wanaokwenda kidato cha kwanza mwaka 2023 wasikose madarasa ya kusomea.

Amesema kuwa mkoa wa Dodoma ulipata shilling billion 6.7 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 339 ambapo fedha hizo zimegawanywa katika shule mbalimbali mkoani hapo.

Aidha amewataka walimu wa Shule ya Sekondari Zuzu kuongeza juhudi ya ufundishaji katika shule hiyo ili kuongeza ufaulu kwa wanafunzi.

Kwa upande wake Mkuu wa Shule ya Sekondari Zuzu Hezron Lupondo amesema kuwa shule yake ilipata shilingi milioni 20 kwa ajili ya ujenzi wa chumba kimoja cha darasa na ofisi huku akimuhakikishia Mkuu wa mkoa wa Dodoma kuwa watafanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha ujenzi huo pamoja na kuongeza ufaulu katika shule hiyo.

Naye Mkuu wa shule ya Sekondari Mnadani Claudian Kabuyombo amesema kuwa anaishukuru Serikali ya Awamu ya sita kwa kuendelea kuimarisha sekta ya elimu.

BODI YA WAHANDISI YASEMA MIRADI YA KIMKAKATI IMEWAONGEZEA UJUZI

Na Wellu Mtaki, Dodoma

BODI ya Wahandisi Nchini (ERB) imesema kuwa uwepo wa miradi mikubwa ya kimkakati inayotekelezwa hapa nchini imekuwa na manufaa kwa Wahandisi wazawa hasa vijana kupata ujuzi na teknolojia mpya.

Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma wakati akielezea shughuli mbalimbali za Bodi hiyo na mwelekeo wa utekelezaji wake kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023 Msajili wa Bodi hiyo Mhandisi Bernard Kavishe amesema kuwa miradi hiyo imekuja na teknojia mpya kabisa.

Mhandisi Kavishe amesema kuwa kwa sasa Tanzania inakadiriwa kuwa na jumla ya Wahandisi 33,773 kati yao 26,000 wapo katika soko la ajiri huku wenye leseni za Uhandisi wakiwa ni 10,000 na wengi wao wanashiriki kwa namna moja au nyingine katika utekelezaji wa miradi hiyo mikubwa inayoendelea.

Amesema kuwa malengo ya Bodi hiyo ni kuongeza ushiriki wa bidhaa za ndani (Local content) katika miradi yote inayoendelea hapa nchini ambapo matarajio makubwa ya Bodi hiyo ni kujenga kituo Cha Umahiri Jijini Dodoma.

Aidha amesema kuwa kutokana na kuwepo kwa Vijana wengi wenye mawazo ya kibunifu ila wanakosa namna ya kuendeleza mpaka kufika sokoni hivyo kituo hicho kitakuwa eneo sahihi la kuendeleza mawazo hayo.

Kwa upande wake Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari Maelezo Gerson Msigwa amesema kuwa kwa sasa nchi ina miradi mingi hivyo Bodi ya Wahandisi ina nafasi kubwa katika kutoa ushauri wa namna nzuri ya kutekeleza miradi hiyo kwa uhakika.




Thursday, November 10, 2022

PSSSF YAPATA FAIDA KUBWA


PSSSF YAPATA FAIDA YA MABILIONI.

Na Wellu Mtaki, Dodoma

KWA mwaka wa fedha ulioishia Juni 2022 mfuko wa PSSSF umepata faida ya uwekezaji kiasi cha shilingi bilioni 581.7.

Hayo yameelezwa na CPA Hosea Kashimba Mkurugenzi mkuu Psssf wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu maendeleo ya mfuko huo.

Kashimba amesema kutokana na uwekezaji huu,mfuko hupata faida ya uwekezaji ( return on investment) wastani wa asilimia 8 kwa mwaka,ambayo ni juu ya mfumuko wa bei na hivyo kufanya uwekezaji huu kuwa na tija.

Amesema kuwa mfuko wa Psssf ni mmoja ya waendelezaji milki (real estate developers) wakubwa nchini,mfuko unamiliki majengo ya kupangisha katika miji mbalimbali ambayo hutumika kwa shughuli za kibiashara asilimia 72,ofisi na makazi asilimia 98.

Aidha amesema kuwa wakati wa kuunganisha mifuko psssf ilirithi madeni ya serikali yaliyohakikiwa yenye thamani ya Tsh 731.40 bilioni,mpaka sasa kiasi cha Tsh 500 bilioni kimelipwa na serikali.

“Nirudie kuishukuru serikali ya awamu ya sita kwa kutambua deni la michango kabla ya 1999 maarufu kama (pre 99 liability) ambalo ni shilingi trilioni 4.6 kwa kutoa hati fungani maalum zenye thamani ya shilingi trilioni 2.1 haya yote yanaleta matumaini ya kuwa na mfuko wenye ustahimilivu na endelevu kwa ustawi wa wanachama,”amesema Kashimba.

Alibainisha kuwa wakati wa kuunganisha mifuko,kiasi kilichokuwa kinalipwa kama pensheni kwa mwezi kwa wastaafu kilikuwa shilingi bilioni 34 lakini mpaka kufikia sasa wastani wa kiasi cha shilingi bilioni 60 kinalipwa bila kukosa kwa wastaafu zaidi ya 150,000 kila ifikapo tarehe 25 kila mwezi.

"Mfuko umewekeza shilingi trilioni 4.5 katika hatifungani za serikali,pamoja na kuleta faida ya uwekezaji kwa mfuko kupitia riba na uwekezaji huu unauwezesha mfuko kutekeleza majukumu yake ya msingi,"amesema Kashimba.

Amesema vilevile mfuko umewekeza zaidi ya shilingi bilioni 500 katika soko la hisa la DSM kupitia makampuni mbalimbali yaliyoorodheshwa,uwekezaji huu mkubwa wa mfuko unasaidia kukuza soko la mitaji nchini na kuchochea uchumi na maendeleo ya mwananchi mmoja mmoja.

“Zaidi ya bilioni 400 zimewekezwa katika amana za muda (fixed deposit) katika benki mbalimbali hapa nchini,uwekezaji huu pia kwa mabenki kutoa mikopo mbalimbali kwa Watanzania na hivyo kuharakisha azma ya serikali kukuza uchumi na kuinua,”amesema Kashimba.

Kwa upande wake Msemaji mkuu wa serikali Ndg.Gerson Msigwa amewapongeza Psssf kwa taarifa za kukua kwa mfuko kwa asilimia 8 na kusema ni jambo zuri na inaonyesha jinsi gani mfuko umeweka mazingira mazuri kwa wanachama.

Msigwa amesema kuwa amepata nafasi ya kutembelea ofisi za Psssf na ameridhishwa na namna ambavyo mfuko unafanya kazi zake na kuimarisha huduma kwa wafanyakazi,pia wafanyakazi ni muhimu kufuatilia michango yao inapowasilishwa na kujiridhishwa.


Wednesday, November 9, 2022

RC ASHIRIKI MSIBA WA MTUMISHI MDH ALIYEFARIKI AJALI YA NDEGE


MKUU WA MKOA WA DODOMA MAZISHI MTUMISHI MDH ALIYEFARIKI AJALI YA NDEGE.

Na Wellu Mtaki, Dodoma

MKUU wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule ameshiriki ibada ya mazishi ya Marehemu Neema Samwel aliyefariki kutokana na ajali ya ndege ya Precision Air Mkoani Kagera ambapo mazishi hayo yaliofanyika nyumbani kwao Ilazo Jijini Dodoma.

Marehemu Neema alikuwa anafanya kazi shirika  (Management and Development for Health) (MDH) ambapo alikuwa anaelekea kwenye ziara ya kikazi mkoani Kagera na kukutwa na umauti.

Senyamule  ameshiriki ibada ya mazishi na kuwapa pole familia ya Marehemu akiwemo mume wa Marehemu,wazazi na ndugu wa Marehemu Kwa kupatwa na msiba huo.

Aidhaa Senyamule amesema kuwa mkoa wa Dodoma umepatwa na misiba miwili kati ya waliofariki kwenye ajali hiyo ambapo Serikali ya Dodoma iliwajibika kushiriki msiba mwingine uliofanyika Wilayani Kondoa.

"Nafahamu Watanzania wengi tumeumia na msiba huu lakini kama mnavyofahamu kuwa Rais Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo tuhakikishe tunashirikiana na tunawapumzisha wenzetu walio tangulia mbele za haki ndio maana nami nipo hapa kuwakilisha Serikali kama tulivyoelekezwa na Rais hivyo nawapa pole wazazi, mume na ndugu kwa msiba mzito uliowapata kubwa ni kuhakikisha tunaendelea kuwaombea katika sala zetu za kila siku,"amesema Senyamule

Pia Sinyamule ametoa pole nyingi kwa shirika la (MDH) kwa kuwapoteza wafanyakazi wengi katika ajali hiyo ya ndege na amesema shirika hilo limekuwa likishirikiana  na serikali kufanya kazi mbalimbali za afya hapa nchini.

Neema Samwel alizaliwa Oktoba 26 mwaka 1994 ambapo alifariki katika ajali ya Ndege ya shirika la Precision Air iliyotokea Novemba 6 ziwa Victoria Bukoba Mkoani Kagera na kusababisha vifo vya watu 19 huku watu 26 wakinusurika kwenye ajali hiyo.

WADAU WATAKIWA KUDHIBITI VITENDO VYA UKATILI

PUNGUZENI VITENDO VYA UKATILI WA KIJINSIA MIMBA ZA UTOTONI

Na Wellu Mtaki, Dodoma

MKURUGENZI wa shirika la Kivulini linalojishughulisha na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia na mimba za utotoni Yasini Ally amesema kuwa hali ya vitendo vya ukatili na mimba za utotoni katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ipo kwa kiwango cha juu hivyo serikali na wadau wote hawana budi kushirikiana ili kuweza kukabiliana na tatizo.

Ally amesema hayo Jijini Dodoma alipokuwa akifanya mahojiano na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari juu ya utendaji kazi wa shirika lake.

Amesema kuwa Utafiti uliofanywa na shirika hilo umebaini katika kipindi cha mwaka 2015/ 2016 vitendo vya ukatili wa kijinsia ulikuwa wa hali ya uu ambapo mkoa wa Shinyanga ni asilimia 78, mkoa wa Mwanza asilimia 60 , mkoa wa Kigoma asilimia 61 na mkoa wa Mwanza pia una asilimia 25 kwa vitendo vya mimba za utotoni.

Aidha amefafanua kwamba hali hiyo pia inaweza kusababishwa pale jamiii ya kanda ziwa inapokuwa na hali nzuri ya kiuchumi kwa mfano wakati wa mavuno baadhi ya watu hutelekeza familia na kwenda kwenye mambo ya starehe.

Mkurugezi huyo ameongeza kuwa shirika Ilo limefanya kazi kubwa ya kujenga uwezo kwa klabu za wanafunzi Ili kudhibiti mimba za utotoni.


Friday, November 4, 2022

LAINI 58.1 ZASAJILIWA


WATUMIAJI WA SIMU WAONGEZEKA NCHINI 

Na Wellu Mtaki, Dodoma

SEKTA ya Mawasiliano ya Simu nchini imeendelea kukua hadi kufikia Septemba 2022 kulikuwa na laini za simu za milioni 58.1 idadi hiyo inahusisha laini zinazotumiwa na watu pamoja na zinatotumiwa kwa ajili ya Mashine (M2M).

Aidha takwimu zinaonesha mikoa mitano inayoongoza nchini kuwa na idadi kubwa ya laini za simu zinazotumika (Active SIM-Cards) hadi kufikia Septemba mwaka huu ni Dar es Salaam laini milioni 9.7, Mwanza milioni 3.7, Arusha 3.4, Mbeya 3.08 na Tabora 3.06.

Akizungumza jiijini Dodoma wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo ,Dk. Jabir Bakari amesema kuwa wanawatoa huduma sita kwenye soko lao ambao ni Airtel, Vodacom, Halotel, Ttcl, Tigo na Smile.

Dk. Bakari ameeleza kuwa mgawanyo wa asilimia za soko kwa kila mtoa huduma ni kwamba Vodacom asilimia 30, Airtel asilimia 28, Tigo asilimia 26, Halotel asilimia 13, Ttcl asilimia 3 na Smile asilimia 0.

Mkurugenzi huyo amesema kuwa takwimu zinaonesha matumizi ya Intaneti yameongezeka kwa asilimia 4.2 kutoka milioni 29 hadi kufikia 31. 12 mwezi Septemba mwaka huu.

Amefafanua kuwa ongezeko la matumizi ya Intaneti limechangiwa na matumizi ya kiswahili na kwamba maudhui hayo kwenye Intaneti yanaongezeka kwa kasi na program tumizi (applications), kwa lugha ya kiswahili nazo zimeongezeka.


KITUO CHA TAALUMA USAFIRI WA ANGA


KITUO CHA TAALUMA USAFIRI WA ANGA KUBORESHWA

Na Wellu Mtaki, Dodoma

TAKRIBANI shilingi bilioni 49 zimekopwa tutoka benki kuu ya Dunia kwa ajili ya kituo cha umahiri cha mafunzo ya taaluma za usafiri wa anga kwa ajili wa utekelezaji wa miundombinu ya chuo hicho.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa chuo cha taifa cha usafirishaji (NIT) Prof.Zacharia Mganilwa wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma kuhusu taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya chuo hicho na vipaumbele vyake kwa mwaka wa fedha 2022/23.

Mganilwa amesema kuwa fedha hizo zimegawanyika katika upande wa ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya kufundishia wataalam ambapo jumla ya majengo matano yatajengwa Dar- es Salaam kwa gharama ya shilingi bilioni 21 na baadaye kujenga majengo mkoa wa kilimanjaro kwa sababu lazima marubani wafundishwe ndani ya viwanja vya ndege.

Amesema kuwa chuo kimenunua ndege mbili zenye injini moja za mafunzo ambazo ziko njiani zinatazamiwa kuletwa Tanzania kwa gharama ya shilingi dola za Marekani milioni 12 huku akieleza kwamba kumfundisha rubani mmoja nje ya nchi ni shilingi milioni 200 hivyo Serikali inapofanya uwekezaji huu inalifanya shirika la ndege nchini kuleta matumaini ya nchi katika kukuza utalii na uchumi kwa sababu wataalam wa usafiri wa anga watafundishwa hapa hapa nchini.

Aidha amesema kuwa Tanzania ina zaidi ya ndege 400 zilizosajiliwa na mamlaka ya usafiri wa Anga ambapo asilimia 60 ya marubani ni wageni,hivyo ndege hizi zitakapofika vijana wa kitanzania wenye sifa za kusomea urubani watafundishwa na kupata ajira ndani ya nchi.

Ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2022/23 chuo kinanunua tena ndege yenye injini mbili kwa ajili ya mwanafunzi kukamilisha mafunzo yake kwa sababu mafunzo ya urubani yanamtaka mwanafunzi ajifunze ndege yenye injini moja na injini mbili.

NIT watawawezesha vijana wengi kunufaika na miradi mikubwa inayoendelea nchini mathalani ndege tano zinatarajiwa kuja nchini,ambapo kwa mwaka 2023 ndege nne zitaingia nchini.


Thursday, November 3, 2022

WIZARA AFYA KUDUMISHA HUDUMA ZA AFYA


WATUMISHI KUWA WAKUTOSHA KWENYE VITUO VYA KUTOLEA HUDUMA ZA AFYA.

Dodoma,

Katibu Mkuu,Wizara ya Afya Prof. Abel Makubi amesema Wizara ya Afya inaendelea kuimarisha huduma za afya kwa kuwa na watumishi wa kutosha kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Prof. Makubi amesema hayo leo tarehe 3 Novemba, 2020 wakati wa kikao cha Sekretarieti ya maandalizi ya Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote na Menejimenti ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI ikiwa ni kuelezea hatua iliyofikiwa pamoja na nini kifanyike kama sekta moja endapo Muswada huo utapitishwa na Bunge na kuwa Sheria.

Aidha, Prof. Makubi amesema Wizara ya Afya inaendelea kuboresha upatikanaji wa Dawa, vifaa tiba na vipimo kwenye vituo vya kutolea huduma za afya ili huduma zinazotolewa ziwe bora.

"Afya ni kitu muhimu na ndio haki ya kwanza ambayo Mungu amempa Mwanadamu hivyo kila mmoja lazima athamini uhai wake kwa kuwa na Bima ya Afya".

Hata hivyo Katibu Mkuu huyo alisema dhana ya bima ya afya kwa wote ni kuchangiana pindi mmoja anapougua aweze kupata matibabu bila kuwa na kikwazo cha fedha.

Naye, Naibu Katibu Mkuu-Afya kutoka TAMISEMI Dkt. Grace Magembe amesisitiza utoaji wa elimu kwa wananchi ngazi zote ili waelewe zaidi dhana nzima ya Bima ya Afya kwa Wote.

HUDUMA ZA NDEGE ZAONGEZEKA NCHINI.

VIWANJA VYA NDEGE VYAONGEZA HUDUMA ZA NDEGE NCHINI.


Na Wellu Mtaki, Dodoma

JUMLA ya ndege 40,323 zilihudumiwa katika kipindi cha mwaka 2021/2022 ikilinganishwa na huduma iliyotolewa mwaka 2020/2021 sawa na ongezeko la asilimia 13. 

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Huduma za Utabiri - Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Hamza Kabelwa wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu majukumu ya Mamlaka hiyo na mwelekeo wa utekelezaji kwa mwaka wa Fedha 2022/23 katika Ukumbi wa Idara ya Habari MAELEZO Novemba 2, 2022 Jijini Dodoma.

Dkt Kabelwa amesema kuwa sekta ya usafiri wa anga inaendelea kukua kutokana na kuzingatiwa kwa mfumo wa kudhibiti ubora wa huduma na ongezeko hilo linatokana na jitihada za kuifungua nchi zinazofanywa na serikali, pamoja na kuendelea kukidhi viwango vya Kimataifa na kuihakikishia dunia usalama wa anga la Tanzania katika masuala ya hali ya hewa kwa ndege zote za kimataifa.

Amesema kuwa mamlaka hiyo katika mwaka 2021/22 iliendelea na utengenezaji wa rada mbili zitakazofungwa katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA) na cha Jiji la Dodoma ambao umefikia asilimia 45.

Ameongeza kuwa Mamlaka imeendelea kutekeleza kwa ufanisi majukumu yake iliyopewa na Shirika la Hali ya Hewa Duniani ya kuwa Kituo cha kutoa mwongozo wa utoaji wa utabiri wa hali ya hewa kwa nchi za ukanda wa Ziwa Victoria (Regional Specialized Meteorological Centre) kwa nchi zilizopo Afrika Mashariki.

Kwa upande wake Msemaji Mkuu wa Serikali na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari Maelezo Gerson Msigwa ametoa wito kwa Wananchi kujenga utaratibu wa kutumia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania.

Majukumu ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA)yamegawanyika katika sehemu kuu tatu ambapo sehemu ya kwanza ni kutoa huduma za hali ya hewa; sehemu ya pili ni kudhibiti shughuli za hali ya hewa hapa nchini kwa mujibu wa Kifungu cha (14) na sehemu ya tatu ni kuratibu shughuli za hali ya hewa nchini Tanzania kulingana na Kifungu cha (5) cha Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na.2 ya Mwaka 2019.

Mwisho