Saturday, March 30, 2013

DC ATAKA WLAIMU WAKAMATWE

Na John Gagarini, Bagamoyo
MWALIMU wa shule ya Msingi Msoga wilayani Bagamoyo mkoani Pwani anatuhumiwa kuwajaza mimba wanafunzi wa shule ya msingi na mwingine wa sekondari Msoga huku mwingne akifumaniwa na mwanafunzi.
Tuhuma hizo zilibainika wakati wa kikao cha pamoja kati ya wazee maarufu viongozi wa dini, wajumbe wa serikali ya Kijiji na watendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Bagamoyo na mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Ahmed Kipozi.
Mwalimu huyo alibainishwa kwenye kikao hicho ni Joel Mjema ambapo mwalimu mwingine ni Samwel Mjema yeye anatuhumiwa kufumaniwa na mwanafunzi wa sekondari ya Msoga lakini wazazi wa mwanafunzi huyo walilimaliza suala hilo kimya kimya.
Kutokana na tuhuma hizo ambazo zinawakabili walimu hao mkuu wa wilaya hiyo Kipozi alitaka walimu hao wakamatwe na kupelekwa kwenye vyombo vya kisheria ili hatua ziweze kuchukuliwa kutokana na matukio hayo.
Akizungumzia tuhuma za walimu hao Kipozi  alisema kuwa mwalimu Joel Mjema ana tuhuma za kumjaza mimba aliyekuwa mwanafunzi wa darasa la sita katika shule hiyo jina tunalo (Tatu Shaabani) hali iliyopelekea mwanafunzi huyo kushindwa kuendelea na masomo yake ya kuhitimu elimu ya msingi.
“Lakini kwa kuona hiyo haitoshi mwalimu huyo huyo akamjaza mimba na kupelekea kumkatisha  masomo mwanafunzi mwingine wa kidato cha tatu wa shule ya sekondari Lugoba na Latifa Shaaban,na kuamua kuishi naye kinyumba kitu ambacho ni kibaya sana kwa mwalimu aliyekabidhiwa dhima ya kulea watoto kimaadili,” alisema Kipozi.
Kuhusiana na mwalimu Samwel Mjema  alisema mwalimu huyo anatuhumiwa kutembea na mwanafunzi (Maimuna Hamis) ambapo alifumaniwa na wazazi wa binti huyo na kitu cha kushangaza suala hio lilimalizwa kimya kimya baina ya mwalimu huyo na wazazi na binti hali aliyosema haikubaliki  na kuagiza mara moja kuchukuliwa hatua kwa wazazi wote ambao wamekuwa wakifikia makubaliano ya kuvunja sheria.
Kipozi alisema kuwa walimu hao kwa nyakati tofauti wamekuwa wakikiuka maadili na kanuni za utumishi kwa kufanya ngono na wanafunzi wao kitu ambacho ni kinyume na kanuni na taratibu za utumishi na sheria za nchi.
“Kwa ujumla hatuwezi kuvumilia uchafu huu wa mtu anayepaswa kuheshimiwa kama mwalimu kuamua kuanza kuwashawishi na kufanya ngono na wanafunzi wake lakini mbaya zaidi ni kuwakatishia masomo watoto hao hivyo naagiza mara moja kukamatwa kwa walimu hao na kufikishwa katika mikono ya sheria,” alisema Kipozi.
Hata hivyo taarifa zilizotufikia zinasema kuwa mwalimu Samwel Mjema alikamatwa kuhusiana na tukio lake na kutarajiwa kufikishwa mahakamani huku mwalimu Joel Mjema akitoroka kuhusiana na tuhuma hizo zinazomkabili.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment