Sunday, November 26, 2017

FUNGENI NDOA KISHERIA MPATE HAKI ZENU WANAWAKE-WAASWA

 Mwenyekiti wa Kituo cha Msaada wa Kisheria Kibaha (KPC) Catherine Mlenga

Na John Gagarini, Kibaha

WATU walioko kwenye mahusiano ya kimapenzi wametakiwa kufunga ndoa kisheria ili waweze kutambulika badala ya kuishi kwenye dhana ya ndoa ambayo imesababisha migogoro mingi mara mahusiano yanapovunjika huku watoto ndiyo wakiwa waathirika wakuu.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mwenyekiti wa Kituo cha Msaada wa Kisheria Kibaha (KPC) Catherine Mlenga wakati wa mafunzo ya utoaji wa elimu juu ya masuala mbalimbali ya Kisehria yaliyoandaliwa na kituo hicho kwa viongozi wa serikali za Mitaa na Kata ya Kibaha.

Mlenga alisema kuwa dhana ya ndoa imekuwa ni tatizo sana ambapo mwanamke anaishi na mwanaume bila ya kufunga ndoa kisheria na kujiita mume na mke lakini mara inapotokea watu hawa wamechoka kuishi pamoja mwanamke hukosa haki zake za msingi.

“Watu wengi wamekuwa wakiishi kwa dhana ya ndoa ambayo haiwatambui kisheria watu hao kama ni wanandoa na kusababishia mara wanapotaka kutengana mwanamke hunyimwa mali ambayo waliichuma katika kipindi walipokuwa wakiishi hivyo ni vema wakafunga ndoa kisheria ili haki ipatikane,” alisema Mlenga.

Alisema kuwa kama watu wanataka kuwa wanandoa kwanini waishi bila ya ndoa kwani hali hii husababisha migogoro mingi ya ndoa hizo ambazo haziko kisheria kwa watu kuchukuana tu na kuishi kama mke na mume.

“Endapo kutakuwa na ndoa iliyo kisheria itasaidia kupunguza migogoro kwani hata kama mahusiano ya kindoa yamekwisha kila mtu atapata haki yake kuanzia mume, mke na watoto lakini watu wakiishi kwa dhana ya ndoa kuna upande ambao hautapata haki licha ya kwamba watakuwa wamfanya maendeleo muda walioishi pamoja,” alisema Mlenga.

Aidha alisema dhana ya ndoa pia husababisha wanandoa kutowajibika lakini kama wamefunga ndoa sheria inawataka kuwajibika na endapo mmoja atashindwa kuwajibika mwanandoa anaweze kumshtaki na mhusika kuwajibishwa.

Kwa upande wake diwani wa Kata ya Kibaha Omary Bula alisema kuwa ndoa nyingi zinaingia kwenye migogoro kutokana na wanandoa hasa wanawake kutojua haki zao za msingi hivyo kujikuta wakinyanyasika.

Bula alisema kuwa ili ndoa iweze kudumu ni kila upande kuwajibika kwa mwenzake kwa kupeana haki zote ndani ya ndoa na kutawaka wadau mbalimbali waendelee kutoa elimu ya sheria mbalimbali si za ndoa tu kwa wananchi kama kilivyofanya kituo hicho.


Mwisho.

No comments:

Post a Comment