Saturday, July 27, 2013

DEREVA BODABODA AFA KWA KUJINYONGA

Na Mwandishi Wetu, Kibaha

tweeterMWENDESHA aliyetambulikia kwa jina moja la Omary (25) mkazi wa mtaa wa Lumumba wilayani Kibaha mkoani Pwani amekutwa amekufa kwa kujinyonga kwenye mkorosho.

Akizungumza na waandishi wa habari leo mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa huo Gidion Tairo amesema kuwa tukio hilo limetokea Julai 25 mwaka huu majira ya saa 2 asubuhi.

Tairo amesema kuwa mwaili wake ulikutwa ukiwa unaninginia huku akiwa amejinyonga kwa kutumia kamba ya Manila huku pembeni yake kukiwa na chupa ya bia aina ya Safari.

Amesema mwili huo uligunduliwa na moja ya majirani zake ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja amabaye alitoa taarifa kwake na yeye kuwasiliana na polisi.

Aidha amesema marehemu ambaye alikuwa akifanyia shughuli zake Kibamba CCM wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam kabla ya mauti kumkuta alikuwa haonekani nyumbani na hakuonekana kuwa na matatizo yoyote.

Amebainisha kuwa marehemu alikuwa akiishi kwenye nyumba na Roja Kwayu wa Jijini Dar es Salaam na ndiye alikuwa akiisimamia nyumba hiyo.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa polisi mkoani Pwani Ulrich Matei amesema kuwa marehemu hakuacha ujumbe wowote.

Matei amesema kuwa polisi wanaendelea na uchunguzi juu ya tukio hilo ili kujua nini chanzo cha kifo chake, na mwili huo umehifadhiwa kwenye hospitali ya Tumbi kusubiri ndugu kwa ajili ya mazishi, baada ya uchunguzi wa daktari.

Mwisho.






DEREVA BODABODA AFA KWA KUJINYONGA

Na Mwandishi Wetu, Kibaha

MWENDESHA aliyetambulikia kwa jina moja la Omary (25) mkazi wa mtaa wa Lumumba wilayani Kibaha mkoani Pwani amekutwa amekufa kwa kujinyonga kwenye mkorosho.

Akizungumza na waandishi wa habari leo mjini Kibaha mwenyekiti wa mtaa huo Gidion Tairo amesema kuwa tukio hilo limetokea Julai 25 mwaka huu majira ya saa 2 asubuhi.

Tairo amesema kuwa mwaili wake ulikutwa ukiwa unaninginia huku akiwa amejinyonga kwa kutumia kamba ya Manila huku pembeni yake kukiwa na chupa ya bia aina ya Safari.

Amesema mwili huo uligunduliwa na moja ya majirani zake ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja amabaye alitoa taarifa kwake na yeye kuwasiliana na polisi.

Aidha amesema marehemu ambaye alikuwa akifanyia shughuli zake Kibamba CCM wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam kabla ya mauti kumkuta alikuwa haonekani nyumbani na hakuonekana kuwa na matatizo yoyote.

Amebainisha kuwa marehemu alikuwa akiishi kwenye nyumba na Roja Kwayu wa Jijini Dar es Salaam na ndiye alikuwa akiisimamia nyumba hiyo.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa polisi mkoani Pwani Ulrich Matei amesema kuwa marehemu hakuacha ujumbe wowote.

Matei amesema kuwa polisi wanaendelea na uchunguzi juu ya tukio hilo ili kujua nini chanzo cha kifo chake, na mwili huo umehifadhiwa kwenye hospitali ya Tumbi kusubiri ndugu kwa ajili ya mazishi, baada ya uchunguzi wa daktari.

Mwisho.






Thursday, July 25, 2013

WALIOACHISHWA TANROADS WALIA

Na John Gagarini, Kibaha

WALIOKUWA wafanyakazi 59 wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani ambao wamepunguzwa kazi wameilalamikia wakala hiyo kwa madai kuwa imevunja mikataba yao na malipo waliyowapa hayalingani na muda waliofanya kazi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini Kibaha mwenyekiti wa kamati ya kufuatiia haki za wafanayakazi hao waliopunguzwa Andrew Lugano alisema kuwa malipo waliolipwa ni kidogo.

Lugano alisema kuwa inashangaza kuona mtu kafanya kazi kwa zaidi ya miaka 10 lakini analipwa shilingi 400,000 ni ndogo na haziwezi kuwasaidia hasa kipindi hichi kigumu cha maisha.

“Jambo la kwanza tumekuwa tukiingia mkataba na mwajiri wetu kila mwanzo wa mwaka lakini cha kushangaza mwaka huu tumekaa hadi Juni 15 ndipo tuliposaini mkataba mpya lakini tukaambiwa mwisho wa ajira yetu ni Juni 30 jambo ambalo tunaona ni kinyume cha taratibu ni vema tungemaliza mwaka huu ndipo wangechukua hatua hiyo,” alisema Lugano.

Alisema kuwa hadi sasa hawajajua sababu ya wao kuachishwa kazi japo kuna tetesi kuwa ni wale wenye elimu ya darasa la saba lakini pia kuna wenye elimu kubwa zaidi ya hiyo lakini wameachishwa hivyo kushindwa kujua kiini hasa nini.

“Sisi tunachotaka ni kulipwa fedha ambazo zionalingana na utumishi wetu na kama ni suala la elimu mbona kuna wenzetu wawili kati ya watu 60 walioachishwa walirudishwa na wana elimu ya darasa la saba?,” aliuliza Lugano.

Aidha akizungumzia suala la elimu alisema kuwa Raisi Jakaya Kikwete alisema kuwa wafanyakazi ambao wanafanyakazi ambao wana elimu ya darasa la saba wasifukuzwe bali waendelezwe kwanini wao wanaondolewa pasipo taratibu kufuatwa.

“Fedha ambazo tumejumlisha kwa haraka haraka kwa watu 28 waliojiorodhesha kudai ni milioni 77 kama tungelipwa kulingana na hali ya sasa hivi, lakini tuliyopewa ni ndogo sana hivyo tunaomba watufikirie kwani hata gharama ya kusafiria kwenda makwetu haitoshi au kuendeshea maisha kwani jambo hili limekuwa la kushtukiza sana,” alisema Lugano.

Aliongeza kuwa walikwenda chama cha wafanyakazi cha TUICO na kupewa barua ya kumpelekea mwajiri wao ili wakutane kwenye baraza la usuluhishi (CMA) mkoa kuzungumzia suala hilo na watumishi waliokumbwa na hali hiyo ni madereva, walinzi, maopareta na wahasibu.

Kwa upande wake meneja wa TANROADS Tumaini Sarakikya alisema kuwa wamefuata taratibu zote za kisheria na juu ya mikataba mwajiri ana maamuzi ya kuongeza au kupunguza mkataba.

“Tayari wameshakwenda kulalamika CMA na sisi tumeshajiandaa tunasubiri muda ufike tukayazungumze masuala hayo, lakini tumewapunguza kwa kuzingatia sheria,” alisema Sarakikya.

Sarakikya alisema kuwa hawajamwonea mfanyakazi yoyote bali ni mabadiliko tu ambayo yametokea na wao wanafahamu hivyo hakuna uonevu.

MWISHO.



KOKA KUWALIPIA BODABODA LESENI

Na John Gagarini, Kibaha

MBUNGE wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka ametoa ofa ya kuwalipia gharama za mafunzo ya madereva wapya wa pikipiki maarufu kama (Bodaboda) ili kila mmoja awe na leseni.

Koka alitoa ofa hiyo jana alipokuwa akizungumza na madereva na wamiliki wa pikipiki, mbele ya mkuu wa wilaya ya Kibaha, uongozi wa halmashauri, maofisa wa mamlaka ya mapato (TRA) na jeshi la polisi mkoa wa Pwani.

Alisema kuwa ameamua kujitolea kuwasaidia madereva wote wapya wa Bodaboda ili wawe na leseni ili wajue kanuni na taratibu za barabarani kwani wengi wao hawana leseni hali inayosababisha ajali nyingi kutokea.

“Lengo langu ni kutaka mfanye kazi kwa kuzingatia sheria na taratibu za usalama barabarani kwani ajali nyingi zinazotokea zinasababishwa na baadhi yenu kutokuwa na leseni kwani wanakuwa hawajapata mafunzo ya matumizi sahihi ya sheria wawapo kazini,” alisema Koka.

Aidha alisema kuwa vijana wamejiajiri kwenye uendeshaji wa pikpiki hivyo lazima wajengewe mazingira mazuri ya kufanyia kazi ili wasipate buguza.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kibaha Halima kIhemba aliwataka madereva hao kuzingatia sheria ili kuepukana na ajali ambazo si za lazima ambazo zinasababisha kupoteza maisha au viungo kwa wateja wao au wao wenyewe.

Kihemba pia aliwataka wawe walinzi wa amani na kukabiliana na vitendo vya uhalifu kwani baadhi ya watu wamekuwa wakiwatumia kwenye vitendo vya kihalifu na vitendo vya vurugu.

Mwisho.




Tuesday, July 23, 2013

MAOFISA MIFUGO WAWE WAZALENDO

Na John Gagarini, Kibaha
 MAOFISA  wa serikali kwenye Idara ya Mifugo wametakiwa kutumia uzalendo wakati wa kuingiza madawa ili kuepuka kuingizwa madawa yasiyo na viwango.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na mwakilishi wa kitaifa wa kampuni ya  Laprovet ya nchini Ufaransa Ephrahim Massawe alipoongea na waandishi wa habari na kusema kuwa baadhi ya maofisa hao wamekuwa wakiingiza madawa yasiyo na viwango.
Massawe alisema kuwa kutokana na kuagizwa madawa yasiyo na viwango kumesababisha madhara makubwa kwa mifugo ikiwa ni pamoja na kufa hivyo wafugaji kupata hasara kubwa.
“Kufa kwa mifugo kunatokana na magonjwa mbalimbali hapa nchini kunatokana na baadhi ya madawa kuwa kwenye kiwango cha chini hivyo kushindwa kuzuia au kutibu magonjwa yanayokabili mifugo,” alisema Massawe.
Aidha alisema kuwa tatizo kubwa ni ubadhirifu na kutokuwa na uadilifu kwa maofisa hao hali ambayo inasababisha mifugo mingi kufa kwa kupata matibabua ambayo hayalingani na uwezo madawa hayo toka nje ya nchi.
“Maofisa hao baadhi yao si waaminifu kwa kuingiza madawa ambayo hayana viwango licha ya kuwa madawa mazuri yapo hasa baada ya kuingia soko huria, hivyo wasiangalie maslahi binafsi bali waangalie utu na uzalendo kwa nchi yao,” alisema Massawe.
Massawe ambaye pia ni makamu mwenyekiti wa waganga wasaidizi wa mifugo nchini (TAVEPA) alisema kuwa endapo maofisa hao watakuwa waadilifu watasaidia kuboresha kipato cha wafugaji.
Alibainisha kuwa ili kuhakikisha wafugaji wanajua matumizi sahihi kampuni hiyo inatoa mafunzo pamoja na ushauri wa namna ya ufugaji wa kisasa ili kuongeza tija kwani ufugaji ni mkombozi wa nchi kwani inaliingizia pato kubwa la Taifa.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
WILAYA ya Bagamoyo mkoani Pwani imeanza mkakati wa kukabiliana na uchafu kwenye Mji huo mkongwe hapa nchini kwa viongozi kushiriki kwenye zoezi la usafi kila mwanzo wa mwezi.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake mkuu wa wilaya hiyo Ahmed Kipozi alisema kuwa mkakati huo una lengo la kuwapa hamasa wananchi kuwa na utamaduni wa kufanya usafi.
Kipozi alisema kuwa tayari mkakati huo umeshaanza kwa viongozi wa wilaya, halmashauri, kata, mitaa na wananchi kufanya usafi kwenye mji huo pamoja na maeneo wanayoishi.
“Usafi bado ni changamoto kubwa kwa wakazi wa Bagamoyo lakini tunajaribu kuwaelimisha wananchi kuona umuhimu wa kusafisha mazingira yao yanayowazunguka na tumeshaanza kuona mabadiliko na mji umeanza kupendeza,” alisema Kipozi.
Alisema kuwa pia wanakabiliwa na ukosefu wa vifaa vya kuhifadhia takataka kwenye maeneo mbalimbali ya mji huo lakini watahakikisha kuwa wanaweka vifaa hivyo ili wananchi wasikose sehemu ya kuhifadhia uchafu.
“Kikubwa tunachoomba ni ushirikiano kwa wananchi ili kuweza kufanikisha usafi kwenye mji wetu ambao ni wa kihistoria na unabeba historia kubwa ya nchi hii hivyo lazima uendane na hali hiyo kwa kuwa kwenye hali ya usafi,” alisema Kipozi.
Alisema kuwa kwa kuwa mji huo tayari umepewa hadhi ya kuwa mji mdogo hivyo lazima usafi uzingatiwe na watatumia sheria ndogondogo za mji ili kukabiliana na wale wote ambao watakuwa wanakwenda kinyume na kanuni za usafai.
Mwisho.      

MATUKIO PWANI

Na John Gagarini,Kibaha

HALMASHAURI ya Kibaha mjini Mkoani Pwani imeanza mchakato wa tathmini ya kutekeleza miradi ya soko pamoja na stendi ya kisasa zitakazojengwa kwenye eneo la kitovu cha Mji huo kilichopo mkabara na barabara kuu ya Morogoro.

Kwa mujibu wa mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa Kibaha Adhudadi Mkomambo alisema kuwa huo ni utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo iliwekewa mkakati mwaka wa fedha wa  2010-2011 ambapo upembuzi upembuzi yakinifu unatarajia kukamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu.

Mkomambo alisema kuwa wameshaingia ubia na banki ya rasilimali (TDB) ambayo ndio itakayosaidia kufanikisha gharama za ujenzi kwa ushirikiano na halmashauri hiyo.

“Taratibu zilizopo sasa ni kufanya tathmini ya uhakika ya gharama za miradi hiyo kabla ya Desemba mwaka huu kisha zoezi la ujenzi litaanza mara moja baada ya tathmini kupatikana,” alisema Mkomambo.

Alibainisha kuwa stendi hiyo itakuwa na uwezo wa kuegesha magari 50 kwa wakati mmoja na upande wa soko la  kisasa litakalokuwa na eneo la soko la kawaida litakalohusisha wakulima wadogowadogo,na soko la kisasa litakalovutia wageni mbalimbali kutoka nje ya nchi.

Mwenyekiti huyo wa halmashauri amebainisha kuwa ujenzi huo unatarajiwa kuanza mapema mwakani na kutarajiwa kukamilika mwaka 2015-2016 na litatumia heka Tisa.
Mwisho.

Na John Gagarini, Kibaha
KAMANDA wa Jumuiya ya vijana (UVCCM) wilaya ya kibaha Mjini Mkoani Pwani Silvestry Koka amesema kuna kila sababu ya kuendelea kuimarisha chipukizi ndani ya chama ili kuwajenga vijana na watoto wakue kwa misingi ya kizalendo.

Akifungua mkutano wa uchaguzi wa viongozi wa Chipukizi wilayani humo, alisema tangu enzi za waasisi wetu walitambua kwa kuweka taratibu ya kuwa na chipukizi kutokana na kuwa  nguzo kwa maslahi ya chama na Taifa.

Koka alisema kuanzia sasa atahakikisha anakuwa mlezi wa kutatua changamoto za chipukizi wilayani humo ikiwa ni sanjali na kuwawezesha kwenye mafunzo mbalimbali, michezo ili kuwalinda na kuwapa motisha .

matokeo ya uchaguzi huo Katibu wa UVCCM kibaha mjini Khalid King alisema viongozi hao wapya wataongoza kwa kipindi kingine cha mika mitatu.

King alimtaja Shadya Ibrahim kuwa ni Mwenyekiti wa chipukizi aliyepata kura 74 baada ya kumshinda mpinzani wake Imran Mohamed aliyepata kura 58.

Katika  nafasi ya Mjumbe wa mkutano mkuu wa chipukizi  ngazi ya mkoa amechaguliwa Jesca Mkenda , mwakilishi wa mkutano mkuu wa Wilaya ikishikiliwa na Zainabu Mpemba ,na nafasi ya kamati ya uendeshaji ya Chipukizi ngazi ya Wilaya ni Joseph Ernest,Marwa Mwise na Neema Ahmed .
 Mwisho

 Na John Gagarini, Kibaha
VIONGOZI wa Skauti nchini wametakiwa wametakiwa kuzingatia uadilifu na weledi katika kutimiza majukumu yao ya kikazi ili kuiletea nchi maendeleo na endapo watakwenda kinyume na taratibu watachukuliwa hatua kali ikiwa ni pamoja na kuondolewa kwenye nyadhifa zao.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Skauti mkuu wa Tanzania Mwantumu Mahiza alipokuwa akimwapisha kamishna mkuu wa Skauti Abulkarim Shah na kusema kuwa sifa kuu ya skauti ni uadilifu.

Mahiza alisema kuwa  ili kiongozi aaminike na jamii  ni lazima aonyeshe  juhudi, weledi uamnifu na ubunifu katika utekelezaji wa majukumu yake.

“Kiongozi anapaswa kuwa mfano kwa jamii na anapaswa kuhakikisha chama kinarudi kwenye mstari na sitasita kumwondoa kiongozi anayeshindwa kutimiza majukumu yake kama katiba inavyosema ili kujenga heshima ya chama hicho ndani na nje ya nchi,” alisema Mahiza.
  
Aidha alibainisha kuwa hatutakuwa tayari kufanyakazi na baadhi ya viongozi walioonekana kupoteza sifa ya chama hicho na badala yake wale wote waliohusika kukipunguzia sifa watabaki kuwa wanachama na kazi ya uongozi tutaendelea na wachache wanaokidhi vigezo.
 MWISHO.
  
Na John Gagarini, Kibaha
MAHAKAMA ya hakimu Mkazi Kibaha Mkoa wa Pwani imemuhukumu  mkazi wa Miembe Saba wilayani Kibaha Amosi Chacha (40)  kwenda jela miaka 6 baada ya kukutwa na hatia katika kesi ya Wizi wa vocha za mtandao wa simu za Tigo pamoja na kukutwa na mihuri bandia.

Mtuhumiwa huyo alikutwa na hatia kwa makosa yote mawili yaliyokuwa yakimkabili Katika kesi iliyokuwa ikisikilizawa na Hakimu Mkazi,  Aziza Mbadyo.

Mwendesha mashitaka wa Serikali  Emmanuel Maleko  ameieleza mahakama kuwa mtuhumiwa  huyo alikutwa akiwa na Mihuri ya Afisa Mtendaji Mtaa wa Kwesimu pamoja na wa Kituo cha Ukaguzi wa Maliasili cha Soni kilichopo Wilaya ya Lushoto Mkoa wa Tanga mnamo tarehe 03 Juni 2013 huko eneo la Sinza Wilaya ya Kinondoni Mkoa wa Dar es Salaam.

Imeelezwa kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa akitumia mihuri hiyo katika usafirishaji wa mali asili kutoka Tanga kwenda Dar es Salaam kwa lengo la kuweza kuvuka vizuizi vya mali asili vilivyopo kwenye barabara kuu.

Aidha Maleko alieeleza mahakama kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa eneo la Kibaha Mkoa wa Pwani akiwa na vocha za muda wa hewani za kampuni ya simu ya Tigo zenye thamani ya Tsh. 5,000,000/= akizisafirisha kwenda Tanga akitokea Dar es Salaam.

Mwendesha Mashitaka huyo wa Serikali aliongeza kuwa makosa yote hayo mawili aliyokutwa na hatiya dhidi yake,  Chacha anadaiwa kuyatenda kwa nyakati tofauti.

Akisoma hukumu hiyo kwa muda wa saa moja na nusu, Mbadyo alisema kuwa Mahakama imeridhika na maelezo ya upande wa Jamhuri hivyo imemtia hatiani Amosi Mwita Chacha kwenda Jela miaka sita ambapo katika kosa la Wizi wa vocha za Tigo alihukumiwa miaka minne na kosa la Kukutwa na Mihuri bandia alihukumiwa miaka miwili  hivyo adhabu zote mbili zitakwenda pamoja na atatakiwa kwenda Jela miaka sita.

Na John Gagarini, Kibaha
 MKAZI wa kijiji cha Nyanduturu Wilaya ya Mkuranga Mkoa wa Pwani, Ally Makakatau (46) amepoteza maisha baada ya kuvamiwa nyumbani kwake na kukatwa na mapanga na watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi.

Kwa mujibu wa kaimu kamanda wa Polisi mkoani Pwani Kamishana Msaidizi wa Jeshi la Polisi Juma Ally alisema kuwa  tukio hilo lilitokea Julai 19 majira ya saa 7:30 usiku baada ya watu wapatao sita kuvamia nyumbani kwa Makakatua na kuvunja mlango wa nyumba aliyokuwemo kisha kumshambulia kwa kutumia mapanga kichwani, mkononi na miguuni.

Ally alisema kuwa watu hao walivamia katika nyumba hiyo na kumtaka marehemu kuwapatia pesa ambazo alikuwa amepata baada ya mauzo ya mafuta aliyokuwa amefanya jioni ya siku hiyo na alipokataa kutoa ndipo waliamua kumkata kwa mapanga sehemu mbalimbali za mwili.

“Watu hao mbali ya kuvunja  nyumba ya mfanyabiashara huyo, pia walivunja duka na kuchukua pesa taslimu shilingi m 2,800,000 ambazo zilikuwa ni za mauzo ya mafuta,” alisema Ally.   

Aliongeza kuwa Jeshi la linawasaka watu hao na kuwataka wanachi kuwapatia taarifa zitakazo saidia kuweza kuwapata waliohusika na tukio hilo.

Aidha alisema kuwa mwili wa marehemu ulifanyiwa uchunguzi wa Daktari na tayari umekabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya taratibu za mazishi.

Katika tukio lingine, JESHI la Polisi Mkoa wa Pwani linawashikilia watu ishirini (20) raia wa Ethiopia kwa kosa la kuingia nchi bila kibali.
Alisema kuwa tukio hilo lilitokea majira ya saa 7:30 usiku eneo la Mkuranga Mjini Wilaya ya Mkuranga.

Kaimu Kamanda huyo alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa watu hao walikamatwa na askari waliokuwa doria wakiwa wanatembea makundi makundi  katika eneo la Mkuranga Mjini.

Alifafanua kuwa watu hao baada ya kuwahoji walibaini kuwa walishushwa kwa gari na kuamua kutembea ili kuweza kuvuka kwenye eneo lililokuwa na kizuizi cha Polisi.

Aliwataja raia hao wa Ethiopia waliokamatwa kuwa ni Habtamu Ambesi (21), Yesak Mishamo (19), Biuk Moltumo (20), Apepe Eshetu, (20), Mesfin Taddes, (20), Debero Shenke, (20), Teamat Kesse, (18), Gerenu Debere, (20), Tofek Anshabo, (25), Lomabebo Gahtchowo, (20) na Asle Mugoro, (20).

Wengine ni Chakiso Eriso, (20), Wondimu Birhanu, (18), Mulatu Menuru, (22), Gezahegn Lire, (21), Tileahnu Desta (20), Muly Geta (21), Abdi Mohamed (22), Ali Lonsako (25), Johann Bincebo (20), Degnat Tesema (16), Femasene Fitamo (17) na Temaggne Kebeda (25).

Aidha Ally alisema pia Jeshi hilo limefanikiwa kumkamata John Kataraya (50) mkazi wa Mbezi Beach Dar es Salaam ambaye alikuwa akiwasafirisha Waethiopia hao.

“Rai hawa waliingia nchini kwa kutumia njia ya usafiri wa gari kutoka Dar es Salaam kwenda Mikoa ya Kusini ili kuweza kwenda nchi jirani ya Msumbiji na watakabidhiwa kwa idara ya uhamiaji kwa ajili ya taratibu zingine za kisheria,” alisema Ally

Aidha, aliwataka wanachi waendelee kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi pindi wanapowatilia mashaka wageni wanaoingia kwenye maeneo yao.
Mwisho


Friday, July 19, 2013

AMUUA MWANAMKE MWENZAKE KISA WIVU WA MAPENZI



Na John Gagarini, Kibaha
TATU Abdala (37) mkazi wa wilaya ya Rufiji mkoani Pwani anashikiliwa na jeshi la polisi tuhuma za kumchoma kisu na kumwua mwanamke mwenzake kwa madai kuwa alikuwa akitembea na mume wake Omary Abdala ambaye waliacha naye mwaka mmoja uliopita.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamimu kamanda wa Polisi mkoani Pwani Kamishana msaidizi wa Jeshi hilo Yusuph Ally alisema kuwa marehemu alichomwa kisu hicho tumboni.
Ally alisema kuwa chanzo cha mauaji hayo kinatajwa kuwa ni wivu wa kimapenzi baada ya kubaini kuwa mume wake wa zamani alikuwa na mahausiano ya kimapenzi na marehemu baada ya wao kuachana.
“Mtuhumiwa huyo alitalakiana na mumewe ambaye walizaa naye watoto watano naalipata taarifa ya mtalaka wake
kujenga mahusiano ya kimapenzi na marehemu Hajra kisha kumfuata
marehemu huyo nyumbani kwake na kumchoma kisu tumboni,” alisema Ally.

Ally alibainisha kuwa mtuhumiwa alipata
urahisi wa kutenda tukio hilo  kutokana na kuishi eneo la jirani na marehemu.

Aidha alisema mara baada ya tukio hilo marehemu alikimbizwa kituo cha afya cha
Muhoro na kabla ya kupatiwa matibabu alifariki dunia.
Aliongeza kuwa Mtuhumiwa
alikamatwa na polisi kujibu mashtaka yanayomkabili.
Mwisho

Thursday, July 18, 2013

DC ANAWA MIKONO MGOGORO WA SHAMBA


Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Halima Kihemba amewataka wananchi kwenye eneo lenye mgogoro wa ardhi uliopo kwenye mtaa wa Mtakuja kulimaliza suala hilo na mmiliki wa eneo hilo kwani yeye hawezi kulitolea maamuzi eneo la mtu ambaye ana hati miliki.
Aliyasema hayo jana kwenye mtaa huo ambako baaadhi ya wananchi kuingia kwenye eneo hilo lenye ukubwa wa hekari zaidi ya 100 kisha kujenga makazi, mali ya Mohamed Suma na kusababisha mgogoro mkubwa.
Kihemba alisema kuwa licha ya kukaa vikao mbalimbali juu ya eneo hilo ambapo watu zaidi ya 600 wameingia kwenye eneo hilo bila ya mmiliki kuwaruhusu kwani alitoa eneo lenye ukubwa wa hekari 16 kwa watu nane tu.
“Nimekuwa nikipata barua nyingi toka kwa kamati ya kushughulikia suala hili wakinitaka nitoe tamko juu ya eneo hili kwani mwenye maamuzi ya eneo hili ni mmiliki mwenyewe na mimi sina uwezo wa kusema lolote,” alisema Kihemba.
Aidha alisema kuwa anashangaa kwamba kama watu hao walipewa bure na baadhi ya viongozi wa mtaa basi waliachie waondoke ni kwanini hawataki kuondoka kama wanataka wafuate sheria kwani anashangaa kuona licha ya kuambiwa wasiendeleze lakini watu wamejenga na wengine wanaendelea na ujenzi.
Mmoja ya wananchi waliouziwa viwanja kwenye eneo hilo Kandege Jafar alisema kuwa wanashangaa halmashauri kuweka matangazo ya kuwataka waondoke ili hali mmiliki mwenyewe alisema kuwa atakapokuja atatoa muafaka wa nini kifanyike.
Jafar alisema kuwa kutokana na hali halisi ilivyo yeye mkuu wa wilaya awasaidie kwani endapo wataendelewa watakuwa wamepata hasara kubwa Kutokana na kuyaendeleza maeneo hayo hivyo ni vema akawasaidia.
“Mkuu wa wilaya sisi tunaomba utusaidie hebu angalia umati wote huu tuko hapa hatujui hatma yetu tunaomba utusaidie ili tusipate haki zetu kwani haitapendeza watu wote kuona wakitaabika bila ya sababu za msingi,” alisema Jafar.
Naye mwenyekiti wa awali wa mtaa huo ambaye ndiye aliyekuwa akisimamia eneo hilo Longino Kasonta alikanusha kuwa aliwauzia wananchi hao maeneo alisema kuwa yeye aliambiwa atoe eneo lenye ukubwa wa hekari 16 kwa watu nane lakini watu wengine yeye hausiki.
“Mimi ndiye niliyeagizwa na mmiliki wa shamba hili nigawe viwanja 16 kwa watu nane ambapo kila mmoja hekari mbili, lakini viongozi wa mtaa nao wakaendelea kuwagawia watu maeneo hadi watu kufikia 600,” alisema Kasonta.
Kasonta alisema kuwa baadhi ya watu walivamia shamba hilo na kuanza kuuza maeneo mengine hasa ikizingatiwa shamba hili ni kubwa sana hivyo watu wanampakazia kuwa yeye kawauzia maeneo jambo ambalo si la kweli.
Mwisho.   

Tuesday, July 9, 2013

FAIDIKA YASAIDIA SHULE MADAWATI

Na John Gagarini, Kibaha
MASHIRIKA na taasisi za biashara zimetakiwa kurejesha faida kwa jamii wanayoihudumia na si kutaka faida pekee ili nao wafaidi uwepo wa vyombo hivyo.
Hayo yalisemwa jana mjini Kibaha na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini mkoani Pwani Silvestry Koka wakati akitoa salamu zake wakati wa kukabidhi madawati 50 kwenye shule za Msingi Jitihada na Lulanzi zilizopo wilayani Kibaha, madawati hayo yaliyotolewa na kampuni ya kutoa mikopo ya Faidika.
Koka alisema kuwa makampuni hayo kwa kuwa yanahudumia jamii lazima yatoe mrejesho kwa kusaidia changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.
“Mashirika haya yasitake kupata faida tu lazima nayo yachangie jamii ili iondokane na changamoto zilizopo kwa kutoa sehemu ya faida wanayoipata katika shughuli zao,” alisema Koka.
Alisema serikali inapaswa kuyaangalia makampuni hayo ambayo yanafanyabiashara kwa jamii ili nayo yatoe sehemu ya faida kwa wananchi kwani mafanikio wanayoyapata ni kutokana na mapato yawananchi hao.
“Lazima nayo yaone umuhimu wa kusaidia jamii kwenye sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja na afya, maji, elimu na zinginezo kwa kuzipatia ufumbuzi,” alisema Koka.
Kwa upande wake mwakilishi wa kampuni ya Faidika Harun Zuberi alisema kuwa kampuni yake mbali ya kutoa mikopo kwa watumishi pia imeweka mkakati wa kurudisha faida wanayopata kwa kuisaidia jamii.
“Tumekuwa tukisaidia sekta mbalimbali ambapo kwa sasa tumeamua kuisaidi sekta ya elimu kwani tunaamini serikali peke yake haiwezi lazima ishirikiane na wadau ndiyo sababu ya sisi kutoa misaada,” alisema Zuberi.
Zuberi alisema kuwa wameona umuhimu wa kuchangia kwenye sekta ya elimu ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wanasoma wakiwa kwenye mazingira mazuri naya kuvutia kwani mazingira ya baadhi ya shule ikiwemo vifaa imekuwa ni tatizo kubwa.
Kwa upande wao walimu wa shule hizo Elizabeth Daniel na Anna Bilal waliipongeza kampuni hiyo kwa kujitolea kusaidia tatizo hilo ambalo ni changamoto kubwa kwa shule zao.

Mwisho.

Sunday, July 7, 2013

HABARI ZA PWANI



Na John Gagarini, Kibaha
MKUU wa mkoa wa Pwani Mwantumu Mahiza amepongeza utaratibu wa viongozi wa dini za kikristo kufunga siku 40 kwa ajili ya kuombea amani ya nchi ili iweze kuondelea baada ya kutokea matukio yaliyokuwa yakiashiria uvunjifu wa amani.
Akizungumza juzi na viongozi wa madhehebu ya dini mbalimbali na uongozi wa jeshi la polisi mkoani humo, alisema kuwa jambo wanalolifanya ni kubwa na linapaswa kuungwa mkono na wapenda amani.
Mahiza alisema kuwa siku za hivi karibuni kulitokea matukio makubwa ya uvunjifu wa amani hapa nchini ikiwa ni pamoja na kutokea milipuko ya mabomu mkoani Arusha ambapo watu kadhaa walipoteza maisha huku wengine wakijeruhiwa.
“Tukikumbuka hata kule Kusini mkoani Mtwara zilizuka vurugu kubwa ambazo nazo matokeo yake hayakuwa mazuri kwani watu kadhaa walipoteza maisha na mali huku wengine wakijeruhi hivyo kuna haja ya kuwa na mkakati wa kukabilina na hali hiyo ikiwa ni pamoja na kuiombea nchi amani,” alisema mahiza.
Aidha alisema kuwa amani kuipoteza ni rahisi lakini gharama ya kuirudisha ni kubwa sana hivyo lazima kila mtu aangalia ni namna gani anaweza kunusuru hali hiyo.
“Tunaunga mkono jitihada za viongozi wa dini kuamua kufunga na kufanya maombi maalumu ili kuinusuru nchi yetu ili isiingie kwenye machafuko ambayo mara nyingi husababisha vifo na watu kushindwa kufanya shughuli za maendeleo,” alisema Mahiza.
Alisema kuwa sehemu yoyote yenye machafuko maendeleo hakuna hivyo kuna kila sababu ya kuiombea nchi ili iepukane na hayo yanayotaka kujitokeza.
Kwa upande wake katibu wa umoja wa makanisa ya kipentekoste mkoa wa Pwani Mchungaji Gervase masanja alsiema kuwa endapo amani itatoweka hata uhuru wa kumwabudu mungu hautakuwepo.
“Baadhi ya watu wameingiza siasa makanisani jambo ambalo linaweza likawa chanzo cha vurugu hivyo tunawaomba waumini wasiiingize siasa kwenye sehemu za kuabudia kwani ni hatari na ndiyo sababu ya sisi kuamua kufunga kuombea amani iliyopo isivunjike,” alisema Mch Masanja.
Kikao hicho pia kiliwajumuisha wakuu wa wilaya, wakuu wa polisi wa wilaya, vyama vya siasa, vyama vya watu wenye ulemavu na watu maarufu ndani ya jamii kwenye mkoa huo.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MAMLAKA ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) mkoa wa Pwani imekunjua makucha yake baada ya kumtaka kondakta wa basi la kampuni ya Mbazi kuwarudishia nauli waliyoizidisha tofauti na ile iliyopangwa na serikali.
Tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki kwenye stendi ya maili Moja wilayani Kibaha baada ya abiria kulalamika kuwa wamezidishiwa nauli wakati wakikata nauli kwenye kituo cha mabasi cha Ubungo Jijini Dar es Salaam.
Kondakta wa basi hilo ambalo linafanya safari zake kati ya Dar es Salaam na Arusha alijikuta matatani baada ya basi lake kuzuiliwa na kurejesha nauli ambazo zilikuwa zimezidi kwa abiria 19.
Baadhi ya abiria ambao waliongea na waandishi wa habari kuhusiana na kuzidishiwa nauli kati yao ni Nagi Nurdin aliyekuwa akienda Moshi alisema kuwa yeye alikatiwa nauli kwa shilingi 29,000 badala ya shilingi 22,700 ambapo alikata kwenye ofisi za basi hilo.
Naye Forida Faustin alisema kuwa yeye naye alikuwa akienda Moshi alitozwa 33,000 huku YUda Nduti akitozwa 30,000 ambapo walianza kumtajia nauli ni shilingi 40,000.
Kwa upande wake ofisa mfawidhi wa SUMATRA Pwani Iroga Nashon alisema kuwa hatua ya kwanza waliyoichukua ni kumwamuru kondakta wa basio hilo lenye namba T 600 APN kuwarejeshea nauli zilizozidi abiria hao.
“Baada ya kurejesha nauli zilizozidi ambazo zilikuwa ni zaidi ya 300,000 pia tuliwapiga faini ya shilingi 250,000 kwa kosa hilo kwa kuzingatia kifungu cha sheria cha 34 na ndipo tuliporuhusu basi hilo kuendelea na safari yake,” alisema Nashon.
Kwa upande wake kondakta wa basi hilo hakuwa tayari kuzungumza na waandishi na kusema kuwa yeye siyo msemaji ambapo alidai abiria hao walikatiwa tiketi stendi ya Ubungo.
Nashon aliwataka abiria kutoa taarifa kuhusiana na wamiliki au makondakta na madereva kuwanyanyasa kwa makusudi huku wakijua sheria za uendeshaji wa mabasi hayo ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwa wanaokiuka.
Mwisho.
Na John Gagarini, Kibaha
MKOA wa Pwani unakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa gari la kunyanyulia vitu vizito (Crane) ikiwemo magari yanayoharibika kwenye barabara za mkoa huo.
Chanagamoto hiyo ilionekana juzi baada ya magari kukwama kwa zaidi ya saa tano baada ya magari mawili kuharibika kwenye daraja linalounganisha mikoa ya Pwani na Dar es Salaam eneo la Kiluvya wilayani Kibaha.
Magari yaliyoharibika ni ya mizigo ambapo la kwanza ni Scania namba T 503 DTJ na Fuso lenye namba za usajili T 515 DSA magari haya yaliziba kabisa barabara hivyo kusababisha magari kushindwa kuingia wala kutoka kwa muda huo.
Akizungumza kwenye eneo la tukio hilo kamanda wa polisi wa kikosi cha usalama barabarani wa mkoa huo Nasoro Sisiwaya alisema kuwa ilibidi watumie nguvu ya ziada kuliondoa gari moja ili magari yaweze kupita kwani lori kubwa liliharibika katikati ya daraja la mto Mpiji.
“Kwa kweli gari la kunyanyua vitu vizito ni changamoto kubwa kwani magari yanayo anguka au kupata ajali yanashindwa kuondolewa kwa wakati kutokana na kukosa huduma ya gari hilo,” alisema Sisiwaya.
Sisiwaya alisema kuwa tayari wameshaiomba serikali na wakala wa barabara TANROADS ili wanunue gari hilo na liwe hapa Kibaha kwani kutegemea litoke Dar es Salaam ni tatizo kubwa.
“Tumeandika sehemu husika kuomba gari hilo ili kukabiliana kwani tukio hili limesababisha usumbufu mkubwa sana kwa magari yanayopita barabara hii ya Morogoro ambayo ndiyo mlango wa kuingilia na kutoka Dar es Salaam.
Aidha alisema wataiomba TANROADS kujenga barabara mbadala kwani kutegemea barabara moja ni tatizo kubwa na kutokana na tukio hili tumeona jinsi gani watu walivyohangaika na kusababisha usumbufu mkubwa.
Mwisho.