Thursday, March 7, 2013

RC AOMBA MSAADA CHUMBA MAITI

Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahizaameiomba ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) kuipatia hospitali ya wilaya ya Tumbi kiasi cha shilingi milioni 160 kwa ajili ya kukarabati chumba cha kuhifadhia maiti ambacho kiko kwenye hali mbaya.
Aliyasema hayo hivi karibuni wakati wa ziara ya siku moja ya Waziri wa TAMISEMI Hawa Ghasia alipotembelea Shirika la Elimu Kibaha (KEC) ambalo linamiliki hospitali hiyo ambalo liko chini ya Wizara hiyo.
Mahiza alisema kuwa chumba hicho kiko kwenye hali mbaya kwani kimekuwa ni kidogo na kimechakaa na hakijafanyiwa ukarabati tangu kuanzishwa miaka ya 70.
“Waziri tunaomba utusaidie kuweza kupata fedha hizo kwani licha ya kuwa na madeni makubwa na mahitaji ya fedha, kikubwa ni chumba hichi ambacho kinahitaji kufanyiwa ukarabati kwani kiko kwenye hali mbaya na kinahitaji msaada wa haraka,” alisema Mahiza.
Alisema maiti zinahitaji kuhifadhiwa katika mazingira mazuru ili kuzienzi lakini kwa hospitali yetu hali si nzuri kwani tutakuwa hatuzitendei haki kwa kuzitunza kwenye mazingira mabaya.
Kwa upande wake mganga mkuu wa hospitali Peter Datan alisema kuwa tatizo la chumba hicho ni kubwa kwani kwa sasa maiti zinakaa mbili mbili ambapo kwa utaratibu wanapaswa kukaa mwili mmoja kutokana na udogo wake.
“Kwa sasa chumba kimekuwa ni kidogo kwani maiti zimeongezeka tofauti na zamani ambapo zilikuwa chache kwani kwa sasa maiti zinazohifadhiwa ni 20, pia maiti nyingine zinakaa muda mrefu hasa zile ambazo zinakuwa zimeokotwa,” alisema Dkt Datan.
Dkt Datan alisema kuwa chumba hicho kinapata mzigo mkubwa wa maiti kutokana na baadhi ya maeneo ya mikoa kama vile Dar es Salaam, Morogoro na Tanga kuletwa TUmbi.
Naye Mkurugenzi wa KEC Dkt Cyprian Mpemba alisema kuwa wanakabiliwa na madeni makubwa ambayo kwa sasa yanafikia zaidi ya bilioni moja hali ambayo ni madai ya wafanyakazi na wazabuni ambao wanatoa huduma kwao.
Kwa upande wake waziri Ghasia alisema kuwa atayafanyia kazi maombi hayo kwa kupeleka ombi maalumu hazina ili kuweza kutatua chanagamoto zilizopo kwenye shirika hilo la Umma ambalo lilianzishwa miaka ya 70 na nchi za Nordic kwa ushirikiano na serikali.
Mwisho.  

No comments:

Post a Comment