Thursday, July 27, 2017

SAMATTA ASAIDIA JEZI CHAMA CHA SOKA KIBITI


                                     Na John Gagarini, Kibaha

CHAMA Cha Soka wilaya ya Kibiti (KFA) mkoa wa Pwani kimemshukuru mwanasoka anayecheza soka la kulipwa kwenye timu ya KRC Genk ya Ubelgiji Mbwana Samatta kwa kuwapatia jozi za jezi kwa ajili ya washindi wa ligi daraja la nne.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi katibu wa chama hicho Rashid Mkinga alisema kuwa wanashukuru msaada huo utakaozisaidia timu zitakazoshinda na kuwakilisha wilaya hiyo kwenye mashindano ya mkoa.

Mkinga alisema kuwa waliandika barua kwa Samata kwa ajili ya kuomba vifaa mbalimbali vya michezo ambapo aliwajibu na kusema kuwa atawapatia.

“Samatta kwa kupitia mwakilishi wake Said Ngulupi alitupatia jozi ya seti tatu ambazo tutawakabidhi washindi watatu wa juu ambao ni wawakilishi wa wilaya yetu,” alisema Mkinga.

Alisema kuwa hawana cha kusema zaidi ya kushukuru kwa msaada huo mkubwa aliowapatia licha ya yeye kuwa mbali lakini anathamini vijana wenzake ambao wanacheza soka hapa nchini.

“Tunamshukuru Samatta kwa mchango wake kwani awali tulikuwa hatuna zawadi za kuwapa washindi zaidi ya kombe kwa ajili ya mshindi wa kwanza kwani ametukomboa kwa kutupa msaada huo,” alisema Mkinga.

Aidha alisema kuwa mpira unachezwa kama kawaida na kuna amani kubwa siyo kama watu wanavyofikiria kwani ulinzi uko wa kutosha na hadi sasa hakuna tukio lolote la kutishia lililotokea.

“Kupitia michezo amani imetawala na hakuna vurugu zozote au tishio lolote la kutishia amani hivyo watu wasiwe na wasiwasi kwenye wilaya yetu ambayo ilikumbwa na mauaji na kuwafanya watu kuwa na hofu,” alisema Mkinga.

Alibainisha kuwa ligi ya Kibiti ndiyo yenye timu nyingi ndani ya mkoa wa Pwani ambapo kwenye ligi daraja la nne jumla ya timu 19 zinachuana na timu zilizosajiliwa ni 31 na bado kuna zingine zinahitaji usajili.


Mwisho.  

No comments:

Post a Comment