Wednesday, March 27, 2024

WANAFUNZI WAASWA KUZINGATIA NIDHAMU


Juma la wadau wa Elimu Mkoa wa Dodoma limehitimishwa kwa viongozi mbalimbali  wa Mkoa wa Dodoma kuzungumza na kushiriki chakula cha mchana na wanafunzi wa Shule za kidato cha sita za Mkoa huo.

Kwa nyakati tofauti akiwa katika shule ya Sekondari ya wavulana Kongwa na Shule ya wasichana Kibaigwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule amewaasa wanafunzi hao kuendelea kudumisha nidhamu hususani katika kipindi hiki wanachojiandaa na mitihani yao na kuachana na marafiki wasiofaa ambao watawasababishia matokeo yatakayogharimu maisha ya ndoto zao.

"Tunataka alama A zenye hapa kuna wenzenu wamechafua jina la Shule na nyie mliopo hapa tunategemea nyie mtabadilisha sura hii ambayo sio njema kwa Mkoa, acheni tabia ya kufuata mkumbo kwa kushawishiana mambo yasiyofaa kwasababu kila mtu ana ndoto yake na kila moja atarudi nyumbani kwao kivyake na usipokuwa makini utaharibu maisha yako kwa mikono yako mwenyewe kwasababu tuu ya ushawishi usiofaa kutoka kwa marafiki zenu.

"Lazima muamue kuachana na baadhi ya mambo na kufuata miongozo yenu na kufanya bidii ili kujitofautisha na wengine na kuongeza ufaulu wenu na kujenga dhana nzuri ya shule Bora ni lazima muwe na ufaulu bora na Shule hii ambayo nyie ndio waanzilishi itapata sifa nzuri na sisi kama Mkoa tunayo matarajio kutoka kwenu kupitia matokeo mazuri mtakayotuletea," ameasa Senyamule

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka Simon amewataka wanafunzi hao kuendelea  kujitunza vizuri  kwa kujiweka bize na masomo na shughuli za kielimu ili kuepukana na vishawishi mbalimbali vitakavyowafanya kupata ufaulu usiofaa na kujenga picha mbaya ya shule yao.

Kwa upande wake ofisa Elimu Mkoa  Mwl. Vincent Kayombo amesema Mkoa wa Dodoma unaendelea na maandalizi ya kuhakikisha Mkoa unapata matokeo mazuri katika mitihani ya kidato cha sita inayotarajiwa kufanyika kuanzia Mei 6, Mwaka huu.

Aidha Mwl.Kayombo ameweka bayana kuwa Mkoa umefanya maandalizi ya kuhakikisha wanafunzi wa shule zenye kidato cha sita za Mkoa huo wanashiriki chakula cha mchana na viongozi mbalimbali ikiwa ni katika kuwahamasisha, kuwatoa hofu na kuwajengea ujasiri wanafunzi hao katika kuelekea mitihani yao ya kuhitimu ngazi hiyo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka Simon amewataka wanafunzi hao kuendelea  kujitunza vizuri  Kwa kujiweka bize na masomo na shughuli za kielimu ikiwemo michezo ili kuepukana na vishawishi mbalimbali vitakavyowafanya kupata ufaulu usiofaa na kujenga picha mbaya ya shule yao.

KATA YA LUPETA WALILIA MAJI

Wananchi wa Kijiji Cha kata Lupeta wilaya ya Mpwapwa Jijini Dodoma  wameiomba serikali kuwapelekea huduma ya maji ili kukabili changamoto hiyo.

Hayo yamebainishwa tarehe 26 Machi 2024 wakati wa ziara ya Mwenyekiti wa UVCCM wilaya ya Mpwapwa Yohana Malogo kukagua uhai wa Jumuiya, kusajili wanachama wapya
 na kuhimiza ulipaji wa ada.

Walisema kuwa kilio cha maji katika Kata yao imekuwa ni changamoto kiasi cha kushindwa kujua tatizo hilo litaisha lini na serikali inampango gani kwao ili kukabili hali hiyo.

Kwa upande wake Fundi Mkuu wa Maji Geogre Francis Theophil amesema kuwa wapo baadhi ya wananchi wanakata mabomba ya maji usiku bila sababu yoyote kiasi Cha kwamba wanakwamisha swala la maji kupatikana Katika Kijiji hicho.

Theophil amesema kuwa kuna changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na baadhi ya watu kukata mabomba hali inayosababisha maji kumwagika chini.

Naye Diwani ya Kata ya Lupeta Sospeter Moonho amewahakikishia wananchi mradi wa maji tiririka kufika mwezi wa nne utaenda ili kusaidiia kumtua mama ndoo kichwani pamoja na kuwahakikishia wananchi pia wanaenda kuanza ujenzi wa jengo la zahanati.

Moonho amesema kuwa atahakikisha ujenzi wa jengo la zahanati linakamilika na kama hajakamilisha aulizwe.

Kwa upande wake Mwenyekiti umoja wa Vijana wa Chama Cha mapinduzi ( UVCCM) Yohana Malogo amewataka viongozi wa kata hiyo kuhakikisha mifuko iliyokopeshwa irudidishwe na ujenzi uanze na amewaomba kisima kijengwe kwenye kata hiyo.

Malogo amesema kuwa wanaenda kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa wahakikishe wanawasaidia wananchi na kiasi cha fedha kilichopo ujenzi uanze kwani hakuna sababu kuweka fedha wakati wote huku wananchi wakitaabika.

Lengo ya ziara hiyo ya mwenyekiti wa UVCCM ni kukagua uhai wa Jumuiya, kukagua madaftari ya wanachama, kusajili wanachama wapya na ulipaji wa ada, kuhamasisha kufanyika semina kwa viongozi wa kata na Mitaa pamoja na kikao cha ndani na wanachama.

Tuesday, March 26, 2024

SERIKALI KUFUATILIA SUALA LA ELIMU NCHINI

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amewataka Maofisa Elimu Kata nchini kufuatilia maendeleo ya shule kwa kuwatembelea walimu na kusikiliza kero zao

Aidha amewataka walimu kuhakikisha wanafanya tathmini ya uelewa wa wanafunzi kwa kuwapatia mazoezi mengi.

Majaliwa ameyasema hayo Machi 25, 2024   kwenye ukumbi wa TAG Mipango Jijini Dodoma wakati wa kilele cha Juma la wadau wa Elimu Mkoa.

Amesema maofisa elimu hao wafuatilie masuala ya walimu na kutatua changamoto zao ili wafanye kazi vizuri.

"Walimu nanyi hakikisheni mnafanya tathmini ya uelewa wa wanafunzi kwa kuwapatia mazoezi mengi kadri iiwezekanavyo,"amesema Majaliwa.

Fedha zinazotolewa kwa ajili ya maendeleo ya Elimu, zitumike kwa ajili hiyo,"amesisitiza Majaliwa.

Amebainisha kuwa Kauli mbiu ya mkutano huo inakwenda sambamba na Sera ya Elimu ya nchi inayosisitiza Uwajibikaji, Utoaji wa Elimu Bora ni vipaumbele vya nchi. 

"Serikali yetu inaimarisha mazingira ya utoaji Elimu kwa kuboresha miundombinu na Elimu bila ada kwani mpaka Sasa shilingi Trilioni 1 zimetolewa kufanikisha hili,"amesema Majaliwa.

Waziri Mkuu ameipongeza Dodoma kwa kuandaa Mkutano huo kwani unakwenda sambamba na Sera ya Elimu ya nchi.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amesema Serikali ya awamu ya Sita imefanya mambo mengi kwenye sekta ya Elimu.

Senyamule amesema kuwa wanamshukuru Rais kwa kuinua sekta ya Elimu Dodoma kwani wameimarika sana kipindi cha miaka hii mitatu Dodoma imepanda ufaulu wa darasa la saba na kuingia kumi bora kitaifa mwaka 2022 kwa ufaulu kupanda kutoka 83% mwaka 2022 hadi 87%mwaka 2023 na wameanza kuweka mikakati ya Mkoa kuhakikisha kila mwaka ufaulu unaongezeka.

Ametaja mafanikio yaliyopatikana kipindi hiki kuwa ni ujenzi wa miundombinu ya elimu iliyogharimu shilingi bilioni 92.4 , miradi ya BOOST shilingi bilioni 10.6 iliyowezesha ujenzi wa madarasa 196 na matundu ya vyoo 154 fedha nyingine ni kutoka miradi ya SEQUIP, SWASH, TEA , EP4R na mingine mingi ambayo kwa pamoja imeboresha kiwango cha elimu.

Mkutano wa wadau wa Elimu Mkoa wa Dodoma umefuatia matukio kadhaa yaliyofanyika kwa Juma zima ikiwemo kukimbia mchaka mchaka kwa wanafunzi, uzinduzi wa Bonanza la michezo, ugawaji wa mipira 1000 kwa shule za Msingi za Mkoa kutoka Shirikisho la michezo nchini (TFF).

Pia Juma hilo limewezesha uzinduzi wa kwaya ya Mkoa wa Dodoma, midahalo kwa wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari na kufunga mafunzo kwa wahitimu wa skauti Mkoa.

Juma la wadau wa Elimu Mkoa wa Dodoma limefikia kilele chake likiongozwa na kauli mbiu ya "Uwajibikaji wangu ni msingi wa kuinua ubora wa Elimu na ufaulu Dodoma".

Lengo hasa la Mkutano huo ni kujadili namna ya kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya Elimu Mkoa wa Dodoma pamoja na kuweka mikakati ya kuinua Taaluma na ufaulu kimkoa pamoja na kuzindua rasmi Mpango Mkakati wa Elimu Mkoa.

Monday, March 25, 2024

VIONGOZI WAPYA WA KANISA WAPEWA NENO

Na Wellu Mtaki, Dodoma 

Viongozi wa kanisa la Dayosisi Central Tanganyika (DCT ) Mtakatifu Paulo Parishi ya Ndachi Dodoma wamewataka viongozi waliosimwikwa katika Kanisa hilo kuwa mfano ili kujenga jamii yenye maadili.

Hayo yamebainishwa na Mchungaji wa Parishi ya Ndachi Msalato Dodoma  Christopher  Njiliho  Leo Machi 24 ,2024 baada ya kumalizika kwa ibada ya kusimikwa kwa viongozi wa idara mbalimbali ndani ya kanisa hilo ambapo wamesema kuwa kanisa lina nafasi nzuri ya kujenga jamii bora.

"Ninawaomba sana viongozi muwe  wa kwanza kuacha dhambi, kuacha vitendo vibaya ili muende kufundisha wengine ukiwa mfano watu watakusikiliza sana na watapokea ujumbe ambao utawapelekea ili kuzuia vitendo viovu,"amesema Njiliho.

Aidha amesema kuwa kanisa linatakiwa kuwa mfano wa kuigwa ili kuhakikisha linajenga Vijana walio imara kwa kuzingatia maadili na taratibu za Taifa la Tanzania.

Kwa upande wake Mlezi wa idara ya kina Mama  Violeth Njiliho amesema kuwa Vijana wengi wamepotea kwa kukosa Maadili hivyo kama kanisa wanapenda kuhamasisha Vijana kushiriki semina mbalimbali ili kubadilisha mwenendo na kuongeza nguvu kazi kwa Taifa na kanisa .

"Vijana ni nguvu kazi ya Taifa pia ni nguvu kazi ya kanisa Vijana wengi wamepotea kwa kukosa maadili kama kanisa tunaenda kuhamasisha  Vijana wetu waweze kupata semina mbalimbali ili waondoke katika hatua waliyonayo ya utandawazi ili warudi kumtegemea Mungu,"amesema Violeth

Naye Mhasibu wa parishi ya Ndachi Amos Mchoro amesema kuwa kanisa linategemea kuanzisha mradi wa Ujenzi wa frem za maduka ambayo yatasaidia kuinua pato la kanisa na muumini mmoja mmoja kwa kutoa na fursa zitokanazo na mradi huo.

"Mpango tulionayo kwa ajili ya Vijana wa mitaani tunategemea kuanzisha mradi wa kufungua frem za biashara kwa ajili ya kukodisha waumini wote na ambao sio waumini,"amesema Mchoro

Pia amesema kuwa kanisa lipo kwenye mchakato wa kutafuta namna ya kukopeshwa mikopo kwa vijana ili kuhakikisha kila kijana ananufaika na mkopo huo ili kuweza kujikwamua kiuchumi.

"Tunakusanya Vijana ambao wapo mtaani ili kuwavuta walijue neno la Mungu pamoja na kutafuta fedha na kuanza kujikopesha kwa watu ambao wanasali katika kanisa hili na wasio wa kanisa hili,"amesema Mchoro.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Vijana Parishi ya Ndachi Msalato Timotheo Hoya amewataka Vijana wamtumikie Mungu na waachane na vitendo rushwa, wizi, ulawiti pamoja na matumizi ya madawa ya kulevya.

"Vijana wa kanisa wamtumikie Mungu kwa kipindi hichi madam Tanzania kwa sasa inakumbana na matatizo mbalimbali kama matatizo ya rushwa, ukatili , wizi,na matumizi ya madawa ya kulevya,"amesema Hoya.

Awali Mwenyekiti wa Idara ya watoto Joyce Jackson amewahimiza wazazi kuhakikisha wanawakuwakumbusha watoto kwenda kanisani ili kuweza kulishika neno na kulitambua ili kuondokana na vitendo viovu vya ulawiti kwa watoto.

"Mtoto akitembea na neno kwa njia ya haki huwezi kumfanyia ulawiti kutokana na mtoto kutambua vitu viovu na anaishi ndani ya maadili pia nawasihi wazazi wawalete watoto wao makanisani nashangaa kuona mzazi anamwacha mtoto chini ya miaka 15 nyumbani bila kumhimiza kufika kanisani," amesema Jackson.

Kanisa la Dayosisi Central Tanganyika (DCT) la Mtakatifu Paulo Parishi ya Ndachi Dodoma limesimika viongozi 70 katika idara mbalimbali huku likiwa linahudumia wazee vijana na watoto.

Friday, March 22, 2024

WALIOKIUKA SHERIA YA MADINI MAOMBI YAO KUFUTWA

 

WAZIRI wa Madini Antony Mavunde amesema wamiliki waliokiuka na kutotekeleza Sheria ya Madini maombi na leseni zao zitafutwa ili kupisha waombaji wengine kupata fursa ya kuomba maeneo hayo.

Ametoa taarifa hiyo Leo Tarehe 22 March 2024 wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu wamiliki waliomiliki Maeneo ya uchimbaji wa Madini bila kuyafanyia kazi. 

Aidha amesema kuwa  kwa wamiliki wa akaunti za uombaji na usimamizi wa leseni kwa njia ya mtandao ambao wameonesha matumizi mabaya ya mfumo huo kwa kuwasilisha maombi kwa lengo la kuhodhi maeneo bila kuendelea na kuratibu upatikanaji wa leseni akaunti zao zitasitishwa. 

Amesema miongoni mwa makosa ambayo yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara ni pamoja na wamiliki wengi wa leseni kutoanza au kutoendeleza maeneo ya leseni zao na badala yake wanahodhi maeneo, hawalipi ada stahiki za leseni, hawawasilishi nyaraka muhimu kama Mpango wa Ushirikishwaji wa Watanzania

"Kutokana na kosa la kutolipa ada stahiki za leseni, kiasi cha takribani Shilingi bilioni 36 zinadaiwa kutoka kwa wamiliki na waliokuwa wamiliki wa Leseni za Utafutaji wa Madini, Leseni za Uchimbaji Mdogo wa Madini na Leseni za Uchimbaji wa Kati wa Madini,"amesema Mavunde.

Pia amesema kuwa Tume ya Madini imetoa Hati za Makosa kwa jumla ya leseni 59 kwa sababu wamiliki wake hawajatekeleza masharti na matakwa mbalimbali ya umiliki wa leseni husika Hivyo, taratibu za kufuta leseni hizo zinaandaliwa ili kuruhusu waombaji wengine kupata fursa ya kufanya uwekezaji.

"Vilevile katika uchambuzi uliofanya na Tume ya Madini imebainika kuwa, hadi Februari, 2024 kuna uwepo wa maombi 409 ambayo wamiliki wake wamelipa ada za maombi lakini hawajawasilisha nyaraka muhimu zinazoambatana na maombi hayo." Amesema Mavunde.

Katika atua ingine amesema kuwa uchambuzi uliofanywa na Tume ya Madini imebainika kuwa  hadi Februari, 2024 kuna jumla ya maombi 2,180 ambayo hayajalipiwa ada stahiki za maombi pamoja na kubaini kuwa kuna watumiaji watano (5) wa mfumo wa uwasilishaji wa maombi kwa njia ya mtandao ambao wamekuwa wakitumia mfumo vibaya kwa kuwasilisha maombi bila kulipa ada stahiki. 

Pia ametoa rai kwa wawekezaji wote wenye leseni za uwekezaji katika Sekta ya Madini kuzingatia matakwa ya Sheria ya Madini, Sura ya 123. 

Aidha, Wizara ya Madini itaendelea kuwapa ushirikiano wawekezaji wote wa ndani na nje ya nchi wenye nia ya kufanya uwekezaji wenye tija na kukuza uchumi wa taifa letu kutokana na uvunaji wa rasilimali madini.

SERIKALI KUHAKIKISHA UJENZI KIWANDA USAFISHAJI MADINI LINATIMIA

Na Wellu Mtaki Dodoma

Waziri wa Madini Anthony Mavunde amewataka wachimbaji wa madini hasa yaliyokuwa na changamoto ya uchenjuaji na kulazimika kusafirishwa kwa mfumo wa makinikia, kuendelea kushirikiana kikamilifu na Serikali ili kuhakikisha lengo la ujenzi wa kiwanda cha usafishaji madini linatimia na linabaki kuwa alama ya ushindi katika usimamizi wa sekta ya madini.

Waziri Mavunde ameyasema hayo  Machi 21,2024 Jijini Dodoma kwenye hafla ya kukabidhi leseni kubwa ya uchimbaji madini na leseni ya usafishaji madini ambapo ameongeza kuwa zoezi hilo linaenda kuongeza idadi ya leseni na kufikia 20.

“Ujenzi wa kiwanda cha multi metal refinery naamini itakuwa ni utatuzi wa changamoto iliyokuwepo kwa wachimbaji wa madini nchini kulazimika kusafirisha makinikia ya metali kwenda kwenye viwanda vya nje ya nchi kwa ajili ya uchakataji ili kupata zao la mwisho au kuuza madini katika hali ya makinikia kwa bei ya chini,”amesema Mavunde.

Aidha Waziri Mavunde ameongeza kuwa katika kuhakikisha kuwa changamoto zinazojitokeza kwenye sekta ya madini nchini Wizara inaendelea kufanya mazungumzo na wawekezaji wa nyanja mbalimbali ikiwemo utafutaji, uchimbaji na ujenzi wa viwanda vya usafishaji madini ili kuingia ubia na watanzania jambo litakaloongeza wigo wa upatikanaji wa mitaji, utaalam pamoja na uhaulishaji wa teknolojia.

“Nitumie nafasi hii pia kutoa wito kwa wachimbaji na wamiliki wa migodi inayozalisha makinikia nchini kutumia kiwanda hiki pindi kitakapo kamilika ili kukuza fursa za ajira na mapato yatokanayo na rasilimali madini, ameongeza Mavunde.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Anamringi Macha amemuahidi Waziri wa Madini Anthony Mavunde kuwa atatoa ushirikiano kwa mamlaka zote katika kuhakikisha Fungani ya Buzwagi inakuwa na mafanikio makubwa kwa wananchi wa Wilaya ya Kahama.

RC Macha ameongeza kuwa wataendelea kuwahimiza wananchi wa Mkoa huo wa Shinyanga kuendelea kuchangamkia fursa zitakazojitokeza kupiti uwekezaji huo.

“Sambamba na uwekezaji mkubwa unaoenda kufanywa kule, na kama ambavyo tayari mmekwisha kunidokeza kuwa kampuni nyingi na kubwa zimekwisha onesha nia ya kuwekeza Mkoani Shinyanga sisi tunawihimiza wananchi wa pale wachangamkie fursa hii,”amesema.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi Dkt. Batilda Burian amesema kupitia uwekezaji huo uliofanywa na Serikali utaenda kuleta fursa mbalimbali kwa wananchi wa mkoa huo ikiwemo kujipatia ajira.

Thursday, March 21, 2024

WAANDISHI WAASWA KUHAMASISHA WANAWAKE KUSHIKA NAFASI ZA UONGOZI

WAANDISHI wa Habari nchini wametakiwa  kutumia kalamu zao kuhamasisha wanawake kushika nafasi mbalimbali za  uongozi na kwenye ngazi za maamuzi kwani uwekezaji kwa wanawake ni fursa na msingi wa kujenga jamii jumuishi. 

Hayo yamesemwa leo Machi Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) Lilian Liundi wakati akifungua mafunzo kwa waandishi wa habari juu ya uandishi unaozingatia jinsia hasa juu ya kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika uongozi.

Liundi amesema kuwa Tanzania imeweka historia ya kuwa na Rais mwanamke kwa mara ya kwanza Dk Samia Suluhu Hassan ambaye ameonyesha dhamira ya kuongeza usawa wa kijinsia.

"Pia tumesha kuwa na Maspika wa Bunge wawili wanawake ambao ni Anne Makinda na Dk Tulia Ackson na mawaziri wanawake walioshika nafasi katika wizara zinazoaminika kuwa ni za wanaume kama Wizara ya Ulinzi-Stigomena Tax, Wizara ya Mambo ya nje, Liberata Mulamula pia katibu wa Bunge Nenelwa Mhambi pia historia ya kuwa na mwanamke wa kwanza kushika nafasi ya Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu Zuhura Yunus,"amesema Liundi.

Kwa upande wake Ofisa Habari na Mawasiliano TGNP Monica John amesema kuwa wamekuwa wakishirikiana na wadau mbalimbali katika uchechemuzi juu ya sera na bajeti zinazozingatia masuala ya jinsia na shughuli zao zinahusisha tafiti mbalimbali ili kuibadilisha jamii juu ya changamoto na mafanikio kwa kuwa na ushirikiano baina ya wanajamii na viongozi.

Mradi huo unatekelezwa kwenye Halmashauri za Dar es Salaam ni Jiji la Dar es Salaam, Temeke na Kinondoni, Pwani ni Kisarawe, Chalinze na Kibaha Mjini, Lindi ni Ruangwa, Nachingwea na  Mtwara ni Mikindani, Mtwara na Tandahimba na Mafunzo hayo ya siku tatu yanaratibiwa na TGNP kwa kushirikiana na TADIO kwa udhamini wa shirika la Umoja wa Mataifa la Wanawake (UN Women).