Thursday, May 29, 2014

BILALI KUZINDUA MFUKO WA ELIMU KIBAHA MEI 31



Na John Gagarini, Kibaha
MFUKO wa elimu wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha mkoani Pwani utazinduliwa Mei 31 mwaka huu ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Gharib Bilali.
Kwenye uzinduzi huo ambao utafanyika mjini Kibaha mgeni rasmi ataongoza matembezi ya hisani kwa ajili ya kuhamasisha uchangiaji wa mfuko huo ambao una lengo la kupata kiasi cha shilingi milioni 300.
Akielezea juu ya tukio hilo mwenyekiti wa mfuko huo Anna Bayi alisema kuwa  katika uzinduzi huo kutatanguliwa na matembezi ya hisani yatakayoanzia maeneo ya Mkoani hadi viwanja vya Maili Moja ambapo ndipo halfa itafanyika.
Bayi alisema kuwa  hadi sasa tayari wameshapata kiasi cha shilingi milioni 180 zitakazosaidia kuiwezesha halmashauri hiyo kukabiliana na changamoto za sekta ya elimu hususan madawati na maabara.
"Mara zitakapopatikana fedha hizo tutaanzia kununulia madawati 1,500 yenye thamani ya shilingi milioni 90 na kujenga maabara tatu kwa shilingi Milion 210,” alisema Bayi.
Alisema uchangiaji huo utakuwa ni zoezi endelevu ili kuhakikisha wanapunguza ama kumaliza kabisa changamoto za kielimu katika halmashauri ya Mji wa Kibaha.
“Kila mwananchi anatakiwa kuchangia kiasi cha shilingi 2,000 wakiwemo  ,wafanyabiashara, wamiliki wa makampuni na wadau wa elimu na hadi sasa mwamko unaonekana kwa wananchi hivyo kuwa na imani ya kuwa mfuko utafanikiwa,” alisema Bayi.
Kwa upande wake  Mkurugenzi wa Halmshauri hiyo, Jeniffer Omolo alisema mfuko huo umeundwa chini ya sheria namba 288 kifungu kidogo namba 80 katika tangazo la serikali namba 218 la tarehe 18 Juni 2010.
“Shule za msingi na sekondari za serikali bado zinakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo zinafanya lengo la utoaji elimu bora kushindwa kufikiwa kikamilifu,” alisema Omolo.
Alibainisha kuwa Shule za msingi zilizopo wilayani Kibaha Mji  zinakabiliwa na uhaba wa madawati 3,488 hali inayopelekea baadhi ya shule hizo wanafunzi kutumia kukaa zaidi ya watatu kwenye dawati moja.
Aidha alisema katika upande wa shule za sekondari kuna upungufu wa maabara 24 ambapo kwa sasa kuna maabara 9 pekee, Halmashauri ya mji wa Kibaha ina jumla ya shule za msingi 47 na shule za sekondari za serikali na binafsi 34 .
Mwisho.

No comments:

Post a Comment