Wednesday, October 7, 2015

WAOMBA KUONDOLEWA 100,000 KWA AJILI YA GARI LA WAGONJWA

Na John Gagarini, Chalinze
WAKAZI wa Kijiji cha Kwaruhombo Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo wametoa kilio chao kwa kuomba viongozi watakaochaguliwa kwenye uchaguzi mkuu kuwaondolea changamoto ya kutozwa kiasi cha shilingi 100,000 kwa ajili ya mafuta ya kuweka kwenye gari la wagonjwa wanaopata rufaa toka kwenye kituo cha afya cha Kwaruhombo.
Akizungumza Kijijini hapo mara baada ya mkutano wa kampeni wa mgombea ubunge jimbo hilo Ridhiwani Kikwete, Ally Rashid alisema kuwa hali hiyo inawapa wakati mgumu kutokana na hali halisi ya kipato chao kidogo.
Rashid alisema kuwa changamoto hiyo ni kubwa kwani wao kupata fedha hizo mzigo mkubwa ikizingatiwa maisha ya Kijijini ni magumu na hawana vyanzo vikubwa vya mapato zaidi ya kilimo ambacho nacho kimekuwa si cha uhakika kutokana na mvua kutokuwa za uhakika.
“Tunaomba viongozi watakaochaguliwa wahakikishe wanashughulikia kero hii kwani kwa sasa ni muda mrefu na tumekuwa tukilalamika lakini hakuna hatua zinazochukuliwa pia tunaomba Halmashauri itenge bajeti kwa ajili ya mafuta ya gari hilo la wagonjwa,” alisema Rashid.
Naye mgombea Udiwani wa kata ya Kwaruhombo ramadhan mahamba alisema kuwa kero hiyo ni kubwa kwa wanakijiji na kumwomba mgombea huyo wa ubunge kuhakikisha nawasemea huko halmashauri ili gari hilo liwe na bajeti ya mafuta.
Mahamba alisema kuwa mbali ya kero hiyo ya wananchi kutakiwa kutoa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kuwekea mafuta ya kuwasafirisha wagonjwa wanapopata rufaa kwenda hospitali kubwa pia kuna tatizo la upungufu wa wahuduma wa afya.
Kwa upande wake Ridhiwani Kikwete alisema kuwa kero hiyo ameisikia na mara atakapochaguliwa atahakikisha anashinikiza kutenga fedha za mafuta kwa ajili ya vituo vya afya ili kuwaondolea mzigo wananchi.
Ridhiwani alisema kuwa utaratibu umewekwa na Halmashauri wa bajeti ya mafuta ya magari hayo hivyo akichaguliwa hiyo ni moja ya vitu atakavyovifuatilia kwa karibu ili kuhakikisha mafuta yanapatikana kwenye gari hilo.
Mwisho.
NA John Gagarini, Chalinze
KIJIJI ch Kwaruhombo Jimbo la Chalinze wilayani Bagamoyo kinakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maji hali inayowafanya wakazi wake kuchota maji ya visima vya kienyeji ambavyo viko chini ya ardhi huku vingine vikiwa na urefu wa futi 12.
Mbali ya visima hivyo kuwa na urefu mkubwa ambapo huwabidi wachotaji wengi wao wakiwa ni wakinamama kushuka kwa kutumia ngazi pia kumekuwa na foleni kubw ahali ambayo inawafanya wakeshe wakisubiri maji ambayo yamekauka kutokana na hali ya kiangazi.
Moja ya wanakijiji aliyejitambulisha kwa jina la Hadija Yusufu alisema kuwa maji ni changamoto kubwa kwao kwani wamekuwa wakitumia muda mrefu wa kusubiria maji hasa kipindi hichi cha kiangazi pia ni hatari kwa maisha yao kutokana na urefu wa visima hivyo.
“Tunaiomba serikali kutusaidia kupatikana maji ili kutuondolea adha hii kwani tumeletewa maji ambapo kuna vioski kwa ajili ya kuchota maji lakini havitoi maji hatujui kuna tatizo gani linalosababisha maji yasitoke hivyo tumebaki tunategemea maji ya visima hivyo vya kienyeji ambavyo navyo ni hatari kweteu,” alisema Yusufu.
Kwa upande wake mgombea udiwani kwa tiketi ya CCM Ramadhan Mahamba alisema kuwa endapo atachaguliwa atahakikisha anafuatilia suala hilo ili maji yaweze kupatikana kwa kutatua changamoto iliyopo ili maji yapatikane na kuwaondolea kero wananchi.
Naye mgombe ubunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete alisema kuwa tatizo la ukosefu wa maji ni kutokana na miundombinu iliyowekwa kuwa ya zamani hivyo kushindwa kuhimili kasi ya maji na kupasuka.
Ridhiwani alisema kuwa endapo atachaguliwa atahakikisha miundombinu mipya ambayo ni mabomba inapatikana ili kuondoa kero hiyo inayowanyima usingizi wananchi hao ambao hicho ni kilio chao kikubwa.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment