Tuesday, December 11, 2012

JUMUIYA YA WAZAZI

Na John Gagarini, Bagamoyo
JUMUIYA ya Wazazi wilaya ya Bagmoyo mkoani Pwani imesema kuwa itawachukulia hatua za kisheria viongozi wote waliohusika kuhujumu mali za chama hicho ikiwa ni pamoja na kuziuza kinyemela.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa mafunzo kwa viongozi wa kata za wilaya ya Bagamoyo mwenyekiti wa Jumuia ya hiyo Bw Abdul Sharifu alisema kuwa baadhi ya viongozi wamehusika kuhujumu mali za Jumuiya hiyo.
Bw Sharifu alisema kuwa Jumuiya hiyo ni moja ya Jumuiya za Chama zenye mali nyingi lakini baadhi ya viongozi wamehusika kuzihujumu.
"Kwa kiongozi yoyote aliyehusika kuhujumu mali za Jumuiaya akae tayari kuwajibika kwa kurudisha mali husika na endapo atashindwa kufanya hivyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake kwani kwa sasa tunataka tuijenge upya Jumuiya yetu ili iwe tegemeo kwa Chama," alisema Bw Sharifu.
Mwenyekiti huyo wa Jumuiya ya Wazazi wilaya ya Bagamoyo ambaye pia ni Meya wa Mji wa Bagamoyo alisema kuwa baadhi ya mali zilizohujumiwa ni pamoja na mashamba viwanja na shule.
"Moja ya mali zilizohujumiwa ni shule ya sekondari ya Kaole ambayo inasemekana imeuzwa kinyume cha taratibu na haikupaswa kuuzwa kwani hiyo ni mali ya Jumuiya na si mali ya mtu binafsi na ni moja ya kitu ambacho kina manufaa makubwa kwa watu kwa kuwaptia elimu," alisema Bw Sharifu.
Akielezea juu ya semina hiyo elekezi alisema ina lengo la kuwaelekeza viongozi kujua wajibu wao kwani baadhi ya viongozi wanaochaguliwa wamekuwa hawajui majukumu yao ipasavyo.
Aidha alisema kuwa yeye wakati anachaguliwa aliahidi kuwapatia semina viongozi wa kata na matawi jambo ambalo ndiyo analitekeleza kwani viongozi hao wa kata mara baada ya kupata semina hiyo nao watakwenda kuwafundisha viongozi wa matawi kwenye kata zao.
mwisho.

No comments:

Post a Comment