Sunday, March 10, 2013

STORY ZA PWANI



Na John Gagarini
 MKUU wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza amesema kuwa serikali haitakaa kimya kuona baadhi ya kinamama wakifanya vitendo vya kinyama ikiwa ni pamoja na kutupa watoto wanaowazaa.
Mahiza aliyasema hayo wakati wa hafla fupi ya kusherehekea siku ya Wanawake Duniani kwenye Halmashauri ya Mji wa Kibaha na kusema kuwa baadhi wanawake wamekuwa wakiwafanyia ukatili hata watoto wao wa kuwazaa.
Alisema kuwa moja ya ukatili ambao umekithiri mkoani Pwani ni kuwatupa watoto jambo ambalo limekuwa likishika kasi siku hadi siku kwenye mkoa huo.
“Serikali haitaweza kuvumilia kuona baadhi ya akinamama wakitenda vitendo vya ukatili kwa watoto wao kwani nao wana haki ya kulelewa na wana haki ya kupata matunzo pamoja na kuishi hivyo ni vema kila mtu akatimiza wajibu wake kwani hiyo ni haki ya msingi ya mtoto,” alisema Mahiza.
Mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa haipendezi kuona wanawake wanakuwa mstari wa mbele kufanya vitendo vya ukatili kwa watoto wao.
“Kama unaona bado hujajianda kulea kwanini uzae kama wewe ungefanyiwa hivyo sasa hivi ungekuwa wapi na mtu wa aina gani ni lazima mjilinde na kuachana na vietendo hivyo kwani ni ukatili ambao hutaweza kuvumiliwa na serikali na hatua kali zitachukuliwa kwa wanaofanya vitendo hivyo,” alisema Mahiza.
Aidha alisema vitendo hivyo ni vibaya kwani mbali ya kuwaua watoto pia ni kuwafanya wawe watoto wa mitaani na kuathirika kisaikolojia  na kuwajengea mazingira mabaya ya kuishi.
Kwa upande wake mke wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Selina Koka alisema kuwa aliamua kuwakusanya wanawake kwa pamoja ili kubadilishana mawazo na kutafakari siku hiyo katika kutimiza majukumu yao kama mama.
Koka alisema kuwa siku hiyo ina maana kubwa kwa akinamama katika kuihudumia jamii na Taifa ambalo linawategemea katika kujenga uchumi wa nchi.
Mwisho.
WAANDISHI wa Habari wa Kanda ya Mashariki wametakiwa kutoa elimu ya kutosha kwa Jamii inayowazunguka ili kuondokana na dhana juu ya chanjo mbalimbali zinazotolewa na serikali kwa watoto kuwakinga na magonjwa yanayosababisha vifo.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na kaimu katibu Tawala mkoa wa Pwani Injinia Michael Mrema wakati akifungua mafunzo ya siku moja juu ya chanjo mpya ya magonjwa ya Nimonia na Uti wa Mgongo ya Rotavirus kwa waandishi wa Kanda ya Mashariki.
Injinia mrema alisema kuwa jamii imekuwa na dhana mbaya kuwa baadhi ya chanjo zina athari kwa watoto hivyo kushindwa kuwapeleka kupata chanjo.
“Waandishi ni watu wanaoaminiwa na jamii hivyo kwa kutumia kalamu zenu mnaweza kutoa elimu juu ya umuhimu wa chanjo hizo kwa  watoto wenye umri chini ya miaka mitano ambao wanakufa kutokana na maambukizi ya magonjwa mbalimbali,” alisema Injinia Mrema.
Alisema kuwa magonjwa kama hayo husababisha vifo kwa asilimia 80 hivyo lazima itumike nguvu ya ziada ya kutoa elimu ili jamii ione umuhimu wa kuwapeleka watoto wao kupata chanjo kwa lengo la kupunguza vifo hivyo visivyo vya lazima.
“Chanjo hii mpya inatoa kinga kwa asilimia 87 hadi 88 ambapo nchi imejitahidi sana kwani imeweza kupunguza vifo toka 99 hadi 51 kwa watoto 1,000 kwa mwaka 2010,” alisema Injinia Mrema.
Aidha alisema kuwa chanjo hiyo ni salama na haina madhara yoyote na endapo jamii itapata taarifa sahihi hawataweza kupotoshwa na watawapeleka watoto wao kupata chanjo hiyo ambayo ni bure na haina gharama zozote.
Kwa upande wake ofisa habari idara ya habari maelezo Veronica Kazimoto alisema kuwa mafunzo hayo kwa waandishi wa habari yatasaidia kufikisha ujumbe sahihi na haraka kwa walengwa hivyo wanaamini kuwa waandishi ni njia sahihi ya kutoa elimu. Mafunzo hayo ya siku moja waliwahusisha waandishi toka mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Morogoro.
Mwisho.
WAKAZI wa Mji wa Kibaha waliojenga vibanda na nyumba kwenye maeneo ya barabara wametakiwa kuvunja mara moja kabla serikali haijavunja ili kupisha matengenezo ya barabara za kuingia kwenye mitaa ya mji huo.
Hayo yalisema na Injinia wa Halmashauri ya Mji huo Ezekiel Kunyaranyara alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari na kusema kuwa tayari watendaji kwenye mitaa hiyo walishapewa barua ya kuwajulisha walengwa.
Kunyaranyara alisema kuwa baadhi ya watu wamejenga vibanda vya biashara na nyumba kwenye eneo la barabara za mitaani na kufanya barabara hizo kushindwa kupitika hasa pale yanapotokea madhara mbalimbali yakiwemo ya moto.
“Athari za watu kujenga kwenye maeneo zinakopita barabara ni nyingi lakini mojawapo ni magari kushindwa kupita hata pale kunapotokea mfano mgonjwa anatakiwa kuchukuliwa na gari na kupelekwa hospitali au moto unapotokea gari la zimamoto linashindwa kupita hivyo kuleta athari kubwa,” alisema Kunyaranyara.
Alisema walitoa maelekezo kwa watendaji wa mitaa yote kwenye maeneo husika na walitoa miezi sita tangu mwaka jana hadi Machi mwaka huu ambapo endapo hawatafanya hivyo wakati wowote watatekeleza kazi hiyo.
“Katika awamu hii tulitenga kiasi cha shilingi milioni 9 kwa ajili ya kuchonga barabara zote za Mji wa Kibaha kwani lengo ni kuhakikisha mji unakuwa na barabara ambazo zinapitika kwa mkipindi chote cha mwaka,” alisema Injinia Kunyaranyara. 
Alisema kuwa hivi karibuni halmashauri ilinunua greda lake hivyo kuanza kukarabati barabara zote kwenye kata zote za halmashauri hiyo 11 zenye mitaa 53.
KUFUATIA kilio cha mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza kuiomba ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuisaidia kupata fedha kiasi cha shilingi miloni 160 kwa ajili ya kukarabati mochwari ya Hospitali ya Rufaa ya Tumbi hatimaye kilio hicho kimesikika ambapo ofisi hiyo imeahidi kutoa fedha hizo.
Akizungumza juzi mara baada ya kutembelea Shirika la Elimu Kibaha (KEC) lililopo wilayani Kibaha mbele ya viongozi wa shirika hilo ambalo linamiliki hospitali hiyo, Kaimu katibu mkuu TAMISEMI Alafayo Kidata alisema watatoa fedha hizo ili kufanya ukarabati wa chumba hicho.
Kidata alisema kuwa chumba hicho ni muhimu hivyo Wizara imeona kuna umuhimu wa kutoa fedha hizo ili kufanya ukarabati kwani haipendezi kuona chumba hicho kikiwa kwenye hali mbaya ambapo marehemu wanahifadhiwa humo.
“CHumba cha maiti ni muhimu sana na kila mtu atapitia hapo hivyo kiubinadamu lazima mazingirra yake lazima yawe mazuri kutokana na maombi toka kwa viongozi wa shirika tumeona mahali hapa panahitaji kuangaliwa mapema huku sehemu nyingine zikifanyiwa kazi,” alisema Kidata.
Aidha alisema kuwa kutokana na umuhimu wa hospitali hiyo kupokea majeruhi wengi wa ajali pamoja na maiti zinazopokelewa hapo ni vema ukarabati ukafanyika ili kuondoa hali mbaya iliyopo.
“Tunatarajia mwishoni mwa mwezi huu fedha zitatolewa ili kuboresha chumba hicho ambacho kwa sasa ni kidogo na kinapokea marehemu wengi,” alisema Kidata.
Alibainisha kuwa madeni mbalimbali ambayo yanafikia kiasic ha shilingi bilioni moja watahakikisha yanalipwa hadi ili huduma ziendelee kutolewa kwani kuna hatari ya baadhi ya watoa huduma kusitisha.
Awali akitoa taarifa ya shirika kwa kaimu katibu mkuu, mkurugenzi wa KEC Dkt Cyprian Mpemba alisema kuwa chumba cha maiti kwa sasa kinahifadhi miili miwili miwili kutokana na udogo wake jambo ambalo si zuri.
Dkt Mpemba alisema kuwa chumba hicho hakijafanyiwa matengenezo tangu hospitali hiyo ilipoanzishwa miaka ya 70 na wafadhili wa nchi za Nordic, pia linakabiliwa na madeni makubwa yanayofikia zaidi ya bilioni moja.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment