Monday, December 5, 2016

HALMASHAURI YA CHALINZE YAANZA KUMWAGA FEDHA KWA WAJASIRIAMALI


Na John Gagarini, Chalinze

HALMASHAURI ya Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani imetoa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 79.8 kwa vikundi vya wajasiriamali 26 vya akinamama na vijana kwenye kata za Halmasahuri hiyo.

Aidha fedha hizo zinatokana na asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri ya robo mwaka ambazo ni kiasi cha shilingi milioni 809 yaliyokusanywa katika kipindi hicho.

Akikabidhi baadhi ya vikundi hivyo vya vijana na akaimama kwenye kata ya Msoga ambapo kila kundi linapata asilimia tano kutokana na mapato hayo Mwenyekiti wa Halmashauri Said Zikatimu alisema kuwa fedha hizo zitakuwa zikitolewa kwa kila robo ya mwaka.

Zikatimu alisema kuwa lengo la kutolewa fedha hizo kwanza ni kufuata sheria ambayo inataka asilimia tano ya mapato yote ya Halmashauri wakopeshwe vijana na asilimia tano kwa ajili ya akinamama kupitia vikundi vya vya uzalishaji mali.

“Tunaomba vikundi vyote ambavyo vinakopeshwa fedha hizi wazirejeshe kwa wakati ili ziwe na mzunguko kwa watu wengine na vikundi vihakikishe vinazitumia kwa malengo waliojiwekea na si kuanzisha miradi ambayo hamjaombea mnaweza kushindwa kurejesha,” alisema Zikatimu.

Alisema kuwa fedha hizo siyo msaada bali ni fedha kwa ajili ya kuboreshea shughuli za ujasiriamali na wanapaswa kurejesha kwa wakati ili vikundi vingi viweze kupata fedha hizo ambazo zinatokana na mapato ya ndani yanayotokana na vyanzo mbalimbali.

“Hizi fedha ni kwa ajili ya wananchi wote na hasa wale waliojiunga kwenye vikundi hivyo zitumike kama zilivyoombewa na siyo kununulia nguo au baadhi huzitumia kwa ajili ya kufanyia starehe mkifanya hivyo mtaharibu maana ya mkopo huu na mtashindwa kurejesha na kujikuta mkishtakiwa,” alisema Zikatimu.

Aidha aliyatakama makundi mbalimbali ya vijana na akimama kujiunga na kuanzisha vikundi vingi kwa ajili ya kukopa kwani fedha si tatizo bali ni wao kujiunga kwa wingi fedha ziko za kutosha.

Kwa upande wake ofisa maendeleo ya jamii na ofisa vijana wa Halmashauri ya Chalinze Felista Kizito alisema kuwa vikundi hivyo vilivyopewa fedha hizo vitapewa mwezi mmoja kabla ya kuanza kurejesha marejesho yao.

Kizito alisema kuwa vikundi hivyo vimegawaanyika kwenye shughuli mbalimbali kutegemeana na mazingira yao na vimepewa fedha kati ya shilingi milioni mbili hadi sita kutegemeana na aina ya mradi ambao waliuanzisha.

Naye diwani wa kata ya Msoga Hassan Mwinyikondo alisema kuwa Halmashauri hiyo imefanya jambo kubwa kwa kutoa fedha hizo ambazo zitasaidia kuboresha maisha ya wananchi.

Mwinyikondo alisema kuwa mikopo hiyo ya Hlamashauri ni nafuu na haina masharti magumu kama ilivyo kwa taasisi za kifedha ambazo watu wengi wameshindwa kukopa kutokana na masharti kuwa magumu.

Mwisho.


 Mwenyekiti wa Halmashauri ya Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Said Zikatimu katikati akiwakabidhi hundi kikundi cha ujasirimali cha Wanawake cha Nianjema cha ufugaji wa Mbuzi Kijiji cha Kwa Konje kushoto ni mwenyekiti wa Kijiji hicho Omary Mbwana anayefuatia ni  diwani wa kata ya Kibindu Ramadhan Mkufya akifuatiwa na Ofisa Maendeleo ya Jamii na Ofisa Vijana Halmashauri ya Chalinze Felista Kizito na mwenyekiti wa kikundi hicho Veronica Chusi

 Kushoto Mwenyekiti wa Halmashauri ya Chalinze Said Zikatimu akiwakabidhi hundi ya fedha wana kikundi wa Muungano Mindukene kata ya Talawanda 

No comments:

Post a Comment