Wednesday, September 27, 2023

TIMU YA NYUMBU YAENDELEA NA MICHEZO YA KUJIPIMA NGUVU YATOKA SARE 1-1 NA POLISI TANZANIA

TIMU ya Soka ya Nyumbu ya Mkoani Pwani inayojiandaa na ligi daraja la Pili imetoka sare ya goli 1-1 na timu ya Polisi Tanzania kwenye mchezo wa kirafiki uliofanyika kwenye uwanja wa Chuo Cha Polisi Kurasini Jijini Dar es Salaam.

Nyumbu huo ni mchezo wake wa pili wa kujipima nguvu ambapo jana ilicheza na timu ya Mashujaa ya Mkoani Kigoma ambayo inashiriki ligi Kuu ya NBC Premium League ambapo pia ilitoka sare ya kufungana goli 1-1 kwenye uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya michezo hiyo kocha mkuu wa timu hiyo Rajab Gwamku amesema kuwa anafurahishwa na viwango vya wachezaji wake kupitia michezo hiyo ya kujipima nguvu waliocheza.

Gwamku amesema wataendelea kucheza michezo ya kirafiki zaidi ili kuiimarisha timu yake kabla ya kuanza kwa michezo ya ligi daraja la pili kwa kipindi itakapopangwa kuchezwa ligi hiyo.

Amewaomba Wanapwani kuiunga mkono timu yao ili iweze kufanya vyema kwenye ligi daraja la pili na kupanda daraja la kwanza huku malengo yakiwa ni kupanda ligi kuu ili kuuwakilisha vyema mkoa huo.

WAFUGAJI WILAYANI KIBAHA WABUNI MBINU YA ULINZI KULINDA MIFUGO YSO



KUFUATIA vitendo vya wizi wa mifugo kushamiri Chama cha Wafugaji Wilaya ya Kibaha mtaa wa Mwanalugali kimeweka mkakati wa kutumia ulinzi shirikishi ili kudhibiti vitendo hivyo.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na mwenyekiti wa chama hicho Haji Myaya alisema kuwa wamefikia maamuzi hayo baada ya kikao na wafugaji ambapo ndani ya wiki moja matukio matatu ya wizi yametokea

Myaya alisema kuwa changamoto ya wizi wa mifugo hasa ng'ombe umekuwa ukijitokeza mara kwa mara na kuwasababishia umaskini wafugaji na kuamua kuwa na walinzi hao.

"Tumekaa kikao na kukubaliana wanachama wote kutoa michango ya kila mwezi ili kuwalipa walinzi hao kupitia ulinzi shirikishi ili watulindie mifugo yetu na hata mali za wananchi,"alisema Myaya.

Alisema kuwa wezi hao huiba na kuwachinja ng'ombe na kisha kuchukua nyama na kwenda kuiuza sehemu zisizojulikana ambapo huacha vichwa na utumbo tu.

Naye Mwenyekiti wa wafanyabiashara wa nyama na mfugaji Aidan Mchiwa alisema kuwa kwa kushirikiana na chama cha wafugaji wamekuwa wakikabiliana na wezi wa mifugo kwa kuwa na mikakati mbalimbali ya kiulinzi.

Mchiwa alisema kuwa moja ya njia ni kuhakikisha nyama inayouzwa inakuwa imethibitishwa na mganga wa mifugo kwa kugongwa muhuri wa serikali ili kuepuka kuuza nyama ya wizi.

Alisema kuwa wafugaji wanashauriwa kuwa na mawasiliano ya simu ili linapotokea tukio la wizi wanaungana kwa pamoja na kufuatilia ng'ombe ambapo juzi walifanikiwa kurudisha ngombe watano ambao waliibiwa na kupelekwa Bagamoyo na wezi kukimbia.

"Tunashirikiana vizuri na jeshi la polisi katika kudhibiti wezi na kuwashauri wafugaji kutoa taarifa mapema wizi unapotokea ili kuwafuatilia wezi kabla hawajawachinja au kuwasafirisha mbali na kwenda kuwauza,"alisema Mchiwa.

Aidha aliwataka wafugaji kuwa na mahusiano mazuri na wafanyakazi wao wa mifugo kwa kuwalipa kwa wakati ili wasiingie vishawishi na kushirikiana na wezi kuiba mifugo.

WAFUGAJI KUTUMIA WALINZI SHIRIKISHI KULINDA MIFUGO YAO

KUFUATIA vitendo vya wizi wa mifugo kushamiri Chama cha Wafugaji Wilaya ya Kibaha mtaa wa Mwanalugali kimeweka mkakati wa kutumia ulinzi shirikishi ili kudhibiti vitendo hivyo.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na mwenyekiti wa chama hicho Haji Myaya alisema kuwa wamefikia maamuzi hayo baada ya kikao na wafugaji ambapo ndani ya wiki moja matukio matatu ya wizi yametokea

Myaya alisema kuwa changamoto ya wizi wa mifugo hasa ng'ombe umekuwa ukijitokeza mara kwa mara na kuwasababishia umaskini wafugaji na kuamua kuwa na walinzi hao.

"Tumekaa kikao na kukubaliana wanachama wote kutoa michango ya kila mwezi ili kuwalipa walinzi hao kupitia ulinzi shirikishi ili watulindie mifugo yetu na hata mali za wananchi,"alisema Myaya.

Alisema kuwa wezi hao huiba na kuwachinja ng'ombe na kisha kuchukua nyama na kwenda kuiuza sehemu zisizojulikana ambapo huacha vichwa na utumbo tu.

Naye Mwenyekiti wa wafanyabiashara wa nyama na mfugaji Aidan Mchiwa alisema kuwa kwa kushirikiana na chama cha wafugaji wamekuwa wakikabiliana na wezi wa mifugo kwa kuwa na mikakati mbalimbali ya kiulinzi.

Mchiwa alisema kuwa moja ya njia ni kuhakikisha nyama inayouzwa inakuwa imethibitishwa na mganga wa mifugo kwa kugongwa muhuri wa serikali ili kuepuka kuuza nyama ya wizi.

Alisema kuwa wafugaji wanashauriwa kuwa na mawasiliano ya simu ili linapotokea tukio la wizi wanaungana kwa pamoja na kufuatilia ng'ombe ambapo juzi walifanikiwa kurudisha ngombe watano ambao waliibiwa na kupelekwa Bagamoyo na wezi kukimbia.

"Tunashirikiana vizuri na jeshi la polisi katika kudhibiti wezi na kuwashauri wafugaji kutoa taarifa mapema wizi unapotokea ili kuwafuatilia wezi kabla hawajawachinja au kuwasafirisha mbali na kwenda kuwauza,"alisema Mchiwa.

Aidha aliwataka wafugaji kuwa na mahusiano mazuri na wafanyakazi wao wa mifugo kwa kuwalipa kwa wakati ili wasiingie vishawishi na kushirikiana na wezi kuiba mifugo.

Tuesday, September 26, 2023

MAOFISA ELIMU WALIMU WA HISABATI MKOANI PWANI WAPIGWA MSASA

WALIMU wanaofundisha somo la Hisabati Mkoani Pwani wametakiwa kutumia ufanisi umahiri na dhana stahiki kupitia mbinu za ufundishaji wa somo hilo ili kuongeza ufaulu.

Hayo yamesemwa Wilayani Kisarawe na Katibu Tawala (RAS) Mkoa wa Pwani Ramadhan Mchatta ambaye aliwakilishwa na Ofisa Elimu Mkoa Sara Mlaki wakati wa Mafunzo kwa viongozi wa elimu kuhusu uboreshaji ufundishaji na ujifunzaji wa umahiri wenye changamoto katika somo la hisabati kwa mkoa huo.

Mchatta amesema kuwa kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya wanafunzi kwenye somo la hisabati ambapo utafiti umebaini baadhi ya wanafunzi kufanya vibaya kwenye mitihani ikiwemo ile ya Mock Wilaya na Mkoa.

Naye mtaalamu kiongozi wa Shule Bora Vicent Katabalo ameupongeza Mkoa wa Pwani kwa kutekeleza vizuri afua mbalimbali za mradi wa Shule Bora na kutaka waendeleze jitihada ili kufikia malengo yaliyowekwa ili kuboresha ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi.

Kwa upande wake ofisa elimu mkoa wa Pwani Sara Mlaki amesema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuimarisha umahiri wa wa walimu na viongozi wa  Elimu  katika kutumia mbinu shirikishi za ufundishaji na ujifunzaji wa somo la Hisabati ili kuleta matokeo chanya kwa wanafunzi wote.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Ofisi ya Rais (TAMISEMI) kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia pamoja na Taasisi ya Elimu Tanzania kupitia Program ya Shule Bora ambayo inatekelezwa katika mikoa tisa ya Tanzania Bara kwa Ufadhili wa Serikali ya Uingereza na kwa Usimamizi wa Cambridge Education.

Mafunzo hayo yameendeshwa na  wawezeshaji kutoka vyuo vya Ualimu vya Tukuyu  na Mpwapwa ambapo washiriki wa  mafunzo hayo ni viongozi wa Elimu kutoka katika ngazi ya Mkoa  wakiwemo Walimu, Walimu  wakuu, Maofisa Elimu Kata, Maofisa Elimu Awali na Msingi kutoka katika Halmashauri tisa na shule teule za Wilaya ya Kisarawe.

Thursday, September 21, 2023

MAAFISA,WAKAGUZI, NA ASKARI POLISI KUTOKA MAKAO MAKUU WANOLEWA NAMNA BORA YA KUSHIRIKIANA NA WANANCHI

 


Na, Benedict Mlawa wa Jeshi la Polisi

MSEMAJI wa Jeshi la Polisi Nchini,Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi (SACP) David  Misime amefunga mafunzo ya siku mbili kwa Maafisa,Wakaguzi na Askari wa Polisi kutoka Makao Makuu na Mkoa wa Dodoma.

SACP Misime amewaeleza Askari hao kuwa mafunzo hayo ni mfululizo  wa mafunzo yanayotolewa kwa Askari  katika Vyuo ndani ya nchi, nje ya nchi na kazini kwa lengo la kuwabadilisha kifikra (mindset change) ili kutoa huduma bora kwa jamii.

SACP Misime amefungua mafunzo hayo Septemba 20, 2023   katika ukumbi wa Polisi Jamii Mkoa wa Dodoma Yakifanyika kwa engo la kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao ya kazi za Polisi kwa Nidhamu, Haki, Weledi na Uadilifu.

"Mkibadilika kifikra na kuhudumia wananchi kwa Nidhamu,Haki,Weledi na Uadilifu mtakuwa na uwezo wa kusimama mbele ya wananchi kifua mbele na kwa kutumia Falsafa ya Polisi,wananchi waka waamini na kuongeza imani kwa Jeshi la Polisi ili waoneshe ushirikiano katika kubaini na kuzuia uhalifu".Amesema Misime.

Pamoja na hayo, Misime amewapongeza Askari kwa kushiriki vyema katika mafunzo hayo na kazi kubwa wanayofanya huku akiwataka kwenda kuyafanyia kazi yale waliojifunza ili wananchi waweze kuona mabadiliko ya kifikra na  kiutendaji kulingana na mageuzi makubwa yanayoendelea ndani ya Jeshi la Polisi.

Awali akizungumza Mkuu wa Kitengo cha Dawati la Jinsia na watoto  kutoka  Makao  Makuu  ya Polisi Kamisheni ya Polisi Jamii  Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Faidha Suleiman amewasisitiza Askari wa Kike kuzingatia maadili, kutunza familia, kujijengea  uwezo wa kujiamini, kuwa wasafi na kuachana na vyanzo vyote vya mawazo kama vile kujiingiza katika mikopo isiyo na msingi ambayo muda mwingi huwapelekea kuwa ni watu wenye mawazo.

Hata hivyo, ACP Faidha Suleiman ambaye ni mratibu wa Dawati la Jinsia na watoto Makao makuu ya Polisi amewataka askari kuhakikisha wanafuata na  kutekeleza miradi ya Polisi Jamii katika majukumu yao ya kila siku kwani miradi hiyo inagusa kila kitengo cha Jeshi la Polisi. 

Amesisitiza katika kuzuia vitendo vya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa watoto katika familia zao na jamii kwa ujumla ikiwemo wao wenye kutokujifanyia ukatili. 

Naye Mkuu wa Dawati la mtandao wa Polisi wananwake (TPF Net) Makao Makuu ya Polisi Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Eva Stesheni amewataka askari kujifunza namna ya kuandika ripoti ya kazi zao ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi  pamoja na kuwasidia katika utunzaji wa kumbukumbu za nyaraka kwa kuwa na mpango kazi ulio mzuri ilikufikia malengo sahihi , Kuwasilisha taarifa, mawazo  na kuendeleza ujuzi  hasa kitengo cha Dawati la Jinsia na Watoto.

Mkuu wa dawati la jinsia na watoto  mkoa wa Dodoma mkaguzi wa Polisi  Teresina  Mdendemi amewataka askari kutoa huduma bora kwa wateja wa ndani na nje  kwani kupitia utoaji wa huduma bora huweza kusaidia kurahisha utendaji kazi wa kila siku na kusaidia katika kupambana na vitendo vya kihalifu hususani unyanyasaji wa kijinsia.

"Tutambue na  kufahamu aina ya wateja  Pamoja na  hisia zao pia tuwe  na moyo wa kusamehe kwa lengo la kuimarisha mahusiano mazuri kati ya Jeshi la Polisi na Jamii  katika kupunguza vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia  na ukatili dhidi ya watoto   na vitendo vyote vya kihalifu".Amesesisitiza Mdendemi

Kwa upande wake Mkuu wa  Dawati la Jinsia  mkoa wa Pwani  Mkaguzi  Msaidizi wa Polisi  Eliezer  Hokororo  amezungumzia  Faida na athari ya afya ya akili na kusema kuwa ukiponya akili umeponya maisha yako yote maana akili ni mfumo mzima maisha ya mwanadamu. 

Hokororo amesema kwamba watu wengi wameathirika na ugonjwa wa Sonona ambao umetokana na kukosekana na ubora wa afya ya akili na   kuchangia kuharibu Fikra, Hisia na Matendo ya mtu kutokana na kutokuwa na afya bora ya akili na mara nyingine kushindwa kabisa kutatua changamoto wananzokutana nazo.

Aidha Mkuu wa Dawati la Jinsia Mkoa wa Njombe Mkaguzi msaidizi wa Polisi Wilfred Willa  aliwataka askari wa kike kutambua na kuzingatia wajibu wao kwa kuihudumia vyema Familia na jamii huku akisema mwanamke anapaswa kuwa kioo na mwenye tabia njema maana ndiye nguzo kwa jamii.


Picha na Benedict Mlawa wa Jeshi la Polisi

Tuesday, September 19, 2023

ASHIKILIWA KWA KUMWAGIA CHAI YA MOTO DADA WA KAZI

JESHI la Polisi Mkoani Pwani linamshikilia mkazi wa Kwa Mathias Wilayani Kibaha Janeth Dominick (26) kwa tuhuma za kumwagia chai ya moto sehemu mbalimbali za mwili dada wa kazi Filomena Erick (17).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mjini Kibaha na Kamanda wa Polisi mkoani humo ACP Pius Lutumo ilisema kuwa mtuhumiwa alimuunguza dada huyo na chai aliyomwagia.

Lutumo amesema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 14 mwaka huu majira ya saa 2:00 asubuhi ambapo  mtuhumiwa ni mwajiri wake alimuunguza maeneo ya shingoni, mkononi, kifuani na tumboni.

"Mtuhumiwa alifikia hatua hiyo kwa kumtuhumu kuiba unga, sukari na simu ya mkononi katika chumba cha mpangaji mwenzao,"amesema Lutumo.

Amesema kuwa mtuhumiwa atafikishwa kwenye mifumo ya kisheria mara upelelezi utakapokamilika kuhusiana na tukio hilo.

"Jeshi la polisi linatoa rai kwa watu wote wanaoishi na wadada wa kazi kuacha kujichukulia sheria mkononi kwani tukio hilo halikubaliki katika jamii na ni kinyume cha sheria,"amesema Lutumo

Sunday, September 17, 2023

MWANAFUNZI ATAKAYE ONGOZA KITAIFA DARASA LA SABA KIPS KUPATA MILIONI TANO


MKURUGENZI wa Kampuni ya Njuweni Ltd Alhaj Yusuph Mfinanga ameahidi kutoa kiasi cha shilingi milioni tano kwa mwanafunzi atakayefaulu na kuongoza kitaifa kwenye mtihani wa kumaliza elimu ya msingi kutoka shule tatu zinazomilikiwa na kampuni hiyo. 

Aidha atawasomesha bure wanafunzi 20 watakaofaulu masomo ya kumaliza elimu ya msingi na kupata alama za daraja A kwa masomo yote ambapo watasoma kwenye shule za sekondari za kampuni hiyo za Vuchama Islamic Secondary School na Mangio Secondary School zilizopo Mkoani Kilimanjaro.

Mfinanga ameyasema hayo wakati wa mahafali ya shule hizo ambazo ni Kibaha Independence School (KIPS), Anex na Msangani zote zilizopo Wilayani Kibaha Mkoani Pwani.

Amesema kuwa ametoa fursa hiyo kama motisha kwa wanafunzi wa shule hizo ili kuhamasisha wafanye vizuri kwenye mitihani yao na kuzifanya shule hizo ziwe na matokeo mazuri.

Kwa upande wake mgeni rasmi Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini Silvestry Koka amesema kuwa sekta binafsi kwenye sekta ya elimu ina mchango mkubwa sana kwani inaipunguzia serikali mzigo wa wanafunzi.

Koka amesema kuwa licha ya ujenzi wa madarasa kujengwa na serikali mara kwa mara lakini bado kuna changamoto kubwa ya upungufu wa madarasa na miundombinu mingine hivyo ushirikiano na sekta binafsi unahitajika.

Kwa upande wake meneja wa KIPS Nuru Mfinanga amesema kuwa wanashirikiana vizuri na serikali katika kukabiana na changamoto mbalimbali zinazojitokeza kwenye sekta hiyo lengo likiwa ni kutoa elimu bora.

Mfinanga amesema kuwa wanaipunguzia mzigo serikali kwa kuwasomesha wanafunzi kupitia sekta binafsi na kuwataka wazazi kuwafuatilia watoto wao ili wafanye vizuri kwenye masomo yao na kuwataka walipe ada kwa wakati ili waweze kujiendesha na kutoa elimu bora.