Sunday, May 26, 2024

TAASISI ZINAZAZOUNGA MKONO CCM ZIKITUMIKIE CHAMA SIYO KUSUBIRI UTEUZI


WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Pwani wametakiwa wasizitumie taasisi mbalimbali zinazomuunga Mkono Rais na chama kama sehemu ya kupata teuzi za kuwa viongozi.

Aidha zimetakiwa zisitembee mifukoni na baadhi ya watu wanaotaka kuwania nafasi za uongozi bali wawaache waliopo madarakani wamalize muda wao wa uongozi.

Hayo yamesemwa Mjini Kibaha na Katibu wa Siasa na Uenezi Mkoa wa Pwani David Mramba wakati wa mkutano na taasisi hizo.

Mramba amesema kuwa baadhi wanajiunga na taasisi hizo ili waonekane wachaguliwe kwenye nafasi mbalimbali za uongozi kwenye chama na serikali.

Kwa upande wake Katibu Mwenezi wa CCM mkoa wa Ruvuma John Haule alizitaka taasisi hizo kuitumia vizuri mitandao ya kijamii kwa kuelezea mambo mazuri yanayofanywa na awamu ya sita.

Naye Katibu Mwenezi wa CCM mkoa wa Morogoro Zangina Zangina amesema kuwa taasisi hizo zihamasishe wale wenye sifa wajiandae kugombea wakati utakapofika.

Thursday, May 23, 2024

CHONGELA AAPISHWA KUWA DIWANI

DIWANI wa Kata ya Msangani kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Gunze Chongela ameapishwa baada ya kushinda uchaguzi mdogo uliofanyika hivi karibuni kufuatia kifo cha aliyekuwa diwani wa kata hiyo Leonard Mlowe .

Chongela alikula kiapo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Hamis Ally wakati wa kikao cha baraza la madiwani wa Halmashauri ya Mji Kibaha.

Gunze ameahidi kuwatumikia wananchi wa kata hiyo kwa kusimamia miradi ya maendeleo kupitia ilani ya CCM.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mussa Ndomba amemtaka diwani huyo kuebdeleza mazuri yaliyoachwa na mtangulizi wake ili kuleta maendeleo kwenye kata hiyo.

Wednesday, May 22, 2024

KILONGA CUP MBIONI KUTIMUA VUMBI

MAANDALIZI ya michuano ya soka ya Kilonga Cup msimu wa tano yameanza ambapo timu zimealikwa kushiriki michuano hiyo ambayo inayotarajia kutimua vumbi huko Bagamoyo Mkoani Pwani.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Mjini Kibaha katibu wa mashindano hayo Idd Mpingo amesema kuwa michuano hiyo inatarajia kuanza mwezi Juni kwenye uwanja wa Mwanakalenge.

Mpingo amesema kuwa maandalizi yanaendelea vizuri ambapo kwa sasa ni usajili wa timu zitakazoshiriki michuano hiyo ambapo timu ya Kiduli imethibitisha kushiriki michuano hiyo.

Amesema kuwa zawadi kwa mshindi mwaka huu zitakuwa nzuri ikilinganishwa na mwaka jana ambapo mwaka jana mshindi alijinyakulia milioni 3 na mshindi wa pili alijinyakulia milioni 1.5.

Kiingilio cha ushiriki kwa timu ni shilingi 150,000 ambapo pia zawadi zitatolewa kwa mchezaji bora, mfungaji bora na kipa bora lengo likiwa ni kuongeza hamasa kwa wachezaji.

Ametoa wito kwa vilabu ndani na nje ya Mkoa wa Pwani kujitokeza kushiriki michuano hiyo na wanawakaribisha wadhamini kujitokeza kudhamini michuano hiyo.

Ameishukuru serikali na vyama vya soka na waamuzi kwa ushirikiano wanaoutoa kwao katika kufanikisha michuano ambayo imeibua vipaji vingi vinavyotamba kwenye ligi mbalimbali nchini.

Tuesday, May 21, 2024



MWAJUMA Makuka ni jina maarufu kwenye Mtaa wa Msangani ambalo limetokana na uongozi wake thabiti akiwa ni mwanamke wa shoka kutokana na jinsi anavyopambana kuwaletea maendeleo wananchi anaowaongoza.

Ubora wake unatokana na umahiri wake wa kutekeleza majukumu yake kikamilifu bila ya kujali jinsi yake na kufanya baadhi ya mambo ambayo watangulizi wake ambao ni wanaume walishindwa katika uongozi wao.

Makuka ni mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Msangani Mtaa ulio jirani na kambi ya Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) Msangani kata ya Msangani Wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani.

"Moja ya vitu vilivyokuwa vikiniumiza kama kiongozi ni kutokuwa na huduma ya uzalishaji mama wajawazito kwenye zahanati yetu ya Kata ya Msangani ambayo iko kwenye mtaa wa Msangani lakini changamoto hiyo iko mbioni kwisha kwani tayari vitanda viwili kwa ajili ya kuzalishia akinamama wajawazito kimepatikana",amesema Makuka.

Amesema kuwa mama wajawazito walikuwa wakipata huduma mbali na hivi sasa tayari vifaa vimeshaletwa ikiwa ni pamoja na vitanda vya kuzalishia na vifaa vingine ambapo huduma hizo zitaanza kutolewa hivi karibuni.

“Kwa kuanzia nyumba ya Mganga iko tayari ambapo kwa sasa imepauliwa baada ya serikali kutoa kiasi cha shilingi milioni 22 kinachosubiriwa ni kumalizia na mganga akiwepo huduma zitatolewa kwa saa 24 kwani kwa sasa huduma hutolewa muda wa kazi lakini baada ya hapo hufungwa hivyo endapo ikitokea changamoto ya mgonjwa huwabidi kumpeleka Tumbi au kituo cha afya Mkoani,”amesema Makuka.

Alisema kwa sasa huduma zote za vipimo zinatolewa lakini huduma za uzalishaji hazifanyiki hapo kutokana na kutokuwa na vifaa vya uzalishaji lakini kwa sasa huduma hizo zitatolewa hapo hali ambayo itawakomboa wanawake wakati wa kujifungua kwani huduma zitakuwa karibu na kupunguza changamoto za uzazi.

Alisema kuwa kutokana na huduma za afya kuwa karibu wanawake amabao wengi wanajishughulisha na shughuli za kiuchumi watakuwa na muda mwingi wa kufanya shughuli zao kwani wanwake wao ndiyo wanaotumia zaidi huduma za afya ambapo wao wakiumwa au watoto wao wakiumwa wao ndiyo huwapeleka watoto hospiatali tofauti na wanaume.

Mbali ya mafanikio ya ujenzi wa zahanati ambayo aliikuta kwenye hatua za awali vitu vingine ambavyo amefanikiwa na anajivunia ni pamoja na ujenzi wa madarasa mawali ya shule ya Msingi Msanagani, ofisi ya serikali ya mtaa ambayo ni ya kisasa ambayo ina vyumba vitatu na wanatafuta fedha kuongeza ili kupata ukumbi.

"Huduma ya maji nayo yalikuwa hayajasambaa kipindi naingia madarakani lakini kwa sasa sehemu kubwa ya mtaa ina huduma ya maji safi ambapo maeneo mawili tu ya Kiembeni na Mwanyundo ndiyo hayana maji pia aliwahi kuwapatia viti mwendo vinne watu wenye ulemavu katika mtaa wake,"amesema Makuka. 

Akizungumzia kuhusu masuala ya uongozi amesema kuwa Wazee wa Mtaa huo ndiyo walimwambia watampigania hivyo hakukutana na masuala ya ubaguzi kwani wazee hao walihakikisha hakuna anayeweza kutumia mila au desturi kumkwamisha katika harakati zake za kuwa kiongozi wanamheshimu sana hakuna mtu ambaye anaongelea masuala ya mapenzi.

“Nashukuru sana kwani kabla ya kuwa mwenyekiti wa mtaa nilikuwa katibu wa Kijiji na katibu wa ccm Msangani wakati huo hivyo sikukumbana na changamoto ya kubaguliwa au kunyanyaswa kijinsia kwani wazee wa kiume ndiyo waliopendekeza niwanie nafasi hiyo,’alisema Makuka.

Alisema kuwa aliingia kwenye uchaguzi wa ndani ya chama akiwa na washindani wenzake wanne wanaume na yeye mwanamke pekee lakini aliwashinda na kuwaacha mbali na yeye kuwa mgombea kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kuwashinda wanaume ambapo hata hivyo hakukuwa na uchaguzi wa vyama vingine baada ya vyama vya upinzani kujitoa kwenye uchaguzi wa serikali za mtaa mwaka 2021.

Je mume wake alimsaidia vipi anasema alikuwa msaada mkubwa kwake kwani alikuwa akimsaidia na hakuwa na wivu naye na wakati akifanya shughuli za kisiasa alikuwa msaada kwake na alimuwezesha masuala mengi ili kuhakikisha shughuli zake zinakwenda vizuri bila ya kukwama na alikuwa msaada na anamkumbuka sana ambaye kwa sasa ni marehemu alikuwa ni mwelewa na hakuwa na wivu kwani alikuwa akitambua kazi za viongozi.

"Nilikuwa nashirikiana naye vizuri kwenye baadhi ya majukumu ya kifamilia ili mimi niweze kutekeleza majukumu yangu ya kisiasa ambapo nikiwa sipo nyumbani mume wangu alikuwa akinisaidia kuhudumia familia kwani tuna watoto ambao walikuwa wakitakiwa kupata huduma mbalimbali,"amesema Makuka.

Pia hutenga muda kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake ya kifamilia na uongozi kwani huwa anatenga muda wake kwa ajili ya kuhudumia familia pale anapomaliza anahudumia wananchi wa mtaa wake na siasa haimfanyi ashindwe kuhudumia familia yake.

Anaelezea kuhusu changamoto ambayo wakati mwingine ni kikwazo kwa wanawake kwenye kuwania nafasi za uongozi ni rushwa ya ngono hakukumbana nayo kwa sababu wazee maarufu ndiyo walimshauri awanie nafasi hiyo hivyo hakukumbana na kikwzo cha kuombwa rushwa ya ngono kwa hilo anamshukuru Mungu kwani hakuna aliyeweza kumtamkia kuhusu masuala ya ngono japokuwa mambo hayo yapo na upande wa mila na desturi ambazo zilikuwa zikiwakandamiza wanawake kadri muda unavyokwenda zinapungua.

Alisema anawashukuru wananchi wakiwemo wanaume ambapo hawa mbezi kwa kusema kauli au misemo mbalimbali kwani anawaongoza anashirikiana nao vizuri kwenye masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na shughuli za kujitolea na wanawake ndiyo wanaojitokeza kwa wingi kwenye shughuli mbalimbali za kimaendeleo. 

Aliongeza kuwa ushauri wake kwa viongozi wanwake na wale wanaotarajia kugombea jambo kubwa wanalotakiwa kulifanya ni kuwa na ujasiri na kutokuwa na woga japo yeye alipoambiwa agombee uenyekiti alikuwa na woga lakini alijipa moyo na kukabili changamoto za uongozi.

Moja ya wakazi wa mtaa huo Ahmed Majengo alisema mwenyekiti wao ni shupavu licha ya kuwa ni mwanamke kwani anapambana sana katika kuhakikisha analeta maendeleo kwenye mtaa wake na pia anakabili changamoto ikiwa ni pamoja na dawa za kulevya na biashara ya wanawake kujiuza ambayo inaongezeka.

Majengo alisema kuwa kitu kinachomsaidia ni mtiifu na anayependa ukweli ambapo hupenda kukemea bilaya kuogopa ambapo matukio hata ya wizi yanapungua na uhalifu kwa ujumla siyo wa kutisha kutokana na hatua anazochukua kwani akijua kuna kijana analeta shida na akijiridhisha anamkamata na kumchukulia hatua.

Naye Amina Matima alisema kuwa mwenyekiti wao anafanyakazi haijalishi kuwa ni usiku au muda gani yeye anafanyakazi bila ya woga na hata ikifika hatua ya kuchangia mfano ujenzi wowote anachangia bila ya shida yoyote.

Salum Abdala anasema kuwa anajua changamoto nyingi na anazikabili licha ya kuwa yeye ni mwanamke haimfanyi kushindwa kuongoza na anasimamia miradi mingi ya maendeleo imefanikiwa kutokana na misimamo yake kwani hakubali kuyumbishwa na mtu yoyote.

Abdala anasema kuwa hawajutuii kumchagua kwani hata kubeba tofali anabeba kufukia mashimo barabarani anafanya kazi zote kama mwanaume kwake hakuna mfumo dume kwani anapambana bila ya hofu yoyote.

Makuka alianza siasa miaka ya 90 ambapo kabla ya kushika nafasi hiyo ya uenyekiti, katibu mwenezi wa kata hiyo kwa kipindi cha miaka mitatu kuwa makamu mwenyekiti wa chama cha ushirika cha msingi cha Msangani, pia aliwahi kuwa mwenyekiti wa kamati ya shule ya Msingi Msangani na ana watoto watatu ambao wote hakuna anayefuata nyayo zake.








Saturday, May 18, 2024

JKT RUVU YAZINDUA BUSTANI YA WANYAMAPORI

MKUU wa Wilaya ya Kibaha Nickson John amezindua bustani ya Wanyamapori ya Kikosi cha  Jeshi cha Ruvu JKT (Wildlife).

John akizindua bustani hiyo iliyopo kwenye eneo la Kikosi  cha 832 KJ Mlandizi Wilayani Kibaha Mkoani Pwani amewataka wananchi kujitokeza kwenda kuangalia wanyama ambao sasa wanapatikana karibu. 

Amesema uwepo wa Mbuga hiyo mbali ya kuwapunguzia gharama wananchi wanaotaka kuangalia wanyama pia itaongeza mapato ya Kikosi hicho na serikali.

Kwa upande wake Mkuu wa Kikosi hicho Kanali Peter Mnyani amesema kuwa wameanza na wanyama wachache lakini watawaongeza ili wawe wengi ambapo watakuwa na fursa ya kupiga picha na wanyama hao.

Mnyani amesema kuwa mwezi Juni wataongeza wanyama wakiwemo Simba ili kuongeza idadi ya wanyama na eneo hilo lina ukubwa wa hekari 70.

Amesema mbali ya kufuga wanyama hao pia wanatunza mazingira kutokana na eneo hilo kuwa na mazingira mazuri na ya asili.


Thursday, May 16, 2024

TUMEPANGA, TUMETEKELEZA, KUTEKELEZA: JAJI MKUU

 

Na Mwandishi Wetu , Dodoma 

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewapongeza watumishi wote wa Mahakama kwa kuendelea kutekeleza Mpango Mkakati wa Miaka Mitano awamu ya pili pamoja na programu ya Maboresho ya Miaka Mitano, ambazo zinalenga pia kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025.

Mhe. Prof. Juma ametoa pongezi hizo kupitia hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Jaji Amidi wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija, leo tarehe 16 Mei, 2024 kwenye Baraza Kuu la Wafanyakazi linalofanyika kwenye Ukumbi wa PSSSF jijini hapa.

“Nina kila sababu ya kuwapongeza wafanyakazi wa Mahakama kutokana na kujituma kwenu kuhakikisha kuwa tunatekeleza kwa ufanisi mipango tuliyojiwekea. Tufahamu kuwa kupanga ni jambo moja na utekelezaji wa mipango ni jambo lingine, kwetu sisi tumepanga, tumetekeleza na tunaendelea kutekeleza,” amesema.

Jaji Mkuu ametoa rai kwa wafanyakazi wote kutokurudi nyuma katika jitihada za kimaboresho kwani Viongozi wa Mahakama wanatambua na kuheshimu mchango wa kila mmoja ambao ndiyo uliowezesha utekelezaji wa programu mbalimbali za kimaboresho.

Ametumia fursa hiyo kuwahimiza watumishi wote kuipokea mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) inayotumiwa na Mahakama ya Tanzania ambayo siyo tu inawalenga wananchi na watumiaji wa huduma za Mahakama kwa kuwapa huduma kwa weledi, ufanisi, uwazi na kwa haraka lakini pia inalenga kuwaboreshea mazingira ya kufanya kazi za utoaji wa huduma.

Jaji Mkuu ametaja mfano wa Mfumo Mpya wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) ambao una faida lukuki zinazolenga kurahisha utendaji kazi kwa watumishi wa Mahakama ya Tanzania. 

Amesema kuwa, badala ya kupitia malundo ya majalada na karatasi kukusanya takwimu, Mfumo huu utakusanya takwimu na taarifa mbalimbali kwa njia ya elektroniki kwa usahihi. 

Jaji Mkuu amesema kuwa takwimu zitasaidia kuona yaliyojificha, hivyo kusaidia katika utekelezaji wa mipango mbalimbali na kuboresha jukumu la utoaji haki. 

“Mfumo huu utasaidia kupima utendaji wa kila mmoja wetu bila ubaguzi au uonevu kwa watumishi. Utaongeza tija, ufanisi na uono wa viwango vya utoaji wa huduma wa kila mtumiaji wa mfumo huu, kwa mfano Majaji, Wasajili, Mahakimu, Masjala za Mahakama, wadau wote wa Mahakama,” amesema.

Jaji Mkuu ametaja faida nyingine ni kupungua kwa watumishi kukutana na wadaawa uso kwa uso na kuondoa lawama za kimaadili kwa vile wadaawa na wananchi watapata fursa ya kuingia katika mfumo kutafuta taarifa bila kumuona mtumishi wa Mahakama. 

“Hakutakuwa na nafasi ya mtumishi kudhaniwa kuwa kapokea rushwa ili atoe huduma. Mfumo huu pia utaboresha usimamizi na ukaguzi. Kwa mfano, Jaji au Hakimu Mfawidhi na Wasajili, wataweza kuona kila hatua ambayo shauri lolote linapitia na kufikia mbele ya Jaji au Hakimu, bila kuliita jalada au kuomba taarifa ya mashauri kutoka kwa aliye na jalada,” amesema.

Jaji Mkuu ametaja Mfumo mwingine wa Tafsiri na Unukuzi (Transcription and Translation Software -TTS) ambao umelenga kuwapunguzia watumishi, hususan Majaji na Mahakimu, mzigo mzito wa kuandika mienendo ya mashauri kwa kalamu ya mkono. 

Ameeleza kuwa Mfumo huo unapokea sauti, uinakili hiyo sauti na kuiweka katika maandishi ya kiswahili na unao uwezo wa kutafsiri hayo maandishi kutoka lugha ya kiswahili hadi kiingereza na pia kutoka lugha ya kiingereza hadi kiswahili.

“Mfumo wa TTS tayari umefungwa na kuanza kutumika katika Mahakama 11, ikiwemo baadhi ya Mahakama Kuu (ambazo pia ni Masjala Ndogo za Mahakama ya Rufani),” Mhe. Prof. Juma amesma. 

Amesisitiza kuwa, mfumo huo wa TTS utaongeza ufanisi katika uchukuaji wa mwenendo wa shauri kwa kumpunguzia Jaji au Hakimu mzigo wa kusikiliza na kuandika kwa wakati mmoja na kuharakisha kupatikana kwa mienendo ya mashauri kwa ajili ya kukata rufani.

TANZANIA YAADHIMISHA MIAKA 60 YA KIDIPLOMASIA KATI YAKE NA CHINA

 

- Filamu ya " Amazing Tanzania " yazinduliwa China

Na Mwandishi Wetu - Beijing 

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeadhimisha Miaka 60 ya Kidiplomasia kati yake na China sambamba na uzinduzi wa mwaka wa Utalii na Utamaduni ulioambatana na  uzinduzi rasmi wa filamu ya “Amazing Tanzania” Mei 15, 2024 jijini Beijing China.

Akizungumza katika Maadhimisho hayo Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) amesema uhusiano kati ya China na Tanzania ulianza tangu kipindi cha Hayati Mwalimu Julius  Kambarage Nyerere.

Aidha,amesema mahusiano kati ya China na Tanzania  ni thabiti chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Xi Jinping.

"Tunapoadhimisha miaka 60 ya uhusiano wetu  na pia tunasherehekea mwaka wa utamaduni na utalii kama ilivyotangazwa na viongozi wetu mwaka 2022 katika ziara ya Kiserikali ya Rais Samia Suluhu alipotembelea nchini China" Mhe. Kairuki amesisitiza.

Katika hatua nyingine Waziri Kairuki ametumia fursa hiyo kumshukuru Rais Samia na Rais wa Zanzibar, Dkt. Hussein Ally Mwinyi pamoja na mwigizaji maarufu wa filamu kutoka China, Jin Dong kwa kushiriki katika uandaaji wa filamu hiyo.

Kufuatia uzinduzi wa filamu ya " Amazing Tanzania " Mhe. Kairuki amesema kuwa filamu hiyo itaonyesha vivutio vya utalii wa Tanzania kwa soko la utalii la China na kwamba Tanzania inatarajia kupokea watalii wengi kutoka nchini China baada ya uzinduzi huo.

Naye,Waziri wa Utamaduni na Utalii wa Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Sun Yeli amesema kuwa urafiki wa jadi kati ya China na Tanzania ulijengwa na viongozi wa kizazi cha zamani wa nchi hizo mbili na kwamba 

tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia miaka 60 iliyopita China Tanzania imestahimili jaribio la mabadiliko ya mazingira ya kimataifa na kuimarika zaidi.

"Leo tunapokutana hapa kuzindua mwaka wa Utalii na Utamaduni wa Tanzania China natumai tutaifanya kuwa mwanzo mpya wa kuendeleza mabadilishano ya kitamaduni na ushirikiano wa Utalii ili kurahisisha ziara zetu za pande mbili,  mabadilishano kati ya taasisi za kiutamaduni na sanaa na vile vile kampuni za utalii kuongeza usambazaji wa bidhaa za utalii." amesisitiza.

Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, wajumbe wa Kamati ya Rais ya Kuitangaza Tanzania akiwemo Katibu Mkuu, Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar, Fatma Mabrouk, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Anderson Mutatembwa, Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo, Dkt. Damas Ndumbaro,Waziri wa Vijana,Utamaduni na Michezo Zanzibar Mhe. Tabia Maulid Mwita  pamoja na maafisa wa taasisi mbalimbali za sekta za umma na binafsi.

Wednesday, May 15, 2024

MAKUMBUSHO YA CHINA NA TANZANIA KUSHIRIKIANA




Na Mwandishi Wetu-Beijing 

Makumbusho ya Taifa  ya China na Tanzania zimekubaliana  kushirikiana katika kubadilishana uzoefu, teknolojia na kuwa na maonesho ya pamoja  kwa lengo  la kuhakikisha kuwa huduma za makumbusho zinakuwa na faida kwa pande zote mbili za nchi hizo.

Makubaliano hayo yamefikiwa katika mazungumzo kati ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (Mb) na Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa la China, Gazo Zheng yaliyofanyika kwenye Makumbusho ya China jijini Beijing Mei 14,2024.

Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Kairuki amesema kwa kuwa Makumbusho ya Taifa la China ina uzoefu wa miaka mingi, ni vyema ikashirikiana na Makumbusho ya Taifa la Tanzania katika dijitali ,kufanya tafiti, kuwa na Maonesho ya pamoja, kuonesha utamaduni na historia ya nchi zote mbili pamoja na kubadilishana uzoefu wa utaalamu katika kutunza na kuhifadhi mikusanyo.
Aidha, Mhe. Kairuki amesema kuwa Tanzania ingependa kujifunza namna ya  kuvutia kizazi cha vijana kinachokua ili kiwe na utamaduni wa kutembelea Makumbusho mbalimbali zilizopo nchini Tanzania.

Amesema  Serikali ya Tanzania kupitia ubalozi wake ulipo jijini Beijing nchini China utahakikisha unafuata taratibu zote za kuwepo kwa  Mkataba wa Makubaliano kati ya makumbusho hizo ili kurasimisha ushirikiano huo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Zheng amesema Makumbusho ya Taifa la China iko tayari kushirikiana na Tanzania katika maeneo yote yaliyopendekezwa.

“Makumbusho ya Taifa la China ina uzoefu mkubwa na ina wataalamu zaidi ya mia moja hivyo ina furaha kushirikiana na Makumbusho ya Taifa la Tanzania hasa katika kuhifadhi mikusanyo, kufanya tafiti, kubadilishana uzoefu na namna ya kuvutia  vijana kuwa na utamaduni wa kutembelea makumbusho” amesema.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, wajumbe wa Kamati ya Rais ya Kuitangaza Tanzania akiwemo Katibu Mkuu, Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar, Fatma Mabrouk, Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Anderson Mutatembwa pamoja na maafisa wa taasisi mbalimbali za sekta za umma.

Waziri Kairuki yuko nchini China kwa ajili ya kushiriki katika Maadhimisho ya Miaka 60 ya Kidiplomasia kati ya Tanzania na China pamoja na uzinduzi wa mwaka wa Utalii na Utamaduni na pia uzinduzi rasmi wa filamu ya “Amazing Tanzania” utakaofanyika Mei 15, 2024 jijini Beijing

Wednesday, May 8, 2024

KUSIMAMA VIVUKONI NI AMRI SIO HIARI

Mkuu wa Dawati la elimu ya usalama barabarani Tanzania Kamishina Msaidizi wa Polisi, Michael Deceli amewataka madereva wa vyombo vya moto kuzingatia alama za barabarani ili kupunguza ajali kwa watumiaji wengine wa barabara.

Akizungumza Leo Mei, 08 baada ya kuhitimisha utoaji wa elimu ya uvukaji wa barabara kwenye vivuko vya waenda kwa miguu kwa wanafunzi wa shule ya msingi Misugusugu Wilaya ya Kibaha Mkoani Pwani Deceli amesema kumekuwepo na baadhi ya madereva wa vyombo vya moto wakiwemo madereva wa serikali kutokusimama kwenye  vivuko vya waenda kwa miguu na kupelekea ajali katika baadhi ya maeneo.

"Suala la kuheshimu alama za barabarani ni la kila dereva anayeendesha  chombo cha moto, Sheria haijabagua madereva wa kuziheshimu alama hizo na wengine kutokuheshimu".

Kadhalika, Deceli amewataka madereva walioweka magari yao ving'ora pasipo kuwa na kibali cha Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kuondoa mara moja na wale watakao kamatwa wakiwa hawana vibali hivyo watachukuliwa hatua za kisheria.

Friday, May 3, 2024

KPC YAWATAKA WANANCHI KUTUMIA KITUO CHAO KUTATUA CHANGAMOTO ZA KISHERIA.

 

WANANCHI wa Halmashauri ya Mji Kibaha wametakiwa kukitumia Kituo cha cha Msaada wa Kisheria (KPC) ili kutatua changamoto zinazohusiana na masuala ya kisheria ili kuokoa muda wa kwenda Mahakamani.


kimeendelea na utoaji elimu na msaada wa kisheria kwa makundi mbalimbali ili kuwajengea ufahamu wa sheria wananchi wa Halmashauri ya Mji Kibaha.

Akizingumza na waandishi wa habari Mjini Kibaha Mkurugenzi wa KPC Catherine Mlenga amesema kuwa baadhi ya masuala ya kisheria yanaweza kutatuliwa kituoni hapo kabla hawajayafikisha Mahakamani.

Mlenga amesema kuwa wananchi wanaweza kutatuliwa changamoto za kisheria na kuokoa muda ambao wangeutumia kwenda mahakamani na kufanya shughuli zao za maendeleo.

Aidha amesema kuwa wanatoa elimu pamoja na msaada kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo serikali kupitia ustawi wa jamii pamoja na mahakama.

Amewataka wananchi wa Kibaha kukitumia kituo hicho ili waweze kusaidiwa pale wanapopata changamoto za kisheria na wasifumbie vitendo vya ukatili ndani ya jamii kwa kutoa taarifa.

Mwisho.

KPC YAENDELEA KUTOA MSAADA NA ELIMU YA KISHERIA KWA WANANCHI WA KIBAHA

KITUO cha Msaada wa Kisheria (KPC) kimeendelea na utoaji elimu na msaada wa kisheria kwa makundi mbalimbali ili kuwajengea ufahamu wa sheria wananchi wa Halmashauri ya Mji Kibaha.

Akizingumza na waandishi wa habari baada ya kutoa mafunzo kwa wanafunzi wa Shule mbalimbali Mkurugenzi wa KPC Catherine Mlenga amesema kuwa elimu hiyo ni kwa wananchi wote.

Mlenga amesema kuwa wanatoa elimu pamoja na msaada kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo serikali.

"Tunaishukuru serikali kwa kutupatia vibali ambavyo vinatuwezesha kutoa elimu na msaada wa kisheria kwa wananchi lengo likiwa ni kuwapa uelewa wa kujua sheria mbalimbali,"amesema Mlenga.

Amesema kuwa elimu ya sheria imekuwa msaada mkubwa kwa wananchi ambapo baadhi wamepata uelewa na kuweza kutoa taarifa pale wanapoona kuna uvunjwaji wa sheria.

"Elimu tunayoitoa ni kuanzia kwa wanafunzi mashuleni, majumbani, masokoni, kwenye nyumba za ibada, kwenye mikutano na mikusanyiko mbalimbali ta kijamii,"amesema Mlenga.

Aidha amesema kuwa wanatoa msaada wa kisheria bure kwa watu wasiokuwa na uwezo hususani wanawake na watoto na kuwapigania hadi kupata haki zao.

"Sheria tunazowafundisha ni zote ikiwa ni pamoja na mirathi, ndoa, ardhi, matunzo ya watoto, haki za watoto, sheria za kazi, mazingira, na nyinginezo,"amesema Mlenga.

Amewataka wananchi wa Kibaha kukitumia kituo hicho ili waweze kusaidiwa pale wanapopata changamoto za kisheria na wasifumbie vitendo vya ukatili ndani ya jamii kwa kutoa taarifa.

Wednesday, May 1, 2024

WAHITIMU JKT KUJITOLEA WATAKIWA KUTANGULIZA UZALENDO

 




Na John Gagarini, Kibaha

VIJANA wanaohitimu mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) wakujitolea wametakiwa kutumia dhana ya uzalendo katika shuguli za ujenzi wa Taifa ili kuiletea nchi maendeleo.

Hayo yalisemwa Mlandizi na Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson John wakati wa kufunga mafunzo ya (JKT) ya kujitolea Operesheni Miaka 60 ya JKT kwenye Kikosi cha Ruvu Kibaha.

John alisema kuwa Vijana hao wameandaliwa vema kulipambania Taifa hivyo wakati wa utekelezaji wa majukumu yao lazima watangulize uzalendo.

"Zingatieni mambo manne muhimu Utii, nidhamu, uhodari na uaminifu haya ndiyo mambo ya kuzingatia hapa ndipo mtakuwa mnafanya uzalendo ambayo ndiyo nguzo kuu ya mafunzo yenu,"alisema John.

Alisema kuwa pia wawe na uhodari kwenye jambo moja ambalo ni fani ili wawe mahiri kwani kuchanganya mambo mengi kwa wakati mmoja hawataweza kuwa mahiri.

Kwa upande wake mwakilishi wa Mkuu wa Majeshi Meja Jenerali Ibrahim Mhona alisema kuwa vijana hao wanapaswa kujilinda kiafya kwani suala la afya ni muhimu sana.

Mhona ambaye pia ni Mkuu wa Mafunzo na Utendaji Kivita Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) alisema kuwa mafunzo hayo ni ya kuwapatia stadi za maisha na baadaye watapata stadi za kazi ikiwa ni hatua ya pili baada ya hatua ya kwanza.

Alisema kuwa mafunzo hayo yamekuza moyo wa uzalendo ukakamavu na kutumia vizuri muda na hawajakosea kujiunga na mafunzo hayo ya kujitolea kwani maamuzi yao ni ya busara na kuwapongeza wazazi na walezi kwa kuwapeleka vijana wao kwenye mafunzo hayo.

Naye mwakilishi wa Mkuu wa JKT Kanali Robert Kessy alisema kuwa wakati wa kutekeleza majukumu yao wahakikishe wanatatua changamoto bila kuvunja sheria na kuwa na nidhamu bila kusahau uhodari kwani Taifa limewekeza sehemu sahihi.

Kessy alisema kuwa vijana wanapaswa kujitolea kulitumikia Taifa na kumuenzi Baba wa Taifa ambaye aliasisi Jeshi hilo na wahakikishe wanaonyesha uzalendo kwa vitendo na weledi na wajiulize watalifanyia nini Taifa siyo Taifa kuwafanyia nini pia wahakikishe wanasimamia viapo vyao.

Awali Mkuu wa Kikosi cha Ruvu 832 KJ Kanali Peter Mnyani alisema kuwa mafunzo hayo ya awali ya kijeshi waliyoyapata vijana hao ni pamoja na ukakamavu ujasiri ambavyo wamefanya kwa vitendo.

Mnyani alisema kuwa mafunzo hayo yalikuwa ya muda wa miezi minne kati ya miezi 24 ya mkataba wao ambapo walijifunza utimamu wa mwili, usomaji ramani, uraia,  usalama na utambuzi na kwata za silaha ndogo ndogo.

Akisoma risala ya wahitimu wa mafunzo hayo Lulu Godfrey alisema kuwa Vijana wa Kujitolea Operesheni Miaka 60 ya JKT walianza mafunzo hayo Desemba 2023.

Godfrey alisema kuwa kwenye mafunzo hayo walifundishwa mbinu mbalimbali ikiwa ni pamoja mbinu za ulinzi, ukakamavu, utii, ulinzi wa taifa ujasiri uvumilivu, na hawatatumia vibaya mafunzo hayo kinyume na malengo ya Taifa.

Jumla vijana 800 walijiunga na mafunzo hayo ambapo waliohitimu walikuwa 776 wavulana wakiwa 438 na wasichana walikuwa 338 na vijana 24 hawakumaliza mafunzo hayo na kwa kipindi cha miezi 20 watakuwa kwenye majukumu mbalimbali ikiwa ni pamoja na malezi, uzalishaji mali na ulinzi.

 Mwisho.