Sunday, August 4, 2024

YPC YAWATAKA VIJANA KUJITOKEZA KUWANIA NAFASI ZA UONGOZI

VIJANA wa kike na kiume wametakiwa kujitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu na uchaguzi mkuu wa mwakani.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa asasi isiyokuwa ya kiserikali ya Ushirikiano wa Maendeleo ya Vijana (YPC) ya Kibaha Israel Ilunde alipokuwa akizungumza na Habarileo ofisini kwake.

Ilunde alisema kuwa wameanzisha mradi uitwao (K-Vote) unaohamasisha ushiriki wa vijana kwenye masuala ya umma, elimu ya mpiga kura, uraia, kuwasaidia na kuwaelimisha vijana wanaotaka kuwania nafasi za uongozi kwenye chaguzi hizo.

"Tume Huru ya Uchaguzi inatarajia kuandikisha wapiga kura wapya vijana milioni tano na wale ambao hawakuwahi kupiga kura miaka ya nyuma tunawasihi wajitikeze kuhakiki taarifa zao itakapofika muda wa kufanya hivyo ili waweze kushiriki kwenye uchaguzi,"alisema Ilunde.

Alisema vijana wanapaswa kushiriki zoezi hilo ambalo ni muhimu sana kwani wasipojiandikisha au kuboresha taarifa zao watakuwa watazamaji na hawataruhusiwa kupiga kura.

"Idadi ya vijana kuwania nafasi mbalimbali za uongozi serikali za mitaa mwaka 2004 na uchaguzi mkuu mwaka 2005 ilikuwa ni asilimia 8 tu na mwaka 2015 iliongezeka na kufikia asilimia 50 na mwaka huu na mwakani itaongezeka,"alisema Ilunde.

Aidha alisema kuwa baadhi ya vijana hao walichaguliwa kwenye nafasi za uongozi ikiwa ni pamoja na ubunge, udiwani, wenyeviti na wajumbe wa serikali za mitaa.

"Tuna mfano wa Dk Zainab Katimba ni Naibu Waziri na mbunge Salome Makamba walifanya vizuri na pia kuachana na dhana kuwa uchaguzi mtaji ni fedha bali ni watu, nidhamu, uchapakazi, kujali watu,"alisema Ilunde.

Aliwataka vijana kutonunua kura kwani zinavunja heshima na zinaaibisha Taifa na uongozi unakuwa wa kulipa madeni pia wafanye siasa za heshima bali ziwe za hoja na kuweka utu mbele na kutofanya vurugu wanaposhindwa na waijali jamii.


Thursday, August 1, 2024

DK BITEKO AMWAKILISHA RAIS MKUTANO MKUU (TLS)

Na Mwandishi Wetu, Dodoma 

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko leo Agosti 1, 2024 amemwakilisha Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Miaka 70 wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) unaofanyika Ukumbi wa Jakaya Kikwete, Jijini Dodoma. 

Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Pindi Chana, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dkt. Eliezer Feleshi, pamoja na Wanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika. 

Itakumbukwa kuwa TLS ilianzishwa mnamo mwaka 1954 ikiwa na mawakili takribani 141 wakiwa ni wakoloni hadi ilipofika mnamo Oktoba 31,1961 ilipopata wakili wa kwanza Mtanganyika.

Hadi sasa TLS ina jumla ya mawakili takribani 12,471 wanaofanya kazi za usaidizi wa kisheria katika taasisi mbalimbali za kisheria nchini.

MH.RAIS DKT. SAMIA SULUHU HASSAN AZINDUA TRENI YA KISASA (SGR)



Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan azindua Rasmi Huduma za Usafiri wa Treni ya Kisasa (SGR) kutoka Dar es Salaam – Morogoro hadi Dodoma, katika eneo la Stesheni Jijini Dar es Salaam, leo 1 Agosti, 2024.

WAZIRI MKUU AFUNGUA MAONESHO YA WAKULIMA NANE NANE

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa leo Agosti 01, 2024 afungua maonesho ya Kimataifa ya Wakulima ya Nanenane ambayo kitaifa yanafanyika  kwenye viwanja vya Nanenane Nzuguni Jijini Dodoma,

Kauli mbiu ya Maonesho hayo ni Chagua Viongozi Bora wa Serikali za Mitaa kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Saturday, July 27, 2024

RIZIWANI KIKWETE NDANI YA BARAZA LA MADIWANI UCHAGUZI MAKAMU MWENYEKITI HALMASHAURI YA CHALINZE

Nimeshiriki kikao cha Baraza la Madiwani Cha Chama Cha Mapinduzi kuchagua diwani atakayegombea nafasi ya Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Chalinze kilichofanyika Chalinze ,mapema leo.#KaziInaendelea

TAKUKURU DODOMA YATOA ELIMU KUELEKEA UCHAGUZI WA MITAA MWAKA HUU

Na Wellu Mtaki, Dodoma

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoani Dodoma imeendelea kutoa elimu kwa Umma kupitia makundi mbalimbali kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa nchini unaotarajia kufanyika mwaka huu.

Naibu Mkuu wa TAKUKURU Mkoani Dodoma Euginius Hazinamwisho amesema kuwa viongozi wa Kisiasa nchini Tanzania hupatikana kupitia uchaguzi unaofanyika kila baada ya miaka mitano kwa namna mbili uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani na uchaguzi wa viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa.

"Mwaka 2024 utafanyika uchaguzi wa Serikali za Mitaa na mwaka 2025 utafanyika uchaguzi wa Serikali kuu,"amesema.

Aidha amesema kuwa kuwepo kwa vitendo vya Rushwa wakati wa kuchagua viongozi huwanyima haki wagombea na kuwakosesha maendeleo wananchi 

"Jitihada za Serikali kuhakikisha uchaguzi unakuwa huru na wa haki kwa wananchi wameweza kutunga Sheria mbalimbali zinazodhibiti vitendo vya Rushwa,"amesema 

"TAKUKURU kwa kuzingatia kifungu cha 4 kifungu kidogo cha 2 na kifungu cha 7(d) vya Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa vina wajibu wa kuwahakikishia wadau kuweka mikakati dhidi ya Rushwa wakati wa uchaguzi.

Hata hivyo amesema kuwa katika utekelezaji wa majukumu yake TAKUKURU mwaka 2014 na mwaka 2019 ilifanya uchambuzi wa ufuatiliaji wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa na mwaka 2020 ilifanya uchambuzi wa mfumo kwa uendeshaji wa uchaguzii mkuu wa Serikali wa Rais, Wabunge na Madiwani katika majimbo yote ya Uchaguzi Tanzania bara.

"Katika chaguzi zote yalikuwepo malalamiko ya vitendo vya Rushwa,katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa Mwaka 2014/2019 vitendo vya Rushwa vilijitokeza kama ifuatavyo kulikuwa na ugawaji wa fedha, ugawaji wa vitu, kama kanga,fulana,vinywaji na vyakula na ahadi za ajira,"amesema

Kwa upande wake Kamishna Msaidizi wa Mamlaka ya kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) Mzee Kasuwi amesema kuwa athari za biashara ya Dawa za Kulevya kwenye uchaguzi wa Kisiasa zinaweza kuwa na madhara makubwa na kuathiri mchakato wa Kidemokrasia na utulivu wa jamii.

Aidha biashara na matumizi ya Dawa za Kulevya ni tatizo linaloathiri nchi nyingi dunia.

"Dawa za Kulevya zina athari Kiuchumi,kiafya, kijamii, Kisiasa, kidiplomasia, Kimazingira na usalama,"amesema

PWANI YAPATIWA WAUGUZI 120




MKOA wa Pwani umepatiwa jumla ya Wauguzi 120 ikiwa ni asilimia 50 ya watumishi walioletwa mkoani humo pia umepatiwa kiasi cha shilingi bilioni 25 kuboresha huduma za afya.

Hayo yamesemwa mjini Kibaha na Katibu Tawala Mipango na Uratibu wa Mkoa wa Pwani Edina Kataraiya ambaye alimwakilisha Naibu Waziri wa Afya Dk Godwin Mollel wakati wa Maadhimisho siku ya Uuguzi Duniani kwa Mkoa wa Pwani.

Kataraiya amesema kuwa serikali imeendelea kutatua changamoto mbalimbali za huduma za afya ikiwa ni pamoja na kuongeza wahudumu wa afya ili kuboresha utoaji huduma.

"Kada ya uuguzi ni uti wa mgongo wa huduma za afya ndiyo sababu serikali inaboresha kwani bila ya wauguzi hakuna huduma hizo hivyo toeni huduma kama kiapo chenu kinavyosema upendo, utu na uadilifu,"amesema Kataraiya.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wauguzi Tanzania (TANNA) Steven Brown amesema kuwa katika Muundo wa Utumishi wa Kada ya Uuguzi na Ukunga ambacho kinamtaka Ofisa Muuguzi kabla hajafikia Kiwango cha mwisho cha Mshahara wake yaani (TGHSG) awe na Masters ambacho ni kikwazo kwa wauguzi.

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani Kusirye Ukio amesema kuwa huduma wanayotoa wauguzi ni ibada na Hospitali ni madhabahu hivyo waendelee kudumisha ibada zao.