Tuesday, July 11, 2023

KAMPUNI YA GGML NA WIZARA YA MADINI KWA KUTOA ELIMU

 

WIZARA ya Madini imepongezwa na  Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) kwa kutoa elimu kwa wananchi na wadau wanaotembelea banda la Wizara, taasisi zake na wadau wa Sekta ya Madini.

Pongezi hizo zimetolewa leo  Julai 11, 2023 na Mwanasheria Mkuu wa kampuni ya GGML  David Nzaligo alipotembelea banda la Wizara ya Madini (MADINI PAVILION) katika Maonyesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) jijini Dar es salaam.

Akizungumza mara baada ya kutembelea banda la Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) Nzaligo ameipongeza kampuni hiyo kwa kuleta Mkaa Mbadala wa Rafiki Briquettes ambao utasaidia kudhibiti uharibifu wa mazingira hapa nchini.

Akiwa katika banda la  kampuni ya GGML ambalo lipo pia ndani ya banda la madini, Nzaligo amewapongeza wafanyakazi wa GGML na kampuni zingine ndani ya banda hilo kwa kuonyesha weledi mkubwa katika kutoa elimu ya shughuli wanazozifanya ikiwemo uchimbaji madini na mnyororo wake.

"Nafahamu GGML wapo vizuri kwenye miradi mingi ya kijamii pamoja na uwezeshaji wananchi kiuchumi. Nafurahi kwamba  mafanikio hayo wanayaelezea vizuri kwa kila mwananchi anayetembelea banda la GGML," alisema.

MAOFISA UTUMISHI WAONYWA

MAOFISA Utumishi wa Halmashauri nchini wameonywa kwa kutakiwa wabadilike na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kuwaondolea kero watumishi.

Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejmenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete alipokuwa akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Mji Kibaha.

Kikwete alisema kuwa baadhi ya maofisa Utumishi wamekuwa hawatoi haki kwa watumishi hali ambayo inasababisha malalamiko kwa watumishi na kushindwa kufanya kazi kwa moyo jambo ambalo ni kinyume cha utaratibu.

"Maofisa Utumishi ni kama vile baba na mama kwa watoto hivyo lazima wawatendee haki lakini baadhi wanafanya mambo ambayo hayapendezi wanasemwa vibaya hatupendi kuona watumishi wanamalalamiko kila mtu atimize wajibu wake kwa weledi na ubunifu kwani watumishi ndiyo msingi wa serikali,"alisema Kikwete.

Alisema kwa upande wa watumishi aliwataka wafanye kazi kwani wao ni chachu ya maendeleo na wawe na utumishi utakaoweza kupimwa kwa kutoa huduma bora kwa wateja.

"Kuna baadhi ya watumishi wanacheza karata ofisini hii inaonyesha ni kukosa ubunifu haipendezi watu wanachangamoto nyingi wanahitaji kupatiwa huduma na nyie mliajiriwa kwa ajili yao hivyo mnapaswa kuwajibika kwa wananchi,"alisema Kikwete.

"Kwa mwaka wa Fedha 2023/2024 Serikali inategemea kutumia jumla ya shilingi bilioni 10.8 kwa ajili ya Bajeti ya Mishahara kwa watumishi wa Umma katika matukio mbalimbali ya kiutumishi,"alisema Kikwete.

Alibainisha kuwa hata kwa bajeti ya nyuma ya mwaka wa Fedha 2022/2023 Serikali ilitegemea kutumia jumla ya shilingi bilioni 9.7 kwa ajili ya Bajeti ya Mishahara kwa watumishi wa Umma katika matukio mbalimbali ya kiutumishi hali inaoonyesha serikali inakabili changamoto za fedha za watumishi wa umma.

Naye Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge alisema kuwa watumishi wanapaswa kuboresha utendaji kazi wao ili malengo ya Rais Dk Samia Suluhu Hassan ya kuwaletea maendeleo wananchi yafikiwe.

Kunenge alisema kuwa endapo kila mtumishi wa umma atawajibika kwenye sehemu yake malalamiko ya wananchi hayatakuwepo hivyo lazima waongeze uwajibikaji.

Mwisho.

Monday, July 10, 2023

HALMASHAURI YA MJI YAPONGEZWA KUPITIA TASAF

HALMASHAURI ya Mji Kibaha imepongezwa kwa kutekeleza kwa vitendo uhawalishaji wa fedha kwa kaya maskini kiasi kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) cha shilingi bilioni 3.1 kwa kaya 2,583.

Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejmenti ya Utumishi wa Umma Ridhiwani Kikwete kwenye mtaa wa Miwaleni kata ya Visiga alipokea akipokea taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini.

Kikwete alisema kuwa katika kipindi cha miaka miwili ya Rais wa awamu ya Sita Dk Samia Suluhu Hassan serikali imetoa bilioni 51 kwa ajili ya mpango huo wa kusaidia wananchi.

Alisema kuwa wakati Rais wa awamu ya tano Dk John Magufuli aliacha mpango huo ukiwa kwenye awamu ya pili na ulikuwa ukitekelezwa kwa asilimia 75 lakini sasa wananchi wote wanafikiwa.

"Hadi sasa watu milioni 1.3 wananufaika na mpango huu wa kunusuru kaya maskini hali ambayo inaonyesha jinsi gani serikali inavyohakikisha wananchi wananufaika na miradi mbalimbali,"alisema Kikwete.

Alisema kata hiyo ulipo mtaa huo miaka tisa ilikuwa ni moja ya maeneo ysliyofanyiwa majaribio lakini leo watu wamenufaika na kuboresha maisha yao.

"Niwapongeze Halmashauri kwani hapa naona mabadiliko ni makubwa fedha zilizotolewa zinaonyesha matunda kwani zimebadili maisha ya watu kwani wamejikomboa kiuchumi,"alisema Kikwete

Aidha alisema kuwa kulikuwa na changamoto ya ucheleweshaji malipo lakini kwa sasa hilo halipo na mambo yanakwenda vizuri ili kila mwananchi anayelengwa na mpango afikiwe.

Akielezea kuhusu mpango huo mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mhandisi Mshamu Munde alisema kuwa katika malipo ya dirishani kwa mwezi Januari na Februari mwaka 2023 kiasi cha shilingi milioni 12.7 kililipwa kwa kaya 312 huku kiasi cha shilingi milioni 91 zililipwa kwa njia ya mitandao ya simu na benki kwa kaya 2,168.

Munde alisema kuwa kwenye miradi ya uendelezaji miundombinu kumefanyika ujenzi wa nyumba ya watumishi zahanati ya Vikawe na ujenzi zahanati ya Mwanalugali zote zikiwa zimepatiwa milioni 91.9 kila moja.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson John alisema kuwa viashiria bora vya wanufaika ni uundaji wa vikundi ambavyo havina upotevu wa fedha.

John alisema kuwa walengwa wanaunda vikundi ambavyo vinajikopesha na kujikwamua kiuchumi kupitia Tasaf ni mkombozi kwa watu ambao walikuwa na hali mbaya ya kimaisha.

Naye Ester Mlinge ambaye ni mnufaika alisema kuwa ameweza kuboresha maisha yake kutoka kwenye kupanga nyumba hadi kumiliki nyumba ambayo anaishi na familia yake.

Mlinge alisema mbali ya kujenga nyumba pia wameanzisha vikundi vya kukopeshana ambapo hadi sasa wana akiba ya shilingi milioni 1.1.

TASAF YATAKIWA KUANDAA TAARIFA ZINAZOAKISI MAFANIKIO YA TASAF


NAIBU Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete amewataka waratibu wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kwenye wilaya nchini kuandaa taarifa zinazoakisi mafanikio au changamoto ya mfuko huo.

Kikwete aliyasema hayo jana akipokea taarifa ya Tasaf kwenye mkoa wa Pwani wakati wa ziara yake aliyoanzia Halmashauri ya Mji Kibaha.

Alisema kuwa taarifa hizo zinapaswa kuwa na uchambuzi wa kina ili kuweza kujua mafanikio ya mpango huo na kama kuna changamoto serikali iweze kufanya maboresho.

"Taarifa inabidi ziakisi ili wale wanaofuzu wawe na vigezo isije wakaondolewa kwenye mpango halafu baadaye wakarudi walikotoka na walio kwenye mpango wajikwamue kiuchumi na kuboresha maisha yao,"alisema Kikwete.

Alisema kuwa baadhi ya maeneo hasa kupitia fedha za kujiinua kiuchumi ambapo wilayani Rufiji limejengwa vizuri sana na akinamama wanne wa mpango huo nao wanafanyabiashara kwenye soko hilo.

Kwa upande wake Mratibu wa Tasaf mkoa wa Pwani Roselyne Kimaro alisema kuwa Uhawilishaji wa fedha kwa kaya maskini (CCT) kwa kipindi cha 2023 ni shilingi bilioni 14.2 zimetolewa kwa walengwa ambapo zimesaidia walengwa kuongeza kipato.

Kimaro alisema kuwa mpango wa kunusuru kaya maskini hadi kufikia Juni 2023 kaya zinazonufaika na mpango ni 35,427 kutoka 37,663 na upande wa ajira za muda mpango katika kipindi hicho zimepokelewa kiasi cha shilingi bilioni 2 ikiwa shilingi bilioni 1.4.

Alisema kuwa malipo ya ujira na ununuzi wa vifaa kiasi cha shilingi milioni 568.6 zilitolewa kwa ajili ya miradi 296 iliyoibuliwa katika vijiji 224 ambapo miradi hiyo imetekelezwa na walengwa 10,904 na mpango huo umetekelezwa kwa Halmashauri nne za Bagamoyo, Chalinze, Kibaha na Kisarawe.


MHE.MASANJA AFANYA MKUTANO WA HADHARA SENGEREMA, AGUSA MAKUNDI MAALUM

 


MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Mwanza na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja amekabidhi baiskeli tano zenye thamani ya shilingi milioni tatu kwa wananchi wenye ulemavu wa miguu Wilayani Sengerema na kuahidi kuwalipia bima ya afya, ikiwa ni mwendelezo  wa ziara yake ya kukutana na makundi maalum katika Jamii Mkoani Mwanza. 


Akizungumza katika mkutano wa hadhara katika eneo la Stendi ya zamani Mhe. Masanja amesema Serikali ya Awamu Sita inayoongozwa na Rais Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan imeweka mikakati ya kutatua changamoto za makundi maalum yasiyojiweza katika jamii hivyo msaada huo ni utekelezaji wa ilani ya CCM.


Mhe. Masanja amewaelekeza Madiwani na viongozi wengine wa Serikali kuibua wananchi wenye changamoto mbalimbali za ulemavu ili Serikali iwafikie na kuwasaidia.


"Kama kuna wananchi huko hawawezi kutembea wengine mmewaficha ndani, na kama kuna watoto wadogo hawawezi kwenda shule waleteni Serikali itawahudumia" Mhe. Masanja amesisitiza.


Aidha, Mhe. Masanja amewataka wananchi kuhakikisha wanaiunga mkono Serikali na kuipigia kura katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu unaokuja. 


Katika mkutano huo, Mhe. Masanja amesikiliza changamoto za baadhi ya wananchi kuhusu kero ya watumishi wa  maliasili kukamata baiskeli na pikipiki za wananchi, kero za maji, kero ya uhaba wa vifaa vya kujifungulia katika vituo vya afya,ardhi, uhaba wa walimu kero za  wafanyabiashara ndogondogo.


Mhe. Masanja ameahidi kuziwasilisha kero hizo katika Sekta husika na kufanyia kazi kero zinazohusu Sekta ya Maliasili na Utalii.

UWEKEZAJI BANDARI MANUFAA UCHUMI WA NCHI

Halmashauri kuu ya ccm Taifa ( NEC) imepokea na kujadili kwa kina taarifa ya makubaliano ya Uwekezaji na uendeshaji wa bandari na kuazimia kwamba Uwekezaji na uendeshaji wa bandari hiyo ni kwa manufaa ya uchumi wa Nchi pamoja na utekelezaji wa vitendo vya Ilani ya CCM ya Mwaka 2020 - 2025.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma katibu wa Halmashauri kuu ya Ccm Itikadi na Uenezi Bi Sofia Mjema amesema halmashauri kuu ya Ccm imekutana Katika kikao Chake Cha kawaida chini ya mwenyekiti wa Ccm na RAIS wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hasani.

Mjema amesema kikao hicho kimeazimia kwamba serikali iongeze kasi ya kutoa Elimu kwa wananchi juu ya uhalisia uliomo Katika makubaliano ya Uwekezaji na uendeshaji wa bandari.

Sunday, July 9, 2023

VYAMA VYA SOKA VYATAKIWA KUWA NA UTAWALA BORA





VYAMA vya Soka Nchini vimetakiwa kuzingatia utawala bora ili kuhakikisha sheria miongozo na taratibu za mpira zinafuatwa ili soka liweze kuimarika na kupata timu na wachezaji bora.

Hayo yalisemwa mjini Kibaha na Mkurugenzi  wa Sheria Habari na masoko kutoka Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Boniface Wambura wakati wa semina elekezi kwa Kamati Mbalimbali za Chama Cha Soka Wilaya ya Kibaha (KIBAFA).

Wambura alisema kuwa utawala bora kwenye mpira unasaidia kuhakikisha mpira unachezwa kwa kuzingatia taratibu za mpira zilizowekwa na chama husika.

"Utawala bora unaonyesha kila mtu anawajibika kwa nafasi yake pasipo kuingiliana kwenye majukumu yao ya kiutendaji,"alisema Wambura.

Alisema kuwa mpira una taratibu zake hivyo ili mpira uchezwe lazima sheria zake zifuatwe kwani tofauti na hapo klabu na nchi haitaweza kuwa na timu wala wachezaji wazuri.

"Kwa sasa mambo yamebadilika tofauti na zamani ambapo kulikuwa na migogoro mingi lakini kwa kuwa mambo yanaendeshwa kwa weledi na mpira umebadilika timu zimekuwa nzuri na wachezaji wana ubora,"alisema Wambura.

Aidha alisema kuwa mpira umekuwa na hadhi kutokana na kuwekwa mifumo mizuri ambapo kila mtu anafanya kazi kwa nafasi yake na huo ndiyo utawala bora.

Kwa upande wake mwenyekiti wa KIBAFA Robert Munis alisema kuwa lengo la kuandaa semina elekezi kwa kamati hizo ni kuwaelekeza viongozi kila mmoja kujua mamlaka yake.

Munis alisema kuwa moja ya changamoto zinazojitokeza ni baadhi ya viongozi kutofahamu majukumu yao hivyo kuwa na mwingiliano kiutendaji.

Awali katibu wa Chama Cha Soka Mkoa wa Pwani (COREFA) Mohamed Masenga alisema kuwa wao wanasimamia wilaya ili kuhakikisha mipra unachezwa.

Masenga alisema kuwa wanakipongeza chama hicho kwa kuandaa semina hiyo na kuvitaka vyama hivyo kuandaa semina kama hizo ili kuwajengea uwezo viongozi.