Tuesday, July 9, 2013

FAIDIKA YASAIDIA SHULE MADAWATI

Na John Gagarini, Kibaha
MASHIRIKA na taasisi za biashara zimetakiwa kurejesha faida kwa jamii wanayoihudumia na si kutaka faida pekee ili nao wafaidi uwepo wa vyombo hivyo.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani Silvestry Koka wakati akitoa salamu zake wakati wa kukabidhi madawati 50 kwenye shule za Msingi Jitihada na Lulanzi zilizopo wilayani Kibaha, madawati hayo yaliyotolewa na kampuni ya kutoa mikopo ya Faidika.
Koka alisema kuwa makampuni hayo kwa kuwa yanahudumia jamii lazima yatoe mrejesho kwa kusaidia changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.
“Mashirika haya yasitake kupata faida tu lazima nayo yachangie jamii ili iondokane na changamoto zilizopo kwa kutoa sehemu ya faida wanayoipata katika shughuli zao,” alisema Koka.
Alisema serikali inapaswa kuyaangalia makampuni hayo ambayo yanafanyabiashara kwa jamii ili nayo yatoe sehemu ya faida kwa wananchi kwani mafanikio wanayoyapata ni kutokana na mapato yawananchi hao.
“Lazima nayo yaone umuhimu wa kusaidia jamii kwenye sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja na afya, maji, elimu na zinginezo kwa kuzipatia ufumbuzi,” alisema Koka.
Kwa upande wake mwakilishi wa kampuni ya Faidika Harun Zuberi alisema kuwa kampuni yake mbali ya kutoa mikopo kwa watumishi pia imeweka mkakati wa kurudisha faida wanayopata kwa kuisaidia jamii.
“Tumekuwa tukisaidia sekta mbalimbali ambapo kwa sasa tumeamua kuisaidi sekta ya elimu kwani tunaamini serikali peke yake haiwezi lazima ishirikiane na wadau ndiyo sababu ya sisi kutoa misaada,” alisema Zuberi.
Zuberi alisema kuwa wameona umuhimu wa kuchangia kwenye sekta ya elimu ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wanasoma wakiwa kwenye mazingira mazuri naya kuvutia kwani mazingira ya baadhi ya shule ikiwemo vifaa imekuwa ni tatizo kubwa.
Kwa upande wao walimu wa shule hizo Elizabeth Daniel na Anna Bilal waliipongeza kampuni hiyo kwa kujitolea kusaidia tatizo hilo ambalo ni changamoto kubwa kwa shule zao.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment