Wednesday, May 21, 2014

MAHIZA APINGA MFUKO WA WENYEVITI WA HALMASHAURI



Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza amezuia bajeti ya fedha iliyokuwa inatengwa kwa ajili ya wenyeviti wa halmashauri za wilaya badala yake fedha hizo zitumike kwenye miradi ya maendeleo ya wananchi.
Fedha hizo ambazo zimekuwa zikitengwa kwenye bajeti za kila mwaka za halmashauri bado hazijaonyeshwa kuwa zinatengwa kwa kanuni gani tofauti na fedha nyingine ndani ya halmashauri.
Akizungumza na wakuu wa wilaya, wenyeviti wa halmashauri, maofisa mipango na waweka hazina wa halmashauri za mkoa huo Mahiza alisema kuwa fedha hizo ni nyingi kwani baadhi ya wenyeviti wamekuwa wakitengewa hadi milioni 11 kw akila bajeti.
Mahiza alifikia kutoa agizo hilo baada ya baadhi ya halmashauri kusema kuwa zimetenga fedha hizo kwa ajili ya wenyeviti wa halmashauri kwa ajili ya matumizi ambayo hayakuwekwa bayana.
“Natoa agizo kuwa mfuko huo wa fedha kwa ajili ya mwenyekiti uondolewe hadi mtakapotoa mwongozo wa mfuko kwani mifuko yote ikiwemo ile ya Jimbo ya Mbunge ipo kisheria na inatambulika je huu umewekwa kwa kufuata sheria ipi,” alisema Mahiza.
Alisema kuwa hana nia mbaya juu ya kuzuia mfuko huo lakini anachotaka ni mwongozo ambao unaelekeza kuwepo kwa fedha hizo ambapo wakurugenzi walishindwa kuonyesha ni sheria gani wanayoitumia kutenga fedha hizo.
“Hadi sasa hakuna anayejua fedha hizi zinatengwa kwa kufuata utaratibu au mwongozo upi hivyo naomba ofisa wa serikali za Mitaa anipatie mwongozo ili mfuko uo uendelee na kama hakuna mwongozo wowote basi fedha ziende kwenye miradi ya maendeleo,” alisema Mahiza.
Aidha alisema hata wakuu wa wilaya hawana fedha kama hizo ambapo wao fedha zao hazizidi zaidi ya milioni tano jambo ambalo liliwashitua watu wengi waliposikia kuhusu mfuko huo wa wenyeviti wa halmashauri.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
ILI kuleta ufanisi wa utendaji kazi kwa wauguzi mkoa wa Pwani utawapatia kiasi cha shilingi 1,000 kwa muuguzi atakayezailisha mama wajawazito kwa usalama.
Pia vituo vya afya na zahanati zinatakiwa kufanya kazi kwa saa 24 ili kuhakikisha wagonjwa wanapata matibabu kwa muda wote tofauti na ili sasa ambapo wahudumu wa afya wanafunga muda wa kazi saa 9:30.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mkuu wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza wakati wa kikao cha kazi ambacho kiliambatana na uingiwaji wa mikataba baina ya wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri za mkoa huo juu ya utendaji kazi kwenye sekta ya afya na makusanyo kwenye bajeti ya mwaka 2014- 2015.
Mahiza alisema kuwa mpango wa kuwapa fedha wauguzi wanaowazalisha mama wajawazito salama ni kuwapa hamasa ili waweze kufanya vizuri katika kuwahudumia akinamama hao.
“Kwa kuwa tayari tumeshaingia mkataba na wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri kwa ajili ya kupunguza vifo vya mama wajawazito, watoto wachanga na watoto wenye umri chini ya miaka mitano lazima tuwape motisha watendaji wa sekta ya afya ili wafanye kazi kwa moyo,” alisema Mahiza.
Aidha Mahiza alisema kuwa kuanzia sasa vituo vya afya na zahanati vifanye kazi kwa saa 24 ili kuweza kufikia malengo ya kupunguza vifo hivyo pamoja na utoaji huduma kwa muda wote kwani ugonjwa hauna saa.



  

No comments:

Post a Comment