Thursday, August 31, 2023

DIWANI KUIPSTIA SHULE PHOTOCOPY MASHINE

DIWANI wa Kata ya Kibaha Goodluck Manyama amejitolea kuipatia Shule ya Msingi Jitegemee mashine ya kudurufu karatasi ili kuipunguzia mzigo shule hiyo gharama za uchapishaji mitihani.

Aidha katika kukabili changamoto ya maji kwenye shule hiyo Halmashauri itapeleka mradi wa kisima cha maji.

Akizungumza shuleni hapo wakati wa mahafali ya darasa la saba alisema kuwa atawanunulia mashine hiyo baada ya shule hiyo kutoa ombi hilo kwake.

Manyama alisema kuwa hiyo ni moja ya changamoto kubwa zinayoikabili shule hiyo hivyo ameona awapunguzie mzigo huo ili kupunguza gharama za kudurusu mitihani na kazi nyingine za shule.

"Nimeona nitoe msaada huu ili iwe chachu na kwa wadau wengine wajitokeze kusaidia changamoto za shule ili wanafunzi waweze kusoma katika mazingira mazuri,"alisema Manyama.

Alisema kuwa atashirikiana na wadau wengine pamoja na wanajamii kuhakikisha wanatatua changamoto za shule hiyo ili itoe elimu bora kwa wanafunzi.

"Tumepata wadau watatuchimbia kisima ili maji yawe ya uhakika na tayari mipango imekamilika na kisima kitachimbwa hivyo tuvute subira baada ya muda mfupi maji yatapatikana,"alisema Manyama.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo Stori Samatta alisema kuwa katika kuhakikisha wanakabili changamoto amekuwa akishirikisha wadau kuchangia elimu shuleni hapo.

Samatta alisema kuwa licha ya kuwa na changamoto kwani baadhi ya wanajamii kutokuwa na moyo wa kuchangia lakini anawapa elimu ya kuwa na moyo wa kuchangia ili iwe faida kwa watoto wao.

Naye mwanafunzi Eveline Samweli alisema kuwa wanakabiliwa na baadhi ya changamoto ikiwa ni pamoja na upungufu wa maji, matundu ya vyoo, kutokuwa na uzio na chumba cha kompyuta na kompyuta.

Samweli alisema kuwa changamoto nyingine ni shule kutokuwa na jengo la utawala ambapo jumla ya wahitimu kwa mwaka huu ni 126 ambapo shule hiyo ina wanafunzi 912 na ilianzishwa mwaka 2004 na ina walimu 24.

JAMII PWANI YATAKIWA KUWALINDA WATOTO ILI WAISHI KWENYE MAZINGIRA MAZURI




WADAU wa Programu Jumuishi ya Taifa ya Malezi Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (PJT-MMMAM) Mkoani Pwani wameshauriwa jamii kuwalinda watoto ili kuepukana na vitendo vya ukatili.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Mkurugenzi wa Anjita Child Development Foundation Janeth Malela wakati wa kikao cha maandalizi ya uzinduzi wa Programu hiyo kwa Mkoa wa Pwani.

Malela alisema kuwa programu hiyo itasaidia kuimarisha ukuaji na maendeleo ya mtoto kikamilifu kimwili, kiakili, kukuza lugha, mawasiliano kijamii na kihisia. 

"Programu hii ni kutoa huduma za Afya, Lishe, Malezi yenye Mwitikio, ujifunzaji wa Awali na Ulinzi na Usalama kwa watoto wa miaka 0 hadi 8 na kuimarisha ushirikiano wa wadau wa sekta mbalimbali katika huduma za MMMAM,"alisema Malela.

Aidha alisema kuwa lengo kuu ni kusaidia watoto kwenye masuala ya malezi,makuzi,ujifunzaji,ulinzi wa mtoto,afya ili wakue katika mazingira mazuri na kukua kutokana na sheria zilizopo.

Kwa upande wake ofisa maendeleo ya jamii mkoa wa Pwani Rachel Chuwa alisema kuwa moja ya changamoto wanazozipata watoto ni baadhi ya wazazi na walezi kutowahudumia watoto wao kwa wakati kutokana na kutafuta mahitaji ya nyumbani.

Chuwa alisema kuwa malezi na makuzi wazazi wanapaswa wawahudumie lakini kwa sasa wanalelewa na televisheni na mitandao na suala la lishe shuleni baadhi wanatoa chakuka lakini waengine hawatoi hivyo mpango huo utasaidia kuondoa changamoto zolizopo ili wapate huduma stahiki.

Naye mkurugenzi wa shirika la maendeleo kwa vijana (YPC) Israel Ilunde alisema kuwa mpango huo ni muhimu sana kwani vijana wanakumbana na changamoto za kimaadili kutokana na kutopata malezi bora kutokana na hali ya kimaisha.

Ilunde alisema kuwa mpango huo utasaidia sana katika kuwalea watoto na kuondoa vitendo viovu kutokana na malezi watakayoyapata hivyo rasilimali zitengwe ili kuwalea watoto katika misingi mizuri ya kimaadili.

Mikoa 10 ambayo imeshazindua programu hiyo ni Tabora, Arusha, Morogoro, Rukwa, Manyara, Mbeya, Dodoma, Dar es Salaam, Kagera na Lindi.

Wednesday, August 30, 2023

TUME YASAJILI WATAALAMU 1,600

 

Mkurugenzi wa Tume ya TEHAMA Dkt. Nkundwe Mwasaga amesema hadi kufikia Juni 31 , 2023  imesajili wataalam wa TEHAMA 1,600 wanaohudumia nchi nzima na bado zoezi la usajili linaendelea.

Dkt.Mwasaga ameyasema hayo leo Jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa shughuli mbalimbali za TUME hiyo na mwelekeo wa utekelezaji wa Bajeti ya Mwaka wa fedha wa 2023/2024.

Akitaja Mafanikio kwa mwaka wa fedha 2023/24 amesema Tume imefanikiwa Kuanzishwa kwa mradi wa kujengwa kituo kikubwa cha Taifa cha Ubunifu Dar Es Salaam kwa ajili ya kutoa huduma kwa wataalam, watafiti, na wabunifu wa TEHAMA. 

"Tunatengeneza mfumo jumuishi utakaounganisha usajili na uendelezaji wa wataalam na wabunifu TEHAMA nchini (ICT human capital development system): lengo la mfumo huu ni kutambua bunifu na kupanua wigo wa ukuzaji wa wabunifu na bidhaa na huduma za TEHAMA zinazozalishwa Tanzania na hivyo kukuza pato la Taifa na kuongeza fursa za ajira kupitia TEHAMA na maendeleo ya kidijitali duniani"Amesema Dkt.Mwasaga.

Aidha ameongeza kuwa wanaandaa mkutano wa mwaka wa TEHAMA (TAIC) na Tuzo ya TEHAMA Tanzania (Tanzania ICT Award)

"Hili lilikuwa kongamano kubwa la mwaka la TEHAMA lililofanyika Zanzibar mwezi Oktoba, 2022 na kuwashirikisha wawekezaji na wadau mbalimbali wa TEHAMA kutoka ndani na nje ya nchi wapatao 1,200"

Sanjari na hayo vipaumbele vya tume kwa mwaka 2023/24 ni pamoja na kuendelea na ukamilishwaji wa vituo vya ubunifu TEHAMA (Soft centers) katika Kanda 5 pamoja na kuanzisha kituo kimoja Zanzibar,kuanzisha kituo cha kutengeneza na kuboresha vifaa vya TEHAMA (ICT Refurbishment and Assembly centre),kuwezesha uanzishaji wa vituo vya majaribio vya ubunifu TEHAMA (District ICT Startups Innovation hubs) katika Wilaya 10,

Aidha vipaumbele vingine ni kufanya tafiti za maendeleo ya TEHAMA nchini na kufanya tathmini ya kitaifa ya hatua za utekelezaji wa mikakati mbalimbali ya TEHAMA,kuratibu na kuandaa matukio ya kuvutia uwekezaji na kutangaza masoko ya bidhaa za TEHAMA ndani na nje ya nchi,kushirikiana na washirika wa maendeleo na kampuni za kimataifa katika kuendeleza bunifu za TEHAMA ikiwemo kuwezesha utengenezaji wa bidhaa za TEHAMA hapa nchini pamoja na kujenga kituo cha Artificial Intelligence kwa ajili ya kuendeleza wataalam wa TEHAMA.

Kwa upande wake Msemaji Mkuu wa Serikali Ndugu Gerson Msigwa amesema Serikali imeamua kuwekeza kwa nguvu kwenye Tanzania ya Kidigitali chini ya Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari ambapo usimamizi m kuu unafanywa na Tume ya TEHAMA.

Ameongeza kuwa hili ni jambo kubwa kwani fedha nyingi imewekezwa kwa ajili ya kuboresha TEHAMA nchini kwani shughuli mbalimbali kwa sasa duniani zinafanyika kwa njia ya kidijitali ikiwemo huduma za malipo mabalimbali, huduma za afya za matibabu, uzalishaji, kilimo, uchimbaji wa madini.

Tuesday, August 29, 2023

PWANI YASHEREHEKEA USHINDI WA KWANZA NCHINI MKATABA WA LISHE

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI Mh. Angela Kairuki, akikabidhi Ngao ya Ushindi wa Kwanza kwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mh. Abubakar Kunenge (katikati pichani) leo Agosti 29, 2023 kwa Mkoa wa Pwani kuibuka mshindi katika utekelezaji wa Mkataba wa Lishe kwa mwaka 2022/23. Mwingine ni Katibu Tawala Mkoa huo na Skauti Mkuu wa Tanzania Rashid Mchata.

*Mkoa wa Pwani waongoza utekelezaji Mkataba wa Lishe kitaifa*

Mkoa wa Pwani umeongoza kwa kushika nafasi ya kwanza kwa tathmini ya Saba (7) ya utekelezaji wa Mkataba wa Lishe kwa Mwaka 2022/2023.

Taarifa zilizotolewa na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa - (OR - TAMISEMI) zimeeleza kuwa Mkoa huo umefuatiwa na Lindi katika nafasi ya pili huku nafasi ya tatu ikienda kwa mkoa wa Iringa.

Kwa upande wa nafasi za Halmashauri, Mkoa wa Pwani umefanikiwa kuingiza halmashauri za Kibaha TC na Kibaha DC katika nafasi kumi za mwanzo.

Kibaha TC imekuwa ya na Kibaha DC ikiwa ni ya 10 huku hamashauri zingine za mkoa huo zikiwa zimeshika nafasi juu ya 100 za mwanzo.

Halamshauri hizo na nafasi zao kitaifa kwenye mabano ni Kisarawe (17), Rufiji (25), Bagamoyo (26) na Kibiti (54).

Zingine ni Chalinze (59), Mafia (91) na Mkuranga (93).

HIFADHI YA TAIFA KITULO KUTANGAZWA KITAIFA NA KIMATAIFA ILI KUVUTIA WATALII NA WAWEKEZAJI

 

Serikali imeendelea kujizatiti kwa  kuitangaza  Hifadhi ya Taifa ya Kitulo  ndani na nje ya nchi lengo likiwa ni kuwavutia watalii na wawekezaji kutoka sehemu mbalimbali Duniani kupitia maonesho, matamasha na kwa  njia ya kidijitali.

Kauli hiyo imesemwa leo Bungeni Jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Makete, Mhe. Festo Sanga aliyetaka kujua mkakati wa Serikali wa kuitangaza Hifadhi ya Taifa ya Kitulo.

Amefafanua kuwa hifadhi hiyo imekuwa ikitangazwa katika matamasha mbalimbali ya Karibu Kusini, Kilifair na Maonesho ya Kimataifa ya Sabasaba na Nanenane na kwa njia ya kidigitali, mitandao ya kijamii, majarida na Safari Channel.

Kufuatia hatua hiyo Serikali imeanza kuboresha  miundombinu ndani ya hifadhi hiyo ikiwemo kufanya ujenzi wa nyumba tatu za malazi ya watalii na pia inatarajia  na kujenga nyumba mbili  na kambi moja  ya kuweka hema katika mwaka huu wa fedha 2023/2024, pamoja na  kukarabati miundombinu ya barabara.

Kuhusu utatuzi wa migogoro ya mipaka kati ya hifadhi hiyo na wananchi, Mhe. Masanja amesema tathmini ilishafanyika na kulielekeza Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kuweka vigingi katika maeneo ambayo yameshaainishwa.

Saturday, August 26, 2023

WANANCHI TUMIENI VITUO VYA MSAADA WA SHERIA KUSULUHISHA KESI ZA MADAI KUPITIA VITUO VYA MSAADA WA SHERIA-KPC

WANANCHI Wilayani Kibaha Mkoani Pwani wametakiwa kutumia vituo vya msaada wa sheria kusuluhisha kesi za madai nje ya mahakama ili kuokoa muda na kuipunguzia mahakama mzigo wa mashauri.
Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na mkurugenzi wa Kituo cha Msaada wa Sheria Kibaha (KPC) Catherine Mlenga alipozungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake.

Mlenga alisema kuwa baada ya bunge kufanya marekebisho sheria inaruhusu wadai kukubaliana nje ya mahakama kwa maridhiano ya pande mbili na kumaliza shauri kisha kufutwa na mahakama.

"Tunawashauri wananchi watumie vituo hivi ili kutatua mashauri ya madai nje ya mahakama endapo watakubaliana na makubaliano hayo yatasajiliwa na mahakama na kuimaliza kesi hiyo,"alisema Mlenga.

Alisema kuwa faida ya kumaliza mashauri ya madai nje ya mahakama ni kuokoa muda na hakutakuwa na uadui baina ya pande hizo mbili tofauti na kuendesha kesi mahakamani.

"Njia hii ya usuluhishi na upatanishi ni nzuri kwani ni rafiki na haina uhasama ambapo kesi inapofanywa mahakamani kunakuwa na uhasama sana hivyo wananchi watumie fursa hii,"alisema Mlenga.

Aidha aliwataka wananchi kutumia zaidi maridhiano katika changamoto za mashauri ya madai ambapo itaipunguzia mahakama mlundikano wa kesi hivyo kutotumia muda mrefu.

Kwa upande wake meneja wa KPC Dismas Chihwalo alisema kuwa kituo chao kinatoa huduma bure kwa watu wenye mashauri mbalimbali ya kisheria.

Chihwalo alisema kuwa wameweza kutatua changamoto nyingi za kisheria na kufanikisha wananchi kupata haki zao kwa njia usuluhishi kwenye mashauri mbalimbali.