Monday, July 20, 2015

NAIBU WAZIRI ATOA MSAADA WA BATI NA SIMENTI KWA SHULE

Na John Gagarini, Iringa

KATIKA kukabiliana na changamoto za ukosefu wa nyumba za walimu Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini wilayani Mufindi mkoani Iringa Mahamoud Mgimwa ametoa bati 70 na mifuko 30 ya Saruji kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu wa shule ya Msingi ya Mpanga Tazara.
Akizungumza na wakazi wa Kijiji hicho alipotembelea kuangalia shughuli za maendeleo alisema kuwa ameamua kutoa vifaa hivyo ili kuhakikisha wlaimu wanakaa kwenye mazingira mazuri.
Mgimwa ambaye ni Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii alisema kuwa wananchi wa Kijiji hicho walikuwa na kilio cha muda mrefu cha walimu kukosa nyumba za kuishi hivyo ameona ni vema akatoa vifaa hivyo ili viweze kusaidia katika ujenzi wa nyumba za walimu.
“Kama mnavyojua mazingira ya huku yako pembezoni hivyo lazima kuyaweka vizuri ili watumishi hao waweze kukaa sehemu ambayo ni nzuri ili waweze kufanya kazi zao kwa amani,” alisema Mgimwa.
Alisema kuwa sekta ya elimu ina changamoto nyingi lakini yeye kwa kushirikiana na wananchi atahakikisha wanazikabili kwa kutoa misaada mbalimbali ili kuboresha mazingira ya usomaji.
“Awali shule hii ilikuwa na tatizo la choo lakini tulipigana na kuhakikisha choo kimejengwa tunakwenda kutatua changamoto zilizopo hatua kwa hatua ili kuhakikisha sekta ya elimu inapata mafanikio,” alisema Mgimwa.
Aidha alisema kuwa wazazi nao wanapaswa kuhakikisha wanachangia michango mbalimbali kwa ajili ya wanafunzi ili waweze kupata elimu inayotakiwa kwani kuna baadhi ya changamoto zinaweza kutatuliwa na wazazi.
Kwa upande wake Diwani wa kata ya Mpanga Tazara Flavian Mpanda alimshukuru mbunge huyo kwa kutoa vifaa hivyo na kusema kuwa vimekuja wakati muafaka kwani ujenzi wa nyumba za walimu ilikuwa ni changamoto kubwa.
Mpanda alisema jitihada zinazofanywa na mbunge huyo kuhakikisha shule hiyo inakuwa na mazingira mazuri zinapaswa kupongezwa na wapenda maendeleo.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment