Saturday, September 26, 2015

KAMPENI CHALINZE





Na John Gagarini, Chalinze
HALMASHAURI ya wilaya ya Bagamoyo imeshauriwa kuisitisha mikata ya umiliki wa ardhi iliyochukuliwa na wawawkezaji ambao hawajaiendeleza ardhi hiyo kwa kipindi cha zaidi ya miaka 15 wairejeshe kwenye serikali za vijiji kwa ajili ya matumizi ya umma.
Hayo yalisemwa na mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete wakati wa mikutano ya hadhara ya kampeni kwenye Vijiji vya Makombe na Kinzagu kwenye kata ya Lugoba na kusema kuwa wamiliki hao kama wameshindwa kuiendeleza ardhi hiyo ni vema wakairudisha kwa wananchi.
Ridhiwani alisema kuwa inashangaza kuona kuwa wananchi kwenye vijiji hivyo wamekuwa wakihangaika kutafuta ardhi kwa ajili ya kilimo pamoja na matumizi mengine lakini wanakosa maeneo ambayo yamehodhiwa na watu wachache.
“Kwa sasa ni vema halmashauri zikasitisha mikata ya umiliki wa ardhi hiyo kutokana na kushindwa kuiendeleza kwa kipindi cha miaka zaidi yha 10 ambapo sheria inataka mwekezaji kuiendeleza ardhi ndani ya kipindi cha miezi 32 na endapo atashindwa kuiendeleza anaweza kufutiwa umiliki,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa haipendezi kuona wananchi wanahangaika kutafuta maeneo huku baadhi ya watu wakiwa wamehodhi maeneo bila ya kuyaendeleza na kuacha yakiwa mapori ambayo yanahatarisha usalama wao.
“Ni vema maeneo hayo yakarejeshwa kwenye serikali za vijiji ili yaweze kugawiwa kwa wananchi kwa ajili ya kilimo kwani itakuwa ni sehemu ya kutoa ajira kwa wananchi hususani vijana,” alisema Ridhiwani.
Kwa upande wake diwani wa kata hiyo ya Lugoba ambaye amepita bila ya kupingwa Rehema Mwene alisema kuwa ni kweli maeneo hayo yalichukuliwa na wawekezaji muda mrefu lakini hayajaendelezwa.
Mwene alisema wananchi wa maeneo hayo hususani vijana hawana ajira lakini endapo ardhi hiyo itarejeshwa itasadia kujiajiri kupitia kilimo ambacho ni ajira ya uhakika lakini wanashindwa kujiajiri kupitia kilimo kutokana na kukosa maeneo kwa ajili ya kulima.
Mwisho.
Na John Gagarini, Chalinze
WANANCHI wa Kijiji cha Makombe wameomba uwekwe utaratibu wa malori yanayobeba kokoto kutoka kwenye machimbo ya kokoto yapimwe uzito ili yabebe uzito kutokana na uwezo wa barabara.
Sambamba na hilo wameomba kuwe na utaratibu wa magari hayo kutoa fedha kwa ajili ya ukarabati wa barabara ambazo zimekuwa zikiharibika vibaya kutokana na kupitishwa malori hayo ambayo yana  uzito mkubwa.
Ombi hilo lilitolewa na Rehema John alipozungumza na waandishi wa habari mara baada ya mkutano wa kampeni wa mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete.
John alisema kuwa barabara hizo zimeharibika vibaya kutokana na magari ya kubebea kokoto ambayo ni mazito na hakuna utaratibu wa kuyapima uzito hali inayosababisha barabara kuharibika.
“Tunaiomba serikali kuweka utaratibu mzuri wa malori hayo yanayobeba kokoto kutoka kwenye machimbo  na kusababisha uharibifu wa barabara inayoelekea kwenye machimbo hayo na kutoka huko kwenda barabara kubwa ya lami,” alisema John.
Alisema kuwa kwa sasa barabara hizo zinazoelekea kwenye machimbo hayo ya kokoto zimeharibika vbaya kutokana na uzito kuwa mkubwa hivyo kushindwa kuhimili uzito.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Lugoba ambaye amepita bila ya kupingwa Rehema Mwene alisema kuwa atahakikisha maombi hayo anayapeleka sehemu husika ili hatua ziweze kuchukuliwa kwani uharibifu ni mkubwa sana.
Mwene alisema kuwa barabara zinazoelekea kwenye machimbo hayo zote ni mbaya kutokana na kutofanyiwa ukarabati ambapo licha ya halmashauri kuzifanyia matengenezo lakini zinaharibika haraka kutokana na uzito mkubwa wa malori hayo.
Kwa upande wake mgombea Ubunge wa CCM Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa kuna haja ya wanaotumia barabara hizo hasa wale wenye magari yanayobeba kukoto pamoja na wawekezaji kwenye machimbo hayo kufanya ukarabati wa barabara hizo.
Ridhiwani alisema kuwa wawekezaji wanapaswa kuboresha huduma mbalimbali ndani ya kijiji ili wananchi waweze kunufaika na uwekezaji wao na hivyo ni vema wakazikarabati barabara hizo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Chalinze
WANANCHI wakiwemo wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) waliojiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura wilayani Bagamoyo hususani wanawake wametakiwa wasikubali kurubuniwa na baadhi ya watu na kuuza shahada zao kwa matapeli kwa madai ya kuipunguzia kura kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba 25 mwaka huu.
Akizungumza kwenye mkutano wa kampeni wa mgombea wa CCM Ridhiwani Kikwete kwenye kijiji cha Lunga kata ya Lugoba wilayani humo katibu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Mwatabu Husein alisema kuwa wapinzani wao wameanza kununua kadi za wapiga kura ili kukipunguzia kura.
Hussein alisema kuwa kuna watu wanapita na kuwarubuni wananchi na wanachama wa CCM ili wawauzie kadi za mpiga kura ili kupunguza idadi ya wapiga kura kwani endapo mtu atakuwa hana kadi ya mpiga kura hatakuwa na haki ya kupiga kura kwenye uchaguzi huo.
“Nawashauri wananchi na wana CCM kuwa makini na watu hao kwani wamekuwa wakitumia njia hiyo ya kuzinunua kadi hizo ili kutuathiri kupata ushindi wa kishindo hivyo mnapaswa kuwa macho hasa wakinamama msikubali kuyumbishwa,” alisema Hussein.
Alisema kuwa tayari wamewashika pabaya wapinzani wao ambao sasa wamenza kuweweseka na kufanya vitendo vinavyoashiria kushindwa na kuanza kutapatapa.
“Wapinzani wetu hawatuwezi wamenza kununua kadi za wapiga kura ili kutupunguzia ushindi wa kishindo lakini tayari wameshachelewa tutawashinda kwa kishindo kikubwa na mwisho wao utakuwa Oktoba 25 mwaka huu,”a lisema Hussein.
Aidha alisema kuwa wapinzani hali yao imekuwa mbaya kwani hawana uwezo wa kuishinda CCM ambayo imejipanga vizuri kwa mikakati yake ya ushindi na washindani wao tayari wameshakubali kushindwa sasa wanatafuta sababu ya kushindwa hata kabla uchaguzi haujafanyika.
Mwisho.








Wednesday, September 23, 2015

WALILIA KISIMA CHA MAJI KILICHOPO HUTOA MAJI KILA BAADA YA MASAA MANNE

Na John Gagarini, Mkange
WANANCHI wa Kijiji cha Gongo kata ya Mkange wilayani Bagamoyo wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji ambapo huweka foleni ya kuchota maji kwenye kisima kilichopo kijijini hapo baada ya wiki mbili.
Kutokana na usosefu huo wa maji wananchi hao wamekuwa wakinunua maji ya bomba ndoo ya lita 20 kati ya shilingi 1,000 na shilingi 1,500 maji ambayo huuzwa kwenye magari au pikipiki hivyo kuwafanya wajikute hawapati maendeleo kutokana na gharama kubwa kuzitumia kununulia maji.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mkutano wa kampeni wa mgombea Ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete, kwenye kata ya Mkange mwananchi wa Kijiji hicho Hungilo Nyoka alisema kuwa maji yamewafanya washindwe kupata maendeleo.
Nyoka alisema kila kaya inatakiwa ichote madumu manne ili angalau kila mmoja apate baada ya hapo maji hukatika ambapo inatakiwa mtu asubirie tena na mzunguko huo hufanya foleni ya mtu mmoja kufikiwa tena baada ya wiki mbili kwani hapa kuna wananchi 1,690.
Alisema changamoto kubwa kwao ni maji ambayo yamekuwa yakiwafanya washindwe kufanya shughuli za maendeleo ipasavyo kwani hata wakipata fedha kutokana na shughuli zao fedha zote huishia kununulia maji.
“Tunawaomba wahusika kutuangalia kwa jicho la huruma maji kwetu ni kikwazo cha kupata maendeleo kwani hata ukipata fedha kiasi gani zote zinaishia kwenye maji hivyo tunaomba tuchimbiwe kisima kwani kilichopo maji ni kidogo sana yanatoka kila baada ya saa moja yanakatika,” alisema Nyoka.
Aidha alisema kuwa maji wanayokunywa ni ya bomba lakini yanatoka vijiji jirani vya Matipwili ambako kuna umbali wa kilomita 11 na kijiji cha Mkange kilomita tisa na alisema kuwa chanzo cha maji ya kisima kutotoka ipasavyo ni kwamba waliochimba kisima hawakuchimba hadi kuuukuta mwamba ambapo chini ya mwamba ndiyo kuna maji mengi.
“Tunaomba wadau wa masula ya maendeleo kutusaidia kuweza kupata maji kwani tunashindwa hata kujiletea maendeleo kutokana ukosefu wa maji na wkati mwingine watoto hushindwa kwenda shule endapo maji yanakuwa ya shida kwani hawawezi kwenda wachafua kwani mimi kwa siku hutumia madumu matatu hadi matano kwa siku,” alisema Nyoka.
Kwa upande wake mgombea udiwani kupitia CCM Injinia Juma Mgweno alisema kuwa tatizo hilo ni kubwa sana lakini atahakikisha maji yanapatikana kwa kuita wadau mbalimbali ili waweze kuwachimbia kisima.
Naye mgombea wa Ubunge kupitia CCM Ridhiwani Kikwete alisema kuwa visima viwili vilivypo kijiji hapo havitoi maji ambapo kimoja kinahitaji pampu ambayo imeharibika atahakikisha inapatikana mpya ili kuwaondolea kero wananchi wa kijiji hicho.
Ridhiwani alisema kuwa mbali ya kuhakikisha pampu mpya inapatikana pia kuna mradi mwingine wa mjai toka Matipwili na ule wa Wami Chalinze atahakikisha maji yanafika kwani mradi huo utavifikia vijiji na vitongoji ambavyo havikupata maji katika awamu mbili zilizopita vitafikiwa na awamu hii.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mkange
KIJIJI cha Gongo kata ya Mkange wilaya ya bagamoyo mkoa wa Pwani kinakabiliwa na ukosefu wa mizani ya kuwapimia watoto wenye umri chini ya miaka mitano hali inayowafanya akinamama kuwapimia watoto wao mzani wa kijiji cha jirani cha Matipwili.
Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea kijiji hicho wakati wa mikutano ya kampeni ya CCM ya kuwania Ubunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwnai Kikwete, moja ya akinamama Mwajuma Juma alisema kuwa hutugemea mizani ya majirani zao ili kupata huduma hiyo.
Juma alisema kuwa kama ujuavyo kiafya watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano hubidi wahudhurie kliniki kila baada ya mwezi ambapo huchunguzwa afya yake na moja ya jambo muhimu ni kupima uzito kwenye zahanati ya kijiji.
“Tatizo lililopo kwenye zahanati yetu ni ukosefu wa mizani ambapo hutubidi tukaazime kwa majirani zetu kijiji cha jirani hivyo kusababisha msongamano mkubwa inapofikia siku ya kwenda kliniki tunaomba tusaidiwe upatikanaji wa mizani kwa ajili ya kurahisisha huduma hiyo ambayo ni muhimu kwa watoto,” alisema Juma.
Alisema kuwa kijiji kinalazimika kutoa kisia cha shilingi 10,000 kwa jili ya kumlipa mhudumu wa afya wa Kijiji hicho cha Matipwili ambaye ndiyo hutoa huduma hiyo ya kuwapima uzito watoto hao wanapokwenda kliniki.
“Tunaomba tusaidiwe kifaa hicho kwani akinamama wanajitihada kubwa ya kuwapeleka watoto wao kliniki lakini changamoto kubwa ni ukosefu wa mizani ya kuwapimia ambapo siku unapokuja siku hiyo inabidi kazi nyingine zisifanyike kwa ajili ya kusubiria foleni kwa ajili ya kuwapima watoto uzito,” alisema Juma.
Kwa upande wake mgombea Udiwani kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi CCM, Injinia Juma Mgweno alisma kipaumbele chake cha kwanza endapo atachaguliwa ni kuhakikisha huduma za afya hasa za mama na mtoto zsinaboreshwa.
Mgweno alisema kuwa akichaguliwa atahakikisha kuwa huduma bora zinapatikana ili akinamama na watoto waweze kuwa na afya bora kwa kupata huduma muhimu za kiafya kwani bila ya afya bora mama hatoweza kuihudumia familia yake.
Naye Mgombe Ubunge wa CCM Ridhiwani Kikwete alisema kuwa chnagamoto ya vifaa tiba pamoja na wahudumu katika zahanati ya kijiji iliyojengwa na Mkapa Foundation anaijua lakini mkakati wake ni kuhakikisha kuwa wahudumu wa afya wanakuwepo pamoja na mganga ili huduma bora ziwepo.
Ridhiwani alisema kuwa atahakikisha wagnga watatu wanaletwa kwenye zahanati hiyo ili kukabiliana na upungufu wa wahudumu wa afya katika zahanati hiyo ambayo inakabiliwa na changamoto mbalimbali.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mkange
MGOMBEA Ubunge kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi( CCM) Ridhiwani Kikwete amesema kuwa endapo atachaguliwa kuwa mbunge wa Jimbo hilo atahakikisha ujenzi wa shule ya Msingi Kwamakulu unakamilika ili kuwaondolea adha wanafunzi kusoma shule ya kitongoji jirani cha Manda.
Aliyasema hayo jana kwenye Kitongoji  cha Kwamakulu kata ya Mkange wilayani Bagamoyo wakati wa mkutano wake wa kampeni kuomba ridhaa ya kuliongoza jimbo hilo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo kwenye uchaguzi utakaofanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Ridhiwani alisema kuwa atahakikisha ujenzi huo unafanyika ambapo kwa sasa wanafunzi wanaotoka kitongoji hicho husomea shule ya Msingi Manda kwenye kitongoji cha jirani kwa kutembea muda wa masaa mawili hadi kufika shuleni hali inayosababisha wengine kushindwa kusoma kutokana na umbali.
“Namshukuru Mungu kunijalia mimi nimesoma kiasi fulani lakini hali kama hii ya kitongoji kukosa shule ya msingi ni jambo ambalo halinifurahishi hata kidogo lakini naomba mnipe ridhaa ya kuwa kiongozi wenu ili niweze kufanya kazi hii ya kuhakikisha shule ya msingi inapatikana hapa ili watoto wafaidi shule,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa elimu ni haki ya msingi ya mtoto lakini pia anapaswa aipate katika mazingira mazuri siyo kugeuka tena mateso kwani umbali wa masaa mawili kwa mwanafunzi wa shule ya msingi ni tatizo kubwa.
“Tumeanza na ujenzi wa darasa la awali ambapo nilitoa mifuko 100 ya simenti nashukuru naona angalau kimepatikana chumba kimoja cha darasa na choo pamoja na nyumba ya mwalimu nitahakikisha ujenzi huu unakamilika na baadaye tutaendelea na ujenzi wa madarasa mengine ili kupata shule hapa badala kwenda Manda,” alisema Ridhiwani.
Kwa upande wake mgombea udiwani wa CCM Injinia Juma Mgweno alisema kuwa kwa kutumia elimu yake akishirikiana na mgombea ubunge watahakikisha kwa pamoja shule inajengwa na inakamilika ili watoto waondokane na adha ya kusoma mbali.
Mgweno alisema kata hiyo inakabiliwa na baadhi ya changamoto ikiwa ni pamoja na ukosefu wa shule kutokana na baadhi ya vitongoji kujigawa kutoka kwenye vijiji hivyo atahakikisha ujenzi wa shule na nyumba za walimu inakuwa kipaumbele chake.
Naye mwananchi wa Kijiji hicho Siyawezi Juma alisema kuwa ujenzi wa shule ya Msingi utasaidia kuwapunguzia adha watoto wao kwenda kusoma umbali mrefu ambapo husababisha wengine kukata tama na kuacha shule kutokana na umbali.
Juma alisema kujengwa kwa shule kitongojini hapo itakuwa ni mkombozi wa watoto wao katika suala la elimu ambayo ni muhimu kwa watoto kwani endapo wataikosa itawasababishia kuwa nyuma kielimu na kuhsindwa kujiendeleza kimaisha.

Mwisho.     

Tuesday, September 22, 2015

KAMPENI ZAENDELEA JIMBO LA CHALINZE

Na John Gagarini, Mandela
MGOMBEA Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi Ridhiwani Kikwete amesema kuwa endapo atafanikiwa kuchaguliwa kwenye nafasi hiyo atahakikisha zahanati inajengwa kwenye Kijiji cha Kibaoni ili kuwaondolea adha wananchi wa kijiji hicho.
Aliyasema hayo jana kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika Kijijini hapo kata ya Mandela na kusema kuwa ilani ya chama anasema kila kijiji lazima kiwe na zahanati huku kila kata ikitakiwa kuwa na kituo cha afya ili kurahishisha upatikanaji wa huduma za afya karibu.
Ridhiwani alisema kuwa hicho kitakuwa moja ya vipaumbele vyake ambavyo atahakikisha kuwa katika kipindi cha miaka mitano ujenzi huo unakamilika na wanakijiji wanapata huduma za afya karibu tofauti na sasa ambapo huwalazimu kwenda kijiji jirani cha Mandela.
“Ilani ya chama inasema kuwa kila kijiji lazima kiwe na zahanati hivyo endapo nikichaguliwa kwenye nafasi hii ya ubunge kwa kushirikiana na wananchi hivyo nitahakikisha zahanati inajengwa ili huduma zipatikane karibu,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa hata kata ya Mandela haina Kituo cha afya ambapo kata hiyo ni mpya ambayo imezaliwa kutoka kata ya Miono na kutaka ujenzi wa kituo hicho cha afya kujengwa kwenye kijiji hicho.
“Katika kipindi cha uongozi wangu wa mwaka mmoja na miezi miwili tumeweza kukarabati zahanati 24 huku nane zikiwa zimejengwa pia tumeweza kufanikisha kujngwa nyumba za waganga pamoja na upatikanaji wa vifaa tiba na dawa,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisema kuwa bado kuna changamoto ya baadhi ya vijiji kukosa zahanati hata hivyo mikakati ni kuhakikisha zinajengwa ambapo mipango inaendelea kwa kushirikiana na wananchi.
Kwa upande wake mgombea udiwani wa kata ya Mandela Madaraka Mbode alisema kuwa tayari kata imetenga eneo lenye ukubwa wa hekari 10 kwa ajili ya ujenzi wa zahanati kwenye kijiji cha Kibaoni.
Mbode alisema kuwa ujenzi wa zahanati hiyo utafanikiwa endapo wananchi watawachagua wgombea kutoka CCM lakini endapo wakiwachagua viongozi wa vyama vya upinzani hawataweza kupata maendeleo.
Naye mkazi wa Kibaoni Ally Athuman alisema kuwa changamoto kubwa inayowakumba wananchi kwenye zahanati wanazokwenda kupata matibabu ni ukosefu wa dawa.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mandela
MGOMBEA Udiwani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Mandela wilaya ya Bagamoyo Madaraka Mbode amemwomba mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kusimamia ujengwaji wa tenki kubwa la maji ili kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa maji.
Mbode aliyasema hayo kwenye Kijiji cha Lupungwi wakati wa mkutano wa kampeni za Ubunge nakusema kuwa Ridhiwani ndiye aliyeanzisha mchakato wa ujengwaji wa matenki kwenye baadhi ya vijiji.
Alisema kuwa awamu ya pili imevifanya vijiji vingi kwenye Jimbo hilo kuwa na maji lakini baadhi bado havijapata huduma hiyo ambapo awamu ya tatu ya mradi wa maji utavifikia vijiji na vitngoji ambavyo havikubahatika kupata maji.
“Wananchi nawaombeni mchagueni Ridhiwani kwani anauwezo wa kutufanikishia kupata maji ambapo kwa sasa maji yanatoka lakini endapo kunatokea tatizo kwenye mtambo maji hayapatikani ndiyo maana ujenzi wa matenki makubwa unaanza ili kuhakikisha maji yanapatikana muda wote,” alisema Mbode.
Aidha alisema kuwa anaomba na yeye achaguliwe kwenye nafasi ya udiwani ili ashirikiane na mbunge huyo kuwaletea maendeleo ambapo kwa sasa kijiji hicho kimewekewa nguzo kwa ajili ya kuwasambaziwa umeme.
Naye Ridhiwani Kikwete alisema kuwa tayari tathmini imeshaanza kufanywa ambapo wataalamu wameshachukua udongo kwa ajili ya kupima kabla ya kujenga tenki hilo ambalo litakuwa na uwezo wa kuhifadhi maji mengi.
Ridhiwani alisema kuwa awamu hii ya tatu ya mradi wa maji wa wami chalinze utavifikia vijiji na vitongoji vyote sambamba na ujengaji wa matenki makubwa kwa ajili ya kuhifadhia maji.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mandela
BAADHI ya waangalizi wa uchaguzi wamesema kuwa Tanzania imeweka historia kwa kuwa na waangalizi wengi kwenye uchaguzi wa mwaka huu hali ambayo itafanya uchaguzi kuwa huru na wa haki.
Hayo yalisemwa jana na mwangalizi wa ndani kutoka (TEMCO) Renatus Mkinga kwenye kijiji cha Lupungwi kata ya Mandela wilayani Bagamoyo wakati wa mkutano wa kampeni wa mgombea ubunge wa Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete.
Mkinga alisema kuwa kwa waangalizi wa ndani ni zaidi ya 6,000 huku wale wa kutoka nje wakiwa ni 600 ambao ni wengi na haijawahi kutokea katika chaguzi zilizopita.
“Sisi hatuna vyama tunachokifanya ni kuangalia ,mwenendo mzima wa uchaguzi kuanzia hatua ya kampeni hadi utakapofanyika uchaguzi Oktoba 25 mwaka huu,” alisema Mkinga.
Alisema kuwa kazi ya wasimamizi ni kuangalia mienendo ya uchaguzi katika kampeni na anaamini kuwa utakuwa huru na haki kwani hadi sasa kampeni zinaendele vizuri.
“Tunahudhuria kwenye mikutano ya vyama mbalimbali ili kuangalia wanapiga kampeni vipi na kuangalia wananchi wanajitokeza vipi kusikiliza sera za vyama husika,” alisema Mkinga.
Aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kusikiliza sera za vyama mbalimbali ili waweze kuangalia ni mgombea gani ambaye anawafaa ili mwisho wa siku waweze kumchagua kiongozi bora na si bora kiongozi.
Mwisho.
   

        

Monday, September 21, 2015

SITA WAFA WANNE WAJERUHIWA

 Na John Gagarini, Mkuranga
WATU sita wamepoteza maisha na wanne kujeruhiwa baada ya basi dogo la abiria kugongana uso kwa uso na basi kubwa la kampuni ya Ibra.
Ajali hiyo ilitokea jana katika kijiji cha Njopeka wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani.
Kamanda wa polisi mkoa wa Pwani Jafari Ibrahim alithibisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa katika ajali hiyo watu sita amekufa na wanne kujeruhiwa.
Ibrahim alisema basi hilo kubwa  lenye namba za usajili T 195 DCE aina ya YU TONG likiendeshwa na Alex Peter (46) liligongangana na gari ndogo iliyokua ikitokea Jaribu kuelekea Mbagala jijini Dar Es Salam lenye namba za  usajili T 782 DC.
Alisema kuwa chanzo cha ajali hiyo kuwa ni dereva wa Basi la Ibra kuendesha zaidi kulia na hivyo kukutana uso kwa uso na kusababisha ajali hiyo.
Aidha alisema baada ya ajali hiyo wamelazimika kuweka askari katika eneo hilo, huku wakiwataka madereva kuwa makini na sheria za barabarani.
Ibrahim aliwasihi wananchi kutoa taarifa kwa Askari wa Usalama barabarani kwa namba zilizopo kwenye mabasi pindi wanapobaini kukiukwa kwa sheria za barabarani kabla ajali haijatokea.
Mwisho.

WENGI WAMUAGA MTOTO WA ALIKUWA KIONGOZI WA WAFUGAJI, RAIS DK JAKAYA KIKWETE ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI

Na John Gagarini, Lugoba
WAGOMBEA wanaowania nafasi za uongozi hapa nchini wametakiwa kukubali matokeo mara uchaguzi utakapofanyika Oktoba 25 mwaka huu kwani kuna maisha mengine baada ya uchaguzi  kuendelea kufanya kampeni zao huku wakiendelea kuhubiri na kulinda amani iliyopo kwani wana nafasi kubwa ya kuwashawishi wafuasi wao wasifanye vurugu au kufanya vitendo vinavyosababisha uvunjifu wa amani.
Pia wagombea watakaoshindwa kwenye uchaguzi mkuu wakubali matokeo kwani kwenye washindani lazima kuwe na washindwa ili kuondoa hali ya mafarakano kwani kwa wale watakaoshindwa wasipokubali matokeo wanaweza kuleta uvunjifu wa amani.
Hayo yalisemwa juzi Kijiji cha Maviayangombe kata ya Lugoba wilayani Bagamoyo mkoani Pwani na Askofu mkuu wa Dayosisi ya Morogoro ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Jacob Mameo Ole Paulo wa Dayosisi ya Morogoro wakati wa mazishi ya mtoto wa aliyekuwa kiongozi wa wafugaji Laban Moreto, Karokya Moreto (33) ambaye alikuwa mwanajeshi wa kikosi cha 04/691 cha Mtwara.
Askofu Ole Paulo alisema kuwa wagombea hao wanauwezo wa kudumisha amani kwa kuhubiri au kuingiza nchi kwenye machafuko endapo watayatumia vibaya majukwaa wakati wa kipindi hichi cha kampeni za uchaguzi.
“Wanapaswa kuhubiri amani na kuacha kutumia maneno yatakayo haribu amani ya nchi iliyopo ambayo imedumu kwa kipindi kirefu tangu nchi ilipopata uhuru miaka zaidi ya 50 hivyo itakuwa ajabu ivunjwe kisa kuwania uongozi tu,” alisema Askofu Ole Paulo.
Aidha alisema kuwa vyama vya siasa vinapaswa kupingana kwa hoja na kwa malumbano ambayo hayana maana bali yanaweza kuleta mitafaruku isiyokuwa ya lazima hasa kwa wale wanaoshindwa kwani wanapaswa kukubali matokeo.
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa amesikitishwa na kifo cha marehemu ambaye alikuwa ni ndugu kwani wamekuwa wakiishi kama familia moja na walikuwa na ushirikiano mkubwa baina ya familia zao.
Ridhiwani alisema kuwa kifo hicho ni pigo kwa familia hiyo pia kwa Taifa kwani alikuwa ni mtumishi wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na alikuwa mtaalamu wa rada hivyo pengo lake haliwezi kuzibika kikubwa ni kumwombea marehemu.
Kufuatia msiba huo Rais Dk Jakaya Kikwete alituma salamu za pole kwa familia hiyo kupitia kwa Mbunge wa Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete na kusema kuwa anatoa pole na Mungu awape nguvu katika kipindi hichi kigumu cha maombolezo na yuko pamoja nao.
Alisema kuwa Rais alishindwa kuhudhuria msiba huo kwani kwa sasa yuko nje ya nchi lakini pindi atakaporudi ataitembelea familia hiyo kwa ajili ya kuifariji kufuatia kifo cha mtoto wa aliyekuwa kiongozi wa kabila wafugaji
Naye mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mathayo Torongei alisema ili amani iendelee kuwepo ni vema dola ikatenda haki badala ya kupendelea upande mmoja.
Marehemu alifariki kwa ajali baada ya gari alilokuwa akiendesha kupasuka tairi la mbele na kusababisha ajali iliyopelekea kifo chake siku ya Septemba 16 mwaka huu  huko Mtwara ameacha mke na watoto watatu.
Mwisho. 







Mgombea Ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete kulia akifurahia jambo na mkuu wa wilaya ya Nachingwea mkoani Lindi Pololet Mgema wakati wa mazishi ya Karokya Moreto (33) mtoto wa alikuwa kiongozi wa wafugaji Laban Moreto huko Kijiji cha Maviyangombe kata ya Lugoba. 

 Baadhi ya Wazee wakiwa wamekaa kwenye msiba huo huko kijiji cha Maviyangombe Lugoba wilayani Bagamoyo. 

Kulia ni Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Morogoro  Jacob mameo Ole Paulo akiwa na mgombea Ubunge jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete. 

Kulia Ridhiwani Kikwete mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia CCM akifuatiwa na mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga, mkuu wa wilaya ya Nachingwea Pololet Mgema na mgombea ubunge Jimbo hilo kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Matayo Torongei wakiwa kwenye msiba huo. 

 Askofu Jacob Mameo Ole Paulo akizungumza wakati wa msiba huo. 

Baadhi ya ndugu wa wakilia kuomboleza kifo cha ndugu yao. 

 baadhi ya ndugu wa wakilia kuomboleza kifo cha ndugu yao.

Akinamama ndugu wa karibu wa marehemu wakilia kuomboleza kifo hicho. 

Baadhi ya askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania JWTZ wakiwa wamebeba jeneza lilokuwa na mwili wa marehemu kuelekea makaburini kwa ajili ya mazishi. 

Baadhi ya waombolezaji wakiaga mwili wa marehemu kabla ya mazishi  

Sehemu ya waombolezaji wa msiba huo. 

Sunday, September 13, 2015

MBUNGE KUTOA M 700 KUSAIDIA WAJASIRIAMALI

Na John Gagarini, Kibaha
MGOMBEA Ubunge wa Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Silvestry Koka ameunga mkono mpango wa kukipatia kila kijiji hapa nchini shilingi milioni 50 za uwezeshaji wajasiriamali kwa kuahidi kutoa kiasi cha shilingi milioni 700 kwa Jimbo hilo kwenye mpango huo.
Alitoa ahadi hiyo  wakati wa uzinduzi wa kampeni kwenye Jimbo hilo zilizofanyika kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja Kibaha mbele ya Mgombea Mwenza wa CCM Samia Suluhu Hassan ambaye alikuwa mgeni rasmi na kusema kuwa mpango huo ni mzuri na unapaswa kuungwa mkono na wadau wa maendeleo.
Koka ambaye alikuwa Mbunge wa Jimbo hilo anatetea kiti chake alisema kuwa tangu achaguliwe amekuwa akiwawezesha wajasiriamali wa Jimbo lote la Kibaha kwa kuwapatia fedha za kuwezesha vikundi vyao pamoja na mafunzo.
“Nimefurahishwa na mapango huo ambao ndiyo ilikuwa ajenda yangu ya kutaka wajasirimali waweze kuendeleza shughuli zao hivyo naipongeza serikali kwa kuona kuwa kuna haja ya kutoa fedha kwa ajili kuongeza pato la wananchi,” alisema Koka.
Alisema kuwa katika muda wake wa Ubunge miaka mitano iliyopita alitoa zaidi ya shilingi zaidi ya milioni 500 kwa wajasiriamali pamoja na kuwapatia elimu ya ujasirimali kupitia vikundi alivyohamasisha kuanzishwa.
“Nitatoa fedha hizo kwa kuiunga mkono serikali ili kuwaletea maendeleo wananchi wa Jimbo la Kibaha Mjini ambao wengi wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa mitaji kwa ajili ya kuendeshea shughuli zao,” alisema Koka.
Naye Mgombea Mwenza Samia Suluhu alisema kuwa mpango huo utawezesha wajasiriamali kukuza mitaji yao na  serikali itasimamia ipasavyo fedha hizo ili zisiweze kutumika vibaya ili ziweze kuleta manufaa kwa wananchi.
Samia alisema kuwa wenyeviti wa Vijiji ambao watazinyemelea fedha hizo kwa manufaa yao binafsi wajiandae kwani wale watakaozitumia kinyume cha taratibu watachukuliwa hatua kali ikiwa ni pamoja na kuwashtaki. Pia fedha kwa akinamama na vijana asilimia 10 kwenye halmashauri atasimamia na kuhakikisha zinatolewa kama taratibu zinavyoonyesha.

Mwisho.  

Sunday, September 6, 2015

BAKWATA WAASA UCHAGUZI MKUU

Na John Gagarini, Kibaha
KAIMU Mufti Mkuu wa Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Abubakari Zuberi amesema kuwa wanasiasa wanaokosa nafasi za uongozi wasiwe chanzo cha kuvunja amani ya nchi katika kipindi cha uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Aliyasema hayo juzi mjini Kibaha wakati wa maombi maalumu ya kuombea amani ya nchi yailiyoandaliwa na BAKWATA mkoa wa Pwani na kuwashirikisha viongozi na waumini wa kiislamu wa mkoa huo pamoja na waumini wa dini mbalimbali.
Mufti Zuberi alisema kuwa kuna baadhi ya viongozi walioshindwa na watakaoshindwa kwenye kuwania nafasi za uongozi wa kisiasa wanaonesha viashiria vya kutaka kuvunja amani iliyopo kutokana na kutokubali kushindwa.
“Kwa sasa tunaona viashiria mbalimbali vya kutaka kuvunja amani ya nchi     kutoka kwa baadhi ya wanasiasa hapa nchini na kutokana na hali hiyo tumeona ni vema tukafanya maombi haya kwa ajili ya kumwomba Mungu atunusuru na hali hiyo ili isije ikajitokeza,” alisema Mufti Zuberi.
Alisema kuwa Tanzania ni kama chumvi ya amani ambayo ikitumika vizuri itaongeza ladha lakini ikitumika vibaya itaharibu kila kitu hivyo ni vema Watanzania wakaendelea kuilinda amani iliyopo kwa sasa kwani baadhi ya majirani zetu wameathiriwa na vita na wanakimbilia kwetu.
“Tumwombe Mungu aendelee kutudumishia amani iliyopo kwa muda mrefu na tusikubali kuivunja amani yetu kwa tama ya baadhi ya watu wenye uroho wa madaraka kwani endapo amani itavunjika tutakuwa hatuna pa kukimbilia kwani majirani zetu wanakuja kwetu je sisi tutaenda wapi endapo amani itatoweka,” alisema Mufti Zuberi.
Kwa  upande wake mkuu wa Wilaya ya Kibaha Halima Kihemba ambaye alimwakilisha mkuu wa mkoa wa Pwani alisema kuwa tayari serikali imeweka mazingira ya uchaguzi kufanyika kwa njia ya amani na utulivu.
Kihemba alisema kuwa viongozi wa dini wanapaswa kuhakikisha amani inaendelea kudumu na kuwataka wawaelekeze waumini wao kufuta taratibu zilizopangwa katika kushiriki uchaguzi na wale wote waliojiandikisha watapiga kura na watakaokwenda kinyume cha sheria hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.
Naye Kadhi mkuu wa mkoa wa Pwani Abbas Mtupa alisema kuwa tayari wametoa maagizo kwa Maimamu na Masheikh wa misikiti yote kufanya maombi maalumu kila Ijumaa kuiombea amani ya nchi ili uchaguzi uwe wa amani.
Mtupa alisema kuwa maombi hayo maalumu ya kumwomba Mungu kwa wale wenye nia mbaya ya kuleta vurugu washindwe na maombi hayo yatakuwa endelevu hadi uchaguzi mkuu utakapoisha ili hali ya amani iendelee kudumu.
Mwisho.

  

     
 









Picha 1914 Kadhi wa mkoa wa Pwani Abbas Mtupa akizungumza kwenye maombi maalumu kuliombea taifa amani lilofanyika kwenye viwanja vya Bwawani Maili Moja Kibaha.

1918 Baadhi ya wakinamama waliohudhuria maombi maalumu ya kuliombea Taifa kuwa na amani katika uchaguzi mkuu wakiewasikiliza viongozi wao
1922 Mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba akihutubia kwenye maombi maalumu ya kuombea amani kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
1923 Sheikh Mtonda akiongea kwenye maombi maalumu kuliombea Taifa kuwa na amani kwenye kipindi cha uchaguzi.
1925 Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Pwani Said Lipambila akiwahutubia waumini wa Kiislamu waliohudhuria maombi maalumu kuiombea nchi kuwa na amani kipindi cha uchaguzi
1933 Kaimu Mufti mkuu wa Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) Abubakari Zuberi akiwahutubia waumini wa dini ya kiislamu waliohudhuria maombi maalumu kuliombea Taifa kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja wilayani Kibaha
1936 Baadhi ya wamini wa dini ya Kiislamu wakiwasikiliza viongozi wao wakati wa maombi ya kuliombea Taifa kwenye uwanja wa Bwawani maili Moja Kibaha
1940 baadhi ya waumini wakisikiliza viongozi wao wakati wa maombi maalumu ya kuliombea Taifa
1947 Kaimu Mufti Mkuu Abubakari Zuberi kulia akizungumza na Kadhi wa mkoa wa Pwani Abbas Mtupa wakati wa maombi maalumu ya kuliombea Taifa kwenye uwanja wa Bwawani Maili Moja Kibaha


Wednesday, September 2, 2015

WATAKA MABADILIKO YA SHERIA ZA MIRATHI

Na John Gagarini, Kibaha
SERIKALI kupitia vyombo vya kutunga sheria likiwemo Bunge vimetakiwa kubadilisha sheria za mirathi ili wanawake na watoto waweze kupata haki zao mara baba anapofariki dunia.
Hayo yalisemwa na baadhi ya madaktari na wauguzi wa Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani, wakati wa mafunzo juu ya kukabiliana na kansa ya kizazi na matiti pamoja na unyanyasaji wa jinsia mafunzo yaliyoandaliwa na Mtandao wa Wanawake Tanzania.
Moja ya washiriki wa mafunzo hayo Mganga wa Kituo cha Afya Mlandizi  Amilen Sam alisema kuwa familia nyingi mara baba anapofariki dunia wanawake wamekuwa hawapati mali yoyote licha ya kuwa wao walihusika katika upatikanaji wa mali hizo.
“Kutokana na sheria  nyingi za mirathi kupitwa na wakati vyombo vya kutunga sheria likiwemo Bunge lazima zibadili sheria hizo ambazo hazimpi nafasi ya kurithi mali ambazo mama kahusika kuzichuma na marehemu mume wake,” alisema Dk Sam.
Kwa upande wake Dk Pascalina Kamba wa Kituo cha Afya Disunyala alisema kuwa baadhi ya mila na desturi nazo ni chanzo cha tatizo hilo kutokana na kutoruhusu mwanamke kuongea lolote juu ya mali walizochuma na mume.
Dk Kamba alisema kutokana na sheria hizo kutungwa miaka ya nyuma ni dhahiri zimepitwa na wakati na hazipaswi kuendelezwa ili mwanamke na mtoto waweze kupata haki zao ikiwa ni matunda ya ndoa na si kuwanufaisha ndugu wa mume ambao hawajui mali hizo zimepatikana vipi.
Kwa upande wake mratibu kutoka mtandao huo wa maendeleo kwa wanawake Tanzania Gaudence Msuaya alisema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuwapa nafasi walengwa kujadili unyanyasaji uliopo ndani ya jamii pia kuchukua hatua mara waonapo dalili mbaya zinazohusiana na magonjwa ya Kansa ya matiti na shingo ya uzazi.
Msuya alisema kuwa lengo lingine ni kuwajengea uwezo madaktari na wauguzi hao ili watoe elimu hiyo kwa jamii pamoja na wteja wao wagonjwa ambao wanawapatia huduma ya matibabu kwenye maeneo yao ya kazi.
Mwisho.
  

SHULE YAFUNGWA BAADA YA MWANAFUNZI KUFA KWA KIPINDUPINDU

Na John Gagarini, Kibaha

KUFUATIA kifo cha mwanafunzi wa wa darasa la tatu Shule ya Msingi Maendeleo wilayani Kibaha mkoani Pwani kufariki dunia kutokana na ugonjwa wa kipindupindu serikali imeifunga shule hiyo kwa muda usiofahamika ili kuwanusuru wanafunzi na ugonjwa huo.

Aidha imepiga marufuku mikusanyiko yote sherehe, misiba, minada ya hadhara na wafanyabiashara ndogondogo wa vyakula kuuza biashara mashuleni, biashara za matunda na vyakula kwenye maeneo ya wazi ili kuepuka kusambaa kwa ugonjwa huo.

Akitoa ufafanuzi juu ya ugonjwa huo kuthibitika kuingia katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo na mkoa wa Pwani mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba alisema kuwa mwanafunzi mwingine anaugua ugonjwa huo hali iliyosababisha serikali wilayani Kibaha kuifunga shule hiyo kwa muda ili kuchukua tahadhari na kuhofia ugonjwa huo usienee kwa wengine.

“Tunasikitika kutokana na kifo cha mwanafunzi huyo na tumeona ili kunusuru wanafunzi wengine kuambukizwa tumeifunga shule hiyo na kupiga marufuku uuzwaji wa vyakula kwenye maeneo ya wazi ikiwemo stendi ya Maili Moja ambapo biashara ya chakula hufanyika nyakati za usiku,” alisema Kihemba.

Kihemba alisema kuwa waliamua kuchukua hatua hizo za dharura ili kupunguza kuenea ugonjwa huo ambao na wafanyabiashara waache tabia ya baadhi ya wananchi ya kutiririsha maji machafu kwenye mitaro na mifereji ya barabarani.

“Nawaomba wananchi kuzingatia maagizo hayo na kuzingatia kanuni za usafi ili kuepuka ugonjwa huo ambao endapo hatua za haraka hazijachukuliwa husababisha kifo,” alisema Kihemba.

Katika hatua nyingine mkuu huyo wa wilaya hiyo amekemea vitendo cha baadhi ya wananchi kwenda kupatiwa matibabu kwenye hospitali za mitaani hali inayosababisha kushindwa kupona ama kugundulika kwa ugonjwa huo hatimaye kusababisha vifo.

“Kwa sasa tayari tumeshachukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuagiza madawa ya kutokomeza ugonjwa huo wa kipindupindu katika mamlaka husika na wanafunzi wa shule ya msingi maendeleo wamepatiwa dawa wote na wanafunzi wote wa shule hiyo wamepatiwa dawa,” alisema Kihemba.

Aidha alisema Idara ya afya mkoani humo imetenga maeneo ya kuwalaza baadhi ya wagonjwa wanaohisiwa kuwa na ugonjwa huo kwa ajili ya kuwapatia vipimo maalumu na kuwaanzishia  tiba mahususi ya ugonjwa huo.
  
“Kuanzia tarehe 24 Agosti mwaka huu wilaya ya Kibaha imepokea wagonjwa wenye dalili za ugonjwa wa kipindupindu wapatao 11 katika kituo cha afya Mlandizi na Mkoani, ambapo wawili kati yao waligundulika kuwa na ugonjwa huo na mmoja ambae ni mwanafunzi alifariki dunia kabla ya matibabu.

Alibainisha kuwa wagonjwa waliopokelewa walikuwa ni kutoka maeneo ya Maili Moja, Muheza, Tangini na Makuruge wilaya ya Kisarawe, Msigani na Mpiji Majohe wilaya ya Kinondoni, Visiga na Magindu Kibaha vijiji , Ruvu Darajani Bagamoyo ambapo kati yao watatu ndio waliogundulika kuwa na ugonjwa huo baada ya kufanyiwa vipimo .

Mwisho

CCM MUFINDI WATAMBA KUSHINDA UCHAGUZI MKUU

Na John Gagarini, Mafinga
KUTOKANA na Utekelezaji wa Ilani kikamilifu chama cha mapinduzi kinatarajia kushinda kwenye uchaguzi mkuu ujao kwenye nafasi zote za Urais Ubunge na Udiwani
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mufindi mkoani Iringa kimeweka mikakati ya kupata ushindi wa kishindo kwa wagombea wake kwenye nafasi tatu za Urais Wabunge na Madiwani kutokana na utekelezaji wa ilani ya chama.
Hayo yalisemwa na mjini Mafinga na katibu wa CCM wilaya ya Mfundi Jimson Mhagama alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake na kusema kuwa ushindi wa chama unatokana na ilani kutekelezwa kwa asilimia 95.
Mhagama alisema kuwa wilaya hiyo ina majimbo matatu ya Mufindi Kaskazini ambalo linaongozwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mahmoud Mgimwa, Mufindi Kusini linaongozwa na Menrad Kigora na Mafinga Mjini litakalowaniwa na Cosatu Chumi pamoja na kata 36 vyote vikiwa chini ya CCM  hivyo wana uhakika wa kuendelea kuyaongoza maeneo hayo.
“Sisi hatuna wasiwasi tunaendelea kuweka mikakati ya suhindi lakini ushindi wetu utatokana na utekelezaji wa ilani ya chama juu ya maendeleo kwenye sekta mbalimbali za huduma za jamii ambazo zimeboreka kutokana na uongozi mzuri wa viongozi wa chama,” alisema Mhagama.
Alisema kuwa mfano kwenye huduma za jamii ujenzi wa baadhi ya barabara kwa kiwango cha lami na changarawe zinazofanya kupitika kwa kipindi chote cha mwaka, uboreshaji wa huduma za afya kwenye Hospitali ya Mafinga na ujenzi wa zahanati kwenye vijiji, uanzishwaji wa vikundi vya ujasiriamali, huduma za taasisi za fedha na ujenzi wa shule za sekondari, uanzishwaji wa vyuo mbalimbali.
Aidha alisema kuwa CCM itaendelea kusimamia ilani yake kwa lengo la kuhakikisha maendeleo yanapatikana ili kuondoa changamoto zinazowakabili wananchi ambao wamekiamini chama kutokana na kuongoza kwa manufaa ya jamii.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mafinga
MGOMBEA Urais wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ambaye aliwahi kuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa amemwagia sifa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mahmoud Mgimwa kutokana na uchapakazi wake kwenye wizara pamoja na kuhamasisha maendeleo kwenye Jimbo la Mufindi Kaskazini analoliongoza.
Akihutubia wakazi wa mji wa Mafinga wakati wa mkutano wake wa kampeni Lowassa alisema kuwa mbunge huyo ni mchapakazi na amefanya mabadiliko makubwa kwenye Jimbo hilo na kwenye Wizara ya Maliasili na Utalii.
Lowassa alisema kuwa Mgimwa ni moja ya viongozi wazuri ambao wanawajibika vizuri katika maeneo ambayo wamepewa kuwajibika lakini angekuwa kwenye chama kama CHADEMA angefanya vizuri zaidi.
“Mgimwa namfahamu ni muwajibikaji mzuri katika maeneo ambayo anayaongoza lakini angekuwa upinzani angefanya vizuri zaidi kwani wapinzani wanafanya kazi sana na wana uwezo wa kuleta maendeleo,” alisema Lowassa.
Kwa upande wake katibu wa CCM wilaya ya Mufindi Jimson Mhagama akizungumzia juu ya kauli ya Lowassa alisema kuwa Mgimwa ni zao la CCM ambalo limeandaliwa kwani ndiyo kazi yao kutengeneza viongozi bora.
Mhagama alisema kuwa kiongozi bora anatoka CCM na kazi ya wapinzani ni kuchukua watu ambao uwezo wao umeshakuwa mdogo hivyo kushindwa kuwajibika hali ambayo haitawaletea maendeleo wananchi.
Aliwataka wananchi kuiunga mkono CCM na kuachana na vyama vya upinzani ambavyo havina sera za kuwaletea maendeleo wananchi badala yake ni kuwagawa na kuendeleza malumbano ambayo hayana faida kwa wananchi.
Naye mkazi wa Mafinga Edina Peter alisema kuwa wao wanataka kiongozi ambaye atawasaidia kukabiliana na changamoto zinazowakabili wananchi na Mgimwa ni moja ya viongozi bora ambao wanajali maslahi ya wananchi.
Mwisho.
    
  

   

WODI YA WAZAZI MAFINGA YAHITAJI MAMILIONI YA FEDHA KWA AJILI YA VIFAA VYA UPASUAJI

Na John Gagarini, Mafinga
HOSPITALI ya wilaya ya Mufindi mkoani Iringa inahitaji kiasi cha shilingi milioni 80 kwa ajili ya upatikanaji wa vifaa vya upasuaji kwenye wodi ya wazazi.
Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake kaimu mganga mkuu wa halmashauri ya Mji wa Mafinga Dk Innocent Mhagama alisema kuwa fedha hizo ni pamoja na ukarabati wa chumba cha upasuaji kwenye wodi hiyo.
Dk Mhagama alisema kuwa jengo hilo la wodi ya wazazi limekamilika na linatumika lakini halina huduma ya upasuaji kwa wanawake wajawazito.
Alisema kuwa wanafanya mipango mbalimbali kwa ajili ya kupata fedha hizo ili kutoa huduma bora za idi ya hapo kwani matatizo yote yatakuwa yakitatuliwa ndani ya jengo hilo pasipo kumhamisha mgonjwa.
“Wodi hii iliyogharimu kiasi cha shilingi milioni 320 imekamilika tangu mwaka jana na inatoa huduma zote isipokuwa upasuaji ambapo kwa sasa tunatafuta fedha hizo ili kuwe na huduma hiyo,” alisema Dk Mhagama.   
 Alisema kuwa kukamilika kwa wodi hiyo kumepunguza tatizo la akinamama kutopata huduma bora lakini sasa huduma zimeboreka.
“Wodi ya awali ilikuwa na uwezo wa kuzalisha akinamama wawili au watatu lakini kwa sasa wanazalisha akinamama nane kwa wakati mmoja ambapo inauwezo wa kulaza akinamama 60 toka 20 kwa  wakati mmoja ambapo wanaojifungua kwa siku ni kati ya 18 na 20 na wanaofanyiwa operesheni kwa siku ni kati ya wanne hadi sita,” alisema Dk Mhagama.
Moja akinamama wanaotumia wodi hiyo Blandina Mpyanga alisem akuwa wanaishukuru serikali na wadau mbalimbali waliofanikisha ujenzi huo.
Mpyanga alisema kuwa kwa kipindi cha nyuma wakinamama wajawazito walikuwa wakilala wanne kwenye kitanda kimoja lakini kwa sasa kila mgonjwa na kitanda chake.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mafinga
KATIKA kukabiliana na changamoto ya baadhi ya wanafunzi wa kike kupata ujauzito pamoja na kuozwa katika umri mdogo Jimbo la Mufindi Kaskazini wilayani Mufindi mkoani Iringa imewekwa mikakati ya ujenzi wa hosteli za wanafunzi kwa shule za sekondari.
Akizungumza na waandishi wa habari mbunge wa Jimbo hilo ambaye anatetea kiti hicho Mahmoud Mgimwa alisema kuwa ujenzi huo ni kwa ajili ya shule zote za kata na zingine ili kukabiliana na changamoto hizo.
Mgimwa ambaye ni Naibu waziri wa Maliasili na Utalii alisema kuwa hadi sasa shule ya sekondari ya Isalavanu tayari imekamilika huku ile ya Kibengu ikiwa ujenzi unaendelea.
“Hii ni moja ya mikakati ambayo nimeiweka kama kipaumbele cha utekelezaji wa ilani ya chama ambapo nimechangia hosteli hizo bati 170 na vifaa mbalimbali katika kukamilisha ujenzi huo,” alisema Mgimwa.
Alisema kuwa endapo kila kata itakuwa na hosteli ni dhahiri tatizo la mimba na wanafunzi kuozwa wakiwa bado wanafunzi litapungua au kwisha kabisa.
“Unajua wanafunzi wa kike wanachangamoto kubwa kwani baadhi ya watu wamekuwa wakiwarubuni kutokana na mazingira wanayoishi hasa kutokana na umbali wa shule wanazosoma lakini wakijengewa mabweni itawasaidia,” alisema Mgimwa.
Mmoja ya wakazi wa Mji wa Mfainga Anna Karoli alisema kuwa mpango huo ni mzuri na utasaidia kuwanusuru wanafunzi wanaopewa mimba na kuozwa.
Karoli alisema wanafunzi wa kike wakikaa shule itawasaidia kujiepusha na vishawishi mbalimbali mara watokapo au kwenda shule.
Moja ya wanafunzi wa kike Anita Michael ambaye ni mwanafunzi wa shule ya Sekondari ya JJ Mungai alisema kuwa mpango huo ni mzuri na utawasadia wanafunzi wa kike kukabiliana na changamoto hizo.
Anita alisema kuwa baadhi ya changamoto wanazozipata ni kurubuniwa na baadhi ya watu wakiwemo madereva wa bodaboda ambao wamekuwa wakiwadanganya kwa kuwapa lifti wakati wakwenda shule.
Mwisho.
Na John Gagarini, Mafinga
WATUMISHI wa Halmashauri ya Mji wa Mafinga wilayani Mufindi mkoani Iringa wametakiwa kuacha kujihusisha na mambo ya siasa ili kutozorotesha utoaji huduma kwenye sehemu zao za kazi.
Hayo yalisemwa na mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Shaib Nnunduma alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Mafinga na kusema kuwa kufanya hivyo ni kosa kisheria.
Nnunduma alisema kuwa kama mtumishi anataka kujihusisha na sisa kuna taratibu ambazo anatakiwa afuate lakini si kufanya siasa akiwa kazini.
“Kufanya siasa ofisini ni kosa kisheria na mtumishi ambaye anafanya hivyo ni kinyume cha sheria za kazi hivyo hawapaswi kufanya hivyo kwani ni kukwamisha utendaji kazi,” alisema Nnunduma.
Alisema kuwa endapo mtumishi anabainika kujihusisha na siasa kazini sheria inambana na anaweza kuchukuliwa hatua kali ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi.
“Kila mtu kuna chama anachokipenda lakini huwezi kuonyesha itikadi zako za chama ofisini kwani kuna baadhi ya watu utawabagua kutokana na vyama vyao hivyo hilo ni kosa kisheria,” alisema Nnunduma.
Aidha alisema kuwa ataandaa mkutano na watumishi wote wa Halmashauri ili kuwajulisha kujiepusha na siasa kazini ambapo wakuu wa shule za sekondari alishaongea nao juu ya kujiepusha na siasa shuleni.
Mwisho.