Monday, May 20, 2013

WAKAZI WAHITAJI DARAJA LA KUDUMU


Na John Gagarini, Kibaha
MTAA wa Lumumba wilayani Kibaha unahitaji zaidi ya shilingi milioni tisa kwa ajili ya kuweka nguzo tatu za daraja la mbao kwenye kivuko cha mto Mpiji mpakani mwa wilaya ya Kibaha na Kinondoni.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mwenyekiti wa mtaa huo Gidion Tarimo alisema kuwa daraja hilo ni muhimu kwao kwa ajili ya kupata mahitaji yao ya kila siku ambayo huyapata mtaa wa Kibwegere wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam.
Tarimo alisema kuwa wilaya ya Kinondoni kwao ni karibu ukilinganisha na Kibaha Maili Moja hivyo daraja hilo linahitaji kufanyiwa matengenezo ili liweze kupitika kwa urahisi hasa kupitisha magari mbapo kwa sasa hayapiti.
“Tumeazimia kujenga daraja hilo hadi magari yaweze kupita ambapo kwa sasa magari hayapiti hata hivyo tumepiga hatua kwani zamani watu walikuwa wakipita mtoni moja kwa moja lakini kwa sasa hawagusi maji na maji yalipokuwa yakijaa watu walikuwa hawawezi kuvuka kwenda ngambo ya pili,” alisema Tarimo.
Alisema kuwa hadi kufikia hatua hiyo wametumia kiasi cha shilingi milioni nane ambapo wananchi wamejitolea huku fedha za mfuko wa Jimbo ni kiasi cha shilingi milioni mbili.
“Changamoto za matumizi ya daraja hili ni kubwa kwani ili mtu upate huduma mbalimbali za kijamii lazima uvuke na kama kuna mamamjamzito lazima ashushwe kwenye pikipiki ambazo hutumika hali ambayo si salama kwa wagonjwa wa namna hiyo,” alisema Tarimo.
Aidha alisema kuwa tayari wameshapeleka barua kwa mkurugenzi wa halmashauri ya Mji wa Kibaha kwa ajili ya kusaidiwa fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo.
Aliwaomba watu na mashirika mbalimbali kuwasaidia ili kufanikisha ujenzi huo ambao unatarajiwa kukamilika ifikapo mwaka 2015 ili kurahisisha mawasiliano na sehemu za huduma.
Mwisho.
    
   
 Mwenyekiti wa mtaa wa Lumumba Gidioni Tarimo akipita juu ya daraja la mbao la Mto Mpiji ambapo wanahitaji kiasi cha shilingi milioni tisa kwa ajili ya kuweka nguzo kwa lengo la kuliimarisha ili liweze kupitika ambapo kwa sasa magari hayawwezi kupita, wakazi wa mtaa huo hupata huduma za Kijamii mtaa wa Kibwegere wilaya ya Kinondoni

No comments:

Post a Comment