Thursday, August 28, 2014

RT YATAKIWA KUANDAA MKUTANO WA KATIBA

Na John Gagarini, Kibaha
CHAMA cha Riadha Tanzania (RT) kimetakiwa kiandae mkutano mkuu wa chama ili kupitia rasimu ya katiba baada ya mkutano kama huo kuahirishwa Juni na kutakiwa kufanyika Novemba mwaka jana lakini hadi sasa hakuna taarifa ya kufanyika mkutano kama huo .
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Kibaha mwenyekiti wa chama cha riadha mkoa wa Pwani (CRAA) Joseph Luhende alisema kuwa baada ya kushindikana kufanyika kwa mkutano kwa ajili ya kupitisha rasimu hiyo huko mkoani Morogoro iliamuliwa kuwa mkutano kama huo ufanyike lakini hadi sasa imekuwa kimya.
Luhende alisema kuwa upitishaji wa rasimu ya chama ilishindikana kutokan na kuchelewa hivyo kupangwa Novemba mwaka jana na hadi sasa hakuna taarifa yoyote ya kufanyika mkutano kwa ajili ya kukamilisha zoezi hilo.
“Mbali ya kushindikana kupitishwa kwa rasimu ya katiba hiyo pia vyama vilitakiwa visitumie katiba ya zamani na tulivyouliza tuliambiwa kuwa tusubiri na sasa inakaribia kufika mwaka lakini hakuna lolote linaloendelea hali ambayo inakatisha tamaa,” alisema Luhende.
Alisema mchezo wa riadha unakumbwa na changamoto nyingi hivyo rasimu hiyo ingepitishwa ingesaidia kuboresha riadha lakini utekelezaji umekuwa mgumu na rasimu ndiyo inayopelekea kupata katiba ambayo ni kila kitu sawa na dira ya mwelekeo wa mchezo huo.
“Utendaji kazi unakuwa mgumu kutokana na kutakiwa tusitumie katiba ya zamani hivyo ni vema rasimu hiyo ikapitishwa ili tuweze kupata katiba mpya ambayo itatuongoza,” alisema Luhende.
Aidha alisema kuwa kutokana na mipango ya RT kutokuwa mizuri kumechangia nchi kufanya vibaya kwenye michuano ya kimataifa mfano ile ya Olimpiki ambapo Tanzania iliambulia patupu kwenye mchezo huo na kuwataka viongozi wa shirikisho hilo kuwa makini katika kutekeleza majukumua yao.
Akijibu kuhusiana na suala hilo kwa njia ya simu katibu mkuu wa RT Suleiman Nyambui alisema kuwa tatizo kubwa lililopo ni ukosefu wa fedha ndiyo inapelekea wao kushindwa kuandaa mkutano mkuu wa kupitisha rasimu hiyo ya katiba ili kupata katiba mpya.
“Tunaendelea kuwasiliana na wafadhili mbalimbali ili tuweze kupata fedha kwa ajili ya kuandaa mkutano huo wa kupata katiba ambayo itaongoza chama baada ya mkutano wa awali kushindwa kuendelea baada ya viongozi wa mikoa ambao walisema hawajaisoma vizuri hivyo ikashindika kuijadili rasimu hiyo,” alisema Nyambui.
Nyambui alisema walipeleka katiba mikoani kwa ajili ya wao kutoa mapendekezo lakini hawakuweza kuyapeleka ambapo ni mikoa mitatu tu ndiyo iliyotoa mapendekezo yake  ambayo ni Dar es Salaam, Arusha na Dodoma huku mingine ikiwa bado.
“Tunatarajia kuitisha mkutano mkuu kabla ya mwaka haujaisha ili kukamilisha zoezi la kupata katiba baada ya marekebisho kufanyika kwenye mkutano na kikwazo kikuu ni ukosefu wa fedha,” alisema Nyambui.
Mwisho.



HALMASHAURI ZAKATAZWA KUTOZA USHURU

Na John Gagarini, Kibaha
HATIMAYE mkoa wa Pwani umetoa tamko la kuzizuia Halmashauri za mkoa huo kuendelea kutoza ushuru wa hoteli na nyumba za kulala wageni ambao ulifutwa na bunge mwaka 2009 huku Halmashauri ya mji wa Kibaha ikiwa inaendelea kuutoza na kusababisha malalamiko ya wafanyabiashara hao.
Kufuatia halmashauri hiyo kuendelea kutoza ushuru huo kupitia umoja wao Wamiliki wa Hoteli wilayani Kibaha mkoani Pwani (UGEHOKI) walipeleka malalamiko yao ofisi ya katibu tawala wa mkoa huo kupinga kutozwa ushuruhuo wa asilimia 20.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha Kaimu Katibu Tawala wa mkoa huo Mhandisi Michael Mrema, alisema kuwa halmashauri zote zilipewa miongozo kutoka Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) juu ya kusitisha utozaji huo hadi watakapopewa utartibu mwingine wa ukusanyaji.
“Tulipokea barua toka kwa wamiliki hao juu ya kulalamikia ushuruhu huo ambao ulisitishwa wakati wizara zinazohusika zitakapokuwa zimeweka utaratibu mwingine wa namna ya ukusanyaji wa ushuru huo ambao ulilalamikiwa na wamiliki hao kuwa ni mkubwa sana,” alisema Mrema.
Mrema alisema kuwa barua hiyo toka TAMISEMI ya kusitisha ushuru huo yenye kumbukumbu namba Na. FA 2/266/01/10 ya Mei ya mwaka 2014 kwa halmashauri zote nchini ambayo ilitokana na barua yenye kumbukumbu Na. CE.325/387/03/47 ya tarehe 16 ya mwezi wa Aprili mwaka 2014 iliyotoa uafafanuzi zaidi.
“Katika ufafanuzi TAMISEMI ilisema kuwa ushuru wa nyumba za kulala wageni umeainishwa katika sheria ya fedha sura 290 kifungu cha 6(1)(q) na 7(1)(u) na kwamba awali ushuru huo ulikuwa ukitozwa kupitia sheria ya hoteli sura 105 ambayo imefutwa baada ya kutungwa sheria mpya sheria ya Utalii na 29 ya mwaka 2008 na kuanza kutumika rasmi Julai Mosi 2009 baada ya kutangazwa kwenye gazeti la serikali namba 212 la tarehe 1 Julai 2009 ni wazi kuendelea kutozwa ni kukiuka sheria za Utalii,” alisema Mrema.
Aidha Mrema alisema kutokana na barua hizo Halmashauri zilipaswa kutoendelea kutoza ushuru huo hivyo hazipaswi kuendelea kuutoza na zikiendelea kutoza kunaweza kusababisha halmashauri na watoa huduma  hao ni kusababisha migogoro mikubwa ya kisheria na kwa sasa wizara za TAMISEMI, Wizara ya Fedha na Wizara ya Maliasili na Utalii zipo katika majadiliano ya kuamua namna bora ya kurejesha ushuru huo.

Alizitaka halmashauri hizo kutekeleza agizo hilo na maagizo mengine yanayotoka ngazi za juu ili kuepusha migogoro na watoa huduma na wananchi katika suala zima la ukusanyaji wa mapato mbalimbali.

Wednesday, August 27, 2014

WALILIA FIDIA YA MASHAMBA YAO

Na John Gagarini, Kibaha
WAKAZI nane wa kitongoji cha Benki kata ya Igunga wilaya ya Igunga mkoani Tabora wameiomba Halmashauri ya wilaya kuwalipa fidia ya mashamba yao ambayo yamechukuliwa na Halmashauri hiyo kwa ajili ya upanuzi wa hospitali ya wilaya.
Wakazi hao walitoa ombi hilo kufuatia Halmashauri hiyo kuwa kimya kwa muda mrefu baada ya mashamba yao kuchukuliwa tangu mwaka 2010 nakufanyiwa tathmini mwezi Februari mwaka huu lakini hadi sasa bado hawajalipwa fidia za maeneo yao.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jana mjini Kibaha mwenyekiti wa kamati ya waathirika hao  Daniel Shamalatu alisema kuwa mashamba yao yana ukubwa wa zaidi ya hekari 24 ambazo zilichukuliwa kwa ajili ya upanuzi huo wa hospitali ya wilaya.
Shamalatu alisema kuwa maeno yao yalichukuliwa bila ya wao kupewa taarifa ambapo mazao yao waliyokuwa wameyapanda yalifyekwa na ujenzi kuanza bila ya kupewa fidia.
“Tulipoona kimya tulikwenda mahakamani ili tuweze kulipwa fidia zetu lakini baraza la madiwani liliingilia kati na kututaka tuondoe kesi mahakamani ili tukubaliane nje ya mahakama, kweli tuliondoa kesi hiyo mahakamani lakini hakuna kinachoendelea ambapo sasa ni karibu mwaka umepita lakini tunaona kimya na tunapofuatilia halmashauri tunaambiwa suala letu linashughulikiwa,” alisema Shamalatu.
Alisema kuwa wao hawapingi ujenzi huo lakini wanachotaka ni kulipwa fidia kutokana na ukubwa wa mashamba yao na si kiwanja kimoja kila heka kama walivyotaka kufanya na pia wanataka kujua malipo yao yatafanyika lini.
 Akitolea ufafanuzi suala hilo kwa njia ya simu mkurugenzi wa halmashauri hiyo Rustika Turuka alisema kuwa ni kweli mashamba yao yalichukuliwa kwa ajili ya upanuzi wa hospitali hivyo kutakiwa kupisha ujenzi huo kufanyika.
Turuka alisema kuwa kwa sasa maeneo hayo tayari yameshafanyiwa tathmini na taarifa ya uthamini imepelekwa wizarani kwa ajili ya kuandaliwa malipo baada ya kujua takwimu sahihi kutokana na maeneo hayo na kiasi ambacho watastahili kulipwa ili halmashauri itenge bajeti kwani maeneo mengine ambayo yalichukuliwa wamelipwa na wao watalipwa mara taratibu zitakapokamilika.
“Mthamini toka Tabora alishafika na kufanya kazi hiyo na kwa sasa tunachokisubiri ni taarifa toka wizarani baada ya kuipitia tathmini hiyo ili watu wanaodai fidia waweze kulipwa hivyo wanapaswa kuwa na subiri kwani mambo haya lazima yafuate taratibu na kila mtu atapewa haki zake pia eneo hilo  kwa sasa ni mji haipaswi kuwa na mashamba,” alisema Turuka
Aidha alisema wanasubiri taarifa hiyo ambayo itaonyesha ni kiasi gani wanastahili kulipwa na ndipo watatafuta fedha hizo kisha kuwalipa watu ambao wanadai ila wanataka walipwe haraka lakini serikali ina taratibu zake za kufanya malipo.
“Masuala ya malipo ya fidia za viwanja si suala la haraka linachukua muda mrefu hivyo lazima wawe na subiri wakati masuala yao yanashughulikiwa ambapo maeneo mengine tayari wameshalipwa hivyo na wao wanapaswa kuwa na subira na kila mtu atapata malipo yake,” alisema Turuka.
Mwisho.

     

Tuesday, August 26, 2014

Na John Gagarini, Kibaha
RAIA wa nchi ya Ethiopia Dawita Alalo (25) amekufa alipokuwa akipatiwa matibabu kwenye kituo cha afya cha Chalinze kata ya Bwiringu wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani.
Marehemu alikuwa ni kati ya raia 48 wa nchi hiyo walikamatwa wakiwa kwenye msitu wa kijiji cha Visakazi Ubena Zomozi tarafa ya Chalinze Agosti 22 mwaka huu, baada ya kuingia nchini bila ya kibali.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha kaimu kamanda wa polisi mkoani humo Mrakibu Mwandamizi (SSP) Athuman Mwambalaswa alisema kuwa marehemu ni miongoni mwa wahamiaji haramu 11 waliokuwa wamelazwa kituoni hapo wakipatiwa matibabu.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 26 majira saa 7:30 usiku alipokuwa akipatiwa matibabu kituoni hapo baada ya kuugua ugonjwa wa malaria.
Wakati huo huo mlinzi wa baa ya Silent Inn Jamat Mandama (55) amefariki dunia baada ya kunywa pombe nyingi bila ya kula chakula.
Alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 27 mwaka huu majira ya saa 1 usiku huko Umwe kata ya Ikwiri wilayani Rufiji.
Aidha alisema kuwa mlinzi huyo alikutwa amekufa akiwa lindoni kwenye baa hiyo.
Na John Gagarini, Kibaha
ASKARI sita wa jeshi la polisi mkoani Pwani wamenusurika kifo kutokana na ajali ya barabarani baada ya gari walilokuwa wakisafiria kugongwa na lori la mizigo.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha kaimu kamanda wa polisi mkoani humo, Mrakibu Mwandamizi (SSP) Athuman Mwambalaswa alisema kuwa askari hao walikuwa doria.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 26 majira ya saa 9:30 usiku eneo la Maili Moja Ujenzi wailayani Kibaha barabara kuu ya Dar es Salaam Chalinze.
Alisema kuwa gari hilo lenye usajili namba PT 2012 lilikuwa likiingia kwenye kituo cha mafuta cha Delina na kugongwa na lori hilo lenye namba za usajili T 927 CAU na tela namba T 769 CJX.
“Lori hilo bada ya kuligonga gari hilo lapolisi kwa nyuma likaenda kugongana na lori lingine lililokuwa likielekea Jijini Dar es Salaam lenye namba T 672 BAC lenye tela namba T 672 BBW,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Alibainisha kuwa askari watatu walijeruhiwa vibaya ambao ni namba F 4333 DC Tamimu ambaye amevunjika mguu wa kulia mara mbili, WP 6100 DC Jaqline ambaye amejeruhiwa kichwani na H 3348 DC Armand ambaye amejeruhiwa kichwani na kifuani.
“Askari wote wamelazwa katika hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani Tumbi kwa matibabu zaidi ambapo tunaendelea kumtafuta dereva wa lori lililosababisha ajali hiyo,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Mwisho.

   

Sunday, August 24, 2014

PINGENI VITENDO VYA UKATILI WA KIJINSIA

Na John Gagarini, Kibaha
WANAWAKE nchini wametakiwa kutokubali kufumbia macho vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa kuhofia kutengwa na familia zao badala yake wawe watoa taarifa ili kuwadhibiti watu wanaoendeleza vitendo hivyo ambavyo ni kinyume cha sheria na uvunjaji wa haki za binadamu.
Tabia ya kuficha ukatili wa kijinsia imesababisha wahusika kujikuta wakiathirika kutokana na vitendo hivyo ambavyo vimeshamiri kutokana na kuendelea kwa usiri ndani ya familia.
Hayo yalisema jana mjini Kibaha na mkurugenzi wa benki ya Wanawake Tanzania Magreth Chacha, wakati wa uzinduzi wa Chama Cha Waandishi wa Habari Wanawake Mkoa wa Pwani (PWMO).
Chacha alisema kuwa baadhi ya wanawake wamekuwa wakificha vitendo hivyo vya kikatili ambavyo vimekuwa vikifanywa na baadhi ya wanaume wasiokuwa na huruma.
“Vitendo vya ukatili wa kijinsi vimekuwa vikifanywa ndani ya familia huku wanawake amabao ndiyo wahanga wa matukio hayo wamekuwa wakikaa kimya kuhofia kutengwa na familia zao jambo ambalo limesababisha vitendo hivi kuendelea,” alisema Chacha.
Alisema kuwa baadhi ya vitendo hivyo vimekuwa vikifanywa na watu wa karibu wa familia wakiwemo wanandoa na ndugu hali ambayo inasababisha taarifa hizo kufichwa huku walengwa wakiendelea kuathiriwa na vitendo hivyo viovu na vya ukatili.
“Baadhi ya vitendo hivyo ni pamoja na wanawake kupigwa, kutumikishwa kingono, kubakwa, watoto kubakwa, kulawitiwa, kufanyishwa kazi licha ya kuwa na umri mdogo na vitendo vingine vinavyokwenda kinyume cha sheria na haki za msingi za binadamu,” alisema Chacha.
Kwa upande wake mwenyekiti wa (PWMO) Mwamvua Mwinyi alisema kuwa lengo la kuanzishwa chama hicho mbali ya kutetea haki za waandishi wanawake pia ni kukabiliana na vitendo vya ukatili wa kijinsia ndani ya mkoa huo na Tanzania kwa ujumla.
“Vitendo vya ukatili wa kijinsia vimekuwa vikiongezeka siku hadi siku kutokana na baadhi ya wanajamii hususani wanawake kutokuwa katika kutoa taarifa za vitendo hivyo hali inayofanya kuongezeka kwa ukatili wa kijinsia,” alisema Mwinyi.
Aliiomba jamii kwa kushirikiana na vyombo vya sheria kwa kutoaa taarifa juu ya watu wanaofanya vitendo hivyo vya ukatili hususani maeneo ya pembezoni mwa miji, chama hicho kilianzishwa mwaka jana na kina jumla ya wanachama 15.

Mwisho.

MWANARIADHA AOMBA WAFADHILI AENDE KAMBINI KENYA

Na John Gagarini, Kibaha
MWANARIADHA John Mwandu wa mkoani Pwani amewaomba wadau mbalimbali kujitokeza kumsaidia kwa hali na mali ili aweze kwenda kambini Eldoret nchini Kenya kwenye kambi aliyotokea mkimbiaji maarufu duniani David Rudisha wa nchi hiyo.
Rudisha ambaye ni bingwa wa dunia wa mbio za mita 800 amekuwa akiwandaa vijana wengi wa nchi ya Kenya kwa ajili ya kuinua vipaji vya vijana ambapo Mwandu ameomba kujiunga na kambi hiyo na tayari amekubaliwa kujiunga nayo kwa ajili ya mazoezi yam bio za mita 1,500.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha Mwandu alisema kuwa tayari ameruhusiwa kwenda kwenye kambi hiyo kwa mwaka mmoja lengo kubwa likiwa ni kujiandaa na mashindano ya Olimpiki ya mwaka 2016 yatakayofanyika Rio de Janeiro nchini Brazil.
 “Lengo langu la kwenda Kenya ni kujifunza mbinu wanazozitumia katika mchezo huo na kuwafanya kuwa mabingwa wa dunia wa riadha, kwani Mungu akipenda Olimpiki ijayo nitahakikisha naiwakilisha nchi yangu na kuiletea medali kwani inawezekana na diyo sababu ya kuanza maandalizi mapema,” alisema Mwandu.
Alisema anatarajia kwenda huko mwezi Desemba mwaka huu kwa ajili ya kambi hiyo ambayo ni nzuri na imetoa wakimbiaji wengi na ana uhakika akifanikiwa kwenda huko atarudi akiwa na mbinu nyingi za ukimbiaji ambazo anaamini zitamfanya aweze kufanya vizuri kwenye mashindano mbalimbali.
“Changamoto kubwa niliyonayo ni ukosefu wa fedha za kuweza kunipeleka kwenye kambi hiyo lakini naamini Mungu ataniwezesha kuweza kufanikisha kwenda kwenye kambi hiyo ambapo tayari nimeshafanya mawasiliano na Rudisha na ameahidi kunisaidia,” alisema Mwandu.
Aidha alisema kuwa Tanzania inashindwa kufanya vizuri kwenye michuano ya kimataifa kutokana na wachezaji wanaochaguliwa hawana uwezo na huchaguliwa kwa upendeleo na wale wenye uwezo kuachwa hali ianayosababisha kutofanya vizuri.
Alibainisha kuwa aliwahi kushinda kwenye mbio za Afrika Mashariki chini ya miaka 17 akiwa anasoma Tegeta High School alikuwa wa pili, Tabora Marathon kilomita 21, mashindano ya Voda Com kilomita tano ambapo alishika nafasi ya pili na Ruaha Marathon kilomita sita ambapo alishika nafasi ya tatu.
Mwisho.

Saturday, August 23, 2014

PWANI WAZINDUA CHAMA CHA WAANDISHI WA HABARI WANAWAKE (PWMO)

 mkurugenzi wa benki ya wanawake Tanzania Margareth Chacha akiongea wakati wa uzinduzi wa chama cha waandishi wa habari wanawake mkoa wa Pwani, kushoto ni mwenyekiti wa chama hicho Mwamvua Mwinyi na kulia ni mlezi wa chama Selina Koka. 


 mwenyekiti wa chama cha waandishi wa habari mkoani Pwani Mwamvua Mwinyi akiongea wakati wa uzinduzi wa chama hicho uliofanyika mjini Kibaha kulia ni mkurugenzi wa benki ya wanawake Tanzania Maragareth Chacha

 mkurugenzi wa benki ya wanawake Tanzania Margareth Chacha katikati akionyesha hati ya busajili ya chama hicho kushoto ni mwenyekiti wa chama hicho Mwamvua Mwinyi na kulia mlezi wa chama Selina Koka.

 mkurugenzi wa benki ya wanawake Tanzania Margareth Chacha katikati akiongea wakati wa uzinduzi wa chama cha waandishi wa wanawake mkoani Pwani

 mkurugenzi wa benki ya wanawake Tanzania Margareth Chacha katikati akiakata utepe kama ishara ya uzinduzi wa chama cha waandishi wa habari wanawake mkoani Pwani kulia ni mlezi wa Selna Koka na kushoto mwenyekiti wa chama hicho Mwamvua Mwinyi

 mkurugenzi wa benki ya wanawake Tanzania Margareth Chacha akikata keki wakati wa uzinduzi wa chama cha waandishi wa habari wanawake mkoa wa Pwani 

 moja ya wadau wa chama cha waandishi wa habari mkoa wa Pwani akiongea kwenye uzinduzi wa chama hicho uliofanyika mjini Kibaha.

















 moja ya waandishi wa habari ambaye alikuwepo kwenye uzinduzi wa chama cha wandishi wa habari wanawake mkoani Pwani akichangia hoja 

 picha ikiwaonyesha viongozi na wadau wa chama cha waandishi wa habari wanawake mkoani Pwani wakiwa kwenye picha ya pamoja mara baada ya uzinduzi wa chama hicho

 wadau wa chama cha waandishi wa habari wanawake mkoa wa Pwani wakiongea na mgeni rasmi wa uzinduzi wa chama hicho Margareth Chacha 





 wadau wa chama cha waandishi wa habari wanawake mkoa wa Pwani wakibadilishana mawazo mara baada ya uzinduzi wa chama hicho.

WAETHIOPIA 48 WASHIKILIWA KWA KUINGIA NCHINI KINYEMELA

Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la Polisi mkoani Pwani linawashikilia raia 48 wa nchi ya Ethiopia kwa tuhuma za kuingia nchini bila ya kibali.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana mjini Kibaha Kaimu kamanda wa Polisi mkoani humo, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Athuman Mwambalaswa alisema kuwa watuhumiwa hao walitelekezwa vichakani.

Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 21 mwaka huu majira ya saa 7 usiku katika Kijiji cha Visakazi Ubena Zomozi tarafa ya Chalinze wilayani Bagamoyo.

Alisema kuwa Wethiopia hao waligunduliwa na askari Magereza wa Gereza la Ubena aitwaye Sospeter ambaye aliwakuta porini alipokuwa akifanya shughuli zake na kutoa taarifa polisi.

"Kati yao 11 wanaumwa na wamepelekwa kituo cha afya cha Chalinze kwa ajili ya matibabu baada ya kuonekana wakitapika baada ya kupewa chakula na walionekana wakiwa na hali mbaya ya kiafya huku wale wengine wakiwa wamehifadhiwa kwenye kituo cha polisi cha kiwilaya," alisema Kamanda Mwambalaswa.

Aidha alisema kuwa raia hao wa Ethiopia wanakadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka 20 na 40 na wanatarajiwa kukabidhiwa idara ya Uhamiaji kwa ajili ya taratibu zingine ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani kwa tuhuma zinazowakabili.

Wakati huo huo mtu mmoja ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja mwenye umri unaokadiriwa kuwa kati ya (25) na (28) amekufa kwa kujinyonga kwa kutumia kamaba ya katani.

Alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 22 mwaka huu majira ya saa 2 usiku Kijiji cha Kibiki kata ya Bwiringu Tarafa ya Chalinze.

"Mfanyakazi wa shambani wa mwenyekiti wa Kijiji hicho alimpa taarifa bosi wake aitwaye Ally Hussein (47) kuwa kuna mtu kajinyonga kwenye banda lake ambaye naye alitoa taarifa polisi kuhusiana na tukio hilo," alisema kamanada Mwambalaswa.

Aliongeza kuwa marehemu aliacha ujumbe amabo uliandikwa kwenye karatasi kuwa anawaachia dunia ili waishi miaka 120, hakuna mtu aliyekamatwa na polisi wanaendelea na uchunguzi juu ya tukio hilo.

mwisho.  

Thursday, August 21, 2014

UTINGO AFA AJALINI OFISA WA OFISI YA DCI ANUSURIKA AJALINI

Na John Gagarini, Kibaha
UTINGO wa lori la mizigo Adam Rashid (28) mkazi wa Bwiringu kata ya Pera wilaya ya Bagamoyo amekufa baada ya lori alilokuwa akisafiria kugongana na lori lingine
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kaimu kamanda wa polisi mkoani humo Mrakibu Msaidizi wa Polisi (SSP) Athuman Mwambalaswa alisema kuwa malori hayo yaligongana uso kwa uso.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 19 mwaka huu majira ya saa 10 jioni eneo la Sweet Corner.
“Marehemu alikuwa kwenye gari namba T 650 BED aina ya Fuso lililokuwa likiendeshwa na na Ramadhan Mwarami (40) mkazi wa Bwiringu likiwa limebeba simenti likitokea Jijini Dar es Salaam kwenda Chalinze,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Alisema kuwa lori alilokuwa amepanda marehemu liligongana na lori lenye namba za usajili T 853 APA aina ya Fuso ambalo lilikuwa likitokea mkoani Mbeya kwenda Dar es Salaam likiwa limebeba Mahindi likiendeshwa na Shan Iddi (28) mkazi wa Mwanga liligongana na lori hilo na kusababisha kifo hicho.
Aidha alisema kuwa dereva wa lori alilokuwa amepanda marehemu aliumia kidogo ambapo marehemu alifariki dunia wakati akipata matibabu kwenye hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani ya Tumbi.
Wakati huo huo Ofisa Mwandamizi wa jeshi hilo anayeshughulikia majalada ya kesi katika ofisi ya mkurugenzi wa makosa ya jinai  (DCI) Ilembo amenusurika kifo baada ya gari alilokuwa akisafiria kugonga mti.
Akifafanua kuhusiana na tukio hilo Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa ofisa huyo alikuwa akitokea mkoani Iringa kikazi.
Alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 20 mwaka huu majira ya saa 9 alfajiri eneo la Vigwaza kata ya Pera wilayani Bagamoyo.
“Chanzo cha ajali hiyo ni gari hilo la polisi kutaka kugongana uso kwa uso na gari lingine baada ya kulipita gari lililokuwa mbele yao na alipotokeza akakutana na hilo gari hali iliyofanya dereva akwepe kisha kuserereka kwenye mtaro na baadaye kugonga mti,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa gari hilo lilipasuka matairi na vioo vilivunjika ambapo gari lililohusika na tukio hilo halikuweza kusimama mara baada ya tukio hilo

Mwisho.

Thursday, August 14, 2014

johngagariniblog: KAMATI ZA MADIWANI SARAKASI TUPU NA DIWANI CHADEMA...

johngagariniblog: KAMATI ZA MADIWANI SARAKASI TUPU NA DIWANI CHADEMA...:  Baadhi ya madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani wakiwa kwenye kikao cha baraza hilo kilichofanyika leo mjini Kibaha  Na...

DEREVA TEXI ALIYEPOTEA SIKU 8 AKUTWA AMEKUFA

Na John Gagarini, Kibaha
BAADA ya dereva wa Texi Richard Ponera (36) mkazi wa Mwendapole wilayani Kibaha mkoani Pwani kupotea kwa siku nane amepatikana akiwa ameuwawa  na kuporwa gari alilokuwa akiliendesha.
Marehemu ambaye alikuwa akifanyia shughuli zake kwenye kituo kikuu cha Mabasi cha Maili Moja wilayani humo alipotea Agosti 6 Mwaka huu majira ya saa 1 usiku alipokodishwa na watu wawili wasio fahamika waliojifanya kuwa ni wateja.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani humo Mrakibu Msaidizi wa Polisi (SSP) Athuman Mwambalaswa alisema kuwa mwili wake ulitupwa vichakani.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa mwili wa marehemu ulikutwa huko eneo la Mihande Mashambani Mlandizi wilayani Kibaha ukiwa umeharibika vibaya huku gari  alilokuwa akiendesha lenye namba za usajili T 905 BHT aina ya Corolla nyeupe.
“Chanzo cha mauaji hayo ni katika kuwania mali ambayo ni gari hilo ambalo halijapatikana na hakuna mtu ambaye amekamatwa hadi sasa na bado uchunguzi unaendelea kuwatafuta watu waliohusika na tukio hilo,” alisema Mwambalaswa.
Alisema kuwa jeshi hilo linaendelea kufuatilia juu ya tukio hilo na halitasita kumchukulia hatua kali za kisheria watu waliohusika na tukio hilo la kusikitisha, marehemu alizikwa juzi na ameacha watoto wawili ambao ni Ruben (14) anayesoma kidato cha kwanza St Anne na Kontrada anayesoma darasa la sita shule ya Msingi Jitegemee Jijini Dar es Salaam.

Mwisho. 

Sunday, August 10, 2014

johngagariniblog: DEREVA TEXI APOTEA MAZINGIRA YA KUTATANISHA ALIKOD...

johngagariniblog: DEREVA TEXI APOTEA MAZINGIRA YA KUTATANISHA ALIKOD...: Na John Gagarini, Kibaha DEREVA wa Texi wa Maili Moja Richard Ponera (36) mkazi wa Mwendapole wilayani Kibaha mkoani Pwani amepotea k...

POLISI YAKANUSHA MTU KUCHUNWA NGOZI PWANI


JESHI la Polisi mkoani Pwani limekanusha uvumi ulioenea na kudai kuwa mkazi wa Kijiji cha Dondo wilaya ya Mkuranga Hamis Mahimbwa (20) kuwa amekufa kwa kuchunwa ngozi mwili mzima ila ni kutokana na kuungua na moto.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana mjini Kibaha kaimu kamanda wa Polisi mkoani humo mrakibu Msaidizi wa Polisi (SSP) Athuman Mwambalaswa amesema kuwa hakuna tukio kama hilo mkoani hapo.
Akifafanua juu ya tukio la mtu huyo kufa amesema kuwa mnamo Agosti 6 mwaka huu majira ya saa 2:00 usiku huko katika kijiji cha Dondo Tutani kata ya Kisiju wilayani humo Hamis Mahimbwa (27) alikutwa na wananchi akiwa ameungua moto mwili mzima.
Kamanda Mwambalaswa amesema marehemu alipiga kelele kuomba msaada baada ya kuungua na moto na kumchukua na kumpeleka hospitali kwenye kituo cha afya cha Kalole Kisiju na kuanza kupatiwa matibabu lakini kutokana na kuungua sana na moto alifariki dunia Agosti 7 mwaka huu majira ya saa 11:00 alfajiri.
Amesema kuwa baada ya kifo hicho ilipelekwa taarifa kwenye kituo cha polisi cha Mkuranga na jalada la uchunguzi MKU/IR/1202/2014 lilifunguliwa ili kubaini kifo chake.
Amebainisha kuwa baada ya kufunguliwa jalada hilo Ofisa Mpelelezi Mkuu wa Polisi wa makosa ya Jinai wa wilaya akiwa na timu ya askari wa upelelezi waliungana na maofisa wa usalama waliungana na Daktari wa wilaya ya Mkuranga Kibela kwenda kwenye eneo la tukio na kituo cha afya cha Kisiju kwa uchunguzi zaidi wa tukio hilo.
Aidha amesema kuwa daktari alichukua sampuli ya ngozi ambapo kwenye eneo la tukio ilikutwa suruali, majivu ya tisheti aliyokuwa amevaa, kandambili, kibiriti, chupa ya plastiki ya soda ambayo ilikuwa na mafuta ya petroli na katika eneo hilo hakukuwa na purukushani ya watu wengi ambapo mashahidi waliokwenda kumsaidia alipopiga kelele walimkuta marehemu akiwa anongea na kudai kuwa ameungua kwa moto bila ya kusema aliye muunguza.
Kaimu kamanda wa polisi huyo wa mkoa wa Pwani amesema baba mlezi wa marehemu Athuman Mahimbwa alipohojiwa alisema kuwa mwanae alikuwa akiugua ugonjwa wa Kifafa kwa miaka 17 na alimwambia kuwa anakufa kwa kuungua na moto na kutokana na uchunguzi uliofanywa na polisi pamoja na daktari umebainisha kuwa kifo chake kimesababishwa na moto na si kuchunwa ngozi.



Saturday, August 9, 2014

DEREVA TEXI APOTEA MAZINGIRA YA KUTATANISHA ALIKODISHWA NA WATU



Na John Gagarini, Kibaha
DEREVA wa Texi wa Maili Moja Richard Ponera (36) mkazi wa Mwendapole wilayani Kibaha mkoani Pwani amepotea katika mazingira ya kutatanisha baada ya kukodishwa na watu wasiofahamika.
Ponera alikodishwa na watu wawili ambao hawakufahamika  Agosti 5 mwaka huu majira ya saa 2:30 usiku akiwa anaendesha gari lenye usajili na T 905 BHT aina ya Corolla nyeupe.
Akizungumza na mjini Kibaha kuhusina na tukio hilo katibu wa Umoja wa madereva Texi Kibaha Mjini (KITAGURO) Fadhil Kiroga alisema kuwa dereva huyo tangu alipoondoka siku hiyo hadi leo hakurudi na hakuna taarifa yoyote  iliyopatikana juu yake.
Kiroga alisema kuwa siku ya tukio hilo Ponera alionekana akipatana na watu hao kwa muda kidogo kama dakika 10 hivi kisha akaondoka na watu hao ambao walikuwa wawili.
“Baada ya mapatano licha ya kuwa madereva wengine hawakuweza kujua walichokuwa wakiongea na Ponera waliondoka na alipofika Mlandizi aliwasiliana na mwenzetu ambaye ni Salum Mbawala na kumwambia kuwa kwa sasa yuko Mlandizi,” alisema Kiroga.
Alisema kuwa baada ya hapo simu yake haikuweza kupatikana tena kwani baada ya kuona harudi wenzake walijaribu kumpigia lakini simu yake haikupatikana tena.
“Ponera hapa alikuwa hana muda mrefu tangu aanze kazi na alipata gari hilo ambalo alikuwa amekabidhiwa kama wiki mbili zilizopita na gari lenyewe halikuwa kwenye hali nzuri sana kusema labda ilikuwa ni kishawishi cha watu labda kutaka kuliiba gari hilo, hatujui kilichomtokea mwenzetu,” alisema Kiroga.
Aidha alisema kuwa wamefanya jitihada mbalimbali ambapo walikwenda polisi kutoa taarifa juu ya tukio hilo na kupewa namba KMM/RB/847/2014 pia walitoa taarifa kwenye vituo vya Mlandizi na Tumbi kisha kutembelea maeneo ya Yombo, Miswe na Mzenga bila ya mafanikio.
Kwa uapande wake mke wa dereva huyo Rosemary Urasa (31) alisema kuwa siku ya tukio hilo alikuja naye hadi Maili Moja yeye akenda sokoni kununua vitu vya nyumbani akamwacha stendi kwa ajili ya kuendelea na shughuli zake kama kawaida.
“Nakumbuka majira ya saa 5 asubuhi nilimpigia simu baada ya gari linguine ambalo liko hapa nyumbani lilikuwa linapiga honi lenyewe nikamwambia aje alizime lakini kwa bahati nzuri kuna mtu alifanikiwa kulizima nikamjulisha alikuwa njiani kuja lakini akarudia eneo linaloitwa Picha ya Ndege, toka hapo kila nikipiga simu simpati,” alisema Urasa.
Alibainisha kuwa mumewe ambaye wamezaa naye watoto wawili walihamia Kibaha baada ya kufanikiwa kujenga na kuzaa watoto wawili ambao ni Ruben (14) anayesoma kidato cha kwanza St Anne na Kontrada anayesoma darasa la sita shule ya Msingi Jitegemee.
Aidha alisema kuwa wakati mwingine mumewe hufanya kazi na kukesha hivyo siku hiyo usiku alijua kuwa atakesha lakini ilipofika asubuhi alishangaa kutokumwona kwani endapo anakuwa amekesha asubuhi ni lazima arudi lakini siku hiyo hakumwona ikambidi aje kwenye eneo analopaki lakini alipouliza wakasema tangu alivyoondoka jana hajaonekana tena.
Naye mmiliki wa gari hilo Athuman Kimia alisema kuwa siku hiyo ya tukio aliwasiliana na Ponera ambapo kulikuwa na tatizo la kulipia gari linapokuwa barabarani na kumpa 170,000 kwa ajili ya kulipia.
Kimia alisema kuwa baada ya kama saa moja alimpigia na kumwambia kila kitu kashalipia hivyo mambo mazuri na ndipo alipoendelea na shughuli kama kawaida.
“Tumekubaliana kila baada ya wiki awe ananipa malipo ya kazi lakini nilipigiwa simu kuambiwa kuwa Ponera aonekani na nilipojaribu kumpigia simu yake haipatikani sijui kilichomtokea ninini kwani yeye huwa ananipigia endapo kumetokea tatizo kwani sasa hivi ni wiki ya pili tangu nimkabidhi gari ,” alisema Kimia.
Mwisho.

Monday, August 4, 2014

WASOMI WATUMIE TAALUMA ZAO KULETA MAENDELEO

Na John Gagarini, Chalinze
WASOMI kwenye Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wametakiwa kutumia elimu yao kukabiliana na changamoto za kimaendeleo zilizopo jimboni humo.
Hayo yalisemwa na Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alipokuwa akizindua maktaba ya shule ya sekondari ya Chalinze iliyojengwa na na kampuni ya kutengeneza saruji ya Tanga Simenti huku taasisi ya Read International ikiwa imetoa msaada wa vitabu.
Ridhiwani alisema kuwa jimbo hilo lina changamoto nyingi ambazo nyingine zitatatuliwa na wasomi wanaotoka eneo hilo na wengine kwa lengo la kuleta maendeleo.
“Elimu mnayosoma iwe chachu na ya maana kwa kuleta maendeleo ya jimbo hili kwani wazazi wenu wanajitolea kuwasomesha ili baadaye na nyie muweze kuwa msaada kwa jamii na  elimu ya sasa inaendana na vitendo ambavyo ndiyo tafsiri  kwa vile wanavyokuwa wamejifunza wanafunzi na si kuwa wasomi jina ambao hawana msaada kwa jamii inayowazunguka,” alisema Ridhiwani.
Alibainisha kuwa maktaba ambayo tumeizindua leo iwe chanzo cha nyie kujifunza kwa bidii kwa kujisomea baada ya walimu kuwafundisha kwani Watanzania kwa sasa bila ya elimu ni kazi bure na hataweza kufanya jambo lololote la kimaendeleo.
Kwa upande wake kaimu meneja biashra wa kampuni ya Tanga Simenti Yasin Hussein alisema kuwa wamejenga jengo hilo kwa lengo la kuhakikisha shule hiyo inakabiliana na tatizo la ukosefu wa maktaba ambapo hutoa asilimia moja ya faida ya mapato wanayopata kwa kurudisha kwa jamii kwa kusaidia masuala mbalimbali yakiwemo ya mazingira, elimu na afya.
“Tumetumia kiasi cha shilingi milioni 47 kwa ajili ya ujenzi huu ambapo mpango ni kujenga maktaba kwenye shule za Mingoyo Lindi na Kinyerezi Jijini Dar es Salaam na watatumia zaidi ya shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa maabara na maktaba kwenye mikoa mbalimbali nchini,” alisema Hussein.
Naye mwalimu mkuu wa shule hiyo Emanuel Kahabi alisema kuwa ufunguzi wa maktaba hiyo utasaidia kukabiliana na changamoto ya maktaba ailiyokuwa inakabili shule yao ambayo ina wanafunzi 879.
Mwisho.

Picha no 1397 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani akiongea wakati wa ufunguzi wa makataba ya shule ya sekondari ya Chalinze kushoto ni mwenyekiti wa bodi ya shule Mbwana Madeni na kulia ni mkuu wa polisi wilaya ya Chalinze Janeth Magori.

picha no 1389 Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akiweka alama kwenye ukuta kama alama ya kumbukumbu baada ya kuizindua makta ya shule ya sekondari ya Chalinze.

picha no 1369 Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya Chalinze wakimsikiliza Mbunge wa Chalinze Riidhiwani Kikwete maara baada ya kuzindua maktaba ya shule hiyo.

picha no 1391 Mwenyekiti wa bodi ya shule ya sekondari ya Chalinze kushoto Mbwana Madeni akiongea katikakati ni Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete na katikati mkuu wa polisi kanda maalumu wilaya ya Chalinze Janeth Magori.

picha no 1371 wanafunzi wa shule ya sekondari ya Chalinze wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete wakati wa uzinduzi wa maktaba ya shule.

 

Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani akiongea wakati wa ufunguzi wa makataba ya shule ya sekondari ya Chalinze kushoto ni mwenyekiti wa bodi ya shule Mbwana Madeni na kulia ni mkuu wa polisi wilaya ya Chalinze Janeth Magori.
 


Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete akiweka alama kwenye ukuta kama alama ya kumbukumbu baada ya kuizindua makta ya shule ya sekondari ya Chalinze.
 

 

Baadhi ya wanafunzi wa shule ya sekondari ya Chalinze wakimsikiliza Mbunge wa Chalinze Riidhiwani Kikwete maara baada ya kuzindua maktaba ya shule hiyo.



Mwenyekiti wa bodi ya shule ya sekondari ya Chalinze kushoto Mbwana Madeni akiongea katikakati ni Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete na katikati mkuu wa polisi kanda maalumu wilaya ya Chalinze Janeth Magori.
 

 

picha no 1371 wanafunzi wa shule ya sekondari ya Chalinze wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete wakati wa uzinduzi wa maktaba ya shule.