Sunday, November 26, 2017

WANAONUNUA KOROSHO KINYUME CHA UTARATIBU WAKAMATWE-RC

Mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akizindua ununuzi wa zao la korosho wilayani Kibiti 

 Baadhi ya viongozi wa wilaya za mkoa wa Pwani wakati wa uzinduzi wa zao la korosho wilayani Kibiti

 Baadhi ya wanunuzi waliohudhuria mnada wa kwanza wa uuuzaji zao la korosho uliofanyika Kibiti mkoani Pwani

 Wadau wa zao la korosho wakiptia taarifa mbalimbali juu ya uuzaji wa zao la korosho mkoani Pwani

Na John Gagarini, Mkuranga

MKUU wa Mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo amewataka wakuu wa Polisi wa wilaya kuwakamata wafanyabiahara ambao watanunua zao la korosho la msimu huu kinyume cha utaratibu ikiwemo wale wanaonunua kwa njia ya “Kangomba”.

Ndikilo aliyasema hayo wilayani Mkuranga wakati wa mkutano na viongozi wa vyama vya wakulima wa zao la Korosho mkoani humo na kusema kuwa kwa msimu huu hataki kuona walanguzi wa zao hilo kwani wanawanyonya wakulima.

Alisema kuwa ununuzi kwa njia ya Kangomba ni marufuku na atakayekamatwa ananunua kwa njia hiyo ambayo inawanyonya wakulima haitakiwi.

“Ununuzi kwa njia ya Kangomba ni marufuku mauzo yote yafanyike kwa njia yam nada kwa kutumia stakabadhi ghalani hayo ndi maelekezo ya serikali atakayenunua tofauti na utaratibu huo akamatwe wakuu wa polisi wa wilaya fanyeni kazi msiwaonee huruma walanguzi wawekeni ndani,” alisema Ndikilo.

Aliitaka bodi ya korosho kuhakikisha inakabili changamoto za upatikanaji wa magunia ili korosho zilizovunwa zisiharibike na kuuzwa kwa bei ndogo kwenye soko la korosho ambapo unuzi unaanza Novemba 8 mwaka huu.

Kwa upande wake meneja wa bodi ya Korosho tawi la Dar es Salaam Mangile Malegesi alisema kuwa msimu wa zoa hilo kwa mkoa wa Pwani utazinduliwa wiki ijayo ambapo kwa mikoa ya Lindi na Mtwara msimu umeshazidnuliwa.

Malegesi alisema kuwa magunia yatapatikana kwa wakati ili wakulima waweze kuhifadhi korosho zao ambapo bei elekezi ni shilingi 1,460 kwa daraja la kwanza na 1,160 kwa daraja la pili.

Naye mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Pwani (CORECU) Rajabu Ngonema alisema kuwa changamoto kubwa iliyopo ni magunia na wakulima kutaka kuuza korosho zao kwenye maghala ya vyama vya msingi badala ya kuuza kwenye maghala makuu yaliyopitishwa na bodi ya Korosho.

Ngonema alisema kuwa maghala ni changamoto kubwa kwani wakulima wanahofia gharama na usumbufu na kutaka wauzie kwenye maghala ya vyama vya msingi.

Mwisho.  

FUNGENI NDOA KISHERIA MPATE HAKI ZENU WANAWAKE-WAASWA

 Mwenyekiti wa Kituo cha Msaada wa Kisheria Kibaha (KPC) Catherine Mlenga

Na John Gagarini, Kibaha

WATU walioko kwenye mahusiano ya kimapenzi wametakiwa kufunga ndoa kisheria ili waweze kutambulika badala ya kuishi kwenye dhana ya ndoa ambayo imesababisha migogoro mingi mara mahusiano yanapovunjika huku watoto ndiyo wakiwa waathirika wakuu.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mwenyekiti wa Kituo cha Msaada wa Kisheria Kibaha (KPC) Catherine Mlenga wakati wa mafunzo ya utoaji wa elimu juu ya masuala mbalimbali ya Kisehria yaliyoandaliwa na kituo hicho kwa viongozi wa serikali za Mitaa na Kata ya Kibaha.

Mlenga alisema kuwa dhana ya ndoa imekuwa ni tatizo sana ambapo mwanamke anaishi na mwanaume bila ya kufunga ndoa kisheria na kujiita mume na mke lakini mara inapotokea watu hawa wamechoka kuishi pamoja mwanamke hukosa haki zake za msingi.

“Watu wengi wamekuwa wakiishi kwa dhana ya ndoa ambayo haiwatambui kisheria watu hao kama ni wanandoa na kusababishia mara wanapotaka kutengana mwanamke hunyimwa mali ambayo waliichuma katika kipindi walipokuwa wakiishi hivyo ni vema wakafunga ndoa kisheria ili haki ipatikane,” alisema Mlenga.

Alisema kuwa kama watu wanataka kuwa wanandoa kwanini waishi bila ya ndoa kwani hali hii husababisha migogoro mingi ya ndoa hizo ambazo haziko kisheria kwa watu kuchukuana tu na kuishi kama mke na mume.

“Endapo kutakuwa na ndoa iliyo kisheria itasaidia kupunguza migogoro kwani hata kama mahusiano ya kindoa yamekwisha kila mtu atapata haki yake kuanzia mume, mke na watoto lakini watu wakiishi kwa dhana ya ndoa kuna upande ambao hautapata haki licha ya kwamba watakuwa wamfanya maendeleo muda walioishi pamoja,” alisema Mlenga.

Aidha alisema dhana ya ndoa pia husababisha wanandoa kutowajibika lakini kama wamefunga ndoa sheria inawataka kuwajibika na endapo mmoja atashindwa kuwajibika mwanandoa anaweze kumshtaki na mhusika kuwajibishwa.

Kwa upande wake diwani wa Kata ya Kibaha Omary Bula alisema kuwa ndoa nyingi zinaingia kwenye migogoro kutokana na wanandoa hasa wanawake kutojua haki zao za msingi hivyo kujikuta wakinyanyasika.

Bula alisema kuwa ili ndoa iweze kudumu ni kila upande kuwajibika kwa mwenzake kwa kupeana haki zote ndani ya ndoa na kutawaka wadau mbalimbali waendelee kutoa elimu ya sheria mbalimbali si za ndoa tu kwa wananchi kama kilivyofanya kituo hicho.


Mwisho.

USALAMA BARABARANI WAFANYA OPERESHENI USIKU WAKAMATA MADEREVA


 Kaimu Kamanda wa Kikosi cha Polisi cha Usalama Barabarani Tanzania (RTO) Mkoa wa Pwani Salum Morimori kulia akimhoji moja ya madereva waliokuika sheria za usalama barabarani huko Msata wilayani Bagamoyo katikati ni Edward Gontako kutoka kikosi hicho.

Na John Gagarini, Chalinze

KIKOSI cha Usalama Barabarani kimefanikiwa kuwakamata madereva saba wa mabasi kwa tuhuma za kufanya makosa mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuendesha kwa mwendo kasi na kuzidisha abiria.

Madereva hao walikamatwa baada ya kikosi hicho kwa kushirikiana na kamati ya usalama barabarani ya mkoa kufanya oparesheni ya kushtukiza usiku kwenye barabara za Morogoro na ile inayoelekea Mikoa ya Kaskazini.

Akiongoza oparesheni hiyo kaimu kamanda wa kikosi hicho RTO mkoa wa Pwani Salumu Moromori amesema kuwa wameamua kufanya oparesheni hiyo usiku ili kubaini makosa yanayofanywa usiku na hapa anaongea na madereva ambao walikamatwa wakiwemo wa kutoka nchi ya Rwanda.

Kwa upande wake mwenyekiti wa kamati uya usalama barabarani mkoa huo Josephine Protas amesema kuwa wamefanya oparesheni hiyo usiku kufuatia malalamiko.

Naye mkaguzi wa magari wa polisi Edward Gontako amesema kuwa wamekuwa wakiwapa elimu ya kuzingatia sheria za usalama barabarani na usalama wa magari.

MWISHO

KIFO MTOTO KUUWAWA SERIKALI KUFANYA UCHUNGUZI



 Mkuu wa wilaya ya Kibaha Assumter Mshama akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Lukenge kwenye mkutano maalumu

 Mke wa mtuhumiwa Zena Manoza

 Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Lukenge waliohudhuria mkutano mkuu maalumu wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Kibaha hayupo pichani

 Mkuu wa wilaya ya Kibaha Assumter Mshama akiangalia nyumba lilipotokea tukio la mtoto kuuwawa kwa kupigwa risasi,kushoto ni matundu ya risasi

Na John Gagarini, Magindu

WAKAZI wa Kijiji cha Lukenge kata ya Magindu wilayani Kibaha wametakiwa kuendelea na shughuli zao na kuishi kwa amani huku serikali ikiendelea na uchunguzi juu ya tukio la mtoto kuuwawa kwa kupigwa na bunduki na baba yake mdogo Ally Sakalawe (43) wakati akijibizana na polisi walipokwenda kukagua silaha.

Akizungumza kwenye mkutano mkuu maalumu wa Kijiji hicho mkuu wa wilaya ya Kibaha Assumter Mshama alisema kuwa serikali inaendelea na uchunguzi na itatoa taarifa ili kuondoa utata ambao umegubika tukio hilo kwa baadhi ya ndugu na wakazi wa kijiji hicho kudai kuwa polisi ndiyo walimwua mtoto huyo aitwaye Mark Joel Modest (15).

Mshama alisema kuwa anajua kuwa tukio hilo limewaumiza sana wakazi hao pamoja na familia husika lakini hawana budi kuwa na subira juu ya uchunguzi ili kubaini ukweili juu ya tukio hilo.

“Nawaomba muishi kwa amani na msiwe na wasiwasi serikali inaendelea na uchunguzi na mtapewa majibu mara uchunguzi huo utakapokamilika watu wanaosema kuwa hawaishi majumbani kuhofia kukamatwa wasiogope kama si wahalifu hawana haja ya kuogopa,” alisema Mshama.

Alisema kuwa vyombo vyote vya ulinzi na usalama vinafanya kazi zake na haki itatolewa kwani jambo hili linasikitisha sana kwani mtoto kapoteza uhai na alikuwa hausiki kwa lolote.

“Tunamasikitiko makubwa ya kumpotez amtoto huyu ambaye hakuwa na hatia lakini ninachowaomba muwe na imani na serikali kwani inalifanyia kazi suala hili ili kuweza kujua ukweli hivyo nanyi mnapaswa kuwa na imani na endeleeni na shughuli zenu za uzalishaji mali msiishi kwa hofu,” alisema Mshama.

Aidha alisema kuwa wananchi hao pia wawe makini katika kumiliki silaha ambapo mtuhumiwa licha ya kutokea kwa tukio hilo la mauaji pia alibainika kuwa alikuwa akimiliki gobore bila ya kibali pia alikutwa na vitu mbalimbali ambavyo vinaleta maswali mengi juu ya matumizi ya silaha hiyo.

“Lazima tujiulize licha ya kifo cha mtoto huyo lakini mtuhumiwa ambaye anashikiliwa na polisi alikutwa na bunduki mbili aina ya gobore, risasi ya mark 4, vipande vya nondo na gololi vyote vikitumika kama risasi hivyo lazima tujiulize matumizi ya silaha hizi,” alisema Mshama.

Awali akielezea juu ya tukio hilo mke wa mtuhumiwa Zaina Manoza alisema kuwa siku ya tukio hilo walikuwa wamelala ndani majira ya saa 8 kwenda saa 9 usiku askari walifika na kuanza kupiga bunduki na wao kuanza kupiga kelele wakiomba msaada kwa majirani.

Manoza alisema kuwa walitakiwa kutoka nje na kuambiwa watoke nje na kujitambulisha kwa majina lakini yeye akawaambia katika hao mtoto mmoja hayupo wakamwambia akamwangalie chumba kingine ambapo alipokwenda alimkuta mtoto huyo akiwa anavuja damu ubavuni.

“Baada ya hapo walinitaka nikamwite mwenyekiti wa kitongoji na alipofika wakawaambia wampeleke mtoto akapate tiba na kunitaka niongozane na huyo mtoto na mwanangu mwingine tukiwa tumembeba nikaona kama hali ni mbaya nikajua tayari kafa,” alisema Manoza.

Kwa upande wake kamanda wa Polisi wa wilaya Caster Ngonyani alisema kuwa wananchi wanapaswa kuishi kwa amani na hawatakiwi kuwa na woga na hawakwenda kwa ajili ya kuwatisha wananchi na wanafanya kazi kwa kufuata sheria.

Ngonyani alisema kuwa ripoti aliyopewa juu ya tukio hilo ilisema kuwa polisi walikwenda kwenye nyumba hiyo baada ya kupata taarifa kuwa kuna silaha aina ya gobore bila ya kibali ambapo taarifa hizo walizipata kutoka kwa wakazi wa kijiji hicho ndipo walipokwenda kwa ajili ya kuzikamata.

“Kulikuwa na wamiliki wawili wa hizo silaha ambao ni Ally Sakalawe na Robinus Almas na hawakutoa taarifa kwa uongozi kwa hofu taarifa kuvuja na walipofika waligonga na kushindwa kuingia ndani baada ya mtuhumiwa kukataa kufungua mlango na kuanza kurusha hewani,” alisema Ngonyani.

Alisema kuwa mwili wa marehemu ulifanyiwa uchunguzi kwenye Hospitali ya Rufaa ya mkoa ya Tumbi mbele ya baba Mzazi Modest na Anna Raphael mama mzazi

“Ndani ya tumbo walikuta kipande cha chuma ambacho ni kipande cha nondo kwenye tumbo la marehemu hali ambayo inaonyesh silaha iliyotumika ni gobore na silaha ya polisi haitumii chuma inatumia risasi na zingekutwa tungejua kuwa polisi walihusika,” alisema Ngonyani.

Aidha alisema kwa mujibu wa ripoti hiyo ni dhahiri kuwa mtoto huyo alipigwa na mtuhumiwa kwani tumboni kilikutwa kipande cha nondo ambazo zimekatwa na hutumika kama risasi kwenye magobore hayo ambapo vipande vingine 10 vilikutwa nyumbani kwa mtuhumiwa.

Tukio hilo lilitokea Oktoba 28 mwaka huu wakati polisi walipokwenda kufanya upekuzi juu ya uwepo wa silaha hizo aina ya magobore ambaye yalikuwa yakitumika kwa uhalifu na uwindaji haramu ambapo licha ya mtuhumiwa wa kwanza kukutwa na silaha hizo pia walimkamata Robson Almas naye akiwa na magobore mawili yakiwa hayana vibali vya umiliki.


Mwisho.

UJUMBE WA WAWEKEZAJI TOKA NCHI YA CHINA WATUA PWANI

 Baadhi ya wawekezaji toka nchini China wakiwa wanamsikiliza mkuu wa mkoa wa Pwani hayuko pichani walipomtembelea ofisini kwake Mjini Kibaha

 Mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akizungumza na ugeni wa wawekezaji toka nchini China waliomtembelea ofisini kwake kulia ni katibu Tawala wa mkoa huo Zuberi Samataba na kushoto mwakilishi wa wawekezaji toka China Liv Ming

 Mkuu wa mkoa katikati waliokaa akiwa na ugeni toka nchi ya China walipomtembelea ofisini kwake mjini Kibaha 

 Mkuu wa mkoa wa Pwani na mgeni wake na katibu tawala wa mkoa wakiwa wanafuatialia mazungumzo

 Mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akimkabidhi zawadi mwakilishi wa wawekezaji toka nchi ya China
Wataalamu wa mkoa
Wataalamu wa mkoa 

 Mkuu wa mkoa wa Pwani akimkabidhi zawadi moja ya wawakilishi wa wawekezaji toka nchi ya China

Na John Gagarini, Kibaha

WAWAKILISHI wa makampuni toka nchi ya China wameonyesha nia ya kuwekeza kwenye sekta mbalimbali mkoani Pwani baada ya kuonyeshwa fursa za uwekezaji kwenye mkoa huo.

Wakizungumza baada ya kumtembelea mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo wawakilishi hao baada ya kuonyeshwa maeneo hayo ya uwekezaji kwa njia ya video waliahidi kuwatuma wataalamu ili waone wawekeze kwenye masuala gani.

Mwakilishi wa wawekezaji hao Liv Ming alisema kuwa wamefurahishwa na nchi ya Tanzania na kikubwa ni uhusiano mzuri uliokuwepo tangu enzi za marais Julius Nyerere na Mao Tse Sung.

“Tumeona fursa nyingi za uwekezaji na tunatarajia kuwatuma wataalamu wetu kujua kuangalia na kutupa ushauri lakini baadhi ya vitu ni uwekezaji kwenye sekta ya umeme, vipuri vya magari na uhifadhi wa mazao,” alisema Ming.

Alisema kuwa wameona maeneo mbalimbali kwa njia ya video ambayo wanaweza kuwekeza na wataendelea kufanya mawasiliano na mkoa kwa ajili ya masuala ya uwekezaji kwenye sekta mbalimbali.

“Tumevutiwa na mambo mengi pia kuna baadhi ya makampuni ya wenzetu kutoka China wamewekeza viwanda mengine yanazaidi ya miaka 20 hivyo tutaendelea kuhamasisha wenzetu nao waje kuwekeza,” alisema Ming.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa ujio wa wageni hao ni faraja kwa mkoa pamoja na nchi kwa ujumla kwani itasaidia azma ya serikali ya kuwa nchi ya viwanda.

Ndikilo alisema kuwa mkoa utaendelea kuhamasisha wawekezaji wa nje na ndani ya nchi ili wawekeze kwenye sekta mbalimbali ikiwemo viwanda ili kufikia malengo ya serikali ya awamu ya tano ya nchi ya viwanda na uchumi wa kati.

Ujio wa wawekezaji hao ni kufuatia ziara ya wiki mbili iliyofanywa na timu ya mkoa wa Pwani ya Viongozi pamoja na wataalamu walioifanya mwezi Oktoba mwaka huu ambapo waliweza kuzungumza na makampuni 106 na 30 kukubali kuja mkoani Pwani kwa ajili ya kuja kuangalia maeneo ya uwekezaji.


Mwisho.

Wednesday, November 22, 2017

TANESCO WATAKIWA WATUMIE NGUZO ZA ZEGE

 Waziri wa Nishati Merdard Kalemani akifurahia jambo wakati akizungumza na baadhi ya viongozi wa wilaya ya Bagamoyo na wafanyakazi wa kiwanda cha kutengeneza nguzo kwa kutumia zege cha East Africa Infrastructure Engineering Ltd kilichopo Kidomole kata ya Fukayosi wilayani Bagamoyo 

 Mkurugenzi wa kiwanda cha kutengeneza nguzo kwa kutumia zege cha East Africa Infrastructure Engineering Ltd kilichopo Kidomole kata ya Fukayosi wilayani Bagamoyo

 Waziri wa Nishati Dk Merdard Kalemani katikati akipata maelezo juu ya uzalishaji wa nguzo kutumia zege


Baadhi ya nguzo zinazozalishwa na kiwanda chaEast Africa Infrastructure Engineering Ltd kilichopo Kidomole kata ya Fukayosi wilayani Bagamoyo

Na John Gagarini, Bagamoyo

SERIKALI imelitaka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuanza kutumia nguzo za umeme za zege kwenye miradi yake mikubwa ukiwemo ule wa Stieglers Gorge wilayani Rufiji mkoani Pwani ambao mara utakapokamilika utazalisha megawati 2,100 ikiwa ni uzalishaji wa megawati nyingi tangu mwaka 1930 uzalishaji ni megawati 1,451 hadi hivi sasa.

Aidha ifikapo Agosti mwakani nchi itaweza kuzalisha megawati 240 kutoka kwenye mradi wa chanzo cha umeme cha Kinyerezi namba mbili ambapo kuanzia Desemba mwaka huu megawati 30 zitakuwa zinaunganishwa kwenye greti ya Taifa kupitia mradi huo na kutosheleza kwa ajili ya viwanda vilivyopo.

Hayo yalisemwa wilayani Bagamoyo na Waziri wa Nishati Dk Merdard Kalemani alipotembelea kiwanda cha kutengeneza nguzo za zege cha East Africa Infrastructure Engineering Ltd kilichopo Kidomole kata ya Fukayosi wilayani Bagamoyo kujionea uzalishaji wa nguzo hizo.

Dk Kalemani alisema kuwa baada ya serikali kupiga marufuku uingizwaji wa nguzo za umeme toka nje na kuruhusu wawekezaji kutengeneza umefika wakati shirika hilo lianze kutumia nguzo za zege kuanzia Desemba mwaka huu kwa kuanzia kewenye mradi huo wa Stiglers Gorge.

“Mradi huo unatarajia kutumia nguzo kati ya 500 hadi 600 na kutokana na ukubwa wa mradi huo lazima tutumie nguzo imara ambazo zinauwezo wa kudumu kwa miaka 70 kuliko kutumia nguzo za miti ambazo zinadumu kwa miaka mitatu kwani ni gharama kubwa ukilinganisha na nguzo za zege,” alisema Dk Kalemani.

“Huwezi kuimarisha uchumi wa viwanda kwa kutegemea malighafi toka nje ya nchi lazima tutegemee vitu vionavyotengenezwa hapa nchini na mmetekeleza agizo la serikali la awamu ya tano kuanzisha viwanda vyetu kwa kutengeneza malighafi wenywe hakuna sababu ya kuagiza vifaa toka nje manufaa yameanza kuonekana tulipozuia wananchi wengi waliomba kuunganishiwa umeme wengine miaka miwili kisa kukosekana nguzo lakini kwa sasa shida hiyo haipo,” alisema Dk Kalemani.

Alisema kuwa walipozuia nguzo zisitoke nje kulikuwa na watu 29,000 walikuhawajaunganishiwa lakioni baada ya hapo watu 20,000 waliunganishiwa umeme na kama kuna mteja hajaunganishiwa umeme zaidi ya mwezi meneja hajafanya hivyo atachukuliwa hatua changamoto kuchelewesha kuunganishiwa hilo ni tatizo la meneja na atachukuliwa hatua kwani hilo ni tatizo lake.

“Utumiaji wa nguzo zinazotumia miti madhara ni kuharibu vyanzo vya maji na mazingira hivyo kaeni na kamapuni hii mshirikiane ili mradi wa Rufiji utakapoanza kutekelezwa zitumike nguzo za zege ambapo kilometa 36 zitatumia nguzo hizo kwani maeneo ya mbugani huwezi kutumia nguzo za miti au kupitisha umeme chini ya ardhi kwani lengo langu ni kuhakikisha kila mwananchi anapata umeme,” alisema Dk Kalemani.

Awali akielezea juu ya kiwanda hicho mmiliki wake Otieno Igogo ambaye anashirikiana na Wachina katika uzalishaji wa nguzo hizo alisema teknolojia hiyo ni ya kisasa kwa umeme na mawasiliano ambayo inadumu kwa zaidi ya miaka 70 hivyo kupunguza gharama za kuweka nyingine kama ilivyo kwa zile za miti.

Igogo alisema kuwa gharama za ujenzi wa kiwanda hicho ni kiasi cha shilingi ni bilioni 13 ambapo changamoto inayowakabili ni kukosa soko kwenye sekta za umma na binafsi na kuiomba serikali kuwaunga mkono kwa kutumia nguzo hizo kwenye miradi mbalimbali ya mawasiliano na umeme.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga kwaniaba ya mkuu wa mkoa wa Pwani alimshukuru Waziri wa Nishati kwa kuendelea kufanikisha upatikanaji wa umeme hasa ikizingatiwa mkoa huo ni moja ya mikoa yenye viwanda vingi hapa nchini.

Mwanga alisema kuwa wilaya ya Bagamoyo na mkoa una mahitaji makubwa ya umeme kutokana na kuwa na uwekezaji mkubwa hasa kwenye sekta ya viwanda ambayo ina mahitaji makubwa ya umeme na kusema mipango mbalimbali ya uzalishaji umeme itasaidia kuondoa tatizo la upungufu wa umeme.

Akishukuru kwa niaba ya wananchi wa Bagamoyo Mbunge wa Jimbo hilo Dk Shukuru Kawambwa alisema kuwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme ukiwemo ule wa REA ni miradi muhimu sana ambayo inakwenda kuondoa kabisa tataizo la umeme.

Dk Kawambwa alisema kuwa anampongeza Rais wa awamu ya tano Dk John Magufuli kwa kuanzisha miradi ya uzalishaji wa umeme ambapo kwa miaka mingi kumekuwa na tataizo la upungufu wa umeme na baadhi ya maeneo kutokuwa na huduma hiyo.
Mwisho.

PWANI WATAKA WATAALAMU WA UWEKEZAJI

Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Zuberi Samataba ambaye aliongoza ujumbe wa viongozi na wataalamu waliotembelea nchi ya China akiongea

Katibu Tawala wa mkoa wa Pwani Zuberi Samataba akielezea jambo kulia ni mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo  


 Baadhi ya wakuu wa wilaya za mkoa wa Pwani kuanzia kushoto Gulmahusein Kifu wilaya ya Kibiti anayefuata Happyness Seneda wilaya ya Kisarawe, Juma Njwayo wilaya ya Rufiji  na Majid Mwanga wilaya ya Bagamoyo

 Baadhi ya washiriki wakijadili baada ya kupokea taarifa ya baadhi ya viongozi na wataalamu waliotembelea nchi ya China 

Na John Gagarini, Kibaha

WATAKA kuwekwa wataalamu wa uwekezaji kwenye kila Halmashauri mkoani humo ili kuwawekea mazingira mazuri ya mawasiliano na wawekezaji.

Ushauri huo ulitolewa mjini Kibaha na baadhi ya wakuu wa wilaya za mkoa huo wakati wa kupokea taarifa toka kwa timu ya wataalamu na viongozi wa mkoa na Halmasahuri ya wilaya ya Kibaha waliokwenda nchini China.

Mkuu wa wilaya ya Mkuranga Filberto Sanga alisema kuwa wataalamu hao wakiajiriwa itasaidia kurahisisha wawekezaji kuwa na mtu maalumu ambaye atakuwa anawajibika kwa wawekezaji wanaokuja mkoani humo.

“Kukiwa na dawati maalumu kwa ajili ya wawekezaji itasaidia kupunguza usumbufu wa mwekezaji kuzungushwa wakati wa kupata vibali mbalimbali vya uwekezaji,” alisema Sanga.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kisarawe Happynes Seneda alisema kuwa mtaalamu huyo atakuwa akiwajibika na suala la wawekezaji kwani kwa sasa nchi imehamasisha ujengwaji wa viwanda hivyo kutakuwa na wageni wengi toka nje ya nchi kwa ajili ya uwekezaji.

Seneda alisema kuwa mtaalamu atajua masuala mbalimbali yanayohusiana na uwekezaji kuanzia masuala ya ardhi, upatikanaji wa vibali mbalimbali na kuwa na mawasiliano na sekta wezeshi kwa ajili ya kutatua changamoto kwa wawekezaji.      

Naye mkuu wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kuwa madawati ya wataalamu wa uwekezaji kwenye Halmashauri pia sekta wezeshi zinapaswa kuwa na wtu watakaokuwa wanahusika na wawekezaji.

Ndikilo alisema kuwa sekta wezeshi kama vile TANESCO, CHALIWASA, DAWASCO, TARURA, TRA, Polisi na Uhamiaji lazima inakuwa na watu wanaofanya kazi ya kushughulikia wageni.

“Tukiwa na wataalamu wa kudili na wageni itakuwa rahisi kutoa huduma kwa haraka na kwa wakati pia itasaidia kuondoa urasimu wakati wa kuwahudumia wawekezaji ili waweze kutekeleza majukumu yao,” alisema Ndikilo.


Mwisho.

Thursday, November 16, 2017

WENGI WAMWAGA ALBERT NGWADA




Katibu wa CCM Mkoa wa Pwani Anastazia Amas akizungumza wakati wa kuaga mwili wa Albert Ngwada kwenye ofisi za CCM Kibaha Mjini.

 Baadhi ya waombolezaji wakiaga mwili wa Ngwada



 Baadhi ya waombolezaji wakiangua vilo baada ya kuuaga mwili wa Ngwada

Vijana wa CCM wakiwa wamebeba jeneza lililokuwa na mwili wa Ngwada 


 Mama wa Marehemu katikati akiwa anabembelezwa wakati wa kuaga mwili wa mwanae kwenda mkoani Iringa kwa ajaili ya mazishi.
 Katibu wa CCM Kibaha Mjini Abdala Mdimu akitoa taarifa fupi ya marehemu wakati wa kuaga kwenye ofisi za CCM Kibaha Mjini 
Na John Gagarini, Kibaha

KATIBU wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Pwani Anastazia Amas juzi aliwaongoza wanachama na wananchi wa wilaya ya Kibaha kuaga mwili wa Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM mkoa wa Pwani kuwakilisha Kata ya Pangani Albert Ngwada kwa ajili ya mazishi mkoani Iringa ambaye alifariki dunia Novemba 13 mwaka huu.

Akiongea wakati wa kuaga mwili wa marehemu Ngwada kwenye ofisi za CCM Kibaha Mjini Amas alisema kuwa chama kimepata pigo kutokana na kifo hicho cha mjumbe wa CCM.

Amas alisema kuwa ili kumkumbuka marehemu wanachama wanapaswa kufanya kazi za chama kwa uaminifu na uadilifu ili kuleta maendeleo ndani ya chama na kwa wananchi wa Kibaha kama alivyokuwa Ngwada.

“Natoa pole kwa ndugu na wote walioguswa na msiba huu ambao umewagusa watu wengi na ndiyo maana watu wamejaa hii yote inaonyesha jinsi gani mlivyokuwa mnamkubali kutokana na utendaji wake kikubwa ni kuenzi utendaji wake,” alisema Amas.  

Awali akitoa maelezo mafupi juu ya marehemu katibu wa CCM Kibaha Mjini Abdala Mdimu alisema kuwa kutokana na utendaji wake kazi mzuri marehemu alipandishwa cheo kutoka Katibu msadizi wa kata ya Pangani na kuwa kaimu katibu msaidizi wa CCM Kibaha Mjini mwaka 2015

Mdimu alisema kuwa marehemu alitumikia nafasi hiyo kama msiadizi wake hadi mwaka 2017 baada ya kuletwa katibu msaidizi toka Magu ambapo Aprili alichaguliwa kuwa mjumbe wa mkutano mkuu wa mkoa toka kata ya Pangani nafasi aliyokuwa nayo hadi anafariki dunia.

Awali marehemu alianza kukitumikia chama mwaka 2007 hadi mwaka 2012 alipochaguliwa kuwa katibu kata Pangani hadi 2017 Juni 2015 alipanda daraja na kuwa Kaimu katibu Msaidizi hadi Aprili 2017.

Alisema kuwa mwaka huu mwezi Mei alichaguliwa kuwa Mjumbe wa mkutano mkuu wa mkoa kupitia kata ya Pangani  na tarehe 4 Oktoba alipata ajali ya Pikipiki huko eneo la Kidimu majira ya saa 1:30 usiku na kupelekwa Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Pwani ya Tumbi na baadaye alihamishiwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Aidha marehemu alifariki dunia wakati akiendelea na kliniki baada ya kutolewa Hospitali na alitarajiwa kuzikwa jana kwao mkoani Iringa na alizaliwa mwaka 1982.

Mwisho.