Tuesday, July 23, 2013

MAOFISA MIFUGO WAWE WAZALENDO

Na John Gagarini, Kibaha
 MAOFISA  wa serikali kwenye Idara ya Mifugo wametakiwa kutumia uzalendo wakati wa kuingiza madawa ili kuepuka kuingizwa madawa yasiyo na viwango.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mwakilishi wa kitaifa wa kampuni ya  Laprovet ya nchini Ufaransa Ephrahim Massawe alipoongea na waandishi wa habari na kusema kuwa baadhi ya maofisa hao wamekuwa wakiingiza madawa yasiyo na viwango.
Massawe alisema kuwa kutokana na kuagizwa madawa yasiyo na viwango kumesababisha madhara makubwa kwa mifugo ikiwa ni pamoja na kufa hivyo wafugaji kupata hasara kubwa.
“Kufa kwa mifugo kunatokana na magonjwa mbalimbali hapa nchini kunatokana na baadhi ya madawa kuwa kwenye kiwango cha chini hivyo kushindwa kuzuia au kutibu magonjwa yanayokabili mifugo,” alisema Massawe.
Aidha alisema kuwa tatizo kubwa ni ubadhirifu na kutokuwa na uadilifu kwa maofisa hao hali ambayo inasababisha mifugo mingi kufa kwa kupata matibabua ambayo hayalingani na uwezo madawa hayo toka nje ya nchi.
“Maofisa hao baadhi yao si waaminifu kwa kuingiza madawa ambayo hayana viwango licha ya kuwa madawa mazuri yapo hasa baada ya kuingia soko huria, hivyo wasiangalie maslahi binafsi bali waangalie utu na uzalendo kwa nchi yao,” alisema Massawe.
Massawe ambaye pia ni makamu mwenyekiti wa waganga wasaidizi wa mifugo nchini (TAVEPA) alisema kuwa endapo maofisa hao watakuwa waadilifu watasaidia kuboresha kipato cha wafugaji.
Alibainisha kuwa ili kuhakikisha wafugaji wanajua matumizi sahihi kampuni hiyo inatoa mafunzo pamoja na ushauri wa namna ya ufugaji wa kisasa ili kuongeza tija kwani ufugaji ni mkombozi wa nchi kwani inaliingizia pato kubwa la Taifa.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WILAYA ya Bagamoyo mkoani Pwani imeanza mkakati wa kukabiliana na uchafu kwenye Mji huo mkongwe hapa nchini kwa viongozi kushiriki kwenye zoezi la usafi kila mwanzo wa mwezi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mkuu wa wilaya hiyo Ahmed Kipozi alisema kuwa mkakati huo una lengo la kuwapa hamasa wananchi kuwa na utamaduni wa kufanya usafi.
Kipozi alisema kuwa tayari mkakati huo umeshaanza kwa viongozi wa wilaya, halmashauri, kata, mitaa na wananchi kufanya usafi kwenye mji huo pamoja na maeneo wanayoishi.
“Usafi bado ni changamoto kubwa kwa wakazi wa Bagamoyo lakini tunajaribu kuwaelimisha wananchi kuona umuhimu wa kusafisha mazingira yao yanayowazunguka na tumeshaanza kuona mabadiliko na mji umeanza kupendeza,” alisema Kipozi.
Alisema kuwa pia wanakabiliwa na ukosefu wa vifaa vya kuhifadhia takataka kwenye maeneo mbalimbali ya mji huo lakini watahakikisha kuwa wanaweka vifaa hivyo ili wananchi wasikose sehemu ya kuhifadhia uchafu.
“Kikubwa tunachoomba ni ushirikiano kwa wananchi ili kuweza kufanikisha usafi kwenye mji wetu ambao ni wa kihistoria na unabeba historia kubwa ya nchi hii hivyo lazima uendane na hali hiyo kwa kuwa kwenye hali ya usafi,” alisema Kipozi.
Alisema kuwa kwa kuwa mji huo tayari umepewa hadhi ya kuwa mji mdogo hivyo lazima usafi uzingatiwe na watatumia sheria ndogondogo za mji ili kukabiliana na wale wote ambao watakuwa wanakwenda kinyume na kanuni za usafai.
Mwisho.      

No comments:

Post a Comment