Friday, October 30, 2015

RIDHIWANI KIKWETE AWASHUKURU WANACHALINZE KUMCHAGUA TENA

Na John Gagarini, Chalinze
MBUNGE Mteule wa Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete amesema kuwa hana chuki kwa wale ambao hawakumpigia kura kwenye uchaguzi uliofanyika Oktoba 25 mwaka huu kwani hizo ni changamoto za uchaguzi.
Aliyasema hayo jana kwenye uwanja wa Miembe Saba Chalinze wilayani Bagamoyo wakati wa mkutano wa hadhara wa kuwashukuru Wanachalinze kwa kumchagua kuwa mbunge kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika Jumapili.
Ridhiwani alisema kuwa licha ya baadhi ya maeneo kutompigia kura za kumchagua kuwa mbunge lakini atawatumikia wananchi wote bila ya kujali kama walimpigia kura au la kwani kila mtu ana haki ya kumpigia kura mgombea yoyote anayempenda.
“Nawashukuru wananchi wote walionipigia kura na hata wale ambao hawakunipigia kura kwani hiyo ndiyo demokrasia nitahakikisha nawahudumia wananchi wote bila ya kuwabagua nitahakikisha napeleka maendeleo kwa watu wote wa jimbo hili,” alisema Ridhiwani.
Alisema kuwa kutopigiwa kura kwa wingi siyo sababu ya kuwagawa wananchi kwani hizo ni changamoto za uchaguzi ambao unakuwa na mambo yake ambapo baadhi ya maeneo walipiga kura kwa kuzingatia ukabila.
“Sitakuwa na chuki wala hasira kwa wale ambao hawakunipigia kura nitashirikiana nao katika suala la maendeleo ili kuhakikisha jimbo letu linakuw ana maendendeleo na wananchi wanaboresha maisha yao ili yasonge mbele,” alisema Ridhiwani.
Aidha alisema kuwa atahakikisha Mji wa Chalinze ambao umekuwa Halmashauri ya Mji Mdogo unajengwa kwa kuwekewa huduma muhimu ili wananchi waweze kuboresha biahara zao hasa ikizingatiwa kuwa mji huo ni wa kibiashara.
“Moja ya mambo nitakayo yafanya ni kufanya Chalinze kuwa makao makuu ya Halmashauri hiyo na baadaye kuwa wilaya kwani mchakato unaendelea na tunaamini baada ya muda tutapewa wilaya hivyo tutaweza kujitegemea na kujiimarisha kiuchumi,” alisema Ridhiwani.
Alibainisha kuwa wananchi wasiwe na wasi wasi kwani kukichagua Chama Cha Mapanduzi CCM ni kuchagua maendeleo hivyo wasubiri kuona jinsi serikali mpya itakavyofanya kazi kwani kwao ni kazi tu.
Kwa upande wake mwenyekiti wa CCM Chalinze Nasa Karama alisema kuwa mbunge huyo ameonyesha uwezo mkubwa kwani kwa kipindi alichochaguliwa cha mwaka mmoja na miezi mitatu ameweza kufanya mambo makubwa ambapo alitumia ziadi ya shilingi bilioni moja na zaidi kwa ajali ya miradi ya maendeleo.
Mwisho.  

 Ridhiwani Kikwete

Sunday, October 25, 2015

RAIS DK JAKAYA KIKWETE ASHIRIKI ZOEZI LA KUPIGA KURA MSOGA

Na John Gagarini, Chalinze
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Jakaya Kikwete amesema kuwa mara atakapostaafu nafasi hiyo Novemba 5 mwaka huu anatarajia kuanzisha taasisi ya maendeleo kwa Afrika na Dunia.
Aidha alisema kuwa atarudi Kijijini kwake Msoga Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani ambapo mbali ya kuanzisha taasisi hiyo ya maendeleo pia ataendeleza ufugaji na kilimo cha mananasi.
Dk Kikwete aliyasema hayo jana katika Kijiji cha Msoga mara baada ya kupiga kura yake kwenye uchaguzi mkuu wa kumchagua Rais, Mbunge na Diwani na kusema kuwa amefurahi sana kuona watu wanapiga kura bila ya usumbufu wowote.
Dk Kikwete alisema kuwa mara baada ya kustaafu na baada ya Rais mpya kuapishwa Desemba 5 atajihusisha na masuala hayo kwani hawezi kukaa tu hivi bila ya kuwa na jambo la kufanya kwani ataendelea kuwa na nguvu.
“Natarajia kuwa mfugaji kwani nina shamba la mifugo pia kuwa mkulima wa mananasi huko Kijiji cha Kiwangwa na ninafurahi kupiga kura kwani nimetumia haki yangu na nanishukuru hadi sasa hatujasikia kama kuna tatizo lolote,” alisema Dk Kikwete.
“Nawaomba wananchi wajitokeze kupiga kura na ningependa na vituo vingine viwe na utulivu kama hichi cha hapa na watu washiriki uchaguzi ili baadaye wasije wakahoji kuwa hata fulani kachaguliwa wakati wao hawakupiga kura kumchagua kiongozi ambaye wanamtaka wao,” alisema Dk Kikwete.
Juu ya uchaguzi wa mwaka huu alisema kuwa chaguzi zote zinakuwa na upinzani mkali na anaomba hali ya amani iendelee hivi ili iwe nchi ya mfano kwa kufanya uchaguzi bila ya kuwa na vurugu.
Kwa Upande wake mgombea wa Ubunge wa (CCM) Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alisema kuwa anashukuru kwani hadi sasa zoezi hilo la upigaji kura linaendelea vizuri na hakuna tatizo lolote na anaamini kuwa uchaguzi utakwenda vizuri.
Ridhiwani ambaye naye alipiga kura kwenye kituo cha Kijiji cha Msoga alisema kuwa kuna changamoto ndogondogo zilizojitokeza ikiwa ni pamoja na baadhi ya watu hawakuona majina yao licha ya kuwa walikuwa na vitambulisho vya kupigia kura huko maeneo ya Miono.
Naye mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mathayo Torongey alisema kuwa amepita kwenye vituo vingi hajaona tatizo lakini kuna baadhi ya maeoneo mawakala wao walitishwa.
Torongey alisema kuwa mawakala hao walitishwa kwenye kituo cha Kijiji cha Msoga lakini baada ya makubaliano waliweka mawakala wengine na wakaendelea na zoezi la kusimamia kwenye vituo walivyopangiwa.
Aidha mkuu wa mkoa wa Pwani Injinia Evarist Ndikilo alisema kuwa hadi mchana kulikuwa hakuna tatizo lililoripotiwa licha ya kuwa baadhi ya maeneo watu walikuwa na hofu kwamba zoezi litaenda taratibu lakini hali hiyo iliondoka na utaratibu kwenda vizuri.
Ndikilo alisema kuwa eneo la Vigwaza kulikuwa na hofu ya upungufu wa karatasi kutokana na idadi kubwa ya watu lakini hali hiyo iliwekwa sawa na mambo yanakwenda vizuri na wameweka ulinzi wa kutosha.
Alibainisha kuwa suala la kukaa mita 200 kwa ajili ya kulinda kura halipo kwani sheria imeelekeza vizuri juu ya watu mara baada ya kupiga kura wanaondoka na hakuna mtu aliyebaki kulinda kura kwani wameondoka na kuendelea na shughuli zao.
Mwisho. 

 Rais Dk Jakaya Kikwete akizungumza na mkuu wa mkoa wa Pwani wapili kulia Injinia Evarist Ndikilo , wakati Rais alipokwenda kupiga kura kwenye kituo cha Kijiji cha Msoga Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani kulia ni mkuu wa wilaya hiyo Majid Mwanga

 Rais Dk Jakaya Kikwete akihojiwa na waandishi wa habara mara baada ya kupiga kura kwenye kituo cha Kijiji cha Msoga 

 Rais Dk Jakaya Kikwete kushoto akisubiri kupewa karatasi kwa ajili ya kwenda kupiga kura


 Rais Dk Jakaya Kikwete akiwa amepanga foleni kabla ya kwenda kupiga kura hata hivyo alisimama kwa muda mfupi kabla ya kutimiza zoezi hilo


Rais Dk Jakaya Kikwete akisalimiana na mkuu wa mkoa wa Pwani Evaristi Ndikilo alipowasili kwenye kituo cha kupigia kura kwenye Kijiji cha Msoga



Baadhi ya akinamama wakiwa wanasubiri kupiga kura kwenye kituo cha Kijiji cha Msoga

 Mgombea Ubunge wa Jimbo la Chalinze kupitia CCM Ridhiwani Kikwete akichukuliwa maelezo kabla ya kupiga kura 

 Ridhiwani Kikwete akiongea na waandishi wa habari mara baada ya kupiga kura kwenye Kituo cha Kijiji cha Msoga

Thursday, October 22, 2015

johngagariniblog: DK MAGUFULI KUUFANYA MJI WA CHALINZE KUWA WA KISAS...

johngagariniblog: DK MAGUFULI KUUFANYA MJI WA CHALINZE KUWA WA KISAS...: Na John Gagarini, Chalinze MGOMBEA Urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk John Magufuli emesema kuwa endapo atachaguliwa kuwa R...

DK MAGUFULI KUUFANYA MJI WA CHALINZE KUWA WA KISASA

Na John Gagarini, Chalinze
MGOMBEA Urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk John Magufuli emesema kuwa endapo atachaguliwa kuwa Rais atahakikisha mji wa Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani unakuwa moja ya miji ya kisasa na wa uwekezaji ambapo utakuwa na barabara za juu Fly Over.
Aidha ujenzi huo ambao utakuwa wa barabara sita hadi jijini Dar es Salaam utagharimu kiasi cha shilingi trilioni 2.3 na Chalinze itakuwa kiunganishi cha njia hizo kwenda mikoa ya Kasakazini na mikoa ya Kati ambapo tayari wataalamu wa upembuzi wa ujenzio huo wamelipwa kiaisi cha shilingi billion 7.7.
Aliyasema hayo kwenye mkutano wa kampeni kwenye Jimbo la Chalinze mkoani humo ambapo alisema kuwa atahakikisha mji huo unakuwa wa kisasa na huduma zote muhimu zinapatikana hapo na kuwa mji mbadala wa Dar es Salaam.
Dk Magufuli ambaye ni Waziri wa Ujenzi na Miundombinu alisema kuwa mji huo utakuwa kituo kikubwa cha uwekezaji hapa nchini kwani faida nyingine iliyopo ni kugunduliwa gesi eneo la Ruvu hivyo kufanya uchumi wa mji huo kuwa juu na wananchi wataboresha maisha yao na kuwa na maisha bora.
“Msiuze kiholela maeneo yenu kwani baadhi ya watu wanauza maeneo kwa bei ndogo lakini watakao nunua watakuja kuuza kwa bei kubwa hivyo huu ni moja ya miji itakayokuwa ya kisasa hapa nchini na sasa maisha bora yanakuja na sitawaangusha naomba mnipigie kura nyingi za kutosha ili niweze kuwa Rais,” alisema Dk Magufuli.
Alisema kuwa kuhusu changamoto ya maji kwenye mji huo alisema kuwa atahakikisha suala hilo linakwisha ambapo aliipongeza awamu ya tatu na nne ambazo zimejitahidi angalau maji yanapatikana kwani mji huo ulikuwa na tatizo kubwa la maji.
Katika hatua nyingine amesema anashangazwa na baadhi ya wanasiasa kusema kuwa fedha zilizokuwa zijenge bandari ya Tanga zimepelekwa Bagamoyo kisa ni wilaya anayotoka Rais Dk Jakaya Kikwete.
“Kauli kama hizo ni za uchonganishi kwani kila eneo limetengewa fedha zake kwa ajili ya ujenzi wa Bandari kuanzia Tanga, Mtwara na Mwanza kote kutajengwa bandari hizo na Bagamoyo ni uwekezaji wa watu binafsi hivyo hakuna sababu ya kuwachonganisha watu kwa maneno ya uongo,” alisema Dk Magufuli.
Alibainisha kuwa hizo ni hoja hafifu na hazina msingi wowote zaidi ya kuleta uchonganishi kwani wanapaswa kutangaza sera zao na si kuongopa hali ambayo inajenga chuki baina ya wananchi wa eneo fulani na eneo jingine.
Alisisitiza kuwa endapo atapata ridhaa ya kuongoza atahakikisha ushuru mdogomdogo unaondolewa ili kuwaondolea kero wananchi ambao wanataka kujiongezea kipato kutokana na shughuli zao za ujasiriamali.
Kwa upande wake mgombea Ubunge wa Jimbo hilo la Chalinze Ridhiwani Kikwete alimshukuru Dk Magufuli kwa mipango hiyo na kusema kuwa changamoto iliyopo ni ujenzi wa kituo cha afya kikub wa ili kukabiliana na uwingi wa wagonjwa pamoja na majeruhi kwenye kituo cha afya chya Chalinze.
Ridhiwani alisema kuwa changamoto nyingine ni maji ambayo licha ya kupatikana bado kuna baadhi ya maeneo hayapati maji hasa kwenye makmao makuu ya vitongoji ambapo kwa makao makuu ya vijiji yote yanapata maji kwa asilimia 94 ambapo Dk Magufuli alisema atashughulikia changamoto hizo endapo atachaguliwa kuwa Rais.
Mwisho   

 Mgombea Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk John Magufuli kulia na mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze wilayani Bagtamoyo mkoani Pwani Ridhiwani Kikwete wakiteta jambo wakati wa mkutano wa kampeni uliofanyika leo mchana kwenye uwanja wa Miembe Saba Chalinze


 Mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze Ridhiwani Kikwete kushoto katikati ni mwenyekiti wa CCM mkoa Mwinshehe Mlao na kulia ni mwenyekiti wa CCM wilaya ya bagamoyo Almasa Maskuzi wakijadili wakati wakimsubiri mgombea Urais wa CCM Dk John Magufuli kwenye uwanja wa Miembe Saba Chalinze.

 Mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze CCM Ridhiwani Kikwete kulia akisalimiana na moja ya wanachama waliojitokeza kwenye mkutano wa kampeni wa Dk John Magufuli kwenye uwanja wa Miembe Saba Chalinze

 Ridhiwani Kikwete akisalimiana na mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi CCM Josia Jackson 

Add caption



 Wagombea Ubunge kupitia CCM Ridhiwani Kikwete Jimbo la Chalinze kulia na Amoud Jumaa Jimbo la Kibaha Vijijini wakifurahi kwenye mkutano wa kampeni wa mgombea Urais kupitia chama hicho Dk John Magufuli. 

 Ridhiwani Kikwete na Dk John Magufuli wakiteta kabla ya kuanza mkutano wa kampeni uliofanyika uwanja wa Miembe Saba Chalinze

 Ridhiwani Kikwete katikati akiteta jambo na mgombea Urais CCM Dk John Magufuli kushoto ni Amoud Jumaa mgombea ubunge Jimbo la Kibaha Vijijini

 Dk Magufuli katikati wakitetea na Ridhiwani Kikwete kushoto na mjumbe wa kampeni Taifa CCM Abdala Bulembo 

 Abdala Bulembo akiwaonyesha wananchi wa Chalinze hawapo pichani namna ya kuwapigia kura wagombea wa CCM ngazi ya Urais

 Ridhiwnai Kikwete akizungumza kwenye mkutano huo wa kampeni

 Mgombea Urais kwa tiketi ya CCM Dk John Magufuli akiongea

 Baadhi ya wagombea udiwani wa CCM kwenye Majimbo ya Chalinze na Bagamoyo wakitambulishwa kwenye mkutano huo wa kampeni

 Dk John Magufuli akifurahi jambo na Ridhiwani Kikwete wakifurahia jambo wakati wa mkutano wa kampeni 

 Baadhi ya wanachama wa CCM wakiwa wamejazana kwenye uwanja wa  Miembe Saba Chalinze kumsikiliza mgombea Urais wa chama hicho Dk John Magufuli

 Sehemu ya umati wa wanachama na wananchi wa Chalinze wakiwa wanawasikiliza wagombea mbalimbali wa CCM 

 Wanachama wa CCM wakiwa wamefurika uwanja wa Miembe Saba Chalinze

 Mgombea Urais kwa tiketi ya CCM Dk John Magufuli kulia na Ridhiwani Kikwete kushoto wakiombewa duwa mara baada ya mkutano wa kampeni kwenye uwanja wa Miembe Saba Chalinze

Monday, October 19, 2015

WANAFUNZI HATARINI KUOZWA

Na John Gagarini, Chalinze
WANAFUNZI wawili wa kidato cha tatu waliokuwa wakisoma shule ya sekondari Msata wilayani Bagamoyo mkoani Pwani ambao mwanzoni mwa mwaka jana walilamikiwa na wanafunzi wenzao kuwa wanajihusisha na vitendo vya ushirikina shuleni hapo hali iliyosababisha washindwe kuendelea na masomo wako katika hatari ya kukatishwa masomo kufuatia taarifa kuwa mmoja kaozeshwa kwa mwanaume na mwingine yuko kwenye mipango ya kuolewa.
Wanafunzi hao ambao wanatoka kijiji cha Mkoko kata ya Msata wilayani humo  wanadaiwa kuwa wako kwenye hatua hizo baada ya wazazi wao na walezi kushindwa kuwafanyia uhamisho kwenda shule nyingine baada ya wanafunzi wenzao kuwakataa kutokana na madai hayo ya ushirikina.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi moja ya wakazi wa kijiji hicho ambaye hakutaka kutajwa jina lake kutajwa alisema kuwa mwanafunzi wa kwanza (17) anaishi na mwanaume baada ya baba yake kumwoza.
Alisema kuwa baba wa mwanafunzi huyo Damian Joseph alifikia hatua hiyo baada ya mwanae kugoma kuendelea kusoma kwenye shule hiyo na kutaka ahamishiwe shule nyingine kutokana na wenzake kumtuhumu kuwa ni mshirikina.
Baba wa mwanafunzi huyo Joseph alipoulizwa juu ya suala hilo alikanusha na kusema kuwa hajamwoza mwanaye na hana mpango wa kumwozesha kwa kuwa bado ni mwanafunzi ila tatizo lilikuwa ni uhamisho na kufiwa na mkewe.
Akielezea juu ya tatizo la mwanae alisema kuwa mwanawe alikuwa ni mnyonge na kukata tamaa ya kusoma kutokana na wanafunzi wenzake kumtuhumu kuwa ni mchaawi na anawaloga wanafunzi wenzake yeye na mwenzake ambao wanatoka Kijiji kimoja hivyo walishindwa kwenda shule na yeye alikataa kurudi shuleni vinginevyo ahamishiwe shule nyingine.
Joseph alisema kuwa jambo lililomfanya ashindwe kumhamisha mwanae ni kutokana na msiba wa mkewe uliomfanya achanganyikiwe hivyo kusimamisha taratibu za kumhamisha shule hata hivyo amesema kuwa atahakikisha mwanae anawekwenda shule.
Kwa upande wa mwanafunzi (17) ambaye alidaiwa yuko kwenye mchakato wa kutolewa mahari na mwanaume kaka wa mwanafunzi huyo Ramadhan Ndege alikanusha taarifa hizo na kusema kuwa mdogo wake yuko kwa bibi yake mzaa mama ambapo kwa sasa anazaidi ya miezi sita hajaenda shule kutokana na kuwa na matatizo ya mapepo.
Ndege alisema kuwa si kweli kuwa mdogo wake yuko kwenye mpango wa kuozeshwa ila yuko kwa bibi yake akipatiwa matibabu ambapo akienda shule hali inakuwa mbaya kutokana na mapepo kumsumbua.
“Changamoto nyingine ni kukosa fedha kwa ajili ya kumfanyia uhamisho kiasi cha shilingi 250,000 ambazo ni gharama zote kuanzia ufuatiliaji pamoja na sare, vitabu na vifaa vinavyotakiwa kwenye shule anayokwenda ya Changarikwa ambayo ni jirani na kijiji hicho,” alisema Ndege.
Alisema kuwa tatizo kubwa linalowasumbua ni ukosefu wa fedha kwani kipato chao ni kidogo na hawawezi kupata fedha hizo kwa mara moja na msaada ni mdogo kwani wazazi wao walishafariki nakuomba kama kuna wafadhili wanaoweza kuwasaidia wajitokeze ili kuwasaidia kumpeleka shule ndugu yao.
Kwa upande wake mwenyekiti wa Kijiji hicho Hamis Buzoza alisema kuwa mambo hayo yalikuwa yakifanywa kifamilia zaidi lakini masuala hayo hayajapelekwa ofisini kwake ila aliwataka wazazi wa familia hizo kutofanya hivyo kwani hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
Mwisho.   
  

WAFUGAJI WALIOINGIA KINYEMELA BAGAMOYO KUONDOLEWA


Na John Gagarini, Chalinze

 

WILAYA ya Bagamoyo imesema kuwa itawaondoa wafugaji wote walioingia kinyemela kwenye wilaya hiyo ili kuepusha migogoro ya wakulima na wafugaji.

 

Hayo yalisemwa na mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Hemed Mwanga, wakati akizungumza na wakazi wa Kijiji cha Kihangaiko wilayani humo.

 

Mwanga alisema kuwa kuna baadhi ya wafugaji wameingia kinyemela kwenye wilaya hiyo jambo ambalo ni kinyume cha taratibu.

 

“Tuna taarifa tunazo kuwa kuna baadhi ya wafugaji wanaingia kinyume cha taratibu hali ambayo inaweza kusababisha vurugu baina ya wakulima na wafugaji,” alisema Mwanga.

 

Alisema kuwa wafugaji wote walioingia kwa njia za panya wataondolewa kwani kila mahali kuna taratibu zake na kama walikuwa wanataka kuingia walipaswa kufuata taratibu.

 

“Wafugaji walioingia kinyume cha utaratibu wataondolewa na tumepata taarifa kuwa baadhi ya mgambo wamekuwa wakihusika kuwaingiza wafugaji hao kinyume cha utaratibu pale Mto Wami,” alisema Mwanga.

 

Aidha alisema kuwa wale wote wanaohusika kuwaingiza wafugaji hao kinyume cha utaratibu watashughulikiwa kwani wanataka kutoletea matatizo.

 

Mwisho.

WAOMBWA KULIPWA FIDIA UPANUZI WA BARABARA


Na John Gagarini, Chalinze

 

WAKAZI wa Kijiji cha Misani kata ya Kiwangwa wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wameiomba serikali kuibana kampuni Eco Energy kuwalipa fidia ya mali zao ili kupisha upanuzi wa barabara ya kuelekea kwenye mradi wa umwagiliaji.

 

Wakizungumza kwenye mkutano wa hadhara wa mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete ambapo wakazi wa Kijiji hicho walisema kuwa tathmini ya upanuzi huo haukuwashirikisha wananchi na utaathiri mali zao.

 

Mkazi wa Kijiji hicho aliyejitambulisha kwa jina la Ally Hemed alisema kuwa mradi huo ambao ni wa kampuni hiyo ambapo imeweka alama za kupita barabara hiyo na kusema kuwa hakutakuwa na fidia yoyote itakayotolewa kwa uharibifu wa mali zao.

 

“Wamekuja hapa kijijini na kuweka alama za kuonyesha barabara itapita wapi ambapo katika maeneo hayo kuna mali zetu zitaathiriwa ikiwa ni pamoja na nyumba, mazao ya nanasi, miti na vitu vingine ambapo tumeambiwa kuwa hatutalipwa chochote jambo ambalo tunaona kuwa hatutatendewa haki mara zoezi hilo litakapoanza,” alisema Hemed.

 

Alisema kuwa kutokana na kutolipwa wao hawako tayari kuruhusu greda la kuchonga barabara kupita kwenye maeneo yao hadi watakapolipwa fidia za mali zao.

 

“Hatuna tataizo na kuchongwa barabara yetu lakini tunachoomba tulipwe kwanza fidia ndipo upanuzi ufanyike kama unavyoona mananasi yetu karibu yatakomaa na nyumba zetu zinaonekana zipo kwenye eneo la upanuzi wao watulipe kwanza ndipo wafanye upanuzi huo,” alisema Hemed.

 

Kwa upande wake mgombea udiwani kata ya Kiwangwa Malota Kwaga alisema kuwa jambo hilo limekuwa ni kero kubwa kwa wakazi hao hivyo ni vema suala lao likaangaliwa kabla ya utekelezaji wake.

 

Kwaga alisema kuwa wananchi wametoa malalamiko yao kwa wahusika lakini hawajaonesha nia ya kutoa fidia kwa watu ambao wataathiriwa na zoezi hilo.

 

Naye Ridhiwani alisema kuwa wahusika hao wanapswa kulipa fidia kabla ya kutekeleza mradi huo kwani haipendezi watu kuharibiwa mali zao bila ya kulipwa fidia.

 

Ridhiwani alisema kuwa tayari amewasiliana na wahusika na kuwaambia kuwa walipe kwanza fidia kabla ya kuanza upanuzi huo wa barabara hiyo inayoelekea kwenye mradi huo.

 

 “Sheria haisemi hivyo lazima unapofanya suala la maendeleo kwenye ardhi lazima ulipe fidia kwenye maeneo ambayo unayaendeleza,” alisema Ridhiwani.

 

Aidha alisema kuwa jambo hilo ni la maendeleo lakini pia liangalie haki za wananchi ambao mali zao zitaathiriwa na maendeleo hayo hivyo kwa sasa hakutafanyika chochote hadi malipo yatakapofanyika.

 

Mwisho.

 

Sunday, October 18, 2015

HABARI MOTO MOTO ZA KAMPENI ZA UCHAGUZI UCHAGUZI JIMBO LA CHALINZE

Na John GagariniChalinze

MGOMBEA Ubunge Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCMRidhiwani Kikwete amekanusha kumtuma mgombea wa Chama Cha (SAUShaban Maulid kugombea Udiwani Kata ya Talawanda.

Akizungumza kwenye mikutano ya kampeni iliyofanyika kwenye Vijiji vya KisangaVundumu na Talawanda kwenye kata hiyo alisema kuwa yeye hajamtuma mtu huyo wala hajawahi kukutana naye.

Ridhiwani alisema kuwa yeye hawezi kumtuma mtu kwenda kugombea na kama ni kumtaka mtu basi angependekeza kutoka chama chake na si chama kingine kwani hakuna ushirikiano na vyama vingine.

“Huyo mtu kwanza na mshangaa kwani sijawahi kumuona wala sijawahi kukutana naye wala sijawahi kumtuma mtu namshangaa unajua wagombea wengine hawana sera hivyo wanatumia majina ya watu kujipatia umaarufu,” alisema Ridhiwani.

Alisema kuwa huo ni uzushi na wananchi hawapaswi kumsikiliza mtu huyo kwani chama chake hakina uhusiano na CCM wala na yeye na hajawahi hata kukutana naye.

“Achaneni na maneno ya kutuvuruga kwani kwa sasa sisi tunafanya kampeni ili kuhakikisha chama cehtu kinashinda kwenye nafasi zote ikiwemo UraisUbunge na Udiwani hivyo wasituvurge wakati huu wa kampeni kama hawana sera wakae pembeni,” alisema Ridhiwani.

Kwa upande wake meneja wa kampeni Jimbo la Chalinze Alhaj Amir Mkangata alisema kuwa anamshangaa mgombea huyo kwani hakuna muungano baina ya CCM na SAU kama ilivyo kwa muungano wa vyama vya upinzani vinavyounda UKAWA.

Alhaj Mkangata alisema kuwa wagombea kama hao hawana uwezo hivyo wanatafuta njia ya kujipenedekeza ili kuonyesha kuwa wametumwa kugombea.

“CCM haijaungana na chama kingine sasa mgombea huyo anavyojitapa kuwa ametumwa na CCM atuambie umoja huo unaitwaje atuambie hapa na tunamshangaa aache kabisa kutengeneza maneno ya uongo,” alisema Mkangata.

Kwa upande wake mgombea udiwani kata ya Talawanda Said Zikatimu alisema kuwa endapo atachaguliwa atahakikisha kuwa changamoto zilizopo kwenye kata hiyo zikiwemo za Afya, Elimu na Maji.

Mwisho.

Na John Gagarini, Chalinze

WAKULIMA na Wafugaji kwenye Kijiji cha Lulenge Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wametakiwa kuheshimiana ili kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza na kusababisha vurugu zinazopelekea kuvunja amani baina ya wananchi.

Hayo yalisemwa na mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete wakati wa mkutano wa kampeni kwenye kijiji cha Lulenge kata ya Ubena.

Ridhiwani alisema kuwa tatizo kubwa la migogoro linatokana na pande mbili hizo kutoheshimu mipaka yao kwani kuna baadhi ya maeneo yametengwa kwa jamii hizo mbili.

“Mnaweza kuepusha migogoro kwa kuheshimiana na kuheshimu mipaka iliyopo kwani kila mmoja akimweshimu mwenzake migogoro haitakuwepo na watu wataishi kwa Amani na upendo,” alisema Ridhiwani.

Alisema kuwa serikali inajitahidi kuhakikisha inaondoa migogoro ikiwa ni pamoja na kutenga maoeneo kwa ajili ya mipango ya matumizi bora ya ardhi wakulima na wafugaji kwa baadhi ya maeneo huku mengine yakiwa yanaandaliwa kufanywa hivyo.

“Nyie ni ndugu hakuna sababu ya kugombana na kuingia kwenye migogoro isiyokuwa ya lazima kwani mtashindwa kufanya shughuli za maendeleo kutokana na migogoro hiyo,” alisema Ridhiwani.

Naye mgombea udiwani kupitia chama hicho Nicholaus Myuwa alisema kuwa atatumia taaluma yake ya kuwa Mwanasheria kuikabili migogoro hiyo kwa kuziweka pamoja jamii hizo.
Myuwa alisema kuwa endapo atachaguliwa kuwa diwani watahakikisha changamoto za maji, zahanati na barabara zinatatuliwa kwa kuwashirikisha wananchi.

Mwisho.

Na John Gagarini, Chalinze

WANANCHI wa Jimbo la Chalinze wametakiwa kutowachagua wagombea wa vyama vya upinzani kwani wengi wao ni viongozi wa msimu ambao wanajitokeza nyakati za uchaguzi.

Hayo yalisemwa na meneja wa kampeni wa Jimbo hilo Alhaj Amir Mkangata wakati wa mikutano ya kampeni ya mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete kwenye kata ya Miono.

Alhaj Mkangata alisema kuwa chama chenye uwezo wa kuwaletea maendeleo wananchi ni CCM na vyama vingine viongozi wao hawana uwezo hivyo ni vema wakaendelea kukiamini chama.

“Msiwachague wapinzani kwani wengi wao wanajitokeza wakati wa uchaguzi lakini uchaguzi ukishaisha hawaonekani hivyo mkiwachagua hamtawapata kwani wengine hawajulikani hata wanapoishi lakini wa CCM wanafahamika na wanatambulika,” alisema Alhaj Mkangata.

Alisema kuwa CCM imechagua wagombea wenye uwezo na wanasifa za kuongoza lakini wagombea wa upinzani hawana uwezo wa kuongoza hivyo hakuna sababu ya kuwachagua.

“CCM imefanya kazi kubwa ya kuwaletea wananchi maendeleo hivyo hakuna sababu ya kuchagua chama kingine kutawala hivyo msihadaike na wapinzani ambao wanaongopa kuwa wataleta maendeleo msikubali kudanganyika,” alisema Alhaj Mkangata.

Aidha alisema kuwa kwa mwaka huu chama kimejipanga kuhakikisha kinapata ushindi wa kishindo ili kiweze kuongoza na kuleta maendeleo kwa wananchi.

Aliwataka wananchi kuichagua CCM kwani ina uwezo wa kuongoza na wagombea walioingia kwenye kinyanganyiro cha ugombea kwenye ngazi mbalimbali wana uwezo kwani wamechaguliwa kwa uwezo wao.

Mwisho.

Na John Gagarini, Chalinze

KIJIJI cha Lulenge kata ya Ubena Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo kinatarajia kuanza ujenzi wa zahanati Desemba mwaka huu ili kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa huduma za afya.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mwenyekiti wa Kijiji hicho Lucas Sultan alisema kuwa ujenzi huo utaanza baada ya kukamilika michango ya kila kaya.

Sultan alisema kuwa walikubaliana kwenye mkutano wa Kijiji kila kaya itoe kiasi cha shilingi 20,000 kwa ajili ya kujenga zahanati kwa ajili ya kuwapatia huduma ya afya.

“Tayari tuna eneo la ukubwa wa hekari tano kwa ajili ya kufanya ujenzi huo kwani ndani ya miezi michache ijayo tutakuwa tumekamilisha michango hiyo ili kuanza ujenzi,” alisema Sultan.

Alisema kuwa kwa kaya itakayoshindwa kutoa mchango huo atapaswa kufanya shughuli za kijamii kama sehemu ya mchango wake ili kila mtu atoe jasho lake kwenye kijiji.

Alisema kuwa kwa sasa wanapata huduma ya afya kwenye zahanati binafsi ambako ni mbali kwani usafiri uliopo ni wa pikipiki ambapo gharama yake ni shilingi 8,000 kwenda na kurudi.

“Gharama za kwenda kupata matibabu ni kubwa sana hivyo ndiyo maana tuliona kuwa kuna haja ya kweza kuanzisha ujenzi wa zahanati ili kukabiliana na changamoto hiyo,” alisema Sultan.

Aidha alisema kuwa changamoto nyingine ni kwamba sehemu kubwa ya kijiji iko kwenye hifadhi ya Wami Mbiki hivyo kushindwa kufanya shughuli za kimaendeleo.

“Suala la Kijiji kuwa kwenye hifadhi linafanyiwa kazi na tunaamini tutapata majibu mazuri na tunaamini mipaka itatengenezwa na tutaishi kwa utaratibu mzuri,” alisema Sultan.

Alisema kuwa Kijiji hicho kina jumla ya wakazi wapatao 2,700 huku kukiwa na mifugo mbalimbali ngombe wakiwa 17,000, mbuzi 4,000 na mbuzi 2,000 ambapo wakazi wake ni wakulima na wafugaji.

Mwisho.

Na John Gagarini, Chalinze

MGOMBEA Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete amesema kuwa endapo atafanikiwa kuwa mbunge atahakikisha anasimamia upelekwaji wa fedha pensheni za wazee kwa wakati.

Aliyasema hayo katika kijiji cha Tukamisasa kata ya Ubena na kusema kuwa wazee wanapaswa kuheshimiwa na kupewa stahiki zao kwani wamefanya kazi kubwa ya kuifanya nchi ifikie hapa ilipo.

Ridhiwani alisema kuwa kwa kuwa sera ya chama inaonyesha kuwa kuanzia mwaka 2016 wazee watakuwa wanapata pensheni zao kwa ajili ya kuwasaidia katika maisha yao.

“Wazee wetu wamefanya kazi kubwa hivyo kuna haja ya kuhakikisha wanapata stahiki zao kwani walifanya kazi kubwa kuikomboa nchi na kuifanya iwe kama ilivyo sasa moja ya vitu nitakavyovisimamia ni kuhakikisha fedha zao zinakuja kwa wakati,” alisema Ridhiwani.

Alisema kuwa wazee wanakabiliwa na changamoto nyingi hivyo wakipata pensheni zao zitawasaidia kuweza kujikimu na kumudu mambo madogomadogo tofauti na ilivyo sasa.

“Wazee wakilipwa pensheni zao zitawasaidia kumudu maisha yao kwani walikuwa wakiishi kwenye hali ngumu kutokana na kukosa fedha hata za kununua vitu vidogovidogo ambavyo vingewasaidia kumudu maisha,” alisema Ridhiwani.

Aidha wazee wamehudumia nchi ya Tanzania na kutumia nguvu zao na jasho lao hivyo ni haki yao sasa kupata pensheni ambayo itawafanya wajisaidie kwenye maisha yao.

“Mbali ya kusimamia malipo hayo pia nitahakikisha wanapata huduma mbalimbali ambao ni fursa kwao ikiwa ni pamoja na matibabu pamoja na mikopo ambayo itawasaidia kwenye ujasiriamali,” alisema Ridhiwani.

Mwisho.