Wednesday, May 21, 2014

MKOA WA PWANI WAINGIA MIKATABA NA WAKUU WA WILAYA



Na John Gagarini, Kibaha
MKOA wa Pwani umeingia umeingia mkataba na wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa halmashauri na wenyeviti wa halmashauri juu ya utekelezaji wa mpango wa kupunguza vifo vya mama wajawazito watoto wachanga na wale wenye umri chini ya miaka mitano.
Pia mkoa umeingia na viongozi hao kwenye mkataba kwa ajili ya makusanyo ya mapato ambayo waliyapitisha kuwa wana uwezo wa kuyakusanya  kwenye halmashauri za wilaya saba za mkoa huo katika kipindi cha bajeti ya mwaka 2014-2015.
Tukio hilo la kihistoria la kusaini mikataba hiyo ya kazi kwa viongozi hao ndani ya mkoa wa Pwani lilifanyika juzi mjini Kibaha na lilisimamiwa na mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza na mwanasheria  wa mkoa Mohamed Magati ambapo viongozi hao endapo watashindwa kufikia malengo yaliyowekwa itawabidi kujieleza.
Wakuu wa wilaya ambao waliingia mikataba hiyo na wilaya zao ni pamoja na Mercy Silla wilaya ya Mkuranga, Fatuma Kimariyo Kisarawe, Nurdin Babu Rufiji, Sauda Mtondoo wilaya ya Mafia, Ahmed Kipozi wilaya ya Bagamoyo  na Halima Kihemba wilaya ya Kibaha.
Akizungumza na watendaji hao kuhusiana na mikata hiyo walioingia na mkoa Mahiza alisema kuwa mikataba hiyo itasaidia uwajibikaji kwa watendaji hao ambao wanawatumikia wananchi katika kuwaletea maendeleo.
“Mikataba hii ni changamoto kwa watendaji wetu hawa na endapo watashindwa kutekeleza majukumu yao kama mkataba unavyoonyesha itabidi wajieleze kwani hata mimi nishaingia mikataba na mamlaka za juu hivyo kila mtu lazima atimize wajibu wake,” alisema Mahiza.
Mahiza alisema kuwa kwa upande wa vifo vya mama wajawazito, watoto wa changa na wale wenye umri chini ya miaka mitano ni tatizo kubwa hivyo mkataba huo utasaidia kupunguza vifo hivyo visivyo vya lazima.
“Kwa upande wa makusanyo kila halmashauri ilileta makadirio yake ya kukusanya mapato kwenye bajeti ya mwaka 2014- 2015 hivyo ni lazima watimize kusudio lao na hakuna sababu ya kusema wameshindwa kuyafikia malengo hayo ya ukusanyaji wa mapato,” alisema Mahiza.
Halmashauri hizo kila moja imejiwekea kiwango chake cha kukusanya kutegemeana na vyanzo vyake vya mapato ambapo Bagamoyo watakusanya bilioni2.6, Kibaha Mjini, bilioni 4.2, Kibaha Vijijini bilioni 2.6, Kisarawe bilioni 3.8, Mafia bilioni 1, Mkuranga bilioni 2.1 na Rufiji bilioni 2.7 ambapo jumla ya makusanyo hayo kwa wilaya zote za mkoa huo itakuwa ni bilioni 8.7
Naye mganga mkuu wa mkoa wa Singida ambaye alishinda tuzo ya Rais ya kupunguza vifo vya makundi hayo Dk Doroth Gwajima alisema kuwa vifo vingi vinatokana na uzembe wa baadhi ya watumishi wasio na maadili ya kazi.
 Dk Gwajima aliwataka wahudumu wa afya kwenye mkoa huo wa Pwani kumtanguliza Mungu wakati wa utendaji wao wa kazi pia kuzingatia maadili ya kazi zao kwani baadhi ya vifo vinatokana na uzembe na si mapenzi ya Mungu. 
Mwisho.

  
  

No comments:

Post a Comment