Tuesday, December 11, 2012

KIKWETE

Na John  Gagarini, Kilwa
RAISI wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete ameutaka uongozi wa halmashauri ya wilaya ya Kilwa mkoani Lindi kuwachimbia visima viwili wakazi wa Kijiji cha Marendego ambapo katika mpango wa uchimbaji wa visima 69 kijiji hicho hakikuwekwa licha ya kuwa na changamoto ya maji.
Alitoa agizo hilo juzi kwa mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilwa Bw Ado Mapunda wakati anasalimiana na wakazi wa Kijiji hicho kilicho jirani na wilaya ya Rufiji mkoa wa Pwani akirejea Ikulu Jijini Dar es Salaam alipokuwa ziarani mkoani Lindi.
Raisi Kikwete alimtaka mkurugenzi huyo kuhakikisha visima hivyo vinachimbwa na mkuu wa mkoa wa Pwani Bi Mwantumu Mahiza atasimamia kuhakikisha suala hilo linakamilika ili kukabiliana na changamoto hiyo ya maji.
Awali mwenyekiti wa Kijiji hicho Bw Omary Mtungunyu alisema kuwa kwa sasa wanategemea kupata maji kutoka kwenye mashimo yaliyochimbwa na kampuni ya ujenzi wa barabara ya Kusini ya Kharafi ambapo visima viwili vilivyopo havitoi maji.
“Hatuna vyanzo vingine vya maji hali ambayo imekuwa ni changamoto kubwa kwetu ambapo watu wanaofanya biashara ya kuuza maji safi huuza kiasi cha shilingi 500 hadi 1,000 kwa dumu la lita 20,” alisema Mtunyungu.
Kutokana na ombi hilo Raisi Kikwete alimwita Bw Mapunda na kumtaka kuelezea mikakati waliyonayo ya kukabiliana na changamoto hiyo ya maji kwa Kijiji hicho ambapo alisema kuwa kijiji hicho hakimo kwenye mpango wa uchimbwaji wa visima 67 katika halmashauri hiyo.
“Kutokana na heshima yako Raisi tutawachimbia visima hivyo viwili lakini hawakuwepo kwenye mpango huo wa kuchimbiwa visima kukabiliana na tatizo la maji katika halamshauri hiyo,” alisema Bw Mapunda.
Kufuatia Bw Mapunda kusema kuwa kuwachimbia visima hivyo viwili ni heshima Raisi Kikwete alipinga na kusema si kwa heshima yake bali ni haki ya wakazi hao vinginevyo iwe kwa heshima yake yeye mkurugenzi.
Raisi Kikwete alimtaka mkurugenzi huyo kuhakikisha anachimba visima hivyo ili wakazi hao wasiendelee kutaabika na maji ambapo kuna njia ya kuweza kupunguza makali ya tatizo hilo.
Katika hatua nyingine alisema chanagamoto ya ukosefu wa zahanati atachangia kiasi cha shilingi milioni mbili kwa ajili ya ujenzi wa zahanati ambao umeanza ambapo wakazi hao huenda umbali wa zaidi ya kilomita 10 kupata huduma za afya.
Mwisho.
  

No comments:

Post a Comment