Wednesday, May 15, 2013

MATAWI YA CCM YATAKIWA KUANZISHA VITEGA UCHUMI


Na John Gagarini, Kibaha
MATAWI ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) nchini yametakiwa kuanzisha vitega uchumi ili kujiongezea kipato badala ya kuyafanya matawi hayo vijiwe vya kukaa bila ya tija.
Hayo yalisemwa na mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa (NEC) kutoka wilaya ya Kibaha mkoani Pwani Rugemalira Rutatina, wakati akizindua tawi la Mtazamo lililopo kata ya Tumbi wilayani humo.
Rutatina alisema kuwa matawi hayo ndiyo msingi wa chama hivyo lazima matawi hayo yajianzishie vyanzo vya kupata mapato badala ya kukaa tu na kubweteka.
“Hili ni kati ya matawi ambayo yameonyesha mwanga kwani kuwa na fedha kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo ni kitu muhimu na si vema tawi kuwa sehemu ya kukaa tu bila ya kubuni vyanzo vya mapato na si kusubiri kusaidiw akwa kila kitu,” alisema Rugemalila.
Alisema kuwa kwa kuwa matawi ndipo sehemu ya kukiimarisha chama lazima matawi hayo yawe na nguvu za kiuchumi ili waweze kukiimarisha chama.
“Mkiwa na uchumi imara mnaweza kuisaidia jamii mfano kutoa vitanda kwa wagonjwa kwenye hospitali au kuihudumia kwa njia yoyote ile ili iwe mfano mzuri,” alisema Rutatina.
Aidha alisema kuwa wanachama wa CCM wanatakiwa kuwaeleza viongozi changamoto zilizopo na si kuanzisha makundi ambayo hayana manufaa.
Aliwataka Watanzania kuwa na imani na chama na kukataa propaganda za wapinzani kuwa hakuna kilichofanyika tangu nchi kupata uhuru jambo ambalo ni upotoshaji.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment