Wednesday, July 22, 2015

POLISI PWANI WAKAMATA SILAHA WALIZOPORWA POLISI NA HABARI MBALIMBALI

Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la Polisi mkoani Pwani limefanikiwa kukamata silaha aina ya Sb Mchine Gun (SMG) ikiwa na risasi 30 kwenye magazini ambayo majambazi waliwapora askari eneo la Yombo Jijini Dar es Salaam Aprili 15 mwaka huu.

Mbali ya silaha hiyo pia walikamata silaha nyinge mbalimbali zikiwemo bunduki nne, risasi 153, mabomu na nyaya za milipuko katika msako maalumu wa kusaka wahalifu wanaodaiwa kuhusika katika matukio kadhaa yakiwemo ya uvamizi wa vituo vya Polisi na taasisi za fedha Mkoani humo na mikoa jirani ukiwemo wa Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa kamanda wa polisi mkoani humo Jafari Ibrahim alisema silaha hiyo iliporwa na majambazi hayo kutoka mikononi mwa polisi waliokuwa doria kisha kutoweka nayo ambayo ilikuwa ni ya kituo cha polisi cha Tazara.

Kamanda Ibrahimu alisema kuwa silaha hiyo ilikuwa na namba 14302621 pia silaha nyingine iliyokamatwa ni Short Gun yenye namba G 74533 ambayo iliporwa Juni 10 mwaka huu kwenye kituo cha mafuta cha Mogas kilichopo Mkata wilaya ya Handeni mkoani Pwani.

“Kukamatwa silaha hizi ni mafanikio ya operesheni iliyofanywa na jeshi katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita na tunawapongeza wananchi kwa ushirikiano waliouonyesha uliofanikisha kukamatwa kwa silaha hizi na vitu vingine,” alisema Ibrahim

Alisema kuwa mbali ya silaha zilizotajwa hapo juu pia waliweza kukamata silaha nyingine ambazo ni Visu 11,Mapanga 4,Majambia 3,Risasi 20 za SMG, Risasi 103 za Shortgun, Milipuko ya mabomu 3,Vipande vidogo vya nondo 42,fyuzi zilizotegwa 24,Fyuzi tupu 56,Water Gel Explosive 3, Silicon Rubber 100% moja, Nyaya 3 za Milipuko, Bunduki 2 zilizotengezwa kienyeji pamoja na bunduki moja aina ya Rifle.

"Sihala hizi zote zipo hapa kwetu na kwa kweli ndugu waandishi kama silaha zingeendelea kuwa mikononi mwa wahalifu ni wazi kuwa madhara kwa mali na maisha yetu yangekuwa hatarini,ninyi kama wadau muhimu katika jitihada za kupambana na wahalifu kupitia vyombo vya habari mnao wajibu wa kuendelea kuelimisha jamii kuendelea kushirikiana na jeshi la Polisi katika mapambano haya yanayohitaji nguvu ya pamoja,” alisema Ibrahim

Aidha alisema kuwa ni wazi kuwa mafanikio haya yametokana na jamii kutoa ushirikiano mkubwa kwa polisi katika kuwabaini wahalifu,kubaini matishio ya kiusalama na maficho ya magenge ya kihalifu kwenye mapori mbalimbali yaliyopo mkoani Pwani.

Alibainisha kuwa mbali ya kukamata silaha hizo pia wamekamata wahalifu 27 wanaotuhumiwa kuhusika katika matukio mbalimbali ikiwemo la uporaji silaha kituo cha polisi Yombo Dar es Salaam na waliohusika kwenye uporaji taasisi za kifedha  na taratibu za kuwafikisha mahakamani zimekamilika.

Mwisho
Na John Gagarini, Kibaha
HUKU mchakamchaka wa kuwania nafasi za ubunge na udiwani zikiwa zinaendelea nchini jumla ya wagombea wanne kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM)Jimbo la Kibaha Mjini watachuana kupata mgombea mmoja atakayepeperusha bendera ya chama hicho kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
Kwa mujibu wa katibu wa CCM Kibaha Mjini Abdala Mdimu alisema kuwa wagombea hao ndani ya chama ndiyo waliorejesha fomu za kuomba ridhaa ya kuchaguliwa na Wanaccm ili kugombea nafasi hiyo.
Mdimu alisema kati ya wagombea hao waliorejesha fomu ni pamoja na aliyekuwa mbunge wa Jimbo hilo Silvestry Koka ambaye atachuana na wanaccm wengine watatu ambao nao wameomba kuwania nafasi hiyo.
Aliwataja wagombea wengine kwenye kinyanganyiro hicho kuwa ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu CCM Taifa NEC Jimbo hilo Rugemalila Rutatina, Idd Majuto, Rashid Bagdela na Abdulaziz Jaab.
Katika Jimbo la Kibaha Vijijini jumla ya wagombea sita wamejitokeza kuwania nafasi hiyo akiwemo aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini Dk Ibrahim Msabaha watakaopambana na Mbunge wa Jimbo hilo Hamoud Jumaa.
Katibu wa CCM Kibaha Vijijini alisema kuwa wengine wanaowania nafasi hiyo ndani ya chama ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa NEC Jimbo hilo Allen Bureta, Hussein Chuma, Janeth Munguatosha na Shomary Sangali.
Mwisho.
Na John Gagarini, Bagamoyo
JUMLA ya wagombe 10 wa nafasi ya Ubunge wamerejesha fomu za kuwania kuchaguliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwenye Jimbo la Bagamoyo Mkoani Pwani ambalo nafasi yake inatetewa na Waziri wa Elimu na Mafunzo Dk Shukuru Kawambwa.
Kwa mujibu wa katibu wa CCM wilaya ya Bagamoyo Kombo Kamote alisema kuwa wengine waliorejesha fomu ni pamoja na Meya wa Mji Mdogo wa Bagamoyo Abdul Sharifu.
Kamote aliwataja wengine kuwa ni Muharami Mkenge, Salim Abeid, Mbonde Mbonde, Methew Yungwe, Maulid Mtulya, Fabian Said, Lekesani, Mvule na Chacha Wambura.
Katika Jimbo la Chalinze mbunge wa Jimbo hilo Ridhiwani Kikwete anatarajiwa kupambana na aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga Iman Madega.
Wengine ni pamoja na Mbaraka Tamimu, Changwa Mkwezu, Omar Kabanga. Katika hatua nyingine  jumla ya wagombea 18 wa ubunge viti maalum mkoani Pwani watawania kuchaguliwa bada ya kurejesha fomu za kuwania nafasi hiyo ndani ya chama.
Mwisho.
Na John Gagarini, Iringa
WAFADHILI toka nchi ya Australia wametoa fedha zaidi ya shilingi bilioni 11 kuchangia mradi mkubwa wa maji kwenye Jimbo la Mufindi Kaskazini wilayani Mufindi mkoani Iringa.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Mafinga Mbunge wa Jimbo hilo Mahmoud Mgimwa alisema kuwa wafadhili hao wametoa fedha hizo ili kukabiliana na changamoto za maji kwenye Jimbo hilo.
Mgimwa ambaye pia ni Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii alisema kuwa fedha hizo zitatumika kwenye mradi mkubwa ambao utaondoa kabisa tatizo la maji kwenye Jimbo hilo.
“Mradi huu ni mkubwa na utaondoa kabisa changamoto hii ya maji kwani baadhi ya maeneo hayapati maji lakini mara utakapokamilika utakabili tatizo hilo na kubaki historia kwani maeneo yote yatapata maji ya uhakika,” alisema Mgimwa.
Alisema kuwa huku wafadhili hao wakitoa fedha hizo serikali nayo itachangia kiasi cha shilingi milioni 130 ambapo wafadhili hao watakuja na kuangalia mradi huo jinsi utakavyoendeshwa.
“Katika bajeti ya mwaka 2014/2015 serikali ilitoa kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kununua pampu tatu kutoka nchini Afrika Kusini na Arusha ambazo zitafanya maji yaweze kutoka kwa uhakika ambapo kwa sasa utokaji wake si mzuri kutokana na uchakavu wa miundombinu yake zikiwemo pampu hizo,” alisema Mgimwa.
Aidha alisema kuwa katika bajeti ya mwaka 2015/2016 serikali imetoa shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya maji ili kukabiliana na uchakavu.
Mwisho.
Na John Gagarini, Iringa
MBUNGE wa Jimbo la Mufindi Kaskazini na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mamhoud Mgimwa amewaomba wadau mbalimbali wa maendeleo kusaidia kupatikana kwa vifaa vya X-Ray kwenye hospitali ya Mafinga ambayo ni ya Wilaya ya Mufindi ili iweze kutoa huduma zake kwa uhakika.
Mgimwa alisema kuwa hospitali hiyo ambayo imeboreshwa na kuwa ya kisasa kupita hospitali zote za mkoa wa Iringa inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa vifaa hivyo.
Alisema kuwa Mgimwa yeye pamoja na wananchi wa Jimbo hilo pamoja na serikali wamefanikiwa kuifanya hospitali hiyo kuwa ya kisasa na kutoa huduma bora lakini changamoto yake ni X-Ray.
“Tunaishukuru serikali kwani ilitoa kiasi cha shilingi milioni 600 ambazo zilitumika kufanya kazi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kujenga wodi nzuri hivyo tunaomba wadau mbalimbali waendelee kujitokeza kuisaidia kukabilina na changamoto zilizopo,” alisema Mgimwa.
Aidha alisema kwa sasa hospitali hiyo ina jumla ya vitenda 10 vya kujifungulia akinamama ambapo kila kitanda kina thamani ya shilingi milioni 1.2.
“Kwa jumla huduma ya afya kwenye hospitali yetu ya wilaya ni nzuri licha ya kwamba kuna changamoto kidogo lakini hata hivyo tunaendelea kukabiliana nazo ili ziweze kuboreka,” alisema Mgimwa.
Alibainisha kuwa kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo watazikabili changamoto zilizopo ili wananchi waweze kupata huduma bora mara waendapo kupata huduma.

Mwisho.  

No comments:

Post a Comment