Na John Gagarini, Pwani
MVUA zinazoendelea kunyesha hapa nchini zimeendelea kuleta
madhara baada ya Mama na watoto wake wawili kufa huku watu wengine watatu
wakijeruhiwa baada ya kupigwa na radi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu
ofisa mtendaji wa kata ya Mchukwi wilaya ya Rufiji mkoani Pwani Ami Lipundundu
alisema kuwa familia hiyo ilikuwa ikiota moto baada ya kuchota maji ya mvua.
Lipundundu alisema kuwa tukio hilo lilitokea Januari 18 mwaka
huu majira ya saa 11 jioni kwenye Kijiji cha Mchukwi B walipokuwa wanaota moto
baada ya mvua kunyesha.
Aliwataja marehemu hao kuwa ni Decilia Simba (42) watoto wake
Debora Simba (4) na Amani Matimbwa 1 na nusu huku waliojeruhiwa wakiwa ni Maua
Ngwande (13) anayesoma darasa la sita shule ya Msingi Mchukwi, Suzana Daudi (12)
na mdogo wa marahemu aitwaye Mama Tariq.
“Marehemu alitoka kwenye kikundi cha kuweka na kukopa cha Jitegemee
ambapo yeye ni mwanachama alipofika nyumbani mvua ikaanza kunyesha akawa
anakinga maji ya mvua yeye na watoto wa ndugu yake,” alisema Lipundundu.
Alisema kuwa baada ya hapo waliwasha moto kwenye jiko lao
ambalo liko jirani na mti wa Mfenesi na kuota kwani walikuwa wameloa ndipo radi
ilipopiga ikakwepa mti ikawapiga wao.
“Marehemu na wanawe walifia njiani wakati wakipelekwa
Hospitali ya Mchukwi kwa ajili ya matibabu ambapo majeruhi bado wamelaazwa
hopsitalini hapo na hali zao zinaendelea vizuri,” alisema Lipundundu.
Aidha alisema kuwa wiki iliyopita mtu mmoja naye alifariki
kwa kupigwa na radi na mwishoni mwa mwaka jana huko Ikwiriri mtu mmoja pia alifariki
dunia. Polisi mkoa wa Pwani walithibitisha kutokea kwa tukio hilo la
kusikitisha.
Mwisho.