Monday, October 19, 2015

WAOMBWA KULIPWA FIDIA UPANUZI WA BARABARA


Na John Gagarini, Chalinze

 

WAKAZI wa Kijiji cha Misani kata ya Kiwangwa wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wameiomba serikali kuibana kampuni Eco Energy kuwalipa fidia ya mali zao ili kupisha upanuzi wa barabara ya kuelekea kwenye mradi wa umwagiliaji.

 

Wakizungumza kwenye mkutano wa hadhara wa mgombea Ubunge Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ridhiwani Kikwete ambapo wakazi wa Kijiji hicho walisema kuwa tathmini ya upanuzi huo haukuwashirikisha wananchi na utaathiri mali zao.

 

Mkazi wa Kijiji hicho aliyejitambulisha kwa jina la Ally Hemed alisema kuwa mradi huo ambao ni wa kampuni hiyo ambapo imeweka alama za kupita barabara hiyo na kusema kuwa hakutakuwa na fidia yoyote itakayotolewa kwa uharibifu wa mali zao.

 

“Wamekuja hapa kijijini na kuweka alama za kuonyesha barabara itapita wapi ambapo katika maeneo hayo kuna mali zetu zitaathiriwa ikiwa ni pamoja na nyumba, mazao ya nanasi, miti na vitu vingine ambapo tumeambiwa kuwa hatutalipwa chochote jambo ambalo tunaona kuwa hatutatendewa haki mara zoezi hilo litakapoanza,” alisema Hemed.

 

Alisema kuwa kutokana na kutolipwa wao hawako tayari kuruhusu greda la kuchonga barabara kupita kwenye maeneo yao hadi watakapolipwa fidia za mali zao.

 

“Hatuna tataizo na kuchongwa barabara yetu lakini tunachoomba tulipwe kwanza fidia ndipo upanuzi ufanyike kama unavyoona mananasi yetu karibu yatakomaa na nyumba zetu zinaonekana zipo kwenye eneo la upanuzi wao watulipe kwanza ndipo wafanye upanuzi huo,” alisema Hemed.

 

Kwa upande wake mgombea udiwani kata ya Kiwangwa Malota Kwaga alisema kuwa jambo hilo limekuwa ni kero kubwa kwa wakazi hao hivyo ni vema suala lao likaangaliwa kabla ya utekelezaji wake.

 

Kwaga alisema kuwa wananchi wametoa malalamiko yao kwa wahusika lakini hawajaonesha nia ya kutoa fidia kwa watu ambao wataathiriwa na zoezi hilo.

 

Naye Ridhiwani alisema kuwa wahusika hao wanapswa kulipa fidia kabla ya kutekeleza mradi huo kwani haipendezi watu kuharibiwa mali zao bila ya kulipwa fidia.

 

Ridhiwani alisema kuwa tayari amewasiliana na wahusika na kuwaambia kuwa walipe kwanza fidia kabla ya kuanza upanuzi huo wa barabara hiyo inayoelekea kwenye mradi huo.

 

 “Sheria haisemi hivyo lazima unapofanya suala la maendeleo kwenye ardhi lazima ulipe fidia kwenye maeneo ambayo unayaendeleza,” alisema Ridhiwani.

 

Aidha alisema kuwa jambo hilo ni la maendeleo lakini pia liangalie haki za wananchi ambao mali zao zitaathiriwa na maendeleo hayo hivyo kwa sasa hakutafanyika chochote hadi malipo yatakapofanyika.

 

Mwisho.

 

No comments:

Post a Comment