Friday, March 22, 2024

WALIOKIUKA SHERIA YA MADINI MAOMBI YAO KUFUTWA

 

WAZIRI wa Madini Antony Mavunde amesema wamiliki waliokiuka na kutotekeleza Sheria ya Madini maombi na leseni zao zitafutwa ili kupisha waombaji wengine kupata fursa ya kuomba maeneo hayo.

Ametoa taarifa hiyo Leo Tarehe 22 March 2024 wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu wamiliki waliomiliki Maeneo ya uchimbaji wa Madini bila kuyafanyia kazi. 

Aidha amesema kuwa  kwa wamiliki wa akaunti za uombaji na usimamizi wa leseni kwa njia ya mtandao ambao wameonesha matumizi mabaya ya mfumo huo kwa kuwasilisha maombi kwa lengo la kuhodhi maeneo bila kuendelea na kuratibu upatikanaji wa leseni akaunti zao zitasitishwa. 

Amesema miongoni mwa makosa ambayo yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara ni pamoja na wamiliki wengi wa leseni kutoanza au kutoendeleza maeneo ya leseni zao na badala yake wanahodhi maeneo, hawalipi ada stahiki za leseni, hawawasilishi nyaraka muhimu kama Mpango wa Ushirikishwaji wa Watanzania

"Kutokana na kosa la kutolipa ada stahiki za leseni, kiasi cha takribani Shilingi bilioni 36 zinadaiwa kutoka kwa wamiliki na waliokuwa wamiliki wa Leseni za Utafutaji wa Madini, Leseni za Uchimbaji Mdogo wa Madini na Leseni za Uchimbaji wa Kati wa Madini,"amesema Mavunde.

Pia amesema kuwa Tume ya Madini imetoa Hati za Makosa kwa jumla ya leseni 59 kwa sababu wamiliki wake hawajatekeleza masharti na matakwa mbalimbali ya umiliki wa leseni husika Hivyo, taratibu za kufuta leseni hizo zinaandaliwa ili kuruhusu waombaji wengine kupata fursa ya kufanya uwekezaji.

"Vilevile katika uchambuzi uliofanya na Tume ya Madini imebainika kuwa, hadi Februari, 2024 kuna uwepo wa maombi 409 ambayo wamiliki wake wamelipa ada za maombi lakini hawajawasilisha nyaraka muhimu zinazoambatana na maombi hayo." Amesema Mavunde.

Katika atua ingine amesema kuwa uchambuzi uliofanywa na Tume ya Madini imebainika kuwa  hadi Februari, 2024 kuna jumla ya maombi 2,180 ambayo hayajalipiwa ada stahiki za maombi pamoja na kubaini kuwa kuna watumiaji watano (5) wa mfumo wa uwasilishaji wa maombi kwa njia ya mtandao ambao wamekuwa wakitumia mfumo vibaya kwa kuwasilisha maombi bila kulipa ada stahiki. 

Pia ametoa rai kwa wawekezaji wote wenye leseni za uwekezaji katika Sekta ya Madini kuzingatia matakwa ya Sheria ya Madini, Sura ya 123. 

Aidha, Wizara ya Madini itaendelea kuwapa ushirikiano wawekezaji wote wa ndani na nje ya nchi wenye nia ya kufanya uwekezaji wenye tija na kukuza uchumi wa taifa letu kutokana na uvunaji wa rasilimali madini.

SERIKALI KUHAKIKISHA UJENZI KIWANDA USAFISHAJI MADINI LINATIMIA

Na Wellu Mtaki Dodoma

Waziri wa Madini Anthony Mavunde amewataka wachimbaji wa madini hasa yaliyokuwa na changamoto ya uchenjuaji na kulazimika kusafirishwa kwa mfumo wa makinikia, kuendelea kushirikiana kikamilifu na Serikali ili kuhakikisha lengo la ujenzi wa kiwanda cha usafishaji madini linatimia na linabaki kuwa alama ya ushindi katika usimamizi wa sekta ya madini.

Waziri Mavunde ameyasema hayo  Machi 21,2024 Jijini Dodoma kwenye hafla ya kukabidhi leseni kubwa ya uchimbaji madini na leseni ya usafishaji madini ambapo ameongeza kuwa zoezi hilo linaenda kuongeza idadi ya leseni na kufikia 20.

“Ujenzi wa kiwanda cha multi metal refinery naamini itakuwa ni utatuzi wa changamoto iliyokuwepo kwa wachimbaji wa madini nchini kulazimika kusafirisha makinikia ya metali kwenda kwenye viwanda vya nje ya nchi kwa ajili ya uchakataji ili kupata zao la mwisho au kuuza madini katika hali ya makinikia kwa bei ya chini,”amesema Mavunde.

Aidha Waziri Mavunde ameongeza kuwa katika kuhakikisha kuwa changamoto zinazojitokeza kwenye sekta ya madini nchini Wizara inaendelea kufanya mazungumzo na wawekezaji wa nyanja mbalimbali ikiwemo utafutaji, uchimbaji na ujenzi wa viwanda vya usafishaji madini ili kuingia ubia na watanzania jambo litakaloongeza wigo wa upatikanaji wa mitaji, utaalam pamoja na uhaulishaji wa teknolojia.

“Nitumie nafasi hii pia kutoa wito kwa wachimbaji na wamiliki wa migodi inayozalisha makinikia nchini kutumia kiwanda hiki pindi kitakapo kamilika ili kukuza fursa za ajira na mapato yatokanayo na rasilimali madini, ameongeza Mavunde.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Anamringi Macha amemuahidi Waziri wa Madini Anthony Mavunde kuwa atatoa ushirikiano kwa mamlaka zote katika kuhakikisha Fungani ya Buzwagi inakuwa na mafanikio makubwa kwa wananchi wa Wilaya ya Kahama.

RC Macha ameongeza kuwa wataendelea kuwahimiza wananchi wa Mkoa huo wa Shinyanga kuendelea kuchangamkia fursa zitakazojitokeza kupiti uwekezaji huo.

“Sambamba na uwekezaji mkubwa unaoenda kufanywa kule, na kama ambavyo tayari mmekwisha kunidokeza kuwa kampuni nyingi na kubwa zimekwisha onesha nia ya kuwekeza Mkoani Shinyanga sisi tunawihimiza wananchi wa pale wachangamkie fursa hii,”amesema.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi Dkt. Batilda Burian amesema kupitia uwekezaji huo uliofanywa na Serikali utaenda kuleta fursa mbalimbali kwa wananchi wa mkoa huo ikiwemo kujipatia ajira.

Thursday, March 21, 2024

WAANDISHI WAASWA KUHAMASISHA WANAWAKE KUSHIKA NAFASI ZA UONGOZI

WAANDISHI wa Habari nchini wametakiwa  kutumia kalamu zao kuhamasisha wanawake kushika nafasi mbalimbali za  uongozi na kwenye ngazi za maamuzi kwani uwekezaji kwa wanawake ni fursa na msingi wa kujenga jamii jumuishi. 

Hayo yamesemwa leo Machi Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) Lilian Liundi wakati akifungua mafunzo kwa waandishi wa habari juu ya uandishi unaozingatia jinsia hasa juu ya kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika uongozi.

Liundi amesema kuwa Tanzania imeweka historia ya kuwa na Rais mwanamke kwa mara ya kwanza Dk Samia Suluhu Hassan ambaye ameonyesha dhamira ya kuongeza usawa wa kijinsia.

"Pia tumesha kuwa na Maspika wa Bunge wawili wanawake ambao ni Anne Makinda na Dk Tulia Ackson na mawaziri wanawake walioshika nafasi katika wizara zinazoaminika kuwa ni za wanaume kama Wizara ya Ulinzi-Stigomena Tax, Wizara ya Mambo ya nje, Liberata Mulamula pia katibu wa Bunge Nenelwa Mhambi pia historia ya kuwa na mwanamke wa kwanza kushika nafasi ya Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu Zuhura Yunus,"amesema Liundi.

Kwa upande wake Ofisa Habari na Mawasiliano TGNP Monica John amesema kuwa wamekuwa wakishirikiana na wadau mbalimbali katika uchechemuzi juu ya sera na bajeti zinazozingatia masuala ya jinsia na shughuli zao zinahusisha tafiti mbalimbali ili kuibadilisha jamii juu ya changamoto na mafanikio kwa kuwa na ushirikiano baina ya wanajamii na viongozi.

Mradi huo unatekelezwa kwenye Halmashauri za Dar es Salaam ni Jiji la Dar es Salaam, Temeke na Kinondoni, Pwani ni Kisarawe, Chalinze na Kibaha Mjini, Lindi ni Ruangwa, Nachingwea na  Mtwara ni Mikindani, Mtwara na Tandahimba na Mafunzo hayo ya siku tatu yanaratibiwa na TGNP kwa kushirikiana na TADIO kwa udhamini wa shirika la Umoja wa Mataifa la Wanawake (UN Women). 


CCM PWANI YAIBUKA NA USHINDI UDIWANI

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoani Pwani kimeshinda Kata zote tatu kwenye chaguzi ndogo zilizofanyika baada ya madiwani wa Kata hizo kufariki dunia.

Chaguzi hizo zilizofanyika kwenye kata tatu za Fukayosi Wilaya ya Bagamoyo Kibaha Mjini na Mlanzi Wilaya ya Kibiti ambapo kote imeshinda wapinzani kwa zaidi ya asilimia 90 ya kura zilizopigwa.

Kwenye uchaguzi wa Kata ya Fukayosi Wilaya ya Bagamoyo mgombea wa CCM Mrisho Some amepata kura 5,883 kati ya kura halali 5,960 sawa na asilimia 98.7 huku vyama vingine vikiwa ni CCK, DEMOKRASIA MAKINI, UDP na UMD.

Katika uchaguzi wa Kata ya Msangani Kibaha Mjini Yohana Gunze alishinda kwa kupata kura 5,862 kati ya kura halali 5,909 zilizopigwa sawa na asilimia 99.2 na kuvishinda vyama vya ADA - TADEA, CCK, DEMOKRASIA MAKINI, DP, N.R.A, UMD na UPDP.

Naye mgombea wa CCM Athumani Mketo Kata ya Mlanzi Wilaya ya Kibiti amepata kura 1,592 kati ya kura halali 1,732 sawa na asilimia 91.9 ambapo vyama vingine vikivyoshiriki ni ACT - WAZALENDO, CUF, DEMOKRASIA MAKINI, N.R.A, UDP, UMD na UPDP.

Akizungumzia ushindi huo Katibu wa Siasa Uenezi na Mafunzo CCM Mkoa wa Pwani David Mramba alisema kuwa ushindi wa CCM ni ishara njema kuelekea kwenye chaguzi zijazo kwani wananchi wana imani kubwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Dk Samia Suluhu Hassan.

Mramba alisema kuwa kwenye uchaguzi ujao wa mwakani wa serikali za mitaa na vitongoji watahakikisha wanapata ushindi wa kishindo kwani huu mdogo ni kama mazoezi kwao.


Wednesday, March 20, 2024

MAMLAKA ZA MAJI ZATAKIWA KULIPA MADENI YATOKANAYO NA TOZO

SERIKALI kupitia wizara ya Maji imezitaka Mamlaka za Maji zote  zinazodaiwa kuwasilisha deni la tozo zake ili kuiwezesha EWURA kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi hii nikutokana na deni la tozo kwa Mamlaka za Maji kufikia takribani shilingi bilioni 4.6. 

Akizindua Taarifa ya Utendaji wa Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira kwa kipindi cha mwaka 2022/23 ambayo ni ya 15 kutolewa na EWURA, Mhandisi Mwajuma Waziri  Katibu Mkuu wa wizara ya Maji  amezitaka mamlaka hizo  zinazodaiwa ankara za maji  zilipe madeni yake mapema ili kuziwezesha kujiendesha na kuweza kutoa huduma kwa ufanisi.

"Kwa Mamlaka za Maji ambazo utendaji wake hauridhishi niseme wazi hatutasita kuzichukulia hatua, nafahamu kuwa baadhi zinashindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za bei ya maji kuwa chini ikilinganishwa na gharama za uendeshaji". Amesema.

Aidha,Katibu mkuu huyo amewasisitiza watendaji wanaohusika katika usimamizi wa miradi ya Maji nchini kutimiza wajibu wao kwa mujibu wa Sheria.

"Kwa wakandarasi wanaotekeleza miradi hii, wahakikishe wanaikamilisha kwa wakati'tunafahamu moja ya changamoto zinazoikabili sekta ya maji nchini ni pamoja na kuchelewa kutekelezwa kwa miradi,sitovumilia kuona hili likijitokeza katika miradi hii mikubwa na yenye maslahi makubwa  kwa taifa"Amesisitiza 

Licha ya hayo,ameziagiza Mamlaka za Maji kushirikiana na  Halmashauri zote za Wilaya kuhamasisha uvunaji wa maji ya mvua katika ngazi zote hasa katika kipindi hiki ambapo mvua zinaendelea kunyesha maeneo mbalimbali nchini.

"Tumejionea mvua hizi katika baadhi yua maeneo zimeleta madhara makubwa, hivyo basi,endapo tutavuna maji haya tutapunguza kama siyo kuondoa kabisa athari zake na pia  kutaiwezesha nchi yetu na wananchi kuwa na akiba ya maji ambayo yatatusaidia kipindi cha ukame". Amesema

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa EWURA Dkt. James Andilile amesema taarifa iliyozinduliwa leo ni ya 15 tangu kuanzishwa kwa Mamlaka hiyo miaka 18 iliyopita na inahusisha uchambuzi wa utendaji wa mamlaka za majisafi na usafi wa mazingira 85 zikiwemo; mamlaka 25 za mikoa, saba (7) za miradi ya kitaifa, 47 za wilaya na Sita (6) za miji midogo.

Dkt.Andilile amesema  Utendaji wa mamlaka za maji na usafi wa mazingira umeendelea kuimarika ambapo kwa mwaka 2022/23, Mamlaka za Maji 78 kati ya 85 zilipata alama kuanzia wastani hadi vizuri sana katika utendaji wa ujumla ikilinganishwa na mamlaka 77 kati ya 90 kwa mwaka 2021/22.

Ameyataja Maeneo yaliyoimarika kwa kiasi kikubwa ikilinganishwa na mwaka 2021/22 kuwa ni pamoja na kuongezeka kwa kiwango cha maji yaliyozalishwa kutoka mita za ujazo milioni 393 hadi 400 sawa na asilimia 1.8 , kuimarika kwa uwiano kati ya watumishi na wateja kutoka 4.2 hadi 3.8 kwa kila wateja 1000 , kuimarika kwa Uwiano wa maunganisho yaliyofungwa dira za maji kufikia asilimia 92 ikilinganishwa na asilimia 90 ,kuongezeka kwa kiwango cha ubora wa maji yanayosambazwa kwa wateja kutoka asilimia 91 hadi 94;

Maeneo mengine ni kuongezeka kwa wateja wa maji wa majisafi kutoka kutoka 1,385,485 hadi 1,532,362 sawa na asilimia 11 na kuongezeka kwa wateja wa mtandao wa uondoaji majitaka kutoka wateja 55,996 hadi wateja 56,899 sawa na asilimia 16.

“Nafahamu kuwa mafanikio hayo hayakuja bure. Naomba nitumie fursa hii kumpongeza na kumshukuru Mh. Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wewe Mheshimiwa Waziri kwa usimamizi wako mahiri wa sekta ya maji kwa kufanya uwekezaji mkubwa kwa lengo la kumtua mama ndoo kichwani na kuimarisha ustawi wa watanzania wote, kwani maji ni uhai,” amesema Dkt. Andilile

Uzinduzi huo umekwenda sambamba na utoaji wa tuzo mbalimbali Kwa Mamlaka zilizofanya vizuri huku zikigawanywa katika makundi Matatu tofauti kulingana na idadi ya wateja inayowahudumia ambapo kundi la kwanza ni Mamlaka za maji zenye wateja chini ya 5000, kundi la pili ni mamlaka za maji zenye wateja chini kati ya 5000 na 20,000 na kundi la Tatu ni mamlaka za maji zenye wateja zaidi ya 20,000.


Tuesday, March 19, 2024

WANANCHI MSANGANI WATAKIWA KUMCHAGUA CHONGELA KUWA DIWANI

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Pwani Jackson Kituka amewataka wananchi wa Kata ya Msangani kumchagua mgombea Udiwani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Gunze Chongela kwenye uchaguzi mdogo utakaofanyika kesho Machi 20.

Uchaguzi huo unafanyika kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani wa kata ya Msangani Wilaya ya Kibaha Leonard Mlowe kufariki dunia hivi karibuni.

Kituka ameyasema hayo wakati wa mkutano wa kufunga kampeni za uchaguzi mdogo kwenye uwanja wa Juhudi Msangani.

Amesema kuwa wamchague mgombea huyo wa CCM kwani ni mchapakazi mwadilifu na mwaminifu na wasipoteze muda kuchagua wagombea wa vyama vingine.

Mwenyekiti wa CCM Kibaha Mjini Mwajuma Nyamka amesema kuwa mgombea huyo ndiyo chaguo sahihi katika kuleta maendeleo kwa wananchi wa kata hiyo.

Nyamka amesema kuwa diwani aliyefariki aliacha mipango mingi ya maendeleo ambayo lazima iendelezwe na diwani anayetokana na CCM hivyo wasipoteze muda kuchagua mgombea wa chama kingine.

Naye mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mussa Ndomba amesema kuwa Kata hiyo imetengewa kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 900 kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Ndomba amesema kuwa fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya miradi mbalimbali kwenye sekta mbalimbali za kijamii.

Mkutano huo uliwahusisha madiwani viongozi wa chama wa ngazi mbalimbali na wanachama wa CCM pamoja na mbunge wa viti maalum Dk Allice Kaijage.

Monday, March 18, 2024

SERIKALI KUIWEZESHA SEKTA YA MADINI KUONDOA CHANGAMOTO WACHIMBAJI WADOGO WADOGO


 Na Wellu Mtaki, Dodoma 

Serikali ya awamu ya sita imedhamiria kuiwezesha sekta ya madini kwa kuchangia asilimia 10 kwenye pato la Taifa ifikapo mwaka 2025 kwa kuondoa changamoto zote zinazowakabili wachimbaji wa madini wadogo wadogo ili kuwezesha shughuli hiyo kuendelea kukua na kukuza uchumi wa nchi ambapo mpaka sasa mchango wa sekta ya madini kwenye pato la nchi umeongezeka kufikia asilimia 9.7

Akizungumza na waandshi wa habari  jijini Dodoma Mkurugenzi wa taasisi ya Tanzanite Fashion na Miss Utalii Eva Raphael amesema madini ya Tanzanite ambayo mauzo yake hufikia mpaka Dola Milioni hamsini kwa mwaka ndiyo upekee  wa kuadhimisha shughuli yetu hi Tanzanite Fashion week.

Aidha amesema kuwa kutakuwa  na  tamasha kubwa la Kitaifa la Tanzanite Fashion week linatarajiwa kufanyika tarehe 4 mwezi 5 Mwaka 2024 jijini Dodoma katika Ukumbi wa Mabeyo Complex. tamasha hilo litaenda kutangaza Utalii wa Madini na Mali asili mbalimbali zilizopo hapa nchini.

"Tunapenda kuwaalika wachimbaji mbalimbali wa Madini, wachimbaji Wanawake na vyama vyao vyote vya Madini, taasisi mbalimbali za kiserikali na binafsi kwenda kushirikiana na sisi katika wiki ya Tanzanite Fashion"Amesema

Aidha amesema kuwa wiki hiyo ni wiki iliyojaa Maudhui mengi,mafundisho pamoja na dhamira nyingi ya kwenda kuigusa jamii na kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Naye Afisa Utamaduni Wizara ya Utamaduni Sana na Michezo Alice John amempongeza Eva kwa ubunifu huo wa kuandaa tamasha hilo na kusema kuwa anaenda kuieleza na kutumia sanaa kama njia bora ya kufikisha ujumbe

"Tunamshukuru dada Eva kwa kuiona sanaa ni njia bora na anakwenda kutumia Sanaa kutangaza Madini"Amesema John

Kwa upande wake Mkurugenzi wa kanzidata ya madini taasisi ya Jiologia na utafiti wa madini amesema kuwa Madini ya Tanzanite ndo Madini pekee yanayopatikana hapa nchini ndo maana ameyachagua katika wiki ya Tanzanite Fashion week tumeona ni vema kumuunga mkono ili tuweze kuyatangaza madini na Wizara ya Madini imeona  frusa hii ni bora kwa wachimbaji wadogo Wanawake.