Tuesday, October 31, 2023

TAKUKURU PWANI YAFANIKISHA MTENDAJI KUREJESHA MILIONI 4 ZA KIJIJI ALIZOZICHUKUA ZA MAUZO YA ARDHI

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Pwani imefanikiwa kurejesha kiasi cha shilingi milioni nne za Kijiji cha Kanga zilifanyiwa ubadhirifu na kaimu mtendaji wa Kata ya Kanga wilayani Mafia.

Aidha fedha hizo ambazo ni asilimia tano ni tozo ya mauzo ya kiwanja cha Kijiji hicho ambacho kiko ufukweni mwa Bahari ya Hindi.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Kibaha Naibu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Pwani Sadiki Alli akitoa taarifa ya miezi mitatu ya utendaji kazi kuanzia Julai hadi Septemba mwaka huu. 

Alli amsema kuwa mtuhumiwa huyo jina linahifadhiwa fedha hizo hakuziwasilisha ofisini wala kuzipeleka benki kwenye akaunti ya kijiji.

Amesema mtuhumiwa huyo ambaye pia ni ofisa mazingira wa kata alibainika kwenye mkutano wa Takukuru Rafiki ambapo wananchi waliibua kero hiyo na ndipo walipofanya uchunguzi juu ya tukio hilo na kufanya ufuatiliaji.

"Baada ya uchunguzi tulibaini kuwa tukio hilo ni la kweli na alirejesha fedha hizo na tumemwandikia mwajiri wake ili achukuliwe hatua zaidi za kisheria kuhusu tukio hilo,"amesema Alli.

Amesema kuwa mafanikio hayo yanatokana na mkutano wa Takukuru Rafiki na kuwataka wananchi watumie mikutano hiyo ili kutoa kero zao juu ya vitendo vya rushwa.

"Wananchi watoe kero zao za rushwa kupitia mikutano tunayoiandaa kupitia Takukuru Rafiki kwani hapo ni moja ya sehemu wanazoweza kutoa taarifa kama watashindwa kutuletea taarifa ofisini,"amesema Alli.

Katika hatua nyingine amesema kuwa jumla ya matukio 126 ambapo 92 yalihusu masuala ya rushwa huku 34 hayakuhusu rushwa na 27 wahusika walipewa ushauri manne yalifungwa na matatu yalihamishiwa idara nyingine.

Ameanisha idara ambazo zinaongoza kwa malalamiko kuwa ni Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) yenye malalamiko 44, na elimu 17, ardhi 15, ushirika sita, binafsi tano na polisi nne.

Ameongeza kuwa idara nyingine ni afya na kilimo tatu, bandari, fedha, madini, maji, misitu na utawala malalamiko mawili kila moja, idara ya biashara, ofisi ya mkuu wa wilaya, mifugo, maendeleo ya jamii, Mamlaka ya Mapato TRA, uchukuzi, ujenzi, Tanesco, utalii na viwanda lalamiko moja moja kila idara.

Wednesday, October 25, 2023

RC KUNENGE ATAKA UJENZI WA MALL YA HALMASHAURI YA MJI UKAMILIKE NDANI YA SIKU 14


MKUU wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ametoa siku 14 kwa Mkandarasi anayejenga Maduka Makubwa (Mall) inayomilikiwa na Halmashauri ya Mji Kibaha kukamilisha ujenzi wa mradi huo wenye thamani ya shilingi bilioni nane.

Ameyasema hayo wakati wa ziara yake kutembelea miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye Halmashauri hiyo ambapo mradi huo uko kwenye kitovu cha mji karibu na stendi mpya ya Maili Moja Kibaha.

Kunenge amesema kuwa mradi huo ni mkubwa ambao utakapokamilika utagharimu kiasi cha shilingi bilioni nane hivyo lazima ukamilike ndani ya muda huo ambapo matarajio ni kuingiza kiasi cha shilingi milioni 450 kwa mwaka.

"Nataka mkandarasi Elray asizidishe zaidi ya wiki mbili ahakikishe anakamilisha ndani ya muda huo tunachotaka akamilishe mradi huu ili biashara zianze kufanyika na Halmashauri ianze kupata mapato,"amesema Kunenge.

Kwa upande wake Mhandisi wa Halmashauri ya Mji Kibaha Brighton Kisheo amesema kuwa Halmashauri hiyo ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni nane mwaka 2018-2019 kwa ajili ya ujenzi wa mradi huo ambapo wafanyabiashara 253 watapata fursa za biashara na litahudumia watu zaidi 2,000 na unatarajiwa kukamilika Novemba mwaka huu.

Naye mwenyekiti wa Wamachinga Mkoa wa Pwani Filemon Maliga amesema kuwa wanaishukuru serikali kwa kuwapatia eneo jirani na Mall hiyo ili wafanye biashara zao na wanamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kulirasimisha kundi lao ambapo sasa wanatambulika na wanapata fursa mbalimbali zikiwemo za mikopo.

Miradi mingine aliyoitembelea mkuu huyo wa mkoa ni barabara, ujenzi wa madarasa ya sekondari kata ya Mkuza na maandalizi ya ujenzi wa kiwanda cha utengenezaji wa mitungi ya gesi ya kampuni ya Taifa Gas.


Mwisho.

Wednesday, October 18, 2023

SOKO LA KISASA KUJENGWA MLANDIZI BILIONI 7 KUTUMIKA

KATIKA kuhakikisha Mji wa Mlandizi unavutia Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha inatarajia kujenga soko kubwa na la kisasa kwa ajili ya wakazi wa mji wa Mlandizi ambalo litagharimu kiasi cha shilingi bilioni saba.

Hayo yamesemwa Mlandizi na Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Michael Mwakamo wakati wa kuhitimisha kampeni ya Simika Bendera kwenye Jimbo hilo.

Mwakamo alisema kuwa eneo maarufu kama kwa Mama Salmini tayari limeshapatikana baada ya kununuliwa na mkandarasi wa ujenzi amepatikana na utaratibu unaanza kwa ajili ya ujenzi.

"Soko la sasa ni dogo lakini eneo tulilopata ni kubwa na litachukua wafanyabiashara wengi na litakuwa na huduma nyingi tofauti na la sasa ambalo hata sehemu ya magari kupaki hakuna,"amesema Mwakamo.

Amesema fedha hizo zimetengwa kwenye baheti ya mwaka wa fedha 2023/2024 na tayari bilioni mbili zimetolewa kwa ajili ya kuanza kazi na litaubadilisha Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mlandizi.

Naye Mwenyekiti wa CCM Kibaha Vijijini Mkali Kanusu alisema kuwa chama kinataka viongozi waliopo kwenye madarakani wawe na mahusiano mazuri na wananchi.

Kwa upande wake katibu wa CCM Kibaha Vijijini Zainabu Mketo amesema kuwa hamasa ya Simika Bendera imeleta mafanikio kwani wamevuna wanachama wapya 3,500 na kupitia mabalozi wote lengo likiwa ni kuimarisha chama ndani ya chama.


Mwisho.

Sunday, October 15, 2023

MAOFISA TEHAMA WATAKIWA KUENDANA NA TEKNOLOJIA

MAOFISA TEHAMA nchini, wameaswa kwenda na wakati ,kupenda kujifunza kulingana na teknolojia inavyobadilika ili kujiongezea uzoefu na ujuzi.

Aidha wawe wabunifu ,wajitume ili kuacha alama na tija katika kada hiyo kwenye maeneo ya kazi

Rai hiyo imetolewa na Katibu Tawala mkoa wa Pwani Rashid Mchatta, wakati alipomwakilisha Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI, kufungua kikao kazi cha mwaka 2023 ,ambacho kimefanyika Kibaha Mkoani Pwani na kukutanisha maofisa hao kutoka mikoa mbalimbali nchini ili kujadili changamoto zinazokikabili kitengo Cha TEHAMA.

 "IT ina mambo mengi sana, inabadilika kama mtu wa Tehama hufanyi updating itakupa wakati mgumu, someni masomo ya ziada kuongeza uzoefu,mkoa wa Pwani ndio mwenyeji mwaka huu tumejipanga kuhakikisha tuliyoyajadili yanafanikiwa"anasema Mchatta.

Mchatta alieleza, kada ya TEHAMA imekua kwa kasi kubwa na kupelekea kuwa mhimili mkubwa katika utendaji kazi na Serikali na Taasisi nyingine binafsi kwenye mifumo mbalimbali ikiwemo ukusanyaji mapato ya ndani ya Mamlaka za Serikali za mitaa ,mfumo wa kusimamia huduma za hospitali.

"Serikali - TAMISEMI imeipa kada hii umuhimu mkubwa kwa kuanzisha wizara rasmi inayoshughulikia TEHAMA ,hivyo tusimuangushe mh Rais"

Awali Melchiory Baltazary, Mkurugenzi Msaidizi-TEHAMA TAMISEMI alieleza kikao hicho ni kikao kazi ambacho kitafanyika siku mbili.




Mwisho

Saturday, October 14, 2023

LIONS CLUB YATOA MISAADA YA VIFAA VYA SHULE


KLABU ya Lions ya Jijini Dar es Salaam imetoa vifaa kwa Shule 15 za Msingi na Sekondari Kata ya Vigwaza Halmashauri ya Chalinze Wilayani Bagamoyo zenye thamani ya zaidi ya milioni sita ili kukabiliana na uhaba wa vifaa kwenye shule hizo.

Hayo yalisemwa kwenye  shule ya msingi Ruvu Darajani kata ya Vigwaza na Rais wa zamani wa klabu hiyo Muntazir Bharwani wakati wa kukabidhi vifaa hivyo kwa shule ambapo ziliwakilishwa na walimu wakuu wa shule hizo.

Bharwani amesema kuwa klabu yao inajihusisha na kusaidia masuala mbalimbali ya kijamii ikiwemo kwenye sekta za elimu, afya na maji na masuala mengine ya kimaendeleo.

"Tumetoa vifaa vikiwemo vitabu vya walimu kwa ajili ya kufundishia, madaftari pamoja na mipira kwa ajili ya kuwaweka wanafunzi kwenye utimamu wa akili,"amesema Bharwani.

Akipokea misaada hiyo ofisa elimu msingi na awali wa Halmashauri ya Chalinze Miriam Kihiyo ameishukuru klabu hiyo na kuomba iendelee kusaidia kwenye sekta hiyo.

Kihiyo amesema kuwa mahitaji kwenye sekta ya elimu ni kubwa kutokana na kuwa na wanafunzi wengi na kuomba wadau wengine waendelee kujitolea misaada mbalimbali.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Vigwaza Musa Gama amesema kuwa anashukuru kwa misaada hiyo ambayo itasaidia kupunguza sehemu ya baadhi ya changamoto.

Gama amesema kuwa msaada huo ni motisha kwa walimu na wanafunzi katika kuhakikisha elimu inaboreka na kuwataka wananchi wawasimamie watoto wao ili wapate elimu ipasavyo.

WATAKA JITIHADA ZIONGEZWE WATU KUKUA KUSOMA KUHESABU NA KUANDIKA

IMEELEZWA kuwa watu wanaojua kusoma kuandika na kuhesabu nchini kwa sasa ni asilimia 77.8 ikilinganishwa na mwaka 1980 ambapo watu hao ilikuwa ni asilimia 9.6.

Hayo yalisemwa Mjini Kibaha na Profesa Michael Ng'umbi Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima Nchini wakati wa ufunguzi wa Kongamano la maadhimisho ya kitaifa ya juma la elimu ya watu wazima kitaifa.

Ng'umbi alisema kuwa mwaka 1980 Tanzania iliweza kufikia kiwango cha juu cha kufuta ujinga kwa watu wasiojua kuandika kuhesabu na kusoma na kufikia asilimia hiyo.

Akifungua mafunzo hayo kaimu mkurugenzi elimu msingi wizara ya elimu sayansi na teknolojia Josephat Luoga alisema kuwa mafunzo hayo yatawezesha kuamsha hamasa ya kutafakuri kuwa tunakwenda wapi katika utoaji elimu.

Luoga alisema kuwa mfumo wa elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi utaweza kubadilisha mtizamo juu ya uendeshaji na usimamizi na tathmini ili kuendana na dira ya maendeleo ya 2025 pamoja na mpango wa maendeleo endelevu 2030.

PROFESA MKENDA AFURAHISHWA TAASISI YA ELIMU YA WATU WAZIMA INAVYOBORESHA MFUMO HUO

WAZIRI wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema kuwa serikali itaendelea kuboresha elimu ya watu wazima nchini.

Mkenda aliyasema hayo wakati wa kufunga Kongamano la maadhimisho ya kitaifa ya juma la elimu ya watu wazima kitaifa lililofanyika Wilayani Kibaha.

Alisema kuwa serikali itaendelea kujenga uwezo na watendaji kwenye Halmashauri kwenye mikoa zitoe kipaumbele kwa program zote za elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Elimu kutoka Ofisi ya Rais Tamisemi Dk Charles Msonde alisema kuwa moja ya mkazo uliowekwa ni kuhakikisha wanafunzi wa darasa la kwanza wanajua kusoma kuandika na kuhesabu.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Profesa Caroline Nombo alisema kuwa jumla ya wanafunzi milioni 5.7 walidahiliwa kwenye elimu changamani kwenye vituo 405.

Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge alisema kuwa baadhi ya changamoto katika utekelezaji wa baadhi ya program ni pamoja na walimu wa kujitolea kutokuwa na mafunzo ufinyu wa bajeti, upungufu wa vitendea kazi na kushindwa kulipa wa wezeshaji.


Mwisho.

MKUU WA MKOA WA PWANI KUNENGE ATAKA VIONGOZI WALIOHUSIKA UUZAJI VIWANJA ENEO LA MITAMBA WAKAMATWE

KUFUATIA viongozi 24 kujihisisha kuwatapeli watu na kuwauzia eneo la shamba la Mitamba mali ya Wizara ya mifugo na uvuvi Mkuu wa mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge ametoa  siku 14  kukamatwa viongozi hao.

Aidha viongozi hao ni pamoja na mabalozi, wenyeviti wa mitaa, watendaji  walioshirikiana na madalali  waliohusika kuwauzia  wananchi viwanja katika eneo la shamba hilo lililopo Halmashauri ya Mji Kibaha.

Kunenge alitoa maagizo hayo wakati wa mkutano wa hadhara na wananchi wa Kata ya Pangani uliowahusisha watalaam kutoka Halmashauri ya Mji Kibaha na mkoa kwa ajili ya kutoa msimamo wa serikali kuhusu maamuzi ya eneo hilo ambalo limevamiwa na wananchi kwa ajili ya makazi.

Alisema orodha na majina ya viongozi hao na madalali  waliohusika kuwauzia kinyemela wananchi viwanja katika eneo hilo ambalo linamilikiwa na serikali na kwamba anayakabidhi kwa Taasisi ya  Kuzuia na Kupambana na Rushwa Takukuru pamoja na Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria.

Naye Mpimaji Ardhi Halmashauri ya Mji Kibaha Aron Shushu alisema kuwa kiwanja hicho kilipimwa upya kwa kuzingatia sheria namba 8 ya mipango miji na kwamba  mwaka 2021 kilifanyika kikao na wananchi hao kwa ajili ya kutoa katazo la kutovamia shamba hilo.

Shushu alisema kuwa jitihada za kuwakataza wazanchi hao ziliendelea huku baadhi wakionekana kuendelea na shughuli za ujenzi   na kukaidi na walipokea mapendekezo kutoa Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Alisema kuwa kuhusu upimaji wa eneo hilo hekta 150 zilitolewa kwa ajili ya Matumizi ya Wakala wa Maabara ya Vetenari Tanzania (TVLA) hekta 188 kwa ajili ya matumizi ya Taasisi za  Umma, 486  uwekezaji wa viwanda na 200  makazi.


Tuesday, October 10, 2023

DC OKASHI ATAKA WAHUJUMU WAFICHULIWE MIRADI YA MAJI RUWASA BAGAMOYO

MKUU wa Wilaya ya Bagamoyo Halima Okashi amewataka wananchi kuwafichua watu wanaohujumu miradi ya maji ambayo serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni 1.9 kwa ajili ya uboreshaji wa  huduma ya upatikanaji maji kupitia Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA).

Ameyasema hayo Wilayani Bagamoyo wakati alipokuwa akifungua mkutano na wadau wa maji kwenye wilaya hiyo ambayo inaundwa na Halmashauri mbili za Bagamoyo na Chalinze. 

Okashi amesema kuwa serikali imetoa fedha hizo kwa lengo la kuhakikisha miradi inatekelezwa ili huduma ya maji safi na salama inapatikana kwa wananchi vijijini kwa umbali usiozidi mita 400.

Kwa upande wake Meneja wa RUWASA Wilaya ya Bagamoyo James Kionaumela amesema kuwa Wilaya ina vyanzo vikuu viwili vya maji ambavyo ni chini ya ardhi kupitia visima vya kuchimba virefu na vifupi kukiwa na visima 215.

Kionaumela amesema kuwa chanzo cha pili ni maji ya juu inayojumuisha maji ya mito, mabwawa na chemichemi na wilaya hiyo ina vyombo vya watoa huduma 17 ambapo imevipunguza na kufikia vyombo vitano.

Naye mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Bagamoyo Abdul Sharifu amesema kuwa wanamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kutoa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya uboreshaji upatikanaji huduma ya maji.

Diwani wa Kata ya Kibindu na makam mwenyekiti wa Halmashauri ya Chalinze Ramadhan Mkufya amesema kuwa Vijiji viwili vya Kwa Msanja na Kwa Konje ndiko kuna changamoto ya maji.

Mwentekiti wa vyombo vya watumiaji maji Wilaya ya Bagamoyo Jitihada Mwinyimkuu ameiomba serikali kuvihudumia vyombo hivyo kwani vingine vinashindwa kufanya kazi kutokana na vifaa kufa na kushindwa kuvikarabati.


Mwisho.

Sunday, October 8, 2023

WAFANYABIASHARA WAZITAKA MAMLAKA KUBORESHA MIUNDOMBINU

WAFANYABIASHARA wa Tengeru Mkoani Arusha wamewataka baadhi ya viongozi wa mamlaka mbalimbali za Serikali Wilayani humo kuboresha miundombinu ili kutekeleza maagizo ya Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan yenye dhamira njema kwa wafanyabiashara.

Hayo yamesemwa leo na wafanyabiashara wa Tengeru wakati wa Mkutano wa viongozi wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT) na wafanyabiashara wa eneo hilo uliofanyika kwa lengo ikiwa ni kupokea, kuchakata na kutolea ufafanuzi wa kero, changamoto na maoni ya wafanyabiashara.

Mmoja wa wafanyabiashara hao Aloyce Mallya amebainisha ukosefu wa soko katika eneo hilo na hata eneo ambalo linatumika kama soko lina miundombinu mibovu ikiwemo huduma za vyoo pamoja na barabara hali inayohatarisha afya za wafanyabiashara na watumiaji wengine wa eneo hilo.

Wamesema kuwa hata hivyo eneo wanalofanyia biashara ni finyu kwa biashara siku za minada hivyo wanaiomba serikali kuwapa eneo ambalo litatumika kufanyia biashara zao.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania Hamis Livembe amesema kuwa  nia ya Serikali ya awamu ya sita ni kutatua kero zote za wafanyabiashara nchini hivyo kero hizo zote wanazifikisha sehemu husika kwa ajili ya kuzipatia ufumbuzi.

Awali  Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania Abdalla Salim amewataka wafanyabiashara wawe wazi kusema kero zao ili kupata ufafanuzi na ufumbuzi wa kero zao na kuwahimiza kujaza fomu ili wasajiliwe na kupata vitambulisho kwani kila Sekta duniani ina utambulisho wake. 

Pia kupitia vitambulisho  hivyo vitawasaidia kutatuliwa changamoto zao na viongozi wa Jumuiya kwa kushirikiana na Mamlaka husika kutatua changamoto hizo.

Naye  Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Mkoa wa Tanga Ismail Masoud amesema kuwa Rais Samia anawapenda wafanyabiashara ndiyo maana ametoa fursa ya kufanya mikutano nchi nzima ili wafanyabiashara waweze kuwasilisha changamoto na kero zao na amewasisitiza wafanyabiashara kutumia Jumuiya kama chombo cha utatuzi wa kero zao.

*WAZIRI KAIRUKI AIPONGEZA TAWA KWA USIMAMIZI BORA WA WANYAMAPORI NCHINI*

WAZIRI wa Maliasili na Utalii Mhe. Angellah Kairuki ameipongeza Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) kwa jitihada za dhati katika kuleta maendeleo ya uhifadhi nchini ikiwa ni pamoja na Usimamizi mzuri wa Wanyamapori 

Mhe. Kairuki ametoa pongezi hizo Oktoba 7, 2023 alipotembelea bustani ya Wanyamapori hai katika maonesho ya Saba ya Kimataifa ya Swahili International Tourism Expo - SITE yanayofanyika Mlimani City Jijini Dar es Salaam

".. niwashukuru wote lakini zaidi niwashukuru TAWA kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya kwa ajili ya maendeleo ya uhifadhi pamoja na kuendelea kusimamia hifadhi zetu mbalimbali na kuhakikisha pia kunakuwa na Utalii ambap ni endelevu unaozingatia masuala mazima ya uhifadhi" alisema Mhe. Kairuki

Aidha Waziri Kairuki amesema Wizara yake kupitia TAWA imepeleka bustani ya Wanyamapori hai katika maonesho hayo ili kuendelea kuhamasisha wananchi kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo nchini ikiwa ni pamoja na kuvitumia na kuona rasilimali tulizonazo kama Taifa.

Maonesho haya  yanafikia tamati leo Oktoba 8, 2023.

JUMUIYA WAZAZI PWANI YATAKA MAMLAKA USIMAMIZI KUSHIRIKIANA


CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kupitia Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Pwani amezitaka mamlaka za usimamizi kushirikiana katika utoaji wa vibali ili kuondoa muingiliano wa kimamlaka.

Hayo yamesemwa na mwenyekiti wa Wazazi mkoa wa Pwani Jackso Kituka wakati wa kikao cha Baraza la Wazazi Mkoa kilichoganyika Mjini Kibaha.

Kituka amesema kuwa baadhi ya mamlaka zimekuwa zikitofautiana kimaamuzi ambapo moja inaweza ikawa inakataa huku nyingine ikiruhusu kuhusu suala fulani.

"Mfano kama vile Baraza la Taifa la usimamizi wa mazingira (NEMC) linakataza upigaji wa muziki wenye kelele ambapo ni uchafuzi wa mazingira lakini ofisi ya utamaduni inaruhusu upigaji wa muziki kwenye kumbi za starehe,"amesema Kituka.

Naye ofisa mazingira kutoka NEMC Joseph Rugatiri akijibu baadhi ya maswali kuhusu mazingira amesema kuwa vibali vya uchimbaji mchanga hutolewa na halmashauri kama taratibu za uchimbaji mchanga zinakiukwa wananchi wanapaswa kutia malalamiko kwenye ofisi za mitaa na kama hakuna marekebisho taarifa zipelekwe kwao ili wachukue hatua na kuhusu kelele za muziki alisema kila eneo lina kiwango cha sauti.

Saturday, October 7, 2023

NSSF PWANI YAWA YA TATU KITAIFA UTOAJI HUDUMAFA

MFUKO wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Mkoani Pwani, umeshika nafasi ya tatu kitaifa katika utoaji huduma kwa ufanisi kwa wateja wake.

Aidha mfuko huo umeahidi utendaji kazi unaoendana na kasi ya Nssf ya sasa ambayo inahitaji ujali kwa wateja na kutoa huduma bora.

Kaimu Meneja NSSF Pwani Rehema Mutungi akifunga maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja kimkoa, alieleza utoaji huduma bora kwa wateja wao ni jadi yao na imeonyesha dhahiri nafasi waliyoipata kitaifa.

"Tunahitaji kufika namba moja ,huu ni utamaduni wetu kuhudumia wateja kwa ubora na kwa wakati ,tunaamini miaka ijayo tutafanya vizuri zaidi"alieleza Rehema.

Rehema anasisitiza ushirikiano,umoja kwa watumishi na watendaji wa NSSF ili kutoa huduma kwa ufanisi.

Vilevile Rehema alihimiza ,kila mmoja kujitathmini na kuchukua hatua za haraka kukabiliana na vitendo vya rushwa ili kudumisha imani kwa wanachama na wadau.

Katika kufunga maadhimisho hayo kimkoa wametoa vyeti na zawadi kwa wa

Friday, October 6, 2023

MKOA WA PWANI KUBORESHA MAZINGIRA YA UWEKEZAJI

SERIKALI ya Mkoa wa Pwani kwa kushirikiana na Serikali Kuu itahakikisha miundombinu muhimu inayotumika kwenye maeneo ya uwekezaji inajengwa ili kuwaondolea usumbufu wawekezaji.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge alipotembelea kiwanda cha King Lion Investment (King Lion Steel Mill) kinachojihusisha na utengenezaji wa bidhaa za chuma kilichopo eneo la viwanda la Zegereni Wilayani Kibaha.

Kunenge amesema kuwa serikali inatekeleza miradi mbalimbali kwenye maeneo ya uwekezaji ikiwemo ya Barabara, Umeme, Maji na Gesi ili kuvutia uwekezaji.

Kwa upande wake meneja wa kampuni hiyo Arnold Lyimo amesema kuwa mradi huo unagharama ya zaidi ya shilingi bilioni 160 na kitakuwa kiwanda kikubwa kwa ukanda wa Afrika Mashariki na utakamilika Juni 2024 na kuanza uzalishaji.

Lyimo amesema kuwa kitakapokamilika kitazalisha chuma tani 350,000 kwa mwaka ambapo malighafi za kuzalishia chuma na zitauzwa ndani na nje ya nchi zikiwemo Uganda, Kenya, Rwanda, Burundi, Kongo na kitatoa ajira 400 za moja kwa moja 5,000 ajira za muda.

Thursday, October 5, 2023

JESHI LA ZIMAMOTO NA UOKOAJI MKOA WA PWANI LATOA TAHADHARI MVUA ZA EL NINO

 

*TAARIFA YA KAMANDA WA ZIMAMOTO PWANI ALIPOKUWA MGENI RASMI MAHAFALI YA 16 SHULE YA SEKONDARI KWALA - KIBAHA*

KAMANDA wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoa wa Pwani SSF Jenifa Shirima kuwakumbusha wananchi  kuzingatia tahadhari zinazoendelea kutolewa kuhusu uwezekano wa kunyesha mvua kubwa za Elninyo.

Shirima ameyasema hayo alikpokuwa mgeni rasmi Mahafali ya 16 ya Kidato cha nne katika Shule ya Sekondari  Kwala iliyopo Kata ya Kwala Wilaya Kibaha na kuwataka watu wote wanaoishi maeneo hatarishi kuondoka kabla ya mvua hizo kuanza kunyesha ili kuepuka madhara.

Aidha amewaahidi kwamba atahakikisha changamoto walizoainisha atazifikisha sehemu husika ili ziweze kupatiwa ufumbuzi ambapo alitoa mchango wake fedha taslimu, vifaa vya kuzima na kung’amua moto kwa uongozi wa shule hiyo.

Pia alitoa zawadi za vifaa vya ki taaluma kwa wanafunzi wahitimu na Wanafunzi Skauti ambapo alipata nafasi ya kugawa vyeti kwa wahitimu pamoja na walimu na wanafunzi waliofanya vizuri zaidi.

NSSF YAPIGA VITA VITENDO VYA RUSHWA

MFUKO wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Mkoani Pwani, imetoa rai kwa Mtumishi ama Mtendaji yeyote anaejihusisha na vitendo vya rushwa kuacha mara moja vitendo hivyo kwani vinachangia kuzorotesha utoaji wa huduma kwa wateja.

Akifungua maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja kimkoa, Meneja wa NSSF Mkoani Pwani, Witness Patrick ,amesema wanashirikiana na Taasisi ya kupambana na kuzuia rushwa (TAKUKURU) kudhibiti mazingira ya vitendo vya rushwa kwenye maeneo ya kazi.

Amewaasa ,kila mmoja kujitathmini na kuchukua hatua za haraka kukabiliana na vitendo vya rushwa ili kudumisha imani kwa wanachama na wadau.

Witness ameeleza kuwa, mfuko hautamvumilia mtendaji yeyote atakaeshindwa kuendana na viwango na kasi ambayo mfuko unatarajia kuifikia.

Anasema, Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan inapinga rushwa kwa vitendo, na Nssf inaunga mkono juhudi hizi za serikali kwa kukemea masuala yote ya rushwa.

Vilevile Witness amewahimiza ,watumishi na wananchi wema kutoa taarifa za vitendo vya rushwa vinavyotendeka katika maeneo yao ya kazi kwani kutokutoa taarifa ni kushiriki rushwa.

Halikadhalika," anawasihi kutumia mfumo mpya wa NISS katika kuandikisha wanachama wengi zaidi wa mfumo wa kujichangia kwa hiari ili kuongeza wigo wa kinga ya Hifadhi ya Jamii kwa wananchi.

Naye mwanachama wa Nssf Kibaha, Vicent Ndumbili ameipongeza Nssf kwa kujali wateja wake.

Maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja ilianzishwa rasmi kimataifa mwaka 1984 kwa lengo la kutambua umuhimu wa huduma bora kwa wateja na juhudi za wafanyakazi wanaotoa huduma bora kwa wateja ambapo mwaka huu 2023 yanaanza octoba 2-octoba 6 kilele.


Mwisho

TCCIA INVESTMENT KUONGEZA MTAJI KUFIKIA BILIONI 47


KAMPUNI ya TCCIA Investment inatarajia kuongeza mtaji wake na kufikia bilioni 47 kutoka bilioni 37 ambazo zimewekezwa kwenye masoko mbalimbali ya hisa.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo Peter Kifungomali wakati akizungumza na wanahisa wa mkoa wa Pwani juu ya hisa walizowekeza.

Kifungomali amesema kuwa ongezeko hilo ni hadi itakapofika mwaka ujao wa fedha ambapo thamani imeongezeka kwa asilimia 53 kwa mwaka 2022.

Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa chemba ya wafanyabiashara ya TCCIA Mkoa wa Pwani sehemu ya biashara Fadhili Gonzi amesema kuwa baadhi ya wanahisa walikuwa na maswali mengi juu ya fedha zao.

Naye mmoja wa wanahisa Ayubu Mtawazo amesema kuwa hisa ni moja ya sehemu salama ya kuwekeza fedha ambapo watu wengi wamenufaika.

Clara Ibihya amesema kuwa manufaa ya hisa ni makubwa kwani ukishawekeza fedha zako hupati tena usumbufu kutakiwa marejesho bali unasubiri kupata fedha.