Sunday, December 23, 2012

WAFUGAJI WATAKIWA KUONDOKA


Na John Gagarini, Bagamoyo
WAFUGAJI wote waliovamia kwenye vijiji mbalimbali kwa ajili ya malisho ya mifugo wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wametakiwa kuondoka ili kuepusha migogoro baina ya wakulima na wafugaji.
Hayo yalisemwa na Meya wa Mji Mdogo wa Bagamoyo Bw Abdul Sharifu kwenye Kijiji cha Kwamduma wakati wa ziara yake kutembelea wilaya hiyo kubaini changamoto zinazowakabili wakazi wa wilaya hiyo, kupitia Jumuiya ya Wazazi (CCM) ya wilaya.
Bw Sharifu alisema kuwa kero ya wafugaji kuingia wilayani humo imekuwa kubwa na kusababisha migogoro kutokana na wafugaji kulisha mifugo kwenye mashamba ya wakulima.
“Kuanzia sasa wale wafugaji wote walioingia katika wilaya hii kwa ajili ya kutafuta malisho waondoke ili kuepusha vurugu ambazo zimekuwa zikitokea mara kwa mara kwa mazao kuharibiwa na mifugo hiyo,” alisema Bw Sharifu.
Alisema kuwa kila kijiji alichotembelea kilio kimekuwa ni wafugaji ambao wamekuwa wakiingiza makundi makubwa ya mifugo hasa ngombe wakitokea mikoa mingine.
“Huko tunakoelekea hali ya amani inaweza kuvurugika kutokana na ngombe kuharibu mazao ya wakulima ambapo wafugaji ambao wamevamia wilaya hii wakitafuta malisho lakini hata hivyo hawathamini wakulima,” alisema Bw Sharifu.
Meya huyo ambaye pia ni mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Bagamoyo alisema kuwa suala la mifugo ndani ya wilaya hiyo limekuwa chanagamoto kubwa kwa viongozi wa wilaya hiyo.
Aidha alisema katika kukabuilina na changamoto hiyo halmashauri imeanzisha mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa baadhi ya vijiji ambapo yametengwa maoeneo ya wakulima na wafugaji.
Mwisho.   

No comments:

Post a Comment