Thursday, July 18, 2013

DC ANAWA MIKONO MGOGORO WA SHAMBA


Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Halima Kihemba amewataka wananchi kwenye eneo lenye mgogoro wa ardhi uliopo kwenye mtaa wa Mtakuja kulimaliza suala hilo na mmiliki wa eneo hilo kwani yeye hawezi kulitolea maamuzi eneo la mtu ambaye ana hati miliki.
Aliyasema hayo jana kwenye mtaa huo ambako baaadhi ya wananchi kuingia kwenye eneo hilo lenye ukubwa wa hekari zaidi ya 100 kisha kujenga makazi, mali ya Mohamed Suma na kusababisha mgogoro mkubwa.
Kihemba alisema kuwa licha ya kukaa vikao mbalimbali juu ya eneo hilo ambapo watu zaidi ya 600 wameingia kwenye eneo hilo bila ya mmiliki kuwaruhusu kwani alitoa eneo lenye ukubwa wa hekari 16 kwa watu nane tu.
“Nimekuwa nikipata barua nyingi toka kwa kamati ya kushughulikia suala hili wakinitaka nitoe tamko juu ya eneo hili kwani mwenye maamuzi ya eneo hili ni mmiliki mwenyewe na mimi sina uwezo wa kusema lolote,” alisema Kihemba.
Aidha alisema kuwa anashangaa kwamba kama watu hao walipewa bure na baadhi ya viongozi wa mtaa basi waliachie waondoke ni kwanini hawataki kuondoka kama wanataka wafuate sheria kwani anashangaa kuona licha ya kuambiwa wasiendeleze lakini watu wamejenga na wengine wanaendelea na ujenzi.
Mmoja ya wananchi waliouziwa viwanja kwenye eneo hilo Kandege Jafar alisema kuwa wanashangaa halmashauri kuweka matangazo ya kuwataka waondoke ili hali mmiliki mwenyewe alisema kuwa atakapokuja atatoa muafaka wa nini kifanyike.
Jafar alisema kuwa kutokana na hali halisi ilivyo yeye mkuu wa wilaya awasaidie kwani endapo wataendelewa watakuwa wamepata hasara kubwa Kutokana na kuyaendeleza maeneo hayo hivyo ni vema akawasaidia.
“Mkuu wa wilaya sisi tunaomba utusaidie hebu angalia umati wote huu tuko hapa hatujui hatma yetu tunaomba utusaidie ili tusipate haki zetu kwani haitapendeza watu wote kuona wakitaabika bila ya sababu za msingi,” alisema Jafar.
Naye mwenyekiti wa awali wa mtaa huo ambaye ndiye aliyekuwa akisimamia eneo hilo Longino Kasonta alikanusha kuwa aliwauzia wananchi hao maeneo alisema kuwa yeye aliambiwa atoe eneo lenye ukubwa wa hekari 16 kwa watu nane lakini watu wengine yeye hausiki.
“Mimi ndiye niliyeagizwa na mmiliki wa shamba hili nigawe viwanja 16 kwa watu nane ambapo kila mmoja hekari mbili, lakini viongozi wa mtaa nao wakaendelea kuwagawia watu maeneo hadi watu kufikia 600,” alisema Kasonta.
Kasonta alisema kuwa baadhi ya watu walivamia shamba hilo na kuanza kuuza maeneo mengine hasa ikizingatiwa shamba hili ni kubwa sana hivyo watu wanampakazia kuwa yeye kawauzia maeneo jambo ambalo si la kweli.
Mwisho.   

No comments:

Post a Comment