Wednesday, June 28, 2023

VITUO MAALUMU 175 KWAAJILI YA HUDUMA MAHUTUTI KWA WATOTO WACHANGA VYAONGEZWA

 

NAIBU Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel amesema, Serikali imeongeza vituo vyenye vyumba maalumu kwa ajili ya kutoa huduma kwa watoto wachanga wenye umri kati ya sifuri mpaka mitano wenye hali mahututi (Neonatal  Care Unit), kutoka 18 mwaka 2017 kufikia 175 mwaka 2023. 

Amesema leo Juni 28 wakati akijibu swali la Mbunge wa viti maalumu Mhe. Zaytun Seif Swai katika kikao cha kumi na mbili, Bungeni Jijini Dodoma. 

"Serikali kupitia wizara ya Afya imeweka mipango ya kupunguza vifo vya watoto wenye umri 0 hadi 1 kwa kuongeza vituo vyenye vyumba maalumu kwa ajili ya kutoa huduma kwa watoto wachanga wenye hali mahututi (Neonatal  Care Unit), kutoka 18 mwaka 2017 kufikia 175 mwaka 2023." Amesema 

Ameendelea kusema, Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kutoa mafunzo kwa watoa huduma juu ya namna ya kutoa huduma jumuishi kwa watoto wachanga na watoto wakubwa (Intergrated Management of Childhood Illness-IMCI) ili kuokoa vifo vya watoto hao vinavyoweza kuepukika. 

Amesema,  Serikali imeendelea kuimarisha huduma za kukinga na kuzuia magonjwa yanayozuilika kwa Chanjo kama vile Surua, Nimonia, kuharisha, donda koo, kifaduro, pepo punda na polio kwa kuongeza utoaji wa chanjo za Watoto chini ya Mwaka mmoja kufikia kiwango cha zaidi ya asilimia 98 ya utoaji wa chanjo ya Penta 3.

Aidha, Dkt. Mollel amesema, Serikali imeongeza vituo vinavyotoa huduma kwa watoto waliozaliwa wakiwa na uzito pungufu (Kangaroo Mother Care) ambapo kwa sasa vituo 72 na Hospitali 175 zinatoa huduma hizi, huku akiweka wazi kuwa, kwa mwaka  2023/2024 Serikali imepanga kuongeza vituo 100 ili kufikia vituo 275 ifikapo mwezi Juni 2024 vitavyosaidia kuongeza huduma hizo nchini.

Sambamba na hilo Dkt. Mollel amesema Serikali imeendelea kuongeza vifaa na vifaa tiba ikiwemo CT-SCAN zimeongezeka kutoka 3 mpaka sasa zipo zaidi ya 50, MRI zilikuwa 2 lakini mpaka sasa zipo zaidi ya 19, hivyo kumtoa kuwaondoa hofu Wabunge kuwa hata vifaa vya huduma hizo vitaenda kuwekwa kwenye vituo vyote 100 vitavyojengwa nchini. 

Kwa upande mwingine Dkt. Mollel amesema, ili kukabiliana na changamoto ya gharama za matibabu kwa wazee, Wizara inaendelea kuhamasisha Wabunge na viongozi wengine pamoja na wananchi kuunga mkono Bima ya afya kwa wote ili kila mwananchi aweze kunufaika na huduma bora bila gharama kuanzia ngazi ya Zahanati mpaka hospitali ya Taifa. 


Tuesday, June 27, 2023

WAFANYABIASHARA WA MAZAO YA MISITU WATAKIWA KUFUATA SHERIA, KANUNI NA TARATIBU ZA UVUNAJI

 

Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imesema  haijazuia biashara ya mazao ya Misitu huku ikiwataka wafanyabiashara wa mazao ya misitu  kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu zilizowekwa ili kuhakikisha kuna kuwa na usawa katika biashara hiyo pamoja na matumizi endelevu ya rasilimali hiyo.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) ameyasema hayo leo Bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kibaha Vijijini Mhe. Michael Costantino Mwakamo, aliyetaka kujua kauli ya Serikali juu ya Wafanyabiashara wa mazao ya misitu wanaozuiwa kufanya biashara na Wakala ya Huduma za Misitu Tanzania (TFS).

”Natoa rai kwa wafanyabiashara wote wenye nia njema ya kuvuna au kufanya biashara ya mazao ya Misitu wafuate Sheria, Kanuni na taratibu zilizowekwa” Mhe. Masanja amesisitiza.

Amesema Sheria ya Misitu Sura ya 323 na Kanuni zake za mwaka 2004 zimeelekeza utaratibu unaopaswa kufuatwa ili kuvuna, kusafirisha na kuuza mazao ya misitu kwa kuzingatia umiliki wa misitu/miti ambao ni ya watu binafsi, Serikali za vijiji, Serikali za mitaa au Serikali Kuu.

Akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum,Mhe. Agnes Mathew Marwa, kuhusu Serikali kuwatafutia eneo mbadala Wananchi wa Vijiji vya Kata ya Nyantwari – Bunda wanaofanyiwa uthamini kupitisha uhifadhi Mhe. Masanja amesema kuwa zoezi la uthamini lipo katika hatua za mwisho na baada ya hapo Wananchi watalipwa fidia kwa mujibu wa sheria itakayohusisha gharama za thamani ya ardhi, mazao, majengo, posho ya kujikimu, usafiri na posho ya usumbufu.

Mhe. Masanja amesema kuwa Serikali kupitia Halmashauri ya Mji wa Bunda imetenga na kupima viwanja 350 katika eneo la Virian-Kata ya Stoo ambapo Wananchi watakaohama kutoka Kata ya Nyantwari watapewa kipaumbele wakati wa uuzaji wa viwanja hivyo.

Aidha, Halmashauri ya Mji wa Bunda imeandaa mpango wa kutwaa na kulipa fidia maeneo mbadala ya makazi yenye ukubwa wa ekari 1,625 katika maeneo ya Manyamanyama/Bitaraguru; Butakale; na Guta/Nyabehu. Maeneo yote hayo yatapimwa na kupewa kipaumbele kwa wananchi wanaotoka Kata ya Nyantwari.

JAMII YAASWA KUWEKEZA UJUZI KWA WATOTO



Jamii imeaswa kuwekeza zaidi kwenye  kuongeza ujuzi wa malezi makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto ili kuwa na Taifa lenye raia wenye misingi imara katika nyanja zote.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mwanaid Ali Khamis wakati akifungua Mafunzo  ya kitaifa ya Sayansi ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya awali ya Mtoto kwa Wadau kutoka mikoa 16 Nchini pamoja na Wizaraa za kisekta ,Mkoani Dodoma, Juni 26, 2023.

“Mafunzo haya yasiishie tu maofisini bali yafike hadi ngazi za Vijiji kwani huko watu huchelewa kupata taarifa za mambo ya msingi. Mnatakiwa mshuke kwa wananchi wa ngazi za chini kwani  Malezi ya awali ni ya muhimu sana katika makuzi ya mtoto”Alisema Mwanaidi.

Akielezea lengo la Mafunzo hayo Naibu katibu Mkuu  kutoka  Wizara ya Maendeleo ya Jamii,Wakili Amon Mpanju amesema  mafunzo hayo ni muhimukwaajili  yakuwaongezea ujuzi Wataalam husika ili waweze kutekeleza Majukumu yao kama inavyostahili

“Lengo la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo bobezi ili waweze kutekeleza inavyostahili,  kwani mafunzo haya yanatolewa na chuo cha Aga khan ambacho kina Mamlaka ya kutoa mafunzo hisika" amefafanua Mpanju

Akiongea wakati wa Mafunzo hayo Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Mtoto kutoka Wizra ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Waanwake na Makundi Maalum, Sebastian Kitiku,  amesema Wizara itaendelea kushirikiana  kwa karibu na wadau wa Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Mtoto ili kuhakikisha kuna mazingira salama ya ustawi na Maendeleo ya Watoto Nchini.

Naye mshiriki Tedson Ngwale ambaye ni Afisa Maendeleo kutokea Shinyanga ameishukuru Serikali kwa jitihada hizo za kuhakikisha inaanda mazingira salama kwa watoto kwa kutoa mafunzo hayo kwa maafisa maaendeleo na Ustawi wa Jamii.

“Tuna ahidi kuitendea haki Serikai kupitia Mafunzo haya  kwa kutekeleza kama tulivyoelekezwa na kama ilivyokusudiwa kwa kuwafikia Wananchi wa ngazi zote hasa vijijini ambako kuna changamoto zaidi”.

KAMATI YA BUNGE YAITAKA TARURA KUTIMIZA AZMA YA SERIKALI

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Dennis Londo ameutaka Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kuendelea  kuaminika na Serikali kwa  kutekeleza majukumu yake ipasavyo ya kujenga mbiundombinu ya barabara ili kuwaondolea adha ya usafiri wananchi.

Mhe. Londo ametoa kauli hiyo Juni 24, 2023 katika ziara ya kikazi ya kukagua miundombinu ya  barabara zilizojengwa chini ya usimamizi wa TARURA Wilaya ya Morogoro.

Mwenyekiti huyo amesema dhamira ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwaongezea bajeti ya sh.  Bilioni 350 kwa mwaka wa fedha 2023/24 ni kuona umuhimu wa taasisi hiyo  katika kutekeleza majukumu yake hasa katika ujenzi na marekebisho ya barabara maeneo  ya vijijini na mijini ili kuwa na miundombinu rafiki kwa wananchi.

Amesema asilimia kubwa ya watanzania shughuli yao kubwa ni kilimo hivyo TARURA wafanye kazi ili barabara  ziwe rafiki kwa watumiaji na kurahisisha maisha yao.

Mhe.Londo ameipongeza TARURA kujengwa barabara yenye kilometa 70 kwenye Wilaya ya Morogoro ambayo imerahisisha kuunganisha vijiji vinne ikiwamo cha Ngerengere na kuhimiza kutunza miundombinu ya barabara hiyo.

"Kujengwa kwa barabara hii kutawezesha kufika kwa urahisi bwawa la Kidunda ambalo ni mradi mkubwa utakaosaidia upatikanaji wa maji kwa wakazi wa Morogoro, Pwani na Dar es Salaam,"amesema.

N





aye, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Deogratius Ndejembi ameishukuru Kamati hiyo ya Bunge kwa maelekezo yake na kuiahidi TAMISEMI itaendelea kutimiza lengo la Serikali kwa kuisimamia TARURA kutoa huduma bora kwa wananchi.

Monday, June 26, 2023

SERIKALI YATAHADHARISHA WANANCHI IRINGA KUACHA KUTEMBEA USIKU KUEPUKA ATHARI ZA KUVAMIWA NA SIMBA

SERIKALI imewatahadharisha Wananchi Mkoani Iringa kuacha kutembea usiku ili kuepukana na madhara ya kuvamiwa na Simba walioingia katika makazi ya watu.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) ameyasema hayo leo jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Grace Tendega aliyetaka kujua nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wananchi wananchi wa Iringa wanaishi kwa uhuru kutokana na changamoto ya Uvamizi wa Simba.

“Niendelee kutoa elimu kupitia Bunge hili kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa Simba wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku lakini pia wenye mifugo wawashe mioto kuzunguka maeneo ya mifugo ili kuepusha Simba wasisogee katika maeneo yao” Mhe. Masanja amesisitiza.

Kufuatia hatua hiyo Mhe.Masanja amesema Serikali tayari imeshapeleka helikopta inayozunguka usiku na mchana kuhakikisha Simba hao wanapatikana na kurudishwa katika maeneo yao ili kuhakikisha  maisha ya Watanzania yanalindwa kwa gharama yoyote

Kuhusu mikakati ya Serikali ya kukabiliana na wanyama wakali na waharibifu, Mhe. Masanja amesema Serikali inatekeleza Mkakati wa kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu wa mwaka 2020 – 2024 ambapo Wizara inatoa elimu juu ya kujikinga na wanyamapori wakali na waharibifu; inajenga vituo vya askari wanyamapori ili kusogeza huduma karibu na wananchi; kuwafunga mikanda (GPS collars) tembo; na kuanzisha timu maalum (Rapid response Teams).

Pia, Serikali inaendelea kuwashirikisha wananchi kwa kutoa mafunzo kwa Askari wa Vijiji (VGS) ili kuongeza nguvu ya kudhibiti tembo katika maeneo ya wananchi.

Aidha, amesema Serikali imeshaweka mipango ya kujenga fensi ya umeme katika baadhi ya maeneo ili kupunguza athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Thursday, June 22, 2023

*MAJALIWA APOKEA TAARIFA YA KAMATI MAALUM ALIYOIUNDA KUFUATILIA CHANGAMOTO ZA WAFANYABIASHARA*


WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa leo Alhamisi, Juni 21, 2023, Jijini Dodoma amepokea taarifa ya Kamati Maalum aliyoiunda kwa ajili ya kupitia, kuchambua na kutoa mapendekezo ya kutatua changamoto za wafanyabiashara nchini. 

Taarifa hiyo imekabidhiwa na Mwenyekiti wa kamati, Dkt. John Jingu ambaye pia ni Katibu Mkuu, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum.

Mkutano huo umehudhuriwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenista Mhagama, Waziri Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Nchemba, Waziri wa Viwanda na Uwekezaji Ashatu Kijaji, Waziri wa Nchi OR – TAMISEMI, Angela

Kairuki, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Ahmad Chande, Makatibu Wakuu, Makamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wanakamati na wataalam kutoka sekta mbalimbali za masuala ya kodi, biashara na uwekezaji.

Akizungumza baada ya kupokea taarifa hiyo, Mheshimiwa Majaliwa amesema Kamati hiyo imefanya kazi kubwa na imeleta majibu ambayo yatatatua changamoto za wafanyabiashara nchini na ameahidi kuwa Serikali imepokeat aarifa hiyo na itayafanyia kazi mapendekezo na ushauri uliotolewa na kamati hiyo.

Kamati hiyo ambayo ilipewa siku 14, imefanya mapitio katika maeneo mbalimbali ya kikodi, bandari na maeneo ya wafanyabiashara kwenye mikoa mbalimbali nchini.

Sunday, June 18, 2023

TAASISI MWALIMU NYERERE YAFANIKISHA UPATIKANAJI DAMU









TAASISI ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Mkoa wa Pwani imefanikisha upatikanaji wa damu uniti 32 ambazo zitatumika kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha.

Akizungumza mara baada ya zoezi la uchangiaji damu lililofanywa kwa pamoja na Taasisi hiyo ya Nyerere kwa kushirikiana na Taasisi ya Chawa wa Mama Kibaha Vijijini  mgeni rasmi Yahaya Mbungulume ambaye alimwakilisha Mganga Mkuu wa Halmashauri hiyo alisema uniti hizo zitasaidia sana wagonjwa.

Mbungulume alisema kuwa zoezi hilo limekuwa na mafanikio makubwa kwani limesaidia upatikanaji wa damu ambayo itasaidia wagonjwa wakiwemo wajawazito, wagonjwa na watu wanaopata ajali.

Kwa upande wake katibu wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Mkoa wa Pwani Omary Pumzi alisema kuwa waliamua kujitolea damu baada ya kupita kwenye Hospitali na kuona jinsi gani kuna uhitaji mkubwa wa damu.

Pumzi alisema kuwa Taasisi hiyo imeendelea kutekeleza malengo ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere ya kukabilana na adui wa maendeleo ambao ni maradhi ujinga na umaskini hivyo afya ni moja ya malengo kwama yalivyo kwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan.

Naye mwenyekiti wa Chawa wa Mama Kibaha Vijijini Rehema Chuma alisema kuwa malengo ya taasisi yao ni kumsaidia Rais katika kuhakikisha nchi inapata maendeleo.

Akiongoza zoezi la uchangiaji damu Katibu Msaidizi wa Taasisi ya Mwalimu Taifa Neema Mkwachu alisema wanamuunga mkono Mwasisi wa Taifa kwa vitendo kwa kushiriki moja kwa moja.

Akielezea mafanikio ya zoezi la uchangiaji damu mratibu wa huduma za maabara Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Nabwike Mwairinga alisema kuwa wamepata uniti 32 kwenye zoezi hilo ambazo zitasaidia kwa kiasi kikubwa kwenye benki ya damu ambapo wanahitaji uniti 40 kwa kila mwezi.