Wednesday, May 31, 2023

WADAU WA MAENDELEO WATAKIWA KUTUMIA TAKWIMU ZA SENSA

KAMISAA wa Sensa Tanzania Bara Anne Makinda amewataka wadau wa maendeleo nchini kutumia takwimu za sensa ambazo zimefanywa kisayansi ili kutumia rasilimali kikamilifu.

Makinda aliyasema hayo Mjini Kibaha wakati wa mafunzo ya sensa kwa kamati ya mkoa na viongozi wa ngazi ya mkoa.

Alisema kuwa kwa kutumia takwimu hizo itasaidia wakati wa kupanga bajeti hivyo kuweka matumizi mazuri ya rasilimali ambapo viongozi mbalimbali wanapaswa kutumia matokeo ya sensa hiyo ili kuleta maendeleo kwa wananchi.

Naye Balozi Mohamed Haji Hamza Kamisaa wa Sensa Tanzania Zanzibar alisema kuwa hadi Juni mwakani machapisho 200 yatatolewa ili kuwajengea watu uelewa juu ya ripoti ya sensa.

Mwakilishi wa mtakwimu mkuu Adela Temba alisema kuwa matokeo ya sensa hutolewa kwa awamu ambapo ripoti kuu nne zimeshazinduliwa na Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ambaye alikuwa mgeni rasmi alisema kuwa takwimu za sensa ni muhimu sana katika matumizi ya rasilimali.


Sunday, May 28, 2023

RC KUNENGE KUIPA KIPAUMBELE MICHEZO

MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge amesema Mkoa utatoa kipaumbele kwenye michezo kwani ni moja ya ajira zenye utajiri mkubwa duniani.

Kunenge ameyasema hayo wakati akifunga michezo ya Umoja wa Michezo Taaluma Sanaa kwa Shule za Msingi Tanzania (UMITASHUMTA) mkoa wa Pwani kwenye viwanja vya Shirika la Elimu Kibaha (KEC) Tumbi.

Alisema kuwa miongoni mwa matajiri wakubwa duniani wanatokana na michezo hivyo ni sehemu ya kutoa ajira kwa watu wakiwemo vijana.

"Mkoa utaunga mkono kwa kuifanya sekta ya michezo kuwa kipaumbele kwa kutoa fursa mbalimbali zinazohusiana na michezo,"alisema Kunenge.

Aidha alisema kuwa ili nchi iweze kuwa na vipaji na wachezaji wazuri lazima michezo ianzie chini kabisa kama nchi ilivyoweka utaratibu wa michezo hiyo kwani washiriki ni watoto wadogo hivyo kuwajengea kujiamini.

"Michezo inakuza uchumi pia ni ajira na ni afya hivyo lazima iwezeshwe kwa kuwajengea vijana mazingira mazuri ya kuendeleza vipaji vyao,"alisema Kunenge.

Alisema kuwa michezo ya mwaka huu imebeba kauli mbiu ya Miundombinu ya elimu na taaluma nchini ni chachu ya maendeleo ya sanaa na Michezo. 

Aliwataka wanamichezo hao kudumisha nidhamu ili kuuletea mkoa ushindi.Jumla ya wanamichezo kutoka Halmashauri tisa zilichuana kwenye michezo mbalimbali. 

Friday, May 26, 2023

DK SAMIA AGAWA ARDHI HEKARI 5,520 KWA WANANCHI

Hayo yamesemwa leo Mei, 26 2023 na Mhe David Silinde (Mb.) Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi wakati wa makabidhiano ya ardhi  iliyokuwa sehemu ya Ranchi ya Ruvu kwenda kwa Wananchi wa Wilaya ya Bagamoyo na Kibaha ambapo pande zote zimeridhia.

Ameeleza uamuzi huo wa  Serikali ni kuwawezesha Wananchi kupata Ardhi kwa ajili ya Shughuli za kilimo, Mifugo na shughuli zingine za kijamii.

Makabidhiano hayo yamefanyika katika Ukumbi wa Ranchi ya NARCO Ruvu ukishuhudiwa na Viongozi wa Wilaya,Tarafa, Kata, Vijiji na Viongozi wa Wakulima na Wafugaji na wawakilishi wa Wananchi kutoka Vijiji 10. 

Akipongeza uamuzi huo Mhe Kunenge Mkuu wa Mkoa wa Pwani  amewaagiza Viongozi wa Mkoa na Wilaya kutimiza wajibu wao wa kusimamia kupanga matumizi ya Ardhi hiyo na kuwataka Wananchi kuheshimu Sheria na kwamba wasivamie tena eneo hilo la Serikali.

MIAKA 30 YA MISA TANZANIA


Na Wellu Mtaki, Dodoma

MSEMAJI  Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa amefungua Maadhimisho ya Miaka 30 ya Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Jangwa la Sahara Tawi la Tanzania (MISA Tanzania) na akiwasisitiza waandishi wa habari kuzingatia maadili ya uandishi wa habari.

Msigwa amesisitiza hilo leo Mei 25,2023 Jijini Dodoma wakati akimwakilisha Naibu waziri wa Habari, Mawasiliano na Tekonolojia ya Habari, Mhandisi Kundo Mathew wakati wa maadhimisho ya miaka 30 ya MISA.

Amesema serikali inaendelea kuboresha mazingira ya vyombo vya habari huku akisisitiza kuwa tangu Rais Samia Suluhu Hassan aingie madarakani hakuna chombo kilichofungiwa na vilivyokuwa vimefungiwa vimefunguliwa.

Aidha amesema katika kipindi hiki mafunzo au semina kwa waandishi zinahitajika hivyo kuiomba Misa Tanzania na wadau wengine kuwapatia mafunzo mbalimbali waandishi wa habari.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa MISA Tanzania, Salome Kitomari amempongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayofanya ya kuwatumikia Watanzania, lakini zaidi kwa namna amechukua hatua kadhaa zilizowezesha waandishi wa habari kutekeleza majukumu yao kwa kuondoa vikwazo vingi.

Kitomari amesema MISA Tanzania imepita kwenye safari ya miaka 30 yenye milima na mabonde na kutokana na mambo yote hayo ameupongeza uongozi, sekretarieti na wanachama wa MISA Tanzania kwa kushikamana mpaka kufikia hatua hiyo.

Sanjari na hayo ameongeza kuwa mafanikio mengine ni pamoja na kutoa mafunzo ya ndani na nje ya nchi kwa waandishi wa habari, Kuwezesha uanzishwaji wa vyombo vingine vya habari zikiwamo Radio za Kijamii na kufanya marekebisho kwenye sheria mbalimbali tangu Sheria ya Magazeti, Sheria ya Huduma za Habari, Sheria ya Haki ya Taarifa na nyinginezo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Misa Tanzania, Elizabeth Riziki amesema Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Jangwa la Sahara,Tawi la Tanzania (MISA Tanzania), inaadhimisha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1993 baada ya kikao cha wanahabari waliokutana Windhoek, Namibia kujadili mambo mbalimbali yaliyokuwa yanaukabili Ukanda wa Nchi za Kusini.

MISA ina matawi tisa katika nchi za Zambia, Msumbiji, Malawi, Lesotho, Botswana, Namibia, Angola, Tanzania na Zimbabwe ambako ndiyo makao makuu ya matawi yote.

Amefafanua kuwa katika mkutano huo wa siku mbili wadau watajadiliana kuhusu kasi ya mabadiliko ya kiteknolojia na namna ambavyo umma unahusishwa kwenye uhuru wa kujieleza na upatikanaji wa taarifa lakini pia watajadili changamoto zilizopo kwenye sekta ya habari na kuweka mkakati wa kuzitatua ikiwamo namna ya kuboresha maisha ya waandishi wa habari.

Pia amesema Majadiliano hayo yana lengo la kuongeza ukaribu na ushirikiano baina ya waandishi wa habari na Jamii, pia kuibua hoja zitakazowaleta pamoja Jamii na waandishi wa habari katika kuwa na mpango kazi wa utekelezaji ili kuhakikisha kila mwanajamii anatumia vizuri nafasi ya uhuru wa kujieleza kupitia vyombo vya habari kwaajili ya maendeleo endelevu.

Ikumbukwe kuwa Misa Tanzania inaadhimisha miaka 30 huku kauli mbiu ikiwa ni "Uhuru wa Kujieleza Msingi wa Haki Zote kwa Maendeleo Endelevu.

Thursday, May 25, 2023

SHULE ZA SEKONDARI TUMBI NA MWANALUGALI ZAPOKEA MILIONI 300

SHULE ya Sekondari ya Tumbi imepokea kiasi cha shilingi milioni 200 kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya shule.

Aidha Shule ya Sekondari ya Mwanalugali imepokea kiasi cha shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa bwalo la chakula.

6,052 WATAMBULIWA MTAA WA LUMUMBA WALIOVAMIA SHAMBA LA MITAMBA

MTAA wa Lumumba Halmashauri ya Mji Kibaha utambuzi wa wananchi waliovamia eneo imefanyika na kukamilika na jumla ya wananchi 6,052 wametambuliwa.

Hayo yalisemwa na Hamis Shomari ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya mipango miji na mazingira na diwani wa Kata ya Kongowe aliyasema hayo kwenye kikao cha kawaida kipindi cha robo tatu Januari-Machi cha baraza la madiwani wa Halmashauri ya Mji Kibaha.

Alisema kazi ya utambuzi wa wananchi waliovamia eneo imefanyika na kukamilika na kazi ua uandaaji michoro nane yenye jumla ya viwanja 7,264 imekamilika.

"Maandalizi ya upimaji katika mtaa wa Lumumba yamekamilika na kazi ya upimaji wa viwanja na matarajio ni kupima viwanja 7,264 ambapo itakamilika ndani ya miezi miwili,"alisema Shomari.


HALMASHAURI YA MJI KIBAHA YAFANYA UTAMBUZI WA WALIOVAMIA ENEO MTAA WA MKOMBOZI

HALMASHAURI ya Mji Kibaha imefanya utambuzi wa wananchi waliovamia maeneo kwenye Mtaa wa Mkombozi ambapo 4,509 wametambuliwa.

Hayo yalisemwa na Hamis Shomari ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya mipango miji na mazingira na diwani wa Kata ya Kongowe aliyasema hayo kwenye kikao cha kawaida kipindi cha robo tatu Januari-Machi cha baraza la madiwani wa Halmashauri ya Mji Kibaha.

Shomari alisema kuwa watu hao wametambuliwa ili kupimiwa viwanja 6,250 kwenye michoro 22 ambayo imeandaliwa na kuidhinishwa. 

"Kazi ya upimaji wa viwanja 6,300 imefanyika na kuwasilishwa kwa ajili ya uidhinishwaji wa ramani kwa mpima ardhi wa mkoa na jumla ya viwanja 3,950 vimeidhinishwa,"alisema Shomari.

Alisema kuwa uuzaji wa viwanja katika mtaa umeanza Machi 24 ambapo wananchi walijulishwa kwa njia ya matangazo na mkutano wa hadhara ambapo hadi Aprili jumla ya ankara ya viwanja 168 vyenye thamani ya shilingi milioni 129.2 zimetolewa.

HALMASHAURI YA MJI KIBAHA YAKUSANYA MABILIONI

HALMASHAURI ya Mji Kibaha imekusanya kiasi cha shilingi bilioni 3.5 sawa na asilimia 78 ya makisio ya mwaka 2022/2023 ikiwa ni mapato ya ndani ambapo ilikadiria kukusanya shilingi bilioni 4.5.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Selina Wilson wakati wa kikao cha baraza la madiwani kwa kipindi cha robo tatu Januari hadi Machi.

Wilson alisema kuwa makusanyo hayo ni kuanzia Julai 2022 hadi Machi 2023 ambapo kwa upande wa vyanzo fungwa makisio ilikuwa ni shilingi milioni 506.7.

"Na kwa kipindi cha kuanzia mwezi Julai 2022 mpaka Machi 2023 kiasi cha shilingi milioni 587.8 kimekusanywa sawa na asilimia 116 ya makisio ya mwaka,"alisema Wilson.


HALMASHAURI YA MJI KIBAHA YAKUSANYA MABILIONI



HALMASHAURI ya Mji Kibaha imekusanya kiasi cha shilingi bilioni 3.5 sawa na asilimia 78 ya makisio ya mwaka 2022/2023 ikiwa ni mapato ya ndani ambapo ilikadiria kukusanya shilingi bilioni 4.5.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Selina Wilson wakati wa kikao cha baraza la madiwani kwa kipindi cha robo tatu Januari hadi Machi.

Wilson alisema kuwa makusanyo hayo ni kuanzia Julai 2022 hadi Machi 2023 ambapo kwa upande wa vyanzo fungwa makisio ilikuwa ni shilingi milioni 506.7.

"Na kwa kipindi cha kuanzia mwezi Julai 2022 mpaka Machi 2023 kiasi cha shilingi milioni 587.8 kimekusanywa sawa na asilimia 116 ya makisio ya mwaka,"alisema Wilson.

Saturday, May 20, 2023

VYAMA VYA USHIRIKA KUUNGANISHWA NA WADAU


Na Wellu Mtaki, Dodoma

JUKWAA la maendeleo ya vyama vya ushirika  mkoa wa Dodoma limepanga kuwaunganisha vyama vya ushirika na wadau mbalimbali wakiwemo mabenki ili kuwawezesha kifedha pamoja na kuimalika kimtaji  viweze kupata maendeleo.

Hayo ameyasema  Jijini Dodoma Kaimu Mrajisi Msaidizi Mkoa wa Dodoma Octavia Bidyanguze wakati wa uzinduzi wa jukwaa la maendeleo ya vyama vya ushirika mkoa wa Dodoma 2023.

Bidyanguze amesema mkoa wa Dodoma una vyama vya ushirika 124 vikiwemo 57 vyama vya kifedha, 49 vyama vya  kilimo na masoko na vyama vinginevyo 18 hivyo kutokana na idadi hii jukwaa la maendeleo ya vyama vya ushirika linakwenda kuwajengea uwezo kwa maana ya kutoa elimu kwa vyama hivyo.

Amesema kuwa mpaka sasa vyama hivyo vimeweza kununua hisa zenye thamani ya 146.3 ili kuwa na uwezo  wa kusaidiana kwa wale wasio na uwezo wa kifedha.

Kwa upande wake Meneja wa UDOM SACCOS LTD Erasmus Tandike amesema kuwa Moja ya mikakati walio nayo ni kujitangaza na kuhakikisha ushirika huu unaazia ngazi ya chini ili kufikia wakazi wote wa Dodoma pamoja na  kuhakikisha kila vyama vinanufaika na vinafikia malengo.

Naye Mjumbe wa bodi ya PCCB SACOOS pia ni   Mratibu wa kongamano la Central Women Connect  Rashida Mfaume amewataka wanawake kukimbilia fursa ili kuweza kujikwamua kiuchumi na kijamii kama ambayo yeye  amenufaika na ushirika huu kwa maana ya kuweza  kuwekeza pamoja na kupata nafasi ya kukopa .

Ikumbukwe kuwa moja ya lengo la jukwaa hili ni kutoa fursa vyama vya ushirika, kuwakutanisha na kubadilishana uzoefu, kuelimishana na kuweza kujifunza mambo mbalimbali ya vyama vya ushirika.




Thursday, May 18, 2023

WIZARA VIWANDA NA BIASHARA KUANDAA MWONGOZO KWA WAFANYABIASHARA

MKURUGENZI wa uwezeshaji wananchi kiuchumi na maendeleo ya sekta binafsi ya TAMISEMI Conrad Milinga amesema kuwa Wizara ya Viwanda na Uwekezaji inaandaa mwongozo wa kuwawezesha wafanyabishara wajasiliamari kutambua kuwa wanapohitaji kuanzisha biashara sehemu ya kuanzia na kuishia.

Milingi ameyasema hayo Jijini Dodoma, katika kikao cha kuthibitisha rasimu ya muongozo wa wataalamu wa biashara na mpango wa kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini kilichofanyika katika ukumbi wa bodi ya wakandarasi.

Aidha amesema kuhusiana na taarifa za mwenendo wa bei za vyakula nchini wanahitaji kuzipata kuanzia kwao lakini zisitofautiane na zile zinazotolewa na wizara, hivyo waweke mfumo wa taarifa watakazo kuwa wanazipata kutoka kwao.

Kwa upande wake katibu tawala masidizi wa viwanda, biashara na uwekezaji mkoa wa Kigoma Deogratias Sangu, amesema kabla ya kuanzishwa kwa idara hiyo wizara ilikuwa ikifanya, kuunda, kupendekeza pamoja na kuanzisha sera ambapo utekelezaji wa chini haukuwa thabiti kwasababu haukuwa na wasimamizi, hivyo kupitia idara hiyo wasimamizi wana mwendelezo wa majukumu yaliyopangwa yatatimizwa.

Naye katibu tawala msaidizi viwanda, bishara na uwekezaji mkoa wa Morogoro Beatrice Njawa amesema kwakuwa wamepitishwa kwenye mpango wa kuboresha mazingira ya kufanyia bishara anaamini wanaenda kusimamia na kuondoa vikwazo vyote vya kibishara na uwekezaji katika mamlaka za serikali za mitaa na mikoani ili kuweza kutangaza uwekezaji unaopatikana katika maeneo hayo.

Njawa ameongeza kuwa wakiweza kuboresha eneo hilo hasa uwekezaji na ujenzi wa viwanda maana yake wanaenda kuzipa nguvu mamlaka za serikali za mitaa na wataongeza mapato na wanaenda kuimalisha mahusiano kati ya mikoa, halmashauri pamoja na sekta binafsi zilizopo katika maeneo yao.

WIZARA YA AFYA YAWEKA JITIHADA KUDHIBITI UGONJWA SHINIKIZO LA JUU LA DAMU

WAZIRI wa Afya Ummy Mwalimu amesema  pamoja na kuimarisha huduma za tiba hapa nchini, serikali imejipanga kuweka jitihada za kipekee ili kuzuia na kudhibiti ugonjwa wa shinikizo la juu la damu na magonjwa yasiyoambukiza.

Waziri Ummy ameyasema hayo leo Mei 17,2023 Jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari ikiwa ni maadhimisho ya siku ya shinikizo la damu Duniani.

Pia amekumbusha umuhimu wa kubadili mtindo wa maisha na kuhimiza wananchi kufanyaji wa mazoezi, kuepuka tabia bwete, kuepuka matumizi ya tumbaku na bidhaa zake, kupunguza matumizi ya vilevi, kuzingatia ulaji unaofaa wa mlo kamili wenye mboga mboga na matunda ya kutosha ili kuimarisha kinga ya mwili dhidi ya magonjwa.

Aidha, amesema kuwa takwimu kutoka kwenye mfumo wa ukusanyaji taarifa za Afya (DHIS2) zinaonesha kuwa jumla ya wagonjwa milioni 2.5 walitibiwa magonjwa yasiyoambukizwa kwenye vituo vya Afya nchini kwa mwaka 2017.

Waziri Ummy amesema kati yao, ugonjwa wa shinikizo la juu la damu ndio uliongoza miongoni mwa magonjwa yasiyoambukiza ambapo waliongezeka kutoka wagonjwa 688,901 kwa mwaka 2017, hadi kufikia wagonjwa milioni 1.3 kwa mwaka 2021 sawa na ongezeko la 95.4% katika kipindi hicho.

Amesema katika uchunguzi uliofanywa katika jamii kwenye mikoa ya Pwani, Arusha, Geita, Mtwara, Lindi, Zanzibar, Iringa na Dar es Salaam takwimu zinaonyesha watu 3-4 kati ya 10 wana shinikizo la juu la damu. 

Shinikizo la juu la damu ni ugonjwa unaosababishwa na nguvu ya msukumo wa damu katika mishipa kuwa kubwa kuliko kawaida kwa muda mrefu na ongezeko hilo huulazimu moyo kufanya kazi kupita kiasi ili uweze kusukuma damu katika mishipa kwa kiwango kilekile kinachohitajika mwilini.

MWENGE WAZINDUA MIRADI KIBAHA

KIONGOZI wa mbio za Mwenge Kitaifa Abdala Shaibu Kaim amewataka Watanzania kutunza mazingira ili kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi ambayo kwa asilimia 95 yanatokana na uharibifu wa mazngira.

Aidha aliwataka wananchi kuwa na utamaduni wa kula kwa mpangilio na kufanya mazoezi ili kujiepusha na magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Aliyasema hayo wakati akizungumza na viongozi na wananchi wa Halmashauri ya Mji Kibaha wakati wa kupokea Mwenge wa uhuru ukitokea Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha.

 Kaim alisema kuwa uharibifu huo wa mazingira unasababisha kushusha uchumi wa nchi kutokana na athari hizo hivyo kuna haja ya Watanzania kusimamia maingira ili yasiharibiwe.

"Tuhakikishe tunalinda mazingira yetu ili kukabiliana na athari hizo ambazo zinaleta changamoto za kimaendeleo,"alisema Kaim.

Alisema kuwa mazingira ni uhai hivyo mazingira  yanapaswa kulindwa kwa nguvu zote ili maisha yaendelee bila ya changamoto ambazo zimesababisha hali ya hewa kuwa mbaya.

Aliongeza kuwa ujumbe wa mwaka huu unasema kuwa Mabadiliko Tabianchi Hifadhi ya Mazingira na utunzaji wa vyanzo vya maji na kauli mbiu tunza mazingira okoa vyanzo vya maji kwa ustawi wa viumbe hai na ustawi wa uchumi wa Taifa.

"Tuendelee kukabiliana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa kula vyakula kwa mpangilio ambavyo vinashauriwa na wataalamu na kuacha ulaji usio na mpangilio na kufanya mazoezi angalau kwa nusu saa,"alisema Kaim.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Simon John alisema kuwa Mwenge huo wa uhuru ulitembelea jumla ya miradi 12 yenye thamani ya shilingi bilioni 3.9.

John alisema kuwa fedha za miradi kati ya hizo milioni 520.2 ni mchango kutoka Halmashauri na milioni 683.7 ni kutoka serikali kuu na bilioni 2.4 ni michango ya wananchi.

Alisema kuwa fedha nyingine ni kutoka kwa wahisani ambapo ni kiasi cha shilingi milioni 293.3 na michango ya mwenge iliyoelekezwa katika miradi ya maendeleo ni shilingi milioni 2.5.

Mwisho.

Wednesday, May 17, 2023

WIZARA YA VIWANDA UWEKEZAJI KUANDAA MWONGOZO KWA WAFANYABIASHARA

 

MKURUGENZI wa uwezeshaji wananchi kiuchumi na maendeleo ya sekta binafsi ya TAMISEMI Conrad Milinga amesema kuwa Wizara ya Viwanda na Uwekezaji inaandaa mwongozo wa kuwawezesha wafanyabishara wajasiliamari kutambua kuwa wanapohitaji kuanzisha biashara sehemu ya kuanzia na kuishia.

Milingi ameyasema hayo Jijini Dodoma, katika kikao cha kuthibitisha rasimu ya muongozo wa wataalamu wa biashara na mpango wa kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini kilichofanyika katika ukumbi wa bodi ya wakandarasi.

Aidha amesema kuhusiana na taarifa za mwenendo wa bei za vyakula nchini wanahitaji kuzipata kuanzia kwao lakini zisitofautiane na zile zinazotolewa na wizara, hivyo waweke mfumo wa taarifa watakazo kuwa wanazipata kutoka kwao.

Kwa upande wake katibu tawala masidizi wa viwanda, biashara na uwekezaji mkoa wa Kigoma Deogratias Sangu, amesema kabla ya kuanzishwa kwa idara hiyo wizara ilikuwa ikifanya, kuunda, kupendekeza pamoja na kuanzisha sera ambapo utekelezaji wa chini haukuwa thabiti kwasababu haukuwa na wasimamizi, hivyo kupitia idara hiyo wasimamizi wana mwendelezo wa majukumu yaliyopangwa yatatimizwa.

Naye katibu tawala msaidizi viwanda, bishara na uwekezaji mkoa wa Morogoro Beatrice Njawa amesema kwakuwa wamepitishwa kwenye mpango wa kuboresha mazingira ya kufanyia bishara anaamini wanaenda kusimamia na kuondoa vikwazo vyote vya kibishara na uwekezaji katika mamlaka za serikali za mitaa na mikoani ili kuweza kutangaza uwekezaji unaopatikana katika maeneo hayo.



Njawa ameongeza kuwa wakiweza kuboresha eneo hilo hasa uwekezaji na ujenzi wa viwanda maana yake wanaenda kuzipa nguvu mamlaka za serikali za mitaa na wataongeza mapato na wanaenda kuimalisha mahusiano kati ya mikoa, halmashauri pamoja na sekta binafsi zilizopo katika maeneo yao.

Saturday, May 6, 2023

WIZARA ZA ELIMU NA UTAMADUNI ZIWASAIDIE VIJANA KUMFAHAMU ZAIDI MWL. NYERERE - MAJALIWA

 

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amezitaka Wizara za Elimu, Sayansi na Teknolojia na ile ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ziandae utaratibu utakaosaidia vijana kujifunza na kumfahamu zaidi hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kuanzia shule za msingi, hadi vyuo vikuu.

Ametoa wito huo leo (Jumamosi, Mei 6, 2023) alipomuwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye kongamano la kumbukizi ya miaka 101 ya hayati Mwalimu Nyerere lililofanyika katika ukumbi wa Chimwaga, Chuo Kikuu cha Dodoma.

Amesema kuwa kama lilivyo lengo la kongamano hilo ni muhimu kuwarithisha vijana wa Kitanzania fikra na falsafa za Baba wa Taifa. “Aidha, nyote mtakubaliana nami kwamba yapo mambo mengi ambayo tungetamani vijana wetu wayafahamu kuhusu urithi aliyotuachia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.”

Mheshimiwa Majaliwa amesema baadhi ya mambo ambayo vijana wanapaswa kurithishwa ni kuyafahamu maisha ya Mwalimu Nyerere hasa baada ya kustaafu uongozi wa nchi na siasa za majukwaani, kutambua juhudi zake katika harakati za kuleta amani na kufanikisha ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika na bara la Afrika.

Ameyataja masuala mengine kuwa ni kufahamu kipaji cha Mwalimu Nyerere katika harakati zake za kupigania uhuru na kuwaunganisha Watanzania na kuwa na uwezo wa kumfahamu na kumuelezea Mwalimu Nyerere alikuwa ni nani katika historia ya Tanzania.

“Miongoni mwa urithi huo ambao tungependa kizazi chetu kiufahamu ni pamoja na kuwa na uwezo wa kumfahamu na kumuelezea Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuwa ni nani katika historia ya Tanzania; kuzielewa na kuzitambua juhudi za zake katika kuimarisha ustawi wa Tanzania hususan kupitia falsafa yake ya kutokomeza maadui watatu yaani ujinga, umaskini na maradhi.”

Wakati huohuo, Mheshimiwa Majaliwa amesema kumekuwa na taarifa za malalamiko kuhusu kuongezeka kwa kelele na mitetemo katika sehemu mbalimbali nchini na maeneo yaliyoongoza kwa kulalamikiwa ni za nyumba za starehe, kumbi za burudani na nyumba za ibada.

Amesema katika kudhibiti kelele na mitetemo kutoka katika kumbi za starehe, Ofisi ya Makamu wa Rais ilitoa maelekezo mahususi yaliyolenga kudhibiti mitetemo iliyopitiliza katika kumbi za starehe hapa nchini. Pia, maelekezo hayo yaliainisha jinsi uratibu unavyopaswa kufanyika katika nyumba za ibada kwa kuwaomba viongozi wa dini kupitia Kamati za Amani kujadili suala la kelele na mitetemo iliyopitiliza kutoka kwa baadhi ya nyumba za ibada ili kupata namna bora ya kuendesha shughuli za ibada.

 Hata hivyo, Mheshimiwa Majaliwa amesema, kumejitokeza taharuki kwa baadhi ya viongozi wa dini wakati Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linashughulikia malalamiko kuhusu ongezeko la kelele na mitetemo.

“Serikali ingependa kutoa ufafanuzi kwamba shughuli za dini ziendelee kufanyika kama kawaida na suala la uratibu wa jambo hilo katika nyumba za ibada liendelee kuratibiwa na viongozi wa dini wenyewe kupitia Jumuiya ya Maridhiano na Amani.”

“Serikali itaendelea kushauriana na jumuiya ya maridhiano na amani katika kuona namna bora ya kuendesha shughuli zao kwa kuzingatia mahitaji ya jamii na kulinda afya za Watanzania,” amesema.

Tanzania, Seattle Sounders, Seahawks, Trailblazers Kushirikiana Kutangaza Utalii



Tanzania, Seattle Sounders, Seahawks, Trailblazers Kushirikiana Kutangaza Utalii

Seattle, Washington State, Marekani

 SERIKALI ya Tanzania imeeleza azma yake ya kuongeza juhudi za kutangaza utalii kupitia michezo pia kushirikiana na taasisi mbalimbali duniani ili kuongeza idadi ya watalii kutoka nje na mapato zaidi kwa Serikali.

Azma hiyo imeelezwa na Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, Mei 5, 2023, wakati wa hafla fupi iliyoandaliwa na kampuni ya Vulcan kwenye Uwanja wa Lumen jijini Marekani na kushirikisha wadau kutoka makampuni mbalimbali yaliyoko jijini Seattle ikiwemo wawakilishi kutoka Google, Starbucks, ofisi ya Meya wa Seattle, Boeing na jumuiya ya wafanyabiashara.

Taasisi ya Vulcan inamiliki hisa katika klabu kubwa za michezo mbalimbali katika ligi kuu za nchini Marekani za Seattle Sounders (mpira wa miguu); Seahawks (soka la Marekani) na Portland Trailblazers (Ligi ya NBA).

“Nimewahi kufika Tanzania, naweza kuwahakikishia kuwa kwa wale ambao hawajafika mfike ni nchi nzuri sana. Tuliwahi kwenda pia Sounders miaka ya 2000 ikacheza na Yanga, Simba na Timu ya Taifa,” alisema Bw. Adrian Hanauer, ambaye kwa sasa ni mmiliki mwenye hisa nyingi wa klabu ya Seattle Sounders akiahidi klabu hiyo na wadau wengine wako tayari kushirikiana kusukuma mbele utalii wa Tanzania.

Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) chini ya Mtendaji wake Mkuu, Damasi Mfugale, imeingia makubaliano ya awali kuelelea ishirikiano kamili na makampuni ya Vulcan.

MAKAMU WA RAIS DKT MPANGO AWASILI BURUNDI

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Melchoir Ndadaye uliopo Bujumbura nchini Burundi na kupokelewa na Makamu wa Rais wa Burundi Mheshimiwa Prosper Banzombaza leo tarehe 06 Mei 2023. 

Makamu wa Rais anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa 11 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Nchi Wanachama wa Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano kwaajili ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Ukanda wa Maziwa Makuu unaofanyika Bujumbura nchini Burundi.