Friday, March 29, 2024

*DKT.SHEMWELEKWA AWAFUNDA WATUMISHI KIBAHA.*

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Dkt.Rogers Shemwelekwa siku ya Jumatano 27 Machi,2024 amefanya kikao rasmi na watumishi kwa lengo la kufahamiana, kujitambulisha na kutoa mwelekeo kiutendaji.

Dkt.Shemwelekwa aliyeteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan tarehe 13 Machi,2024 kuwa Mkurugenzi wa Kibaha Mji amesifu mifumo mizuri iliyowekwa na Watangulizi wake akiwemo Bi.Jenifa Omolo ambaye kwa Sasa ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mhandisi Mshamu Munde aliyehamishiwa Halmashauri ya Nanyamba na kwamba kazi yake Sasa ni kutengeneza kemia mpya itakayotumika ili kufikia malengo ya Serikali ya kuwahudumia wananchi 

Dkt.Shemwelekwa amewataka watumishi kutoa huduma Bora kwa wananchi wakiwa na furaha,kuondoa hofu,woga na wasiwasi na kwamba unapokuwa ofisini mwananchi ana matumaini makubwa nawe ya Kusikilizwa na kutatuliwa changamoto zake.

Aidha,Dkt.Shemwelekwa amewaasa watumishi kuwa wanyenyekevu kwa wananchi,kutumia lugha za staha,kuheshimiana,kushirikiana,kupendana na kusaidiana ili kufanya kazi zenye matokeo na zinazoacha alama za kukumbukwa huku akikemea vikali tabia za kufanyakazi kwa mazoea zisizokuwa na tija kwa Taifa letu.

"Watumishi wa Umma tuache kulalamika,tujielekeze kwenye kuondoa malalamiko na kero za wananchi.Tuwasikilize vizuri na kuwahudumia tukiwa na furaha"...amesema Dkt.Shemwelekwa.

Akizungumzia ukusanyaji wa Mapato ametoa rai kwa watumishi wote kushiriki na sio kuwaachi Kitengo cha fedha na Divisheni ya Biashara pekee kama ilivyozoeleka huku akitoa rai ya kuongeza uadilifu,uaminifu na kuziba mianya yote inayovujisha ama kuchepusha Mapato na kwamba atakayefanya hivyo hata mvumilia.

"Ndugu zangu tukakusanye Mapato kwa uaminifu na uadilifu ili yatumike kwa Maslahi mapana ya watu wote,atakaye thubutu kwenda kinyume atakumbana na mkono wa sheria" ameongeza

Dkt.Shemwelekwa amekumbusha watumishi kuwahi Kazini kama sheria,Kanuni na taratibu za Utumishi wa Umma zinavyoelekeza na kwamba hiyo sio hiari ni takwa la Kisheria linalomtaka mtumishi kufanya kazi kwa saa nane kwa siku

Mary Chimoto na Hassan Ngonyani  wamesifu utaratibu mpya kiutendaji wa Mkurugenzi Dkt.Shemwelekwa na kwamba kilichobaki ni utekelezaji 

Mkuu wa Divisheni na Utumishi na rasilimali watu Dibogo Protas amesema kazi yake kwenda kutafsiri sheria,Kanuni na taratibu kwani watumishi Sasa wamekumbushwa upya wajibu wao.


Dkt.Rogers Shemwelekwa ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kutumiza miaka mitatu Madarakani kwa kuendelea kuwekeza kwenye Miradi mikubwa ya Kimkakati nchini ikiwemo Kibaha Mji ambayo imenufaika na Soko kubwa lenye thamani ya Bilioni nane

MWENYEKITI UVCCM WILAYA YA MPWAPWA AFURAHISHWA NA SOKA



Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana UVCCM Wilaya ya Mpwapwa Yohana Malogo ameendelea na ziara yake katika Kata ya Godegode kimagai na vingh'awe katika kijiji cha isingh'u

Akiwa katika kata ya Vingh'awe kijiji cha Ising'u ameshudia mechi Kati ya Miondo Fc dhidi ya Bondeni Fc

Ambapo amesema Mpira ni Mchakato na mwezi wa tano watakuwa na ligi ya Ngo'mbe

"Tumeona tufike hapa tuone mchezo wenu lakini pia tuwasalimie na tufahamiane"Amesema Malogo

"Tuwaombe tushirikiane,karibuni Ofisini kwetu ile Ofisi siyo ya kwangu,wala siyo ya katibu ni Ofisi yenu vijana Wilaya nzima yakuwasilisha changamoto na matatizo na adha zote zinazohusu vijana kwenye idara ya michezo na idara zingine"Amesema

Naye Katibu wa Umoja wa Vijana UVCCM Wilaya hiyo Alhabib Kibamba amesema kuwa kwa sababu ya serikali imesimama vizuri chini ya Chama Cha Mapinduzi ndo maana tuna amani na tunacheza tukiwa na furaha

Kwa Upande wake Diwani wa kata hiyo ya Vingh'awe Mahuwi Dickson amesema kuwa lengo la bonanza ni kuwaweka vijana pamoja,na Kujenga Mahusiano mazuri baina ya vijana

"Mashindano haya ni ya kata ni vijana ambao wanatoka katika eneo langu la kata mwisho wa siku nahitaji vijana hawa nipate timu bora ambayo sasa nitashirikisha na kata ya jirani"amesema

Aidha ameongeza kuwa mei mosi wataanza tena mashindano ya kushindania Ngo'ombe.

Wednesday, March 27, 2024

BMH YAITEMBELEA WIZARA YA AFYA NA HOSPITALI YA LUMUMBA ZANZIBAR

Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) ya jijini Dodoma inatarajia kuanzisha ushirikiano wa matibabu na Hospitali ya Rufaa ya Mjini Magharibi (Lumumba), Zanzibar katika huduma za kibingwa. 

Ushirikiano huu utalenga kubadilishana uzoefu kati ya Hospitali hizi mbili za umma.

Akiongea, Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mhe.Hassan Khamis Hafidh, amepongeza ujio wa Viongozi wa BMH na kuwa Hospitali ya Lumumba itanufaika kwa kubadilishana uzoefu.

"Nimefika Hospitali ya Benjamin Mkapa Dodoma nikajionea utayari wa Madaktari Bingwa na Vifaa vya kisasa mnavyovitumia, nimefika kwenye wodi maalumu ya Uloto nikiri kwamba naona fahari kuja kwenu hapa maana yapo mengi tutakayo chukua kupitia ushirikiano huu," amesema Mhe Naibu Waziri.

Ameyasema hayo wakati uongozi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa ulipomtembelea ofisini kwake.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu Bi. Prisca Lwangili, akimwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa BMH, amesema "Hospitali ya Benjamin Mkapa imekuwa kwa kasi na kutoa matibabu ambayo hayapatikani Afrika Mashariki na Kati.

"Hivyo tumeona ni muhimu kusogeza huduma hizi hapa Zanzibar kwa kuwa hapa pia kuna uhitaji wa huduma za Upandikizaji Uloto ili kutibu seli mundu," amesema. 

Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi wa Utafiti na Mafunzo wa BMH, Bi. Monica Kessy, uhusiano huu ni sehemu ya wajibu wa BMH ili kubadilishana uzoefu kati ya hospitali za umma.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Upasuaji BMH, Dkt. Januarius Hinju, ameeleza utayari kwa Madaktari Bingwa wa BMH katika huduma.

"Madaktari Bingwa wa BMH tupo tayari kushirikiana na wenzetu ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora," ameongeza.

WANAFUNZI WAASWA KUZINGATIA NIDHAMU


Juma la wadau wa Elimu Mkoa wa Dodoma limehitimishwa kwa viongozi mbalimbali  wa Mkoa wa Dodoma kuzungumza na kushiriki chakula cha mchana na wanafunzi wa Shule za kidato cha sita za Mkoa huo.

Kwa nyakati tofauti akiwa katika shule ya Sekondari ya wavulana Kongwa na Shule ya wasichana Kibaigwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule amewaasa wanafunzi hao kuendelea kudumisha nidhamu hususani katika kipindi hiki wanachojiandaa na mitihani yao na kuachana na marafiki wasiofaa ambao watawasababishia matokeo yatakayogharimu maisha ya ndoto zao.

"Tunataka alama A zenye hapa kuna wenzenu wamechafua jina la Shule na nyie mliopo hapa tunategemea nyie mtabadilisha sura hii ambayo sio njema kwa Mkoa, acheni tabia ya kufuata mkumbo kwa kushawishiana mambo yasiyofaa kwasababu kila mtu ana ndoto yake na kila moja atarudi nyumbani kwao kivyake na usipokuwa makini utaharibu maisha yako kwa mikono yako mwenyewe kwasababu tuu ya ushawishi usiofaa kutoka kwa marafiki zenu.

"Lazima muamue kuachana na baadhi ya mambo na kufuata miongozo yenu na kufanya bidii ili kujitofautisha na wengine na kuongeza ufaulu wenu na kujenga dhana nzuri ya shule Bora ni lazima muwe na ufaulu bora na Shule hii ambayo nyie ndio waanzilishi itapata sifa nzuri na sisi kama Mkoa tunayo matarajio kutoka kwenu kupitia matokeo mazuri mtakayotuletea," ameasa Senyamule

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka Simon amewataka wanafunzi hao kuendelea  kujitunza vizuri  kwa kujiweka bize na masomo na shughuli za kielimu ili kuepukana na vishawishi mbalimbali vitakavyowafanya kupata ufaulu usiofaa na kujenga picha mbaya ya shule yao.

Kwa upande wake ofisa Elimu Mkoa  Mwl. Vincent Kayombo amesema Mkoa wa Dodoma unaendelea na maandalizi ya kuhakikisha Mkoa unapata matokeo mazuri katika mitihani ya kidato cha sita inayotarajiwa kufanyika kuanzia Mei 6, Mwaka huu.

Aidha Mwl.Kayombo ameweka bayana kuwa Mkoa umefanya maandalizi ya kuhakikisha wanafunzi wa shule zenye kidato cha sita za Mkoa huo wanashiriki chakula cha mchana na viongozi mbalimbali ikiwa ni katika kuwahamasisha, kuwatoa hofu na kuwajengea ujasiri wanafunzi hao katika kuelekea mitihani yao ya kuhitimu ngazi hiyo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka Simon amewataka wanafunzi hao kuendelea  kujitunza vizuri  Kwa kujiweka bize na masomo na shughuli za kielimu ikiwemo michezo ili kuepukana na vishawishi mbalimbali vitakavyowafanya kupata ufaulu usiofaa na kujenga picha mbaya ya shule yao.

KATA YA LUPETA WALILIA MAJI

Wananchi wa Kijiji Cha kata Lupeta wilaya ya Mpwapwa Jijini Dodoma  wameiomba serikali kuwapelekea huduma ya maji ili kukabili changamoto hiyo.

Hayo yamebainishwa tarehe 26 Machi 2024 wakati wa ziara ya Mwenyekiti wa UVCCM wilaya ya Mpwapwa Yohana Malogo kukagua uhai wa Jumuiya, kusajili wanachama wapya
 na kuhimiza ulipaji wa ada.

Walisema kuwa kilio cha maji katika Kata yao imekuwa ni changamoto kiasi cha kushindwa kujua tatizo hilo litaisha lini na serikali inampango gani kwao ili kukabili hali hiyo.

Kwa upande wake Fundi Mkuu wa Maji Geogre Francis Theophil amesema kuwa wapo baadhi ya wananchi wanakata mabomba ya maji usiku bila sababu yoyote kiasi Cha kwamba wanakwamisha swala la maji kupatikana Katika Kijiji hicho.

Theophil amesema kuwa kuna changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na baadhi ya watu kukata mabomba hali inayosababisha maji kumwagika chini.

Naye Diwani ya Kata ya Lupeta Sospeter Moonho amewahakikishia wananchi mradi wa maji tiririka kufika mwezi wa nne utaenda ili kusaidiia kumtua mama ndoo kichwani pamoja na kuwahakikishia wananchi pia wanaenda kuanza ujenzi wa jengo la zahanati.

Moonho amesema kuwa atahakikisha ujenzi wa jengo la zahanati linakamilika na kama hajakamilisha aulizwe.

Kwa upande wake Mwenyekiti umoja wa Vijana wa Chama Cha mapinduzi ( UVCCM) Yohana Malogo amewataka viongozi wa kata hiyo kuhakikisha mifuko iliyokopeshwa irudidishwe na ujenzi uanze na amewaomba kisima kijengwe kwenye kata hiyo.

Malogo amesema kuwa wanaenda kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa wahakikishe wanawasaidia wananchi na kiasi cha fedha kilichopo ujenzi uanze kwani hakuna sababu kuweka fedha wakati wote huku wananchi wakitaabika.

Lengo ya ziara hiyo ya mwenyekiti wa UVCCM ni kukagua uhai wa Jumuiya, kukagua madaftari ya wanachama, kusajili wanachama wapya na ulipaji wa ada, kuhamasisha kufanyika semina kwa viongozi wa kata na Mitaa pamoja na kikao cha ndani na wanachama.

Tuesday, March 26, 2024

SERIKALI KUFUATILIA SUALA LA ELIMU NCHINI

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amewataka Maofisa Elimu Kata nchini kufuatilia maendeleo ya shule kwa kuwatembelea walimu na kusikiliza kero zao

Aidha amewataka walimu kuhakikisha wanafanya tathmini ya uelewa wa wanafunzi kwa kuwapatia mazoezi mengi.

Majaliwa ameyasema hayo Machi 25, 2024   kwenye ukumbi wa TAG Mipango Jijini Dodoma wakati wa kilele cha Juma la wadau wa Elimu Mkoa.

Amesema maofisa elimu hao wafuatilie masuala ya walimu na kutatua changamoto zao ili wafanye kazi vizuri.

"Walimu nanyi hakikisheni mnafanya tathmini ya uelewa wa wanafunzi kwa kuwapatia mazoezi mengi kadri iiwezekanavyo,"amesema Majaliwa.

Fedha zinazotolewa kwa ajili ya maendeleo ya Elimu, zitumike kwa ajili hiyo,"amesisitiza Majaliwa.

Amebainisha kuwa Kauli mbiu ya mkutano huo inakwenda sambamba na Sera ya Elimu ya nchi inayosisitiza Uwajibikaji, Utoaji wa Elimu Bora ni vipaumbele vya nchi. 

"Serikali yetu inaimarisha mazingira ya utoaji Elimu kwa kuboresha miundombinu na Elimu bila ada kwani mpaka Sasa shilingi Trilioni 1 zimetolewa kufanikisha hili,"amesema Majaliwa.

Waziri Mkuu ameipongeza Dodoma kwa kuandaa Mkutano huo kwani unakwenda sambamba na Sera ya Elimu ya nchi.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Senyamule amesema Serikali ya awamu ya Sita imefanya mambo mengi kwenye sekta ya Elimu.

Senyamule amesema kuwa wanamshukuru Rais kwa kuinua sekta ya Elimu Dodoma kwani wameimarika sana kipindi cha miaka hii mitatu Dodoma imepanda ufaulu wa darasa la saba na kuingia kumi bora kitaifa mwaka 2022 kwa ufaulu kupanda kutoka 83% mwaka 2022 hadi 87%mwaka 2023 na wameanza kuweka mikakati ya Mkoa kuhakikisha kila mwaka ufaulu unaongezeka.

Ametaja mafanikio yaliyopatikana kipindi hiki kuwa ni ujenzi wa miundombinu ya elimu iliyogharimu shilingi bilioni 92.4 , miradi ya BOOST shilingi bilioni 10.6 iliyowezesha ujenzi wa madarasa 196 na matundu ya vyoo 154 fedha nyingine ni kutoka miradi ya SEQUIP, SWASH, TEA , EP4R na mingine mingi ambayo kwa pamoja imeboresha kiwango cha elimu.

Mkutano wa wadau wa Elimu Mkoa wa Dodoma umefuatia matukio kadhaa yaliyofanyika kwa Juma zima ikiwemo kukimbia mchaka mchaka kwa wanafunzi, uzinduzi wa Bonanza la michezo, ugawaji wa mipira 1000 kwa shule za Msingi za Mkoa kutoka Shirikisho la michezo nchini (TFF).

Pia Juma hilo limewezesha uzinduzi wa kwaya ya Mkoa wa Dodoma, midahalo kwa wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari na kufunga mafunzo kwa wahitimu wa skauti Mkoa.

Juma la wadau wa Elimu Mkoa wa Dodoma limefikia kilele chake likiongozwa na kauli mbiu ya "Uwajibikaji wangu ni msingi wa kuinua ubora wa Elimu na ufaulu Dodoma".

Lengo hasa la Mkutano huo ni kujadili namna ya kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya Elimu Mkoa wa Dodoma pamoja na kuweka mikakati ya kuinua Taaluma na ufaulu kimkoa pamoja na kuzindua rasmi Mpango Mkakati wa Elimu Mkoa.

Monday, March 25, 2024

VIONGOZI WAPYA WA KANISA WAPEWA NENO

Na Wellu Mtaki, Dodoma 

Viongozi wa kanisa la Dayosisi Central Tanganyika (DCT ) Mtakatifu Paulo Parishi ya Ndachi Dodoma wamewataka viongozi waliosimwikwa katika Kanisa hilo kuwa mfano ili kujenga jamii yenye maadili.

Hayo yamebainishwa na Mchungaji wa Parishi ya Ndachi Msalato Dodoma  Christopher  Njiliho  Leo Machi 24 ,2024 baada ya kumalizika kwa ibada ya kusimikwa kwa viongozi wa idara mbalimbali ndani ya kanisa hilo ambapo wamesema kuwa kanisa lina nafasi nzuri ya kujenga jamii bora.

"Ninawaomba sana viongozi muwe  wa kwanza kuacha dhambi, kuacha vitendo vibaya ili muende kufundisha wengine ukiwa mfano watu watakusikiliza sana na watapokea ujumbe ambao utawapelekea ili kuzuia vitendo viovu,"amesema Njiliho.

Aidha amesema kuwa kanisa linatakiwa kuwa mfano wa kuigwa ili kuhakikisha linajenga Vijana walio imara kwa kuzingatia maadili na taratibu za Taifa la Tanzania.

Kwa upande wake Mlezi wa idara ya kina Mama  Violeth Njiliho amesema kuwa Vijana wengi wamepotea kwa kukosa Maadili hivyo kama kanisa wanapenda kuhamasisha Vijana kushiriki semina mbalimbali ili kubadilisha mwenendo na kuongeza nguvu kazi kwa Taifa na kanisa .

"Vijana ni nguvu kazi ya Taifa pia ni nguvu kazi ya kanisa Vijana wengi wamepotea kwa kukosa maadili kama kanisa tunaenda kuhamasisha  Vijana wetu waweze kupata semina mbalimbali ili waondoke katika hatua waliyonayo ya utandawazi ili warudi kumtegemea Mungu,"amesema Violeth

Naye Mhasibu wa parishi ya Ndachi Amos Mchoro amesema kuwa kanisa linategemea kuanzisha mradi wa Ujenzi wa frem za maduka ambayo yatasaidia kuinua pato la kanisa na muumini mmoja mmoja kwa kutoa na fursa zitokanazo na mradi huo.

"Mpango tulionayo kwa ajili ya Vijana wa mitaani tunategemea kuanzisha mradi wa kufungua frem za biashara kwa ajili ya kukodisha waumini wote na ambao sio waumini,"amesema Mchoro

Pia amesema kuwa kanisa lipo kwenye mchakato wa kutafuta namna ya kukopeshwa mikopo kwa vijana ili kuhakikisha kila kijana ananufaika na mkopo huo ili kuweza kujikwamua kiuchumi.

"Tunakusanya Vijana ambao wapo mtaani ili kuwavuta walijue neno la Mungu pamoja na kutafuta fedha na kuanza kujikopesha kwa watu ambao wanasali katika kanisa hili na wasio wa kanisa hili,"amesema Mchoro.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Vijana Parishi ya Ndachi Msalato Timotheo Hoya amewataka Vijana wamtumikie Mungu na waachane na vitendo rushwa, wizi, ulawiti pamoja na matumizi ya madawa ya kulevya.

"Vijana wa kanisa wamtumikie Mungu kwa kipindi hichi madam Tanzania kwa sasa inakumbana na matatizo mbalimbali kama matatizo ya rushwa, ukatili , wizi,na matumizi ya madawa ya kulevya,"amesema Hoya.

Awali Mwenyekiti wa Idara ya watoto Joyce Jackson amewahimiza wazazi kuhakikisha wanawakuwakumbusha watoto kwenda kanisani ili kuweza kulishika neno na kulitambua ili kuondokana na vitendo viovu vya ulawiti kwa watoto.

"Mtoto akitembea na neno kwa njia ya haki huwezi kumfanyia ulawiti kutokana na mtoto kutambua vitu viovu na anaishi ndani ya maadili pia nawasihi wazazi wawalete watoto wao makanisani nashangaa kuona mzazi anamwacha mtoto chini ya miaka 15 nyumbani bila kumhimiza kufika kanisani," amesema Jackson.

Kanisa la Dayosisi Central Tanganyika (DCT) la Mtakatifu Paulo Parishi ya Ndachi Dodoma limesimika viongozi 70 katika idara mbalimbali huku likiwa linahudumia wazee vijana na watoto.