Monday, December 24, 2012

WALIONUNUA MAENEO YA WAZI KUSHUGHULIKIWA


Na John Gagarini, Bagamoyo
MJI Mdogo wa Bagamoyo mkoani Pwani umewataka watu wote walionunua maeneo ya wazi kwenye kata ya Magomeni na kujenga nyumba waondoke kabla ya hatua za kisheria kuchukuliwa dhidi yao.
Akizungumza na wakazi wa kitongoji cha Magomeni wilayani humo Meya wa Mji huo Bw Abdul Sharifu alisema kuwa kwa kushirikiana na baadhi ya maofisa wa ardhi wasio waaminfu wamenunua maeneo hayo kinyume cha sheria.
Bw Sharifu alisema kuwa maeneo yote ya wakazi katika kata ya Magomeni yameuzwa yote kinyume cha sheria jambo ambalo linasababisha kata hiyo kushindwa kupewa miradi ya maendeleo kwa ajili ya huduma za kijamii.
“Wale wote walionunua maeneo hayo ya wazi waondoke mara moja kwani endapo hawataondoka wataondolewa kwa nguvu kwani haiwezekani tukakosa eneo kwa ajili ya huduma za kijamii kutokana na watu ambao wanavunja sheria hivyo lazima waondoke,” alisema Bw Sharifu.
Aidha alisema kuwa tayari baraza hilo limewaagiza watu wa ardhi kuyaainisha maeneo yote yale ya wazi ambayo yameuzwa.
“Wilaya ina eneo kubwa lakini cha kushangaza watu wananunua maeneo ya wazi ambayo yametengwa kwa ajili ya huduma za jamii lakini baadhi ya watu wenye kutaka maslahi yao binafsi wanavunja sheria,” alisema Bw Sharifu.
Alisema kwa sasa wanataka kujenga soko na zahanati lakini hakuna eneo la wazi kwa ajili ya kujenga vitu hivyo kutokana na maeneo hayo kuhujumiwa hivyo watu wengi kukosa fursa ya kujengewa miundombinu.
Aliwataka maofisa ardhi watakaotembelea maeneo hayo kuyaanisha maeneo hayo kwa kutumia ramani za zamani ili kubaini watu waliokiuka taratibu za ujenzi kwa kujenga maeneo ya wazi.
Mwisho.
      

No comments:

Post a Comment