Saturday, December 24, 2016

FAMILIA YA WATU SABA WASIOONA YASAIDIWA

 FAMILIA ya Watu saba wasioona
Na John Gagarini, Kibaha
JUMUIYA ya Maili Moja A ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Usharika wa Maili Moja imetoa misaada ya nguo na vyakula kwa familia yenye wasioona saba inayoishi kwenye Mtaa wa Simbani wilayani Kibaha mkoani Pwani.
Akizungumza na gazeti hili mara baada ya kukabidhi misaada hiyo ambayo ilipelekwa na Jumuiya hiyo mwenyekiti Jacob Samson alisema kuwa waliamua kupeleka misaada hiyo baada ya kupata taarifa za familia hiyo.
Samson alisema kuwa wametoa misaada hiyo pia ni katika kuwafanya nao waweze kusherehekea siku kuu ya X- Mass na wenzao wakiwa na furaha hasa ikizingatiwa wao ni wahitaji na wanahitaji misaada mbalimbali.
“Tunaamini kusaidia jamii zenye mahitaji ni ibaada kamili na inawatia moyo na kujiona kuwa hawako peke yao kwani kuna watu wanawaunga mkono na kushiriki nao kwa pamoja,” alisema Samson.
Alisema kuwa Jumiya yao hufanya ibaada za nyumba kwa nyumba ambapo hutembeleana na kushirikiana kwenye masuala mbalimbali ya kijamii pamoja na ya kiimani.
“Jumuiya yetu iko kwa ajili ya kusaidiana kwenya matatizo na furaha hivyo wanajumuiya walisema kuwa twende kwenye hiyo familia iwe sehemu ya ibaada ya yetu ya kila Jumamosi ili kuwafariji na wamejitolea sana ili kuhakikisha familia ile nayo inafurahia kipindi hichi cha mwisho wa mwaka,” alisema Samson.
Aidha alisema kuwa wanaomba watu wengine nao wajitokeze kuisaidia familia hiyo ambayo ina hitaji misaada mbalimbali kutokana na kuwa kwenye mazingira magumu.
“Kutoa ni moyo na si utajiri kwani watu wenye moyo wanapaswa kwenda kuwasaidia kwa jambo lolote la kijamii hasa ikizingatiwa familia hiyo inasimamiwa na mwanamke ambaye alitengana na mumewe,” alisema Samson.
Kwa upande wake mama wa familia hiyo Mwajuma Maulid alisema kuwa anaishukuru Jumuiya ya maili Moja kwa kuwapatia misaada hiyo ambayo wameitoa kwani wameonyesha moyo wa kipekee.
Maulid alisema kuwa vyakula vilivyotolewa vitawasaidia katika kusherehekea sikukuu ya X-Mass kwa furaha kama wanavyofurahia watu wengine na kuwataka watu wengine waendelee kuwasaidia.
“Tuko kwenye mazingira magumu sana kwani hali yetu si nzuri ambapo tunaishi maisha ya kubahatisha kwa hiyo wanapokuja watu kama hawa na kutupa misaada tunashukuru sana,” alisema Maulid.
Familia hiyo inaishi mtaa wa Simbani kata ya Kibaha ina watu saba ambao hawaoni ambapo wasioona ni mume wake ambaye walitengana,watoto wanne wasioona na  wajukuu wawili wote hawaoni na inaishi kwa kutegemea kuchoma mkaa na kusuka mikeka.

Mwisho.     

zee wa Kanisa kutoka Jumuiya ya Maili Moja A Samwel Luhembe kushoto akikabidhi sabuni iliyotolewa na jumuiya hiyo ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania KKKT usharika wa Maili Moja anayepokea ni mama wa familia ya watu wasioona saba Mwajuma Maulid kulia  
  Mzee wa Kanisa kutoka Jumuiya ya Maili Moja A Samwel Luhembe kushoto akikabidhi unga uliotolewa na jumuiya hiyo ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania KKKT usharika wa Maili Moja anayepokea ni mama wa familia ya watu wasioona saba Mwajuma Maulid kulia 

Mzee wa Kanisa kutoka Jumuiya ya Maili Moja A Samwel Luhembe kushoto akikabidhi nguo zilizotolewa na jumuiya hiyo ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania KKKT usharika wa Maili Moja anayepokea ni mama wa familia ya watu wasioona saba Mwajuma Maulid kulia 


Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maili Moja A ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania KKKT usharika wa Maili Moja Jacob Samson kushoto akimkabidhi moja ya msaada uliotolewa na Jumuiya hiyo kwa familia ya watu saba wasioona anayepokea ni Mwajuma Maulid ambaye ndiye mama anayeihudumia familia hiyo

Wednesday, December 14, 2016

MSOGA KUJENGA UWANJA WA KISASA



Na John Gagarini, Msoga

MKOA wa Pwani unatarajiwa kuwa na uwanja wa kisasa ambao utasaidia kukuza soka la vijana na kuinua michezo kwenye mkoa huo ambao umepania kuwa moja ya mikoa itakayolea vipaji.

Uwanja huo unatarajiwa kujengwa kwenye Kijiji cha Msoga kata ya Msoga Halmashauri ya Chalinze wilayani Bagamoyo na serikali ya watu wa China lengo likiwa ni kukuza sekta ya michezo kwa vijana kwenye mkoa na nchi kwa ujumla.

Akizungumza katika hafla maalumu iliyoandaliwa kwa ajili ya kwenda kutembelea eneo ambalo litajengwa uwanja huo Dk Kikwete alisema kwamba uwanja huo wa wa mpira wa miguu utajengwa  kwa ufadhili wa serikali ya watu wa china na kuongeza kuwa  utakuwa ni mkombozi mkubwa katika kukuza na kuinua vipaji kwa vijana wadogo.

“Tumehamasisha wadau wa michezo kujenga uwanja lengo lake kubwa ni kuhakikisha kwamba Tanzania katika siku za usoni inakuwa ni wachezaji wengi wenye vipaji ambao wataweza kuunda timu nzuri ya Taifa ambayo itaweza kufanya vizuri katika mashindano mbali mbali ya Kimataifa,” alisema Dk Kikwete.

“Uwanja huu wa mpira wa miguu pindi utakapokamilika utaweza kuwa ni mkombozi mkubwa wa vijana wadogo hususan wale wa shule, hivyo nimeshazungumza na rafiki zetu wa serikali ya china na wamekubali kutujengea kwa hivyo ni jambo la msingi sana katika kuendeleza sekta ya michezo kwa watoto wetu hawa mbao wataweza kuleta mafanikio makubwa katika siku zijazo,”allisema Kikwete.

Dk Kikwete alisema kuwa anaipongeza serikali ya china kwa kuona umuhimu wa kusaidia kujenga kiwanja hicho, na kuongeza kuwa pindi kitakapokamilika kitakuwa na michezo mingine ambayo itakuwa ikifanyika mbali na mchezo huo wa soka lengo ikiwa ni kuwapa fursa vijana kuweza kuonyesha vipaji walivyonavyo.

Naye Mwakilishi wa balozi wa China nchini Tanzania Yang Tong aliahidi kuendelea kutoa ushirikiano wa dhati katika kukuza sekta ya michezo hususani kwa  vijana wadogo ikiwa ni sambamba  na kujenga viwanja ili watoto wasiweze kucheza katika viwanja vya vumbi.

Naye Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kwamba lengo lake kubwa ni kuhakikisha anakuza michezo wa vijana wadogo katika jimbo lake hivyo kukamilika kwa ujenzi wa uwanja huo kutaweza kuwasaidia vijana  kukuza vipaji vyao.

Nao baadhi ya wadau wa mchezo wa soka katika kijiji hicho cha Msoga akiwemo Michael James pamoja na Mohamed Halfan wamempongeza Rais mstaafu Dk Jakaya Kikwete kwa ubunifu wa ujenzi huo wa uwanja kwa ajili ya vijana wadogo kwani kutaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kuleta mabadiliko chanya katika michezo ukiwemo wa soka.

Mwisho.

CCM WAANZA MCHAKATO WA KUMPATA MGOMBEA UDIWANI MISUGUSUGU

Na John Gagarini, Kibaha

RAMADHAN Bogas ameshinda kura za maoni za kumpata mgombea udiwani kata ya Misugusugu kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya kupata kura 43 huku aliyeshinda udiwani kabla ya mahakama kutengua matokeo Addhu Mkomambo akiambulia kura mbili.

Uchaguzi huo ambao ulifanyika Misugusugu ulisimamiwa na Yusuph Mbonde, Selina Wilson na Mohamed Mpaki ambao ni wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM wilaya, ulihusisha wagombea saba.

Akizungumza na waandishi wa habari katibu wa CCM Kibaha Mjini Abdala Mdimu alisema kuwa kura zilizopigwa zilikuwa 115 na hakuna kura iliyoharibika.
Mdimu akitaja matokeo alisema kuwa mshindi wa pili alikuwa Eliasi Masenga aliyepata kura 37, Ramadhan Mataula aliyepata kura 15 huku Salumu Mkali akipata kura 14, huku watano akiwa Mkomambo aliyepata kura mbili, Francis Alinamiswe alipata kura mbili na Laurence Likuda naye kura mbili.

Alisema kuwa bado vikao mapendekezo vinaendelea kukaa ambapo jana kilitarajiwa kukaa kikao cha kamati ya siasa ya kata ambapo leo kikao cha kamati ya Usalama na maadili wilaya kinakaa.

“Desemba 16 kamati ya siasa ya wilaya itakaa na baadaye vitaendelea vikao vya mkoa na Desemba 19 Halmashauri Kuu ya mkoa itafanya uteuzi wa mwisho wa mgombea atakayekiwakilisha chama kwenye uchaguzi huo,”alisema Mdimu.

Uchaguzi huo mdogo wa udiwani unarudiwa baada ya mahakama ya mkoa kutengua matokeo kutokana na malalamiko yaliyotolewa na diwani wa Chadema ambapo mgombea wa CCM Addhu Mkomambo alikuwa ameshinda.

Mwisho.      




Monday, December 5, 2016

ZAIDI YA 15 WAFAULU DARASA LA SABA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha

JUMLA ya wanafunzi 15,528 mkoani Pwani wamefaulu kwenda shule za sekondari kwa mwaka 2017 baada ya kufanya mtihani wa kumaliza darasa la saba mwaka huu.

Aidha wanafunzi 9,290 wamefeli sawa na asilimia 37.4 na wanafunzi wote waliofaulu wamechaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari ambapo wamefaulu kwa kupata alama zaidi ya 100 kati yao 288 wamepata daraja la A.

Hayo yamesemwa mjini Kibaha na Kaimu ofisa elimu mkoa wa Pwani Modest Tarimo wakati wa uchambuzi wa matokeo ya mtihani wa kuhitimu eilimu ya msingi mwaka 2016 ya mkoa na kusema kuwa wanafunzi waliofanya mtihani walikuwa ni 24,818.

Tarimo amesema kuwa wanafunzi 2,636 walipata daraja B, wanafunzi 12,604 wamepata daraja C na wote waliopata daraja A na C wote wamechaguliwa kujiunga na sekondari

Amesema kuwa wanafunzi waliokuwa wakitarajiwa kufanya mtihani walikuwani 24,913 ambapo waliofanya walikuwa ni 24,818 wavulana wakiwa ni 11,334 na wasichana walikuwa ni 13,484 sawa na asilimia 99.9.

Ameeleza kuwa ufaulu kwa mwaka huu umeshuka kwani ni asilimia 62.5 ikilinganishwa na mwaka 2015 ambapo ufaulu ulikuwa ni asilimia 63.1 matokeo haya hayaridhishi kwani ufaulu badala ya kupanda lakini umeshuka kwa asilimia 0.5 na kwa matokeo hayo mkoa umeshika nafasi ya 21 kitaifa.

Amebainisha kuwa watahiniwa 95 hawakufanya mtihani sawa na asilimia 0.3 kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoro, wanafunzi 75, mimba mwanafunzi mmoja, vifo 11, ugonjwa wawili na sababu nyingine sita ambapo wadau wanapaswa kupiga vita utoro ambao umepungua 204 ikilinganishwa na mwaka jana.

Kaimu ofisa elimu huyo wa mkoa ambaye ni ofisa taaluma amesema serikali iliweka wastani wa asilimia 80 ya ufaulu kwa shule za msingi ikiwa ni mkakati wa kufikia mpango wa matokeo makubwa sasa BRN ambapo wadau wa elimu wanapaswa kukabiliana na changamoto zinaosababisha ufaulu kushuka.

Naye Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Pwani Edward Mwakipesile amesema kuwa wadau wa elimu wanapaswa kushirikiana na idara ya elimu ya mkoa ili kuhakikisha matokea ya wanafunzi yanakuwa mazuri ambapo kwa mwaka huu yanaonekana kushuka.

Mwakipesile amesema kuwa mbali ya changamoto ya matokeo hayo pia changamoto iliyopo ni vyumba vya madarasa ambavyo ni vichache na kusababisha madawati kukosa sehemu ya kukaa baada ya zoezi la utengenezaji madawati kufanikiwa.


Mwisho.

HALMASHAURI YA CHALINZE YAANZA KUMWAGA FEDHA KWA WAJASIRIAMALI


Na John Gagarini, Chalinze

HALMASHAURI ya Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani imetoa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 79.8 kwa vikundi vya wajasiriamali 26 vya akinamama na vijana kwenye kata za Halmasahuri hiyo.

Aidha fedha hizo zinatokana na asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri ya robo mwaka ambazo ni kiasi cha shilingi milioni 809 yaliyokusanywa katika kipindi hicho.

Akikabidhi baadhi ya vikundi hivyo vya vijana na akaimama kwenye kata ya Msoga ambapo kila kundi linapata asilimia tano kutokana na mapato hayo Mwenyekiti wa Halmashauri Said Zikatimu alisema kuwa fedha hizo zitakuwa zikitolewa kwa kila robo ya mwaka.

Zikatimu alisema kuwa lengo la kutolewa fedha hizo kwanza ni kufuata sheria ambayo inataka asilimia tano ya mapato yote ya Halmashauri wakopeshwe vijana na asilimia tano kwa ajili ya akinamama kupitia vikundi vya vya uzalishaji mali.

“Tunaomba vikundi vyote ambavyo vinakopeshwa fedha hizi wazirejeshe kwa wakati ili ziwe na mzunguko kwa watu wengine na vikundi vihakikishe vinazitumia kwa malengo waliojiwekea na si kuanzisha miradi ambayo hamjaombea mnaweza kushindwa kurejesha,” alisema Zikatimu.

Alisema kuwa fedha hizo siyo msaada bali ni fedha kwa ajili ya kuboreshea shughuli za ujasiriamali na wanapaswa kurejesha kwa wakati ili vikundi vingi viweze kupata fedha hizo ambazo zinatokana na mapato ya ndani yanayotokana na vyanzo mbalimbali.

“Hizi fedha ni kwa ajili ya wananchi wote na hasa wale waliojiunga kwenye vikundi hivyo zitumike kama zilivyoombewa na siyo kununulia nguo au baadhi huzitumia kwa ajili ya kufanyia starehe mkifanya hivyo mtaharibu maana ya mkopo huu na mtashindwa kurejesha na kujikuta mkishtakiwa,” alisema Zikatimu.

Aidha aliyatakama makundi mbalimbali ya vijana na akimama kujiunga na kuanzisha vikundi vingi kwa ajili ya kukopa kwani fedha si tatizo bali ni wao kujiunga kwa wingi fedha ziko za kutosha.

Kwa upande wake ofisa maendeleo ya jamii na ofisa vijana wa Halmashauri ya Chalinze Felista Kizito alisema kuwa vikundi hivyo vilivyopewa fedha hizo vitapewa mwezi mmoja kabla ya kuanza kurejesha marejesho yao.

Kizito alisema kuwa vikundi hivyo vimegawaanyika kwenye shughuli mbalimbali kutegemeana na mazingira yao na vimepewa fedha kati ya shilingi milioni mbili hadi sita kutegemeana na aina ya mradi ambao waliuanzisha.

Naye diwani wa kata ya Msoga Hassan Mwinyikondo alisema kuwa Halmashauri hiyo imefanya jambo kubwa kwa kutoa fedha hizo ambazo zitasaidia kuboresha maisha ya wananchi.

Mwinyikondo alisema kuwa mikopo hiyo ya Hlamashauri ni nafuu na haina masharti magumu kama ilivyo kwa taasisi za kifedha ambazo watu wengi wameshindwa kukopa kutokana na masharti kuwa magumu.

Mwisho.


 Mwenyekiti wa Halmashauri ya Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Said Zikatimu katikati akiwakabidhi hundi kikundi cha ujasirimali cha Wanawake cha Nianjema cha ufugaji wa Mbuzi Kijiji cha Kwa Konje kushoto ni mwenyekiti wa Kijiji hicho Omary Mbwana anayefuatia ni  diwani wa kata ya Kibindu Ramadhan Mkufya akifuatiwa na Ofisa Maendeleo ya Jamii na Ofisa Vijana Halmashauri ya Chalinze Felista Kizito na mwenyekiti wa kikundi hicho Veronica Chusi

 Kushoto Mwenyekiti wa Halmashauri ya Chalinze Said Zikatimu akiwakabidhi hundi ya fedha wana kikundi wa Muungano Mindukene kata ya Talawanda 

Friday, October 21, 2016

WALIBYA WASAIDIA MRADI WA MAJI MKURANGA


Na John Gagarini, Mkuranga

WANANCHI wametakiwa kuwa na utamaduni wa kulipa kodi mbalimbali za serikali ili ziweze kutumika kwa ajili ya maendeleo kama wanavyofanya wananchi wa Libya.

Hayo yalisemwa wilayani Mkuranga na mkurugenzi wa Taasisi ya World Islamic Call Society iliyopo chini ya ubalozi wa Libya hapa nchini Ammara Zaiyani wakati akikabidhi mradi wa kisima cha maji kwenye Kijiji cha Binga–Kisiju.

Zaiyani alisema kuwa fedha ambazo zimesaidia ujenzi wa kisima hicho cha maji ya kunywa chenye thamani ya shilingi milioni 18 zimetokana na kodi za wananchi wa Libya kwa ajili ya kusaidia watu wenye changamoto mbalimbali za kimaendeleo.

“Wananchi wa Libya wanajitolea kuwasaidia wenzao hivyo na nyie mnapaswa kuwa na utamaduni wa kuwasaidia wengine kupitia kwenye malipo mbalimbali ya serikali yenu ambayo ina sema hapa Kazi Tu,” alisema Zaiyani.

Naye mwakilishi wa Ubalozi wa Libya hapa nchini Mohamed Atoumi alisema kuwa serikali ya Libya kupitia taasisi hiyo imekuwa ikipokea maombi mbalimbali na imekuwa ikisaidia kadiri ya uwezo unapokuwepo.

Atoumi alisema kuwa wamekuwa wakisaidia kwenye sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja kwenye huduma za afya, maji na shughuli nyingine za maendeleo lengo likiwa ni kudumisha ushirikiano uliopo na Tanzania.

Kwa upande wake kadhi mkuu wa mkoa wa Pwani Sheikh Hamis Mtupa alisema kuwa wanashukuru kwa msaada huo kwani umesaidia kuwaondolea adha wananchi wa Kijiji hicho ambao walikuwa wakishinda wakitafuta maji ambayo siyo safi wala salama.

Mtupa alisema kuwa wananchi wanapaswa kulinda miundombinu ya kisima hicho ili isiharibike kwani maji hayo ni kwa wananchi wote bila ya kujali dini ya mtu na ni huduma muhimu kwa binadamu.

Naye mkazi wa kijiji hicho Mwanahawa Maulid alisema kuwa wamekuwa wakihangaika kutafuta maji ambayo yanapatikana mbali na wamekuwa wakitumia muda mwingi kusubiria maji.

Maulid alisema kuwa maji waliyokuwa wakiyatumia ni ya kuchimba chini ambayo si salama kiafya na yamekuwa wakiwasababishia magonjwa mbalimbali kama vile kuhara na UTI.

Mwisho.





Mkurugenzi wa Taasisi ya World Islamic Call Society ya Libya tawi la Tanzania Ammara Zaiyani kulia aliyeshika ndoo ya maji baada ya kumtwisha ndoo ya maji Saida Ally mkazi wa Kijiji cha Binga-Kisiju kata ya Dondo wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, kushoto kadhi mkuu wa mkoa wa Pwani Sheikh Hamis Mtupa (Picha na John Gagarini)
Mkurugenzi wa Taasisi ya World Islamic Call Society ya Libya tawi la Tanzania Ammara Zaiyani katikati akielezea jambo kulia ni kadhi mkuu wa mkoa wa Pwani Sheikh Hamis Mtupa na kushoto ni mwakililishi wa balozi wa Libya Mohamed Atoumi wakati wa uzinduzi wa mradi wa maji kwenye Kijiji cha Binga Kisiju- kata ya Dondo wilaya ya Mkuranga mkoa wa Pwani Picha na (John Gagarini)

Mkurugenzi wa Taasisi ya World Islamic Call Society ya Libya tawi la Tanzania Ammara Zaiyani akifungua bomba la maji baada ya uzinduzi wa kisima cha maji kwenye Kijiji cha Binga-Kisiju wilayani Mkuranga mkoani Pwani kushoto kwake ni mwakililishi wa balozi wa Libya Mohamed Atoumi (Picha na John Gagarini)  

      

Monday, October 3, 2016

MWANAMKE ATUMIKA WIZI CWT WALINZI WAWILI WASHIKILIWA

Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la la polisi mkoani Pwani linawashikilia walinzi wawili wa jengo la ofisi ya Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) mkoa baada ya watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kuvunja na kuiba fedha kiasi ambacho bado hakijajulikana na computer za ofisi hizo.

Akizungumzia na waandishi wa habari mjini Kibaha kuhusiana na tukio hilo katibu wa (CWT) Nehemiah Joseph amesema kuwa tukio limetokea usiku wa octoba mosi kuamkia octoba 2 mwaka huu.

Joseph amewataja walinzi hao kutoka kampuni ya Noble security Tanzania Ltd ya Kibaha kuwa ni Hamad Kisoki (32) mkazi wa Maili Moja na Said Mohammed (39) mkazi wa Mwanalugali.

Amesema siku ya tukio walinzi waliotakiwa kuingia zamu walikuwa ni wawili lakini Said Mohammed pekee ndiye aliyefika kazini na mwenzake Hamad Kisoki haikuweza kufahamika mara moja ni kwa sababu gani hakuingia kazini.

Aidha amesema kuwa Said Mohamed alipokuwa kwenye lindo lake anadaiwa kupatiwa chips na juisi vinavyosemekana kuwa na madawa ya kulevya kutoka kwa mwanamke asiyefahamika.

Katibu huyo wa CWT mkoa wa Pwani ameeleza kuwa baada ya kupatiwa chakula hicho mlinzi alipoteza fahamu na hivyo kutoa mwanya kwa watu hao kuvunja milango ya ofisi hizo na kuingia na kuiba vitu hivyo ambavyo thamani yake bado haijafahamika.

Ametaja ofisi zilizopo kwenye jengo hilo ambazo zimeibiwa ni pamoja na CWT mkoa ,CWT wilaya,beem financial services (BFS) ,Chodawu,Tuico na TCCIA ambapo kwasasa wameshafikisha taarifa hizo polisi kwa hatua zaidi na ofisi ya chama hicho imeshakaa na taasisi zote zilizopanga jengo hilo kufanya tathmini.

hata hivyo amesikitishwa sana kutokea kwa wizi huo na kushangazwa na mlinzi huyo kula ama kununua vyakula kwa watu wasiowajua kwani kwa kufanya hivyo kumesababisha kuwapa wahalifu urahisi kutekeleza tukio hilo ambalo limesababisha hasara kwa wamiliki wa ofisi hizo.

Kwa upande wake kamanda wa polisi mkoani Pwani,Bonaventure Mushongi ,amekiri kutokea kwa tukio hilo ambapo amesema taarifa ya tukio hilo ilitolewa  saa 5 asubuhi kutoka kwa Elizabeth Thomas ambae ni katibu wa chama CWT wilaya ya Kibaha huko mkoani A ,kata ya Tumbi.

Mushongi amesema kuwa baada ya kufanya wizi huo watu hao walitokomea kusikojulikana na jeshi hilo bado linawatafuta,huku akiomba ushirikiano kwa wananchi kuwafichua watu wanaowadhania kuhusika na wizi huo na kwasasa wanawashikilia walinzi hao kwa ajili ya uchunguzi juu ya tukio hilo.

Mwisho













      

Monday, September 26, 2016

MAJALIWA AWASIMAMISHA MAOFISA MISITU RUFIJI

Na John Gagarini,Rufiji
WAZIRI mkuu Kassim Majaliwa amemsimamisha kazi Meneja wa Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) wilaya ya Rufiji mkoani Pwani Suleiman Bulenga kwa kushindwa kudhibiti na kusimamia mapato yatokanayo na shughuli za misitu hivyo kuikosesha mapato Serikali.
Mbali ya meneja huyo maafisa misitu watatu nao wamesimamishwa kutokana na kushindwa kudhibiti na kusimamia shughuli za uvunaji misitu na kusababisha wilaya kukosa mapato .
Maofisa misitu waliosimamishwa ni pamoja na Ofisa maliasili na mazingira wa wilaya Dk Paul Ligonja,Ofisa misitu Gaudence Tarimo na Jonas Nambua ambao watsimamishwa hadi hapo uchunguzi utakapokamilika.
Majaliwa alichukua hatua hiyo wilayani Rufiji wakati akizungumza na watumishi wa halmashauri ya wilaya ya Rufiji na wananchi wa wilaya hiyo  na kusema kuwa sekta ya misitu ni tatizo kwa kila wilaya na Rufiji ni moja ya wilaya hizo .
“Magogo yanasafirishwa bila utaratibu,na ndio wanakata miti kwenye misitu ya Utete na kupiga nyundo maeneo ya Kilwa,” alisema Majaliwa.
Alisema kuwa hakuna manufaa na TFS hivyo ameamua kusimamisha shughuli zote za uvunaji,katika wilaya hiyo na watumishi hao hadi wizara itakapotoa maelekezo mengine.
“Wilaya ya Rufiji inaongoza katika suala la utoroshaji wa misitu na kuruhusu uvunaji holela suala ambalo halikubaliki na nataka uwajibikaji na uadilifu katika maeneo ya kazi na watumishi wanapaswa wabadilike na waache kufanya kazi kwa mazoea,” alisema Majaliwa. 
Aidha Majaliwa alikemea utozwaji wa ushuru kwa watu wanaochoma mkaa unaofanywa na halmashauri ya Rufiji kwani kwa kufanya hivyo ni kuruhusu ukataji ovyo wa miti.
“Mkuu wa wilaya na mkurugenzi wa halamshauri ya Rufiji mnapaswa kusimamia mapato na matumizi ya fedha ili kuongeza mapato ya halmashauri iweze kupiga hatua ya kimaendeleo,”alisema Majaliwa.
Naye mbunge wa Rufiji,Mohammed Mchengelwa alisema kuwa nidhamu kwa watumishi inaonekana kupungua kwa baadhi ya watumishi kwenye halmashauri hiyo.

Mwisho




Friday, September 23, 2016

WAWILI WAFA AJALINI MMOJA ACHOMWA MOTO

Na John Gagarini, Kibaha

WATU wawili wamefariki dunia na wengine 11 kujeruhiwa mkoani Pwani kufuatia ajali iliyohusisha mabasi madogo mawili ya abiria kugongana uso kwa uso huko Kiparanganda wilayani Mkuranga.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mjini Kibaha na Kamanda wa Polisi mkoani humo Bonaventura Mushongi alisema kuwa watu hao walifariki papo hapo.

Mushongi alisema kuwa ajali hiyo ilitokea Septemba 21 mwaka huu majira ya saa 10:30 jioni T363 DCV likiendeshwa na Zidadu Mohamed (25) mkazi wa Dar es Salaam akielekea Kimazinchana liligongana na T363DHD yote aina ya Toyota Hiace likiendeshwa na Miraji Mlonga (22) akielekea Dar es Salaam.

Aliwataja waliokufa kuwa ni Zuhura Haji (21) na Neema Julius (25) wote wakazi wa Kimazinchana wilaya ya Mkuranga ambapo miili yao imehifadhiwa kwenye Hopsitali ya Wilaya ya Mkuranga kusubiri ndugu kwa ajili ya mazishi.

Aidha aliwataja watu waliojeruhiwa kuwa ni Majeruhi ni Mariamu Aloyce (46) wa Kimazinchana Mariamu Sultan (60) mkzai wa Chanika, Yusufu Maziku (33) mkazi wa Kimazinchana,Kulwa Abdala (30) makzi wa Mbagala,Ibrahim Hamis (3) mkazi wa Mbagala na Fatma Abdul (25) mkazi wa Chanika.

Wengine ni Salum Mohamed (54) mkazi wa Mwalusembe, Litus Mwarami (26) mkazi wa Kimazinchana Kidawa Abdala (30) mkazi wa Mbagala, Issa Hemed (2) mkazi wa Kimazinchana na Greyson Ernest (23) mkazi wa Kimazinchana.

“Tuna washikilia madereva wote waili kutokana na kusababisha ajali hiyo na watafikishwa mahakamani mara upelelezi wa kesi hiyo utakapokamilika ili kujibu tuhuma hizo zinazowakabili,” alisema Mushongi.

Kwenye tukio lingine mkazi wa Kwa Mathias Hamis Tenende (38) aliuwawa kwa kupigwa kisha kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kali kwa madai ya kutaka kuiba pikipiki eneo la Umwelani.

Mwisho.
 








Monday, September 12, 2016

WAPONGEZA IDD EL HAJI KUFANYIKA KWA PAMOJA


Na John Gagarini, Kibaha

KUFUATIA sherehe ya Idd el Haji ambayo inahusisha na uchinjaji kufanyika jana ambapo waumini wa dini ya Kiislamu walisherehekea kwa pamoja tofauti na miaka mingine ambapo kila dhehebu lilikuwa likifanya siku tofauti safari hii wamefurahi kufanya kwa pamoja.

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha baadhi ya waumini wa Kiislamu wamesema kuwa utaratibu wa kusherehekea kwa pamoja ni mzuri kwani unaonyesha umoja na ni vema ukaendelea hata kwa siku zijazo.

Mrisho Halfan “Swagala”  alisema kuwa hakuna sababu wao kama waumini wa imani moja kufanya sherehe kwa wakati tofauti na kufanya kama ni imani tofauti.

“Tunaomba viongozi wa taasisi hizi za dini yetu wakae kwa pamoja na kufanya vitu kwa pamoja kwani kama mwaka huu sikukuu imependeza kwani wote tumejumuika na hali hii imeondoa tofauti na kutufanya kitu kimoja,” alisema Swagala.

Alisema kuwa kuna haja ya kuunganisha umoja wa waislamu kama hivi kwa kiufanya sherehe hiyo ambayo ni kubwa kwa Waislamu kote duniani kukumbuka yale yaliyofanywa na mtume ikiwa ni kufanya mambo yanayompendeza Mungu.

Kwa upande wake Abubakari Lipambila kutoka Masjidi Hazarajii Maili Moja Kibaha alisema kuwa sikukuu hiyo ni kwa ajili ya kurejesha furaha kwa watu wote.

Lipambila alisema kuwa waumini wa dini ya kiislamu wanapaswa kujihadhari na shetani katika kipindi hichi cha sherehe kwani naye yuko kazini kwa kuwapotosha watu ili waende kinyume na imani kwa kujiingiza kwenye vitendo viovu.

Mwisho.

Wednesday, September 7, 2016

BINTI AZAA MTOTO AMTUPA

Na John Gagarini, Kibaha

BINTI aliyetambulika kwa jina la Judith Paulo anayekadiriwa kuwa na umri katia ya miaka (18) na (22) anatuhumiwa kuzaa mtoto wa jinsia ya kike kisha kumtupa mwanae jirani na jalala.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu mwenyekiti wa Kitongoji cha Pera kata ya Pera Chalinze Mjini Hussein Mramba alisema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 7 majira ya saa 12 asubuhi eneo la Kwa Mwarabu.

Mramba alisema kuwa kichanga hicho chenye uzito wa kilogramu 3.2 kiliokotwa baada ya watoto waliokuwa wakiokota vitu mbalimbali jirani na jalala huku kikiwa kimewekwa kwenye mfuko wa Rambo.

“Watoto hao ndiyo waliogundua na ndipo walipotoa taarifa kwa watu wazima na kwenda kumchukua ambapo walimkuta mtoto huyo akiwa na afya njema huku akiwa hajavalishwa nguo yoyote mwilini mwake na jambo la kumshukuru Mungu kuwa mtoto huyo hakupata madhara yoyote,” alisema Mramba.

Alisema kuwa baada ya hapo ilibidi wasamaria wema wampeleke Hospitali ili kuangalia namna ya kumsaidia mtoto huyo ambaye kwa sasa yuko kwa mama mmoja ambaye amejitolea kukaa naye wakati taratibu nyingine zinafanyika ili apelekwe sehemu stahiki.

“Kwa maelezo tuliyopata baada ya kwenda Kituo cha Afya cha Chalinze ili kujua kama alijifungua hapo ilibainika kuwa binti huyo alijifungua kituoni hapo juzi majira ya saa 4 baada ya kufika hapo majira ya saa 3 usiku akiwa na uchungu wa kujifungua huku akiwa hajaongozana na mtu yoyote,” alisema Mramba.

Mramba ambaye pia ni mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mdogo wa Chalinze alisema kuwa baada ya kujifungua alikaa kama masaa mawili kisha kuomba kuondoka baada ya kujifungua salama na alimwomba muuguzi aondoke kwani alikuwa hajafunga mlango wa nyumba anayoishi hivyo ana hofu ya kuibiwa vitu vyake.

“Kutokana na utetezi wake huo ilibidi baadhi ya wazazi wamsaidia fedha kwa ajili ya kulipia teksi baada ya kumuonea huruma ambapo yeye alifika hapo kituoni kwa kutumia bodaboda,” alisema Mramba.

Aidha alisema kuwa binti huyo alionekana kuwa na wasiwasi alipofika kituoni hapo lakini hata hivyo baadhi ya wazazi waliokuwa hapo walijaribu kumweka sawa ili aone jambo la uzazi ni la kawaida.

Alisema kuwa taarifa hizo wamezitoa sehemu mbalimbali ikiw ani pamoja na polisi kwa ajili ya kusaidia kupatikana kwa binti huyo ambapo mita kama 100 aliposhushwa na teksi wamejaribu kuulizia lakini inavyoonekana kuwa hakuwa anakaa maeneo hayo kwani jina hilo hakuna mtu anayelifahamu.


Mwisho.

Tuesday, August 30, 2016

BOMOABOMOA YALETA KIZAZAA MAILI MOJA KIBAHA


Na John Gagarini, Kibaha

WANANCHI wa eneo la Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani wamelia na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani kuwa wawafikirie kwa kuwalipa fidia wakati wa zoezi la bomobomoa ambalo linatarajiwa kufanyika Novemba 23 mwaka huu.

Hataua hiyo imekuja baada ya TANROADS kutoa barua kwa watu waliojenga kwenye eneo la hifadhi ya barabara inayomilikiwa na wakala hiyo kwa wale waliojenga umbali wa mita 120 kwa kila upande wa barabara kuu ya Dar es Salaam Morogoro kuanzia Kiluvya hadi Tamco waanze kubomoa kabla ya zoezi hilo kwa kuwapa siku 90 kufanya hivyo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mwenyekiti wa chama cha ACT-Wazalendo mkoa wa Pwani Mrisho Swagala alisema kuwa mbali ya kuwtowlaipa fidia pia eneo linalopitiwa na zoezi hilo ni kubwa sana ikilinganishwa na maeneo mengine.

“Hatukati zoezi hilo kufanyika lakini wangeangalia namna ya kuwafidia wananchi kwani kuwabomolae bila ya kuwapa fidi itakuwa ni kitendo cha ukatili na kinakwenda kinyume cha haki za binaadamu kwani bomoa hiyo itawaacha watu wengi wakiwa hawana mahali pa kuishi na kwa wafanyabiashara hawatakuwa na sehemu ya kufanyia biashara,” alisema Swagala.

Alisema kuwa alisema kuwa sheria ya barabara iliyotungwa mwaka 1932 ambapo inadaiwa kuwa watu walilipwa fidia jambo ambalo kwa kipindi hicho fedha ilikuwa ni ndogo ukilinganisha hali halisi ya sasa hivyo kuna haja ya kuwafikiria.

Naye Ally Gonzi mwenyekiti wa ushirika wa wafanyabiashara wa soko la mkoa la Maili Moja alisema kuwa wao kama wafanyabiashara wansikitishwa na hatua hiyo kwani hadi sasa hawajui watakwenda kufanyia biashara wapi.

Gonzi alisema kuwa waliahidiwa kuwa watajengewa soko la kisasa lakini hadi sasa soko halijajengwa ambapo wao wako hapo kwa zaidi ya miaka 35 na Halmashauri ambao wao wako chini yao.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Mtaa wa Maili Moja Athuma Mkongota alisema kuwa wananchi wengi wamekwenda ofisini kwake kwenda kulalamika juu ya zoezi hilo ambalo litawakumba watu wengi ambao wako katikati ya mji huo.

Mkongota alisema kuwa ubomoaji huo umekuja baada ya kuisha kwa kesi iliyofunguliwa na wananchi kupinga hatua hiyo lakini walishindwa hata hivyo alisema kuwa hukumu ya kesi hiyo bado hajaipata.

Awali mkaguzi wa barabara wa mamlaka hiyo Livingston Urio alisema kuwa kwa sasa wanaendelea na zoezi la kutoa barua ambapo idadi kamili ya nyumba na vibanda vya biashara vitakavyobomolewa itajulikana.

Urio alisema kuwa ilikuwa ifanyike mwezi Agosti lakini waliongeza hadi Novemba lakini miaka ya nyuma tayari walishawawekea alama ya X mwaka 2004 lakini zoezi hilo halikufanyika lakini kwa sasa zoezi hilo linafanyika.

Alisema kuwa wananchi walipoenda mahakamani walishinda na kuonekana kuwa eneo hilo ni mali ya mamlaka hiyo na kuwa eneo hilo magari yanakwenda taratibu hivyo barabara kuharibika na baada ya bomoa hiyo eneo hilo litawekwa stendi kubwa na patapangwa vizuri ili mji uonekane vizuri.

“Kulingana na sheria ya barabara ya mwaka 1932 na kufanyiwa marekebisho 1958 kifunga na 52 na marekebisho ya sheria ya barabara na 13 ya mwaka 2007 sambamba na taratibu za sheria za usimamizi wa barabara kifungu na 30 (b) eneo la hifadhi ya barabara sehemu iliyotajwa hapo juu ni mita 120 sawa na futi 400 kwenda kila upande kutoka katikati ya barabara ni marufuku kufanya maendelezo yoyote katika eneo hilo,” alisema Urio.


Mwisho.