Friday, October 24, 2014

POLISI WAKAMATA LUNDO LA SILAHA, FEDHA NA VITU MBALIMBALI

Na John Gagarini, Kibaha
WATU watatu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wamekamatwa wakiwa na silaha aina ya Short Gun yenye namba 07019302 ikiwa na risasi nane.
Hayo yamesemwa na kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei alipoongea na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mohamed Kalipa (20) dereva wa Bajaji mkazi wa Mbagala Rangi Tatu, Salum Shekivui (20) mkazi wa Buza na Seuli Lucas (18) makazi wa Mbagala Rangi Tatu Jijini Dar es Salaam.
Kamanda Matei alisema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa Oktoba 20 mwaka huu majira ya saa 2:30 huko Mlandizi wilaya ya Kibaha.
“Mbali ya silaha pia walikutwa na fedha taslimu kiasi cha shilingi milioni 6,611,800, vocha mbalimbali za simu zenye thamani ya shilingi milioni 2,185,500 na simu za mkononi sita za aina mbalimbali ambazo thamani yake bado hazijafahamika,” alisema Kamanda Matei.
Aaidha alisema kuwa watuhumiwa hao wanadaiwa kuwa walifanya tukio la unyanganyi wa kutumia silaha huko Kijiji cha Mbwewe wilaya ya Bagamoyo kwenye duka la Twaha Mbuta siku ya Oktoba 19 saa 1:30 usiku na kupora kiasi cha shilingi milioni 30,000,000.
“Baada ya kukamatwa walimtaja mtuhumiwa mwenzao ambaye  walikuwa wakishirikiana naye Samwel Joseph mkazi wa Kongowe Kibaha ambapo baada ya upekuzi walimkuta na risasi sita za Short Gun ambazo alikuwa akizimiliki bila ya kibali hata hivyo mtuhumiwa huyo alitoroka,” alisema Kamanda Matei.
Katika tukio lingine watu wawili walikamatwa kwa tuhuma za wizi wa ngombe 61 wenye thamani ya shilingi milioni 27,450 ,000 mali ya Keke Furaha (37) kwa kutumia silaha aina ya sime.
Alibainisha kuwa tukio hilo limetokea Oktoba Mosi mwaka huu majira ya saa 5 asubuhi huko Lulenge kata ya Ubena wilayani Bagamoyo ambapo watuhumiwa ni Sadala Lupoto (25) mkazi wa Kimamba Kilosa na Luseky Sogoyo (25) na juhudi za kuwatafuta ngombe wengine 39 zinaendelea.  
Katika tukio lingine watu wawili wanashikiliwa kwa tuhuma za kukutwa na silaha aina ya gobore bila ya kibali  huku wengine 11 walikamatwa kwenye matukio ya kukutwa na bangi gunia mbili na kete 250 pamoja na lizla zipatazo 100.
            
Mwisho.









Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Ulrich Matei akionyesha moja ya silaha zilizokamatwa kwa watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi. 

Silaha mbalimbali ambazo jeshi la polisi mkoani Pwani limezikamata mara baada ya kufanya misako maeneo mbalimbali ya mkoa huo. 

 Redio na deki vilivyoibiwa na kukamatwa kwa watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi. 

  Bunduki, tv, simu na vifaa vingine ambavyo vilikamatwa na polisi baada ya kuibiwa kwa watu mbalimbali mkoani humo.

Silaha pamoja na kiasi kikubwa cha fedha ambazo ziliibiwa kwa mfanyabiashara Twaha Mbuta wa huko Mbwewe. 

Sehemu ya fedha, vocha na risasi zilizokamatwa na polisi baada ya kufanya masako wa kusaka majambambazi.

 Redio zilizoibiwa kwa watu mbalimbali mkoani Pwani baada ya polisi kufanya misako mkoani humo
Kamanda wa Polisi Mkoani Pwani Ulrich Matei akiongea na waandishi wa habari mjini Kibaha hawapo pichani

Sunday, October 19, 2014

GOMBO GAMBUSI




 Mtumishi wa Mungu wa kituo cha maombezi cha Gombo Gambusi kilichopo Kibamba kwa Waitara Mwalimu Allister Albano akiwa anahubiri kituoni hapo Jumapili hii. 

 Mtumishi wa Mungu Mwalimu Allister Albano kushoto akiwa na mkewe wakifanya maombi kwa waumini kituoni hapo Jumapili hii

 Mtumishi wa Mungu Mwalimu Allister Albano kushoto akimwombea mgonjwa wakati wa ibada iliyofanyika kituoni hapo Jumapili hii 

 Baadhi ya waumini wakiwa kwenye maombi kwenye ibaada iliyofanyika Jumapili hii 

 Baadhi ya waumini wakiwa wanafanyiwa maombi na mtumishi wa Mungu Mwalimu Allister Albano 

 Mmoja ya waumini akiwa ameanguka chini baada ya kufanyiwa maombi kwenye ibaada ya Jumapili iliyofanyika kituoni hapo 

 Waumini wa kituo hicho wakiwa wanamsikiliza Mwalimu Allister Albano wa kituo hicho hayupo pichani alipokuwa akihubiri Jumapili hii 

 Waumini wakiwa wanaomba wakati wa ibaada hiyo Jumapili hii.

WACHINA WAVUTIWA BAGAMOYO

Na John Gagarini, Bagamoyo
JIMBO la Jilin nchini China limekubali kuwekeza hapa nchini kwenye eneo la Uwekezaji la (EPZ) la Kamal lililopo Kijiji cha Kerege kwa Kiwete wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.
Uwekezaji huo utafanyika baada ya ujio wa baadhi ya viongozi wa Jimbo hilo kutembelea maeneo mbalimbali ya uwekezaji wilayani humo na kuonekana kuvutiwa na sehemu hiyo.
Akizungumza jana mara baada ya kutembelea maeneo kadhaa akiongozana na mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza na sekretarieti ya mkoa wa Pwani na kuvutiwa na eneo hilo la uwekezaji la EPZ, Naibu Gavana wa Jimbo hilo Zhoncheng Sui alisema ameridhika na eneo hilo.
Sui alisema kuwa kutokana na urafiki wa kihistoria uliyopo kati ya Tanzania na China toka enzi za viongozi wa mataifa hayo Mwalimu Julius Nyerere na Mao Tse Sung kumekuwa na ushirikiano ambao ni wa damu hivyo lazima udumishwe kwa ushirikiano wa kimaendeleo.
“Tumeona mambo mengi ambayo tunaweza kushirikiana ambapo moja ni pale kwenye eneo la uwekezaji ambapo tutakuja kuwekeza hapo kwani kuna miuondombinu mizuri ya barabara, maji na umeme pia waiteni na wenzetu waliopo hapa Tanzania ili nao waje wajionee na kuangalia namna wanavyoweka kuwekeza kwenye mkoa huu wa Pwani,” alisema Sui.
Awali akimkaribisha naibu gavana wa Jimbo hilo la Jilin mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza alisema kuwa mkoa wa Pwani una mambo mengi ambayo wawekezaji wanaweza kuwekeza ikiwa ni pamoja na kwenye kilimo, uvuvi, utalii na mifugo.
“Fursa zipo nyingi ndani ya mkoa wetu na hata miundombinu ya barabara, anga, bandari, uememe na reli viko vizuri kwa ajili ya kufanikisha uwekezaji ambao una hitaji uwepo wa mawasiliano mazuri,” alisema Mahiza.
Ujumbe huo ulikuwa na ziara ya siku moja wilayani Bagamoyo kutembelea  maeneo ya uwekezaji kwenye ujenzi wa soko la kimataifa la samaki, eneo itakapojengwa bandari na eneo la uwekezaji la Kamal.

Mwisho.
 Mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza katikati mwenye kilemba akiwa na ugeni toka nchini China wakiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa wilaya ya Bagamoyo mara baada ya kumaliza mkutano wa pamoja uliofanyika kwenye hoteli ya Oceanic bay Hotel $ Resort  

 Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza kulia akiteta jambo na kiongozi wa ujumbe  kutoka Jimbo la Jilin nchini China Zhongcheng Sui wali[potembelea wilaya Bagamoyo kuangalia maeneo ya uwekezaji 



 Mkuu wa mkoa katikati na ugeni kutoka nchini China wakiangalia bomba ambalo limetoboka na maji kumwagika, kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Ahmed Kipozi

Monday, October 13, 2014

WAIMBAJI NA KWAYA ZA INJILI ZIJIUNGE NA BASATA

Na John Gagarini, Kibaha

KWAYA na Waimbaji wa nyimbo za Injili nchini wameshauriwa kujisajili Baraza la Sanaa ili watambulike kisheria kwa lengo la kuepuka kudhulumiwa haki za kazi zao.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha mwishoni mwa wiki na Naibu Waziri wa Sheria na Katiba Angella Kairuki wakati alipokuwa mgeni rasmi katika hafla ya kuchangia fedha za kununulia vifaa vya mawasiliano na kurekodi albamu ya video ya kwaya ya kanisa la Sabato la Maili Moja Kibaha mkoani Pwani.

Waziri Kairuki alisema kuwa baadhi ya kwenye makanisa ya na waimbaji mbalimbali hawajaona umuhimu wa kujisajili ili ziweze kutambulika na kunufaika kama zilivyo kazi nyingine za sanaa.

“Kwaya na waimbaji wa nyimbo za injili nazo zinawajibu wa kujisajili katika baraza hilo ili ziweze kupata haki zao pamoja fursa mbalimbali pia kukabiliana na baadhi ya watu wanaotumia kazi zao kujinufaisha binafsi huku walengwa wakiwa hawaambulii kitu hivyo sio vyema kukaa bila kujisajili rasmi,” alisema Waziri Kairuki.

Alisema ameona ni vyema akawahimiza kwani  jambo hilo lina manufaa kwa waimbaji na kwaya za makanisa ili waweze kupiga hatua kama ilivyo kwa baadhi ya wasanii wengine wa nyimbo za injili ambao tayari wamepiga hatua.

Alibainisha kuwa muziki unachangia amani,upendo na mshikamano hivyo wajitahidi pia kuimba nyimbo za kuiombea nchi yetu kwa masuala hayo muhimu pamoja na kumtukuza mungu.

“Nawaomba wanakwaya wa nyimbo na waimbaji wa nyimbo za injili kutengeneza albamu za video zenye maadili kwa michezo na mazingira yake pasipo kwenda kinyume na maadili ya kidini na kugeuza injili kuwa biashara, kwani zipo baadhi ya kanda za wasanii wengine ambazo hazionyeshi maadili mazuri,” alisema Waziri Kairuki.

Waziri Kairuki alisema serikali ipo pamoja na wasanii wa aina zote na inatambua kazi za sanaa ,tasnia ya wasanii na ndio maana katika katiba inayopendekezwa walihakikisha wanatambua kazi za wasanii, katika hafla hiyo kulipatikana zaidi ya sh m 22 ambapo ahadi zilizotolewa ni zaidi ya Mil 19.

Mwisho



WLAC YAPONGEZWA KUSAIDIA WANANCHI MASUALA YA SHERIA BURE

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Halima Kihemba amekipongeza kituo cha Msaada wa Kisheria  kwa Wanawake (WLAC) kwa kujitolea kutoa huduma za kisheria bure kwa wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za kuwalipa wanasheria.
Aliyasema hayo mjini Kibaha wakati akifunga mafunzo ya wasaidizi wa Kisheria wilayani humo ya siku 25 yaliyoandaliwa na Kituo cha Msaada wa Kisheria kwa Wanawake (WLAC).
Kihemba alisema kuwa kituo hicho kimeonyesha umuhimu wa kutoa msaada wa kisheria ni muhimu kwa watu hususani wanawake na watoto ambao wamekuwa wakipoteza haki zao kutokana na baadhi ya watu kutumia unyonge wao wakutokuwa na sauti ndani ya jamii kuwadhulumu haki zao.
“Huduma ya kisehria ni muhimu ndani ya jamii lakini watu wengi wamekuwa wakishindwa kumudu gharama hizo hivyo kushindwa kupata haki zao hivyo mashirika kama haya ni ya kuigwa,” alisema Kihemba.
Aidha alisema kuwa makundi hayo mawili ndiyo yamekuwa yakidhulumiwa haki zao kwa kiasi kikubwa hivyo mashirika kama WLAC yanayojitolea lazima yaungwe mkono na wadau mbalimbali ikiwemo serikali.
Awali akimkaribisha mkuu wa wilaya mkuu wa idara ya Mafunzo ya WLAC Magdalena Mlolere alisema kuwa lengo la kituo hicho ni kuhakikisha kuwa watu wanapata haki zao ambazo ni za msingi na ziko kikatiba.
Mlolere alisema kuwa lengo la kutoa mafunzo hayo kwa wasaidizi wa kiseheria wa vituo vya KPC na KPP ni ili waweze kusaidia wananchi kutatua migogoro inayojitokeza kabla ya kufika kwenye vyombo vya kisheria ikiwemo mahakama na polisi.
“Mafunzo hayo pia yatasaidia kupunguza kesi zinazopelekwa mahakamani ambazo nyingine zimekuwa zikitumia muda mrefu kuamuliwa na kuwafanya wahusika kutumia muda mwingi kwenda mahakamani huku wakishindwa kufanya shughuli zao za maendeleo,” alisema Mlolere.
Akisoma hotuba mbele ya mgeni rasmi moja ya wahitimu wa mafunzo hayo kwa niaba ya wahitimu John Gagarini alisema kuwa changamoto zinavyovikabli vituo hivyo ni baadhi ya wanajamii kutokuwa wawazi katika kuyapeleka mashauri hayo kwenye vituo hivyo pia ni ukosefu wa usafiri wa kuweza kufika kwenye maeneo hasa yale ya vijijini, jumla ya wahitimu 32 walihitimu mafunzo hayo na kukabidhiwa vyeti na mkuu huyo wa wilaya ya Kibaha Halima Kihemba.
Mwisho.
  


WAZIRI KAIRUKI ALITAKA KANISA KUOMBEA AMANI YA NCHI


Na John Gagarini, Kibaha

NAIBU Waziri wa Sheria na Katiba Angella Kairuki amewataka waumini wa Kanisa la Sabato Maili Moja Kibaha mkoani Pwani na wananchi kuendelea kuiombea nchi isiingie kwenye machafuko .

Waziri Kairuki aliyasema hayo mjini Kibaha katika kanisa hilo alipokuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya kuchangia fedha za kununulia vifaa vya mawasiliano na kurekodia vya kwaya ya kanisa hilo na kusema kuwa wasikubali kutumiwa na baadhi ya watu kwa mambo ambayo ni kinyume na sheria za nchi.

Alisema nchi imekuwa na amani kwa miaka mingi sasa ikiwa ni mfano wa kuigwa na nchi nyingine hivyo haina budi kila mmoja akasali kuliombea taifa ambalo pia likielekea kwenye chaguzi mbalimbali.

“Msiwakubali watu ambao wamekuwa wakitumia wananchi ili kuvuruga amani ya nchi na wamekuwa wakitaka kuungwa mkono lakini wanaokuja kupata matatizo ni wananchi na siyo wao hivyo msikubali kufuata mkumbo,” alisema Waziri Kairuki.
Aidha Waziri Kairuki alisema hakuna haja ya kuendelezwa kwa mijadala ya katiba inayopendekezwa ama kuibua hoja zisizo na tija kwa maslahi ya taifa kwani muda wake umekamilika na hatua inayosubiriwa ni tamko kutoka kwa Mh Rais litakaloeleza wakati wa kupiga kura ya maoni kwa wananchi.

Kwa upande wake Mchungaji wa Kanisa la Sabato Maili Moja Eliasi Timasi alimshukuru Waziri Kairuki kwa nasaha zake na kusema wataendelea kuhimiza amani kwa kufanya mawasiliano ya karibu na serikali pamoja na kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili waumini wa kanisa hilo.

Katika shughuli hiyo ya kuchangia vifaa vya mawasiliano ya kanisa na kurekodia  kwaya kulipatikana zaidi ya sh m 22 ambapo ahadi zilizotolewa ni zaidi ya m 19.

Mwisho.

Thursday, October 2, 2014

WANAFUNZI WAASWA KUHUSU TEKNOLOJIA

Na John Gagarini, Kibaha
WAZAZI wilayani Kibaha mkoani Pwani wametakiwa kuwalinda watoto wao waepukane na matumizi mabaya ya Teknolojia ya mawasiliano ili wasifuate tamaduni mbaya za nchi za Magharibi ambazo zimewaharibu vijana Tanzania.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha,  Jenifa Omollo wakati wa mahafali ya tisa ya darasa la saba ya shule ya awali na Msingi ya Kibaha Independent (KIPS).
Omollo alisema kuwa teknolojia ya mawasiliano ni nzuri endapo inatumiwa vizuri lakini ina athari endapo itatumiwa vibaya hasa kwa vijana kuiga tamaduni za nje zinazohamasisha vitendo viovu.
“Tuko kwenye utandawazi ambao unatumia teknolojia ya mawasiliano na kuifanya dunia kuwa Kijiji na kumekuwa na muingiliano mkubwa wa tamaduni ambazo nyingine ni mbaya zinazokinzana na maadili ya kitanzania ikiwa ni pamoja na mavazi, ngono, matumizi ya dawa za kulevya na matumizi mabaya ya mitandao ya kuangalia picha za ngono,” alisema Omollo.
Alisema kuwa kundi la vijana limeathiriwa kwa kiasi kikubwa na tamaduni hizo mbaya ambapo vijana hao wanafikiri ndiyo kwenda na wakati kumbe wanajiharibia maisha yao ya baadaye.
“Kwa sasa kuna matumizi mabaya ya teknolojia kupitia njia za simu, kompyuta na televisheni hivyo lazima wazazi wawaelekeze matumizi sahihi ya vifaa hivyo ambavyo endapo vitatumiwa vizuri vinaweza kuwa na manufaa mazuri kwa watumiaji,” alisema Omollo.
Awali akimkaribisha mgeni rasmi mkurugenzi wa shule hiyo Said Mfinanga alisema kuwa shule yao moja ya vitu inavyozingatia ni maadili mazuri ya Kitanzania ili wanafunzi wanapotoka hapo wawe na tabia njema.
Mfinanga alisema kuwa licha ya shule kufundisha masomo ya mawasiliano ya Kompyuta lakini wanazingatia maadili ili kuepuka na matumizi mabaya ya Teknolojia na kuzingatia kutoa elimu bora.
Shule hiyo ni ya kutwa na bweni ilianzishwa mwaka 2002 na ina jumla ya wanafunzi 480 na ni miongoni mwa shule zinazofanya vizuri kwenye wilaya hiyo pamoja na mkoa ambapo mwaka huu jumla ya wahitimu 39 walipewa vyeti vya kuhitimu darasa la saba.

Mwisho.       

KIBAKA AUWAWA KWA KUCHOMWA MOTO KWA WIZI WA PIKPIKI

Na John Gagarini, Kibaha
KIJANA mwenye umri kati ya miaka (25) na (30) anayedahaniwa kuwa ni kibaka ambaye jina lake halikuweza kufahamika ameuwawa kwa kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kwa tuhuma za kuiba pikipiki.
Wananchi hao walifikia hatua hiyo baada ya kubaini kuwa mtuhumiwa huyo akiwa na mwenzake waliiba pikipiki hiyo huko Gairo mkoani Morogoro na kutaka kuiuza Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kaimu kamanda wa Polisi mkoani humo Athuman Mwambalaswa alisema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 25 mwaka huu majira ya saa 1 asubuhi eneo la Pera Chalinze wilaya ya Bagamoyo.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa watuhumiwa hao wawili walikuwa na pikipiki ainaya ya Toyo yenye namba za usajili T 336 BZC ambayo inadhaniwa kuwa waliiba huko Gairo na walifika Chalinze kwa lengo la kutaka kuiuza.
“Vijana hao ambao ni wa kabila la Kimasai walifika hapo huku wakitafuta wateja wa pikipiki hiyo na wananchi hao walipowauliza uthibitisho wa pikipiki hiyo yaani kadi walishindwa kuonyesha na ndipo walipoanza kuwapiga na mmoja alifanikiwa kukimbia huku mwingine akipigwa kisha kuchomwa moto,” alisema Kamanda Mwambalaswa.
Alisema kuwa mwili wa marehemu ulikutwa mashambani ukiwa umechomwa moto na kuharibika vibaya sehemu mbalimbali za mwili.
Aidha aliwataka wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi kwani ni kinyume cha sheria na kuwataka kuwapeleka kwenye vyombo vya sheria ikiwa ni pamoja na polisi ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.
Mwisho.


SHERIA ZA USHIRIKA ZIMEPITWA NA WAKATI, UMRI WA URAIS UPUNGUZWE

Na John Gagarini, Mkuranga
MKUU wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza amesema kuwa sheria za Ushirika  zimepitwa na wakati hali ambayo inasababisha baadhi ya watu kutumia mwanya kuwadhulumu wakulima wa zao hilo hapa nchini.
Kutokana na fedha nyingi kutumiwa kwa matumizi binafsi na baadhi ya viongozi wa vyama vya ushirika kumesababisha chama kikuu cha ushirika cha mkoa CORECU kuwa na madeni makubwa ambapo mabenki yamekataa kukikopesha fedha kwa ajili ya ununuzi wa zao la korosho.
Aliyasema hayo wilayani Mkuranga wakati wa mkutano wa mfuko wa wakfu wa kuendeleza zao la korosho (CIDTF) kwa wakulima  na wataalamu wa mkoa wa Pwani na bodi ya zao la korosho nchini juu ya msimu mpya wa uuuzaji na ununuzi wa zao hilo.
Mahiza alisema kuwa baadhi ya viongozi wa vyama vya ushirika vya zao la korosho mkoani humo wamewadhulumu wakulima malipo ya korosho walizo wauzia wanunuzi hali iliyosababisha hasara kubwa kwa mkoa.
“Mfano mkoa wa Pwani ulikidhamini chama kikukuu cha ushirika cha mkoa (CORECU) kupata mikopo toka kwenye mabenki ambapo CRDB ilitoa bilioni 6 na NMB ilitoa biloni 3 lakini fedha hizo zimeshindwa kurejeshwa hali ilioyosababisha chama hicho kishindwe kukopeshwa tena,” alisema Mahiza.
Alisema kuwa kila wanapojaribu kuwachukulia hatua viongozi hao inashindikana kutokana na sheria zilizopo za ushirika ambazo zinaonekana zinawalinda viongozi hao hivyo kushindwa kuadhibiwa huku wakulima wakiendelea kudai fedha zao.
“Ukiwashitaki kwa makosa ya jinai ushirika unasema huwezi kuwashitaki kwa kosa la jinai lakini baada ya kufuata taratibu za kisheria tayari tunaweza kuchukua hatua ambazo ni stahiki kwa viongozi hao ambao baadhi yao wamezitumia fedha hizo kwa manufaa binafsi,” alisema Mahiza.
Aidha alisema kuwa sheria hizo si nzuri kwani zinawaumiza wakulima lakini kwa sasa mkoa umefikia hatua nzuri za kuweza kuwashtaki waliohusika na kula fedha za wakulima kwani ushirika sio kudhulumu watu bali ni kuboresha maslahi ya wakulima.
Kwa upande wake mwenyekiti wa mfuko wa kuendeleza zao la korosho Athuman Nkinde alisema kuwa maandalizi ya msimu wa kilimo kwa zao hilo tayari zimeanza na mkoa wa Pwani utapatiwa pembejeo za dawa za kupulizia pamoja na miche bora ya zao hilo ipatayo 70,000.
Nkinde alisema kuwa matarajio ni mkoa huo kuzalisha zao hilo kwa wingi ili kuboresha kipato cha wakulima kwani zao hilo ni utajiri endapo wakulima na wataalamu watawaelekeza kilimo bora cha zao hilo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MWENYEKITI wa Umoja wa Vijana (UVCCM) Taifa Sadifa Juma ameomba suala la umri wa kugombea Uspika na Urais liangaliwe ili kuwapa nafasi vijana kuweza kugombea nafasi hizo kwa kupunguza umri wa sasa wa miaka 40 na kuwa 30.
Aliyasema hayo wakati wa akiwahutubia vijana wa umoja huo kutoka Jimbo la Kibaha Mjini, alipokuwa akifunga kambi ya mafunzo ya vijana ya siku 10 ambayo yalifunguliwa na katibu mkuu wa Abdulrahman Kinana Septemba 19.
Sadifa alisema kuwa kwenye Ubunge unaruhusu umri wa kuanzia miaka 21 lakini kwenye nafasi hizo umri ni kuanzia miaka 40 jambo ambalo ameona kuwa vijana hawatendewi haki.
“Kama ubunge ni miaka 21 na Uspika pamoja na Urais angalau iwe kuanzia miaka 30 na kuendelea kwani kwa umri huo bado kijana ana nguvu na anaweza kutekeleza vema majukumu yake tofuati na kumchagua Rais mwenye umri mkubwa,” alisema Sadifa.
Alisema kuwa mambo yanabadilika ifike wakati sasa vijana nao wapate nafasi kutokana na uwezo wake kwani vijana ndiyo wenye nguvu na wanauwezo mkubwa wa kutekeleza majuku yao ikiwa ni pamoja na kuongoza.
“Nchi kama Kongo na Korea Marais wao ni vijana lakini wanaongoza vizuri hivyo hakuna sababu ya kuwawekea mazingira magumu ya kugombea nafasi hizo za juu wapewe nafasi kama watafanikiwa kuchaguliwa basi wachaguliwe kwani kiongozi siyo umri bali ni uwezo wa kuongoza,” alisema Sadifa.
Kw upande wake kamanda wa Vijana wa Kibaha Mjini Silvestry Koka alitoa sare 50 kwa makamanda wa umoja huo Green (Guard) zenye thamani ya shilingi milioni 2.5 na kuwataka vijana hao kuyatumia mafunzo hayo kukiimarisha chama.
 Awali akisoma risala ya kambi hiyo ya vijana katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM Kibaha Mjini Khalid King alisema kuwa kambi hiyo iliwafundisha vijana 101 juu ya masuala mbalimbali yakiwemo ya itikadi za chama, ujasiriamali, uongozi na masuala mbalimbali ya kisiasa.
Mwisho.



WATOTO WANUNUA SIMU KUWASILIANA NA WAPENZI WAO

Na John Gagarini, Kibaha
IMEBAINIKA kuwa baadhi ya watoto wanaojishughulisha na biashara ndogondogo wilayani Kibaha mkoani Pwani wamejiingiza kwenye mahusiano ya kimapenzi ambapo fedha wanazopata wananunulia simu za mkononi ili kuwasiliana na wapenzi wao.
Watoto hao licha ya kuwa na umri mdogo lakini tayari wanajiingiza kwenye masuala ya mapenzi jambo ambalo ni hatari na linalosababisha kuingia kwenye ngono wakiwa na umri mdogo hivyo kuongeza vitendo vya ubakajiani ndani ya jamii.
Akizungumza mjini Kibaha wakati wa mafunzo ya kupinga vitendo vya ukatili kwa watoto kwa timu za kuzuia vitendo hivyo ndani ya jamii kwenye kata ya Kibaha wilayani humo mwenyekiti wa mafunzo hayo Alkhas Katopola alisema kuwa baadhi ya watoto wanamiliki simu ambazo wanazitumia kwa ajili ya mawasiliano na wapenzi.
“Inashangaza sana kuona watoto wadogo wanamiliki simu za mkononi na kikubwa wanachokifanya na hizo simu ni masuala ya mapenzi hivyo kutokana na umri wao kuwa mdogo ni kama vile wanabakwa kwa sasabu wengi wana mahusiano ya kimapenzi na watu wazima,” alisema Katopolo.
Katopola alisema kuwa wengi wa watoto hao ni wale ambao hawakupata nafasi ya kwenda au kuacha shule kutokana na sababu mbalimbali za kimaisha au wenyewe kukataa kuendelea na masomo.
“Pia baadhi ya watoto hawa wanategemewa na familia zao kwa ajili ya mahitaji ya nyumbani hivyo wazazi au walezi wanashindwa kuwadhibiti mara wafanyapo vitendo visivyofaa ikiwa ni pamoja na kujihusisha kwenye masuala ya mahusiano ya kimapenzi,” alisema Katopola.
Kwa upande wake mratibu wa shirika lisilo la kiserikali la (KICODET) la Kibaha lililoandaa mafunzo hayo Dk Rose Mkonyi alisema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kukabiliana na vitendo vya ukatili kwa watoto kwenye Halmashauri ya Mji wa Kibaha.
“Vitendo vya ukatili kwa watoto ni vingi na ndiyo sababu ya kuandaa mafunzo hayo ili jamii iweze kujua namna ya kutoa taarifa kwenye vyombo vya sheria na si kuvifumbia macho kama baadhi ya familia zinavyofanya kwani baadhi ya wanaofanya vitendo vya ukatili ni ndugu hivyo kuhofia mahusiano kuvunjika,” alisema Dk Mkonyi.
Dk Mkonyi alisema kuwa mafunzo hayo ambayo yatatumika kuunda timu za ufuatiliaji wa matukio mbalimbali ya ukatili kwa watoto yamewajengea uwezo wa kuweza kuwa na mtandao baina yao na vyombo vya sheria kama vile viongozi wa mitaa, waalimu, jeshi la polisi, mahakimu na wadau wengine wanaohusika kukabiliana na vitendo hivyo.
Kwa upande wake mwezeshaji wa mafunzo hayo Faustina Kayombo ambaye ni ofisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha alisema kuwa tatizo kubwa ni usiri unaofanywa na umaskini imekuwa ni vyanzo chanzo vikuu vya kuendela kwa vitendo hivyo.
Mradi huo ni wa miaka miwili ambapo mafunzo hayo yamefadhiliwa na Plan International, UNICEF, Save the Children na Jumuiya ya Ulaya na serikali kwa kushirikiana na shirika hilo la KICODET.
Mwisho.

  


MABANDA UMIZA YAONGEZA VITENDO VYA UBAKAJI

Na John Gagarini, Kibaha
BAADHI ya wadau wa watoto wilayani Kibaha mkoani Pwani wameiomba serikali kuyafutia usajili mabanda ya video ambayo yamekuwa chanzo kikuu cha watoto wadogo kufanyiwa vitendo vya ubakaji.
Mabanda hayo yamekuwa yakitumiwa na baadhi ya watu wazima ambao wanawafanyia watoto hao vitendo hivyo baada ya kuwarubuni kuwaingiza kwenye mabanda hayo kisha kuwapakata na kuwaingilia watoto hao ikiwa ni pamoja na kinyume cha maumbile.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mratibu wa shirika lisilo la kiserikali la (KICODET) Dk Rose Mkonyi wakati wa mafunzo ya kupinga vitendo vya ukatili kwa watoto kwa wadau mbalimbali kwenye kata ya Kibaha wilayani humo  alisema moja ya vyanzo vya ongezeko la vitendo vya ubakaji watoto ni mabanda hayo.
“Vitendo vya ubakaji watoto ambapo ni moja ya ukatili vimekithiri na kuongezeka wilayani Kibaha na moja ya sababu ni mabanda hayo ambayo yanaonyesha video chafu za ngono bila ya kujali umri,” alisema Dk Mkonyi.
Dk Mkonyi alisema kuwa mabanda hayo yamejaa kwenye mitaa na vijiji hayajali umri licha ya sheria kutaka watoto wenye umri chini ya miaka 18 kutoingia lakini wamiliki wamekuwa wakiwaruhusu watoto hao ambao ni wanafunzi kuingia pia kufunguliwa muda wa kazi ambapo wanafunzi hao wamekuwa wakiishia humo na kuacha kwenda shule.
Kwa upande wake mwezeshaji wa mafunzo hayo Faustina Kayombo ambaye ni ofisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha alisema kuwa tatizo kubwa ni usiri unaofanywa na umaskini imekuwa ni chanzo kikuu cha kuendela kwa vitendo hivyo.
Naye mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ambaye ni mwenyekiti wa mafunzo hayo Alkhas Katopola alisema kuwa mafunzo hayo yamtawafanya waweze kujua namna ya kukabilina na vitendo hivyo ndani ya jamii ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa kwenye vyombo vya sheria.
Katopolo alisema kuwa baadhi ya matukio hayo yamekuwa yakiendelea kutokana na wanafamilia kuficha kuogopa mahusiano mabaya au kurubunia kwa kupewa fedha ili wasitoe taarifa za vitendo hivyo.
Mradi huo ni wa miaka miwili ambapo mafunzo hayo yamefadhiliwa na Plan International, UNICEF, Save the Children na Jumuiya ya Ulaya na serikali kwa kushirikiana na shirika hilo la KICODET.
Mwisho.

   



WANAFUNZI KIDATO CHA SITA WAZAWADIWA FEDHA


Na John Gagarini, Kibaha
SHIRIKA lisilo la Kiserikali la Piniel Medical Mission la Jijini Dar es Salaam limewapa fedha wanafunzi wanne wa shule ya sekondari Kilangalanga ambao wamefaulu daraja la kwanza kwenye mtihani wa Taifa wa kidato cha sita.
Waliozawadiwa fedha hizo ni pamoja na Peter Didas, Ally Makutubu, Obote Juma na Venance Peter ambao kila mmoja alikabidhiwa kiasi cha shilingi 100,000 kila mmoja.
Akiwakabidhi fedha hizo mgeni rasmi kwenye makabidhiano hayo ambayo yalifanyika shuleni hapo Mlandizi Kibaha mwakilishi wa ofisa elimu wilaya ya Kibaha Blandina Mwenura aliwapongeza wanafunzi hao na kuwataka wanafunzi watakaofanya mitihani hiyo kutoogopa masomo ya sayansi.
Mwenura alisema kuwa wanafunzi wengi wamekuwa wakifanya vibaya kutokana na kuyaogopa masomo hayo ambayo ndiyo masomo muhimu katika kupata wataalamu mbalimbali.
“Nalipongeza shirika hili kwa kujitolea kuhamasisha masomo haya ambayo wanafunzi wamekuwa wakiyakimbia na kukimbilia masomo ya Sanaa wakidhani kuwa ndiyo rahisi,” alisema Mwenura.
Aidha aliwataka wadau wengine kujitokeza zaidi kuwatia moyo wanafunzi wanaosoma masomo hayo ili kujenga nchi yenye wataalamu wenye uwezo mzuri kwani watafanya kazi kwa mapenzi kwa kile walichokisomea.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa shirika hilo Jaqline Ngoma alisema kuwa walitoa ahadi kwa wanafunzi wa shule hiyo kuwa endapo mwanafunzi wa kidato cha sita atapata daraja la kwanza watampatia kiasi hicho cha fedha na huo ndiyo utekelezaji wa ahadi hiyo.
“Lengo letu ni kuwatia moyo wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi wawe na ujasiri na kuondoa woga kwani wataalamu kwa sasa wanapungua mfano wataalamu wa afya hivyo lazima tutumie njia ya kuwahamasisha ili wengi wajiunge na masomo hayo,” alisema Ngoma.
Shule hiyo ya serikali ni ya kutwa ni ya wavulana na wasichana na bweni kwa wanafunzi wa kidato cha tano na sita wavulana wanaochukua masomo ya mchepuo wa Sayansi.
Mwisho.