Tuesday, April 30, 2024

*BMH YAHUDHURIA UFUNGUZI WA MKUTANO WA 24 BARAZA LA MAWAZIRI* *SEKTA* *YA* *AFYA* *EAC*

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) imehudhuria ufunguzi wa Mkutano wa Kawaida wa 24 wa Baraza la Mawaziri la sekta ya Afya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) jijini Dar es Dar es Salaam. 

Mkutano huo wa siku tano, ulioanza leo tarehe 29 Aprili hadi Mei 3,  unafanyika kwa njia ya mseto (video na ana kwa ana) umeanza katika ngazi ya wataalam ukilenga kufanya tathimini ya utekelezaji wa maagizo na makubaliano yaliyofikiwa katika mkutano wa 22 wa Baraza hiloa mbapo taarifa itawasilishwa katika Mkutano wa Makatibu Wakuu.

Mkutano utafuatiwa na ngazi ya Makatibu Wakuu tarehe 2 Aprili 2024, ambapo taarifa itawasilishwa, Makatibu na kuhitimishwa na Mkutano ngazi ya Mawaziri ukaofanyika Mei 3.

Mbali na kufanya tathimini ya utekelezaji wa maagizo na makubaliano yaliyofikiwa katika mkutano wa 22 wa Baraza hilo, Mkutano huo utajadili agenda nyingine zinazotarajiwa ikiwemo Mkutano taarifa za Vikundi Kazi (Technical Working Group – TWG) sita (06) vya Sekta ya Afya na mapendekezo ya Tanzania ya kuanzisha Kituo cha Umahiri cha Upandikizaji Uloto na Sayansi ya Matibabu ya Magonjwa ya Damu chini ya Hospitali ya Benjamin Mkapa. 

Akizungumza katika ufunguzi wa Mkutano huo, Mganga Mkuu wa Serikali wa Tanzania Prof. Tumaini Nagu, ametoa rai kwa wataalamu wa sekta ya Afya ya EAC kutoa michango itayosaidia Jumuiya kuimarisha miundombinu ya huduma ya afya ili kukabiliana na matishio ya kiafya kwa magonjwa yanayoambukiza na yasiyoambukiza.

“Tumekuja kujadili na kutoa suluhisho na majawabu yatakayotusaidia kukabili changamoto za kiafya katika Jumuiya yetu kwa kuzingatia ubunifu na weledi katika mifumo yetu ya afya huku tukiwa wamoja na wenye nguvu zaidi” amesema Prof. Nagu

Pro. Nagu amehimiza umuhimu wa Sekta ya Afya katika Jumuiya kuendelea kufanya kazi kwa ufanisi na umoja katika utekelezaji progamu mbalimbali za Afya ikiwemo miradi ya Sekta ya Afya na mikakati inayopangwa ili kufikia mafanikio yanayotarajiwa kwa wakati.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Sekta ya Jamii katika Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dkt. Irene Isaka, ameeleza kuwa kupitia mkutano huo nchi wanachama watapata fursa ya kusikia taarifa zitakazowasilishwa na kila nchi ili kwa pamoja kuweza kuchangia na kushauri namna bora ya kusimamia na kutekeleza programu, miradi na miundombinu ya Afya katika Jumuiya.

Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo umeongozwa na Mganga Mkuu wa Serikali, Prof. Tumaini Nagu na wajumbe kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambapo imewakilishwa na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Miundombinu ya Uchumi na Huduma za Jamii Mhandisi Abdillah Mataka. 

Wengine kutoka Tanzania walioshiriki Mkutano huo ni pamoja na Wizara za Afya (Tanzania Bara na Zanzibar), Hospitali ya Benjamin Mkapa, Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Kituo cha Umahiri cha Magonjwa ya Moyo na Mishipa ya Damu cha Afrika Mashariki, Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Mamlaka ya Chakula na Dawa (TMDA), Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Ukimwi (NACP), Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS) Bohari ya Dawa (MSD), Maabara Kuu ya Taifa, Mpango wa Kitaifa wa Kudhibiti Malaria (NAMCP) na Mamlaka ya Chakula na Dawa Zanzibar (ZFDA).

Monday, April 29, 2024

MWENGE KUPITIA MIRADI YA TRILIONI 8.6

MWENGE wa Uhuru umeanza mbio zake Mkoani Pwani ukitokea Mkoani Morogoro ambapo utapitia miradi 126 ya maendeleo yenye thamani ya shilingi trilioni 8.5.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Mkoa huo Abubakar Kunenge alipoupokea Mwenge huo eneo la Bwawani Halmashauri ya Chalinze Wilaya ya Bagamoyo, kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Adam Malima.

Kungenge alisema kuwa kati ya miradi hiyo 18 itawekewa mawe ya msingi 22 itazinduliwa 86 itakaguliwa.

"Miradi hiyo imefanikiwa kutokana na Rais kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na ushirikiano kati ya viongozi, wananchi na wadau wa maendeleo katika kutafuta fedha hasa ikizingatiwa Pwani ni Mkoa wa kimkakati,"alisema Kunenge.

Kwa upande wake kiongozi wa mbio za Mwenge Godfrey Eliakim Mzava alisema kuwa wanapofika kwenye miradi ya maendeleo wakute taarifa sahihi za utekelezaji wa miradi ya maendeleo pia nyaraka zote za msingi zinazoeleza utekelezaji wa miradi iliyoyopo na wataalamu watoe maelezo ya kina na vifaa vya upimaji ubora wa miradi viwepo.

Mwisho. 




Saturday, April 27, 2024

MKUU WA MKOA WA PWANI ABUBAKAR KUNENGE ATAKA SHERIA ICHUKUE MKONDO WAKE WALIOMDHALILISHA DK KAWAMBWA

MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amelitaka jeshi la Polisi Wilayani Bagamoyo kumchukulia hatua za kisheria Hassan Usinga "Wembe" kwa tuhuma za kumdhalilisha aliyewahi kuwa Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo na Waziri wa Miundombinu Dk Shukuru Kawambwa.

Kunenge ameyasema hayo wakati wa kikao baina ya Dk Kawambwa na Wembe na baadhi ya viongozi wa Wilaya ya Bagamoyo akiwemo Mkuu wa Wilaya Halima Okash na Mkurugenzi wa Halmashauri Shauri Selenda na baadhi ya wakuu wa idara mbalimbali. 

Alisema kuwa suala hilo limesababisha kuhatarisha usalama wa Mkoa na taharuki kwa baadhi ya watu nchini kutokana na kitendo hicho cha udhalilishaji ikiwa ni pamoja na kufungwa pingu kwa kiongozi huyo mstaafu ambapo serikali haikubaliani nacho.

"Mwekezaji wa machimbo hayo ya mchanga ana vibali vyote vya umiliki na uchimbaji lakini changamoto iliyotokeza ni uharibufu wa barabara uliofanywa na malori ya yanayopita hapo yanayobeba mchanga na kuharibu barabara kutokana na uzito mkubwa na kusababisha wananchi kuifunga,"alisema Kunenge.

Naye Dk Kawambwa alisema kuwa alifungwa pingu na mtuhumiwa huyo akishirikiana na mgambo Abdala Mgeni na kusukumwa hali ambayo ilimfanya ajisikie vibaya.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo Halima Okash alisema kuwa mwekezaji aliomba kibali cha shughuli za uchimbaji mchanga na baraza la madiwani likamkubalia baada ya kufuata taratibu zote kuanzia ngazi ya chini.

Meneja wa Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) Wilaya ya Bagamoyo Bupe Angetile alisema kuwa walizuia kutumika barabara hiyo ilifungwa kutokana na kuharibika lakini bado iliendelea kutumika kupitisha malori ya mchanga ambapo inauwezo wa kutumika na malori yenye uzito wa tani 10.

WAWILI MATATANI KUMDHALILISHA DK KAWAMBWA

JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani limewakamata watuhumiwa wawili Hassan Usinga au Wembe na Abdallah Mgeni kwa tuhuma za kumdhalilisha aliyewahi kuwa Waziri wa Miundombinu Dk Shukuru Kawambwa.

Aidha Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linamtaka mtu aliyechukua na kusambaza video hiyo mitandaoni ajisalimishe kituo cha Polisi Bagamoyo
mara moja.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha Kamanda wa Polisi Mkoani Pwani (SACP) Pius Lutumo alisema kuwa tukio hilo lilitokea Aprili 24 saa 8 mchana huko Kitopeni Wilaya ya Bagamoyo.

Lutumo alisema kuwa tukio hilo lilionekana kupitia mitandao ya kijamii ambapo video ilionekana ikimwonyesha Waziri na Mbunge mstaafu Dk Shukuru Jumanne Kawambwa akishambuliwa kwa maneno makali na kudhalilishwa kwa kufokewa na
kutishiwa kufungwa pingu kama mhalifu na watuhumiwa hao hali ambayo iliyosababisha taharuki kubwa kwa jamii.

"Video hiyo ilionyesha Dk Shukuru Jumanne Kawambwa na mtu mwingine aitwaye Cathbert Enock Madondola walishambuliwa ambapo watuhumiwa hao baadae walipewa dhamana kwa mujibu wa sheria na watafikishwa mahakamani mara upelelezi utakapokamilika,"alisema Lutumo.

Alisema kuwa Wembe alifanya tukio hilo akiwa na askari mgambo aitwaye Abdala Mgeni ambapo chanzo cha tukio hilo ni magari ya mchanga ya mtuhumiwa kuharibu barabara na mashamba.

"Mtuhumiwa alifikia hatua hiyo baada ya magari yaliyokuwa yakienda kuchukua mchanga kwa mbali ya kuharibu barabara wakati yakipita kwenda kubeba mchanga eneo hilo hali iliyosababisha wananchi kufunga barabara kwa magogo ili kuzuia uharibifu huo wa barabara,"alisema Lutumo.

Kamanda Lutumo alisema kuwa Dk Kawambwa ni moja ya  wakazi wa eneo hilo ambapo walijaribu kuyazuia magari hayo ili kupunguza uharibifu.

Thursday, April 25, 2024

TFS YATOA MILIONI 20 KWA WANANCHI WA RUFIJI NA KIBITI WALIOKUMBWA NA MAFURIKO

WAKALA wa Misitu Tanzania (TFS) imetoa fedha kiasi cha shilingi milioni 20 kwa ajili ya wananchi wa Wilaya za Rufiji na Kibiti Mkoani Pwàni ambazo zimekumbwa na mafuriko.

Akikabidhi mfano wa hundi Meneja Uhusiano wa (TFS) Johary Kachwamba kwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amesema kuwa fedha hizo ni kusaidia mahitaji mbalimbali.

Kachwamba amesema kuwa wana misitu zaidi ya 10 yenye ukubwa wa hekari 32,000 hivyo wameona watoe pole kwa wananchi waliokumbwa na changamoto ya mafuriko.

Amesema kuwa wataendelea kushirikiana na serikali kusaidia sehemu mbalimbali zilizokumbwa na changamoto kama hizo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Pwani ameishukuru TFS kwa kujitolea fedha hizo kwani zitaweza kusaidia wananchi hao kuweza kukabili baadhi ya mahitaji.

Kunenge amesema kuwa mbali ya kutoa fedha hizo pia wametoa eneo kwenye Kitongoji cha Chumbi B ambapo wananchi wa Muhoro watahamishiwa hapo.

Amesema wanaishukuru TFS katika jitihada za kulinda na kutoa elimu juu ya kuhifadhi mazingira na kuhamasisha matumizi ya nishati mbadala.

Aidha amesema wanashauri wananchi kuondoka kwenye eneo ambalo ni mkondo wa Bonde la Mto Rufiji na wananchi wakae maeneo ambayo si hatarishi kwa mafuriko.

Wednesday, April 24, 2024

PROFESA MKENDA ATAKA WATOTO WENYE CHANGAMOTO MAFURIKO WASAKWE WAENDE SHULE

WANAFUNZI ambao shule zao zimekumbwa na mafuriko nchini wataruhusiwa kusoma shule ambazo ziko jirani na wanakoishi ili wasikose masomo.

Hayo yalisemwa na Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda alipotembelea kujionea hali halisi kwenye maeneo yenye taasisi za shule ambao zimekumbwa na mafuriko na kutoa misaada ya vifaa vya shule kwa baadhi ya Shule kwenye Wilaya ya Rufiji na Kibiti Mkoani Pwani.

Mkenda alisema kuwa wanafunzi ambao Shule zao zimekumbwa na mafuriko na hawataweza kusoma kutokana na mazingira hayo kuwa hatarishi na Shule kufungwa wanafunzi hao watasoma maeneo ambayo wazazi wao wamehamia ili wasikose elimu.

“Mfano tumejionea Shule ya Msingi Muhoro ili wanafunzi waende Shule inabidi wapande Mitumbwi kama sisi tulivyoapanda kiusalama siyo sawa kwani ni hatari kwa maisha yao na hata nyumba za walimu tumeona zimezingirwa na maji kwa hali hiyo ni vigumu Shule hiyo kuendelea kutumika hivyo wanafunzi hao wasome popote pale walipo ambapo ni jirani na wanapoishi kwani serikali haitaki mtoto akose elimu,”alisema Mkenda.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Caroline Nombo alisema kuwa wanaendelea kufuatilia maeneo yote nchini ambayo yanachangamoto za mafuriko ili kuhakikisha wanafunzi wanasoma pia kutoa vifaa kwa wanafunzi na walimu ili kwa wale ambao vifaa vyao vimeharika na mafuriko wanapatiwa vingine ili masomo yaendelee.

Naye mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge alisema kuwa wamechukua jitihada mbalimbali za kukabili changamoto hiyo ya mafuriko ambapo kwenye Shule ya Msingi Muhoro wameifunga Shule hiyo na nyingine na kuruhusu wanafunzi  kusoma kwenye Shule ambazo wako jirani nazo na hazina changamoto ya mafuriko.

Naye Ofisa Elimu Mkoa wa Pwani Sara Mlaki alisema kuwa Shule zilizoathirika na mafuriko Wilaya ya Rufiji ni 11 zenye wanafunzi 7,264 wasichana wakiwa ni 3,657 na wavulana 3,607 walimu 58 ambao nyumba zao zimeathirika.

Monday, April 22, 2024

SERIKALI IMEENDELEA KUTENGA FEDHA MIRADI YA NISHATI

 

Wellu Mtaki, Dodoma 

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kutenga fedha za kutekeleza miradi ya nishati ambapo katika kipindi cha miaka mitatu zaidi ya shilingi trilioni 8.18 zilitolewa.

“Maono na maelekezo yake kuhusu usimamizi wa sekta hii yamekuwa na mchango mkubwa katika ufanisi wa shughuli za sekta, katika hili, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuweka kipaumbele kikubwa katika utekelezaji wa miradi ya nishati.”

Aidha amesema kuwa Katika kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa umeme nchini, tayari nchi yetu imeanza kutumia umeme wa bwawa la Julius Nyerere Hydropower Project (JNHPP). Huu ni ushindi na kielelezo tosha kwamba Mama yupo kazini.

Ametoa pongezi hizo jioni (Ijumaa, Aprili 19, 2024) wakati akifunga Maonesho ya Wiki ya Nishati yaliyofanyika kwenye viwanja vya Bunge jijini Dodoma.

Waziri Mkuu amelipongeza Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kwa kuweza kuzalisha umeme zaidi ya mahitaji yaliyopo sasa. 

“Leo tarehe 19 Aprili, 2024 uzalishaji wa umeme ni mkubwa. Shirika letu la TAMESCO limemudu kuzalisha umeme zaidi ya mahitaji tuliyonayo na bwawa la Julius Nyerere Hydropower Project limeanza kazi na tayari megawati 235 ziko kwenye mfumo.”

Ameitaka Wizara hiyo iweke mkakati wa kuhakikisha maonesho hayo yanakuwa endelevu ili Waheshimiwa Wabunge waweze kupata fursa ya kuwasilisha hoja zao mahsusi na kutatua kero za wananchi wanaowawakilisha.

Kutokana na kuongezeka kwa idadi ya washiriki wa maonesho hayo ikilinganishwa na miaka miwili iliyopita, Waziri Mkuu ameitaka Wizara hiyo ione uwezekano wa kuandaa maonesho kama hayo katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri. “Wakurugenzi wa Kanda na Mameneja wa Mikoa na Wilaya mko hapa. Nendeni mkae na muangalie jinsi ya kutekeleza jambo hilo,” amesisitiza.

Ameitaka Wizara hiyo iweke mkakati wa kuhakikisha wananchi wote wanapata ufafanuzi wa masuala mbalimbali kuhusu fursa zinazopatikana kutokana na miradi inayotekelezwa na sekta ya nishati. “Pamoja na kuyaleta maonesho hapa Bungeni, kuna haja ya kupeleka maonesha kama haya kwenye maeneo ya katiati ya mji ili muweze kuwafikia wananchi wengi zaidi na kujibu hoja zao,” amesema.

Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na wadau mbalimbali walioshiriki  maonesho hayo, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko ameipongeza TANESCO kwa kuendelea kufanya kazi nzuri ya kuhakikisha wananchi wanapata nishati ya umeme.

Naye, Spika wa Bunge la Tanzania, Dkt. Tulia Ackson amesema sekta ya nishati ni kati ya sekta mtambuka kwa sababu inalisha sekta nyingine nyingi na ikitikisika, inatikisa na maeneo mengine pia.

Amesema pamoja na utoshelevu wa umeme kwenye gridi ya Taifa, ili kuwe na maendeleo bado nchi inahitaji umeme wa kutosha na hasa kwenye viwanda na siyo kuwasha taa za majumbani.

Ameitaka Serikali itafute njia ya kutumia vizuri maji yanayotoka kwenye bwa la JNHPP ili yaweze kuwanufaisha wananchi wanaoishi maeneo ya jirani na bwawa hilo. “Bwawa limejaa kwa hiyo Serikali ihakikishe maeneo ya jirani yanapata maji ya kutumia. Tuanzishe gridi ya maji kama ilivyo kwenye gridi ya umeme. Kule chini tutengeneze njia ya kutunza maji kwa ajili ya matumizi ya umwagiliaji na mifugo,” amesema.

Naye, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Mhandisi Felchesmi Mramba amesema ushiriki wa mwaka huu umevunja rekodi kwani watu zaidi ya 480 walitembelea maonesho hayo ambapo 267 walikuwa ni Waheshimiwa Wabunge.

Ameyataja maeneo ambayo washiriki walikuwa wakiulizia zaidi ni umeme, nishati ya jua, nishati jadidifu, nishati safi ya kupikia, mafuta na gesi.

Amesema ili kujenga uelewa mpana kwa wananchi, wanapanga kuandaa kongamano maalum juu ya gesi asilia ambalo linatarjiwa kufanyika Mei, mwaka huu.