Thursday, July 27, 2017

MJI KIBAHA KUJENGA STENDI YA KISASA KWA MABILIONI

Na John Gagarini, Kibaha

HATIMAYE Halmashauri ya Mji Kibaha mkoani Pwani imeanza mradi wa ujenzi wa stendi ya kisasa wenye thamani ya shilingi billion 3.4.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha ofisa habari wa Halmashauri hiyo Innocent Byarugaba amesema kuwa stendi hiyo itaondoa tatizo la mji huo kutokuwa na stendi ya uhakika kwa kipindi cha takribani miaka 40.

Byarugaba alisema kuwa stendi ambayo inatumika kwa sasa ni ndogo na imejengwa kwenye hifadhi ya barabara na ambapo iko ndani ya mita 60 ikitakiwa kuondolewa na ina hudumia mabasi ya mikoa 24.

“Stendi mpya mara itakapokamilika inatarajiwa kuwa na uwezo wa kuhudumia mabasi 60 kwa wakati mmoja na itajengwa kipindi cha miezi sita na kukamilika mwishoni mwa mwaka huu au Januari mwakani,” alisema Byarugaba.

Alisema kuwa fedha zinazotumika kwenye ujenzi huo ni ufadhili kutoka benki ya dunia kupitia benki kuu ya Tanzania kwenye mradi wa uendelezaji wa Miji (ULGSP) unaoendeshwa kwenye miji 18 hapa nchini.

“Stendi itakuwa na miundombinu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kituo cha polisi, ofisi za mabasi, sehemu ya texi, Bajaji, pikipiki, huduma ya vyoo, vibanda vya kupumzikia abiria, Atm, kituo cha mafuta,gereji, hoteli na kizimba cha kuhifadhia takataka na huduma nyingine muhimu,” alisema Byarugaba.

Aliwataka watu wenye viwanja vinavyozunguka stendi hiyo kujenga ambapo ramani iliyopitishwa ni kuanzia ghorofa moja na kuendelea pamoja na wale walioko kwenye eneo la kitovu cha mji kufanya ujenzi kama sheria zinavyowataka.

Aidha alisema kuwa ujenzi huo unafanywa na kampuni ya Group Six International Ltd ambayo ilijenga stendi ya kisasa ya Msamvu mkoani Morogoro chini ya wataalamu washauri Ace Consult, Lupta Consult na Mhandisi.


Mwisho.

No comments:

Post a Comment